Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya Mwaka

Chapter 2


Tanzania

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya Mwaka

Sura ya 2

  • Ilianza tarehe 26 Aprili 1977
  • [Hili ni toleo la hati hii katika 31 Julai 2002.]
  • [Taarifa: Sheria hii imekaguliwa na kufanyiwa marekebisho kamili chini ya usimamizi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, kwa kuzingatia Sheria ya Ufanyaji Tathmini Na. 7 ya 1994, Sheria Zilizorekebishwa na Ukaguzi wa Kila Mwaka (Sura 356 (R.L.)), na Sheria ya Ufafanuzi wa Sheria na Vipengele vya Kawaida Na. 30 ya 1972. Toleo hili lina taarifa za hivi karibuni hadi tarehe 31 Julai 2002.]
[C.A. Acts Nos.; 1 of 1977; 2 of 1977; Sheria Na.; 14 ya 1979; 1 ya 1980; 28 ya 1980; 21 ya 1982; 15 ya 1984; 14 ya 1990; 16 ya 1990; 4 ya 1992; 20 ya 1992; 7 ya 1993; 34 ya 1994; 12 ya 1995; 3 ya 2000; T.S. Na. 133 la 20011]1T.S. Na. ina maana Tangazo la Serikali namba 133 la 2001.
KWA KUWA SISI Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeamua rasmi na kwa dhati kujenga katika nchi yetu jamii inayozingatia misingi ya uhuru, haki, udugu na amani: 22Sheria Na. 15 ya 1984 ib. 3NA KWA KUWA misingi hiyo yaweza tu kutekelezwa katika jamii yenye demokrasia ambayo Serikali yake husimamiwa na Bunge lenye wajumbe waliochaguliwa na linalowawakilisha wananchi, na pia yenye Mahakama huru zinazotekeleza wajibu wa kutoa haki bila woga wala upendeleo wowote, na hivyo kuhakikisha kwamba haki zote za binadamu zinadumishwa na kulindwa, na wajibu wa kila mtu unatekelezwa kwa uaminifu:KWA HIYO, BASI, KATIBA HII IMETUNGWA NA BUNGE MAALUM LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, kwa niaba ya Wananchi, kwa madhumuni ya kujenga jamii kama hiyo, na pia kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Tanzania inaongozwa na Serikali yenye kufuata misingi ya demokrasia na ujamaa.

Sura ya Kwanza
Jamhuri ya Muungano, vyama vya siasa, watu na siasa ya ujamaa na kujitegemea (Ib. 1—32)

Sehemu ya Kwanza – Jamhuri ya Muungano na Watu (Ib. 1—5)

1. Kutangaza Jamhuri ya Muungano

Tanzania ni nchi moja na ni Jamhuri ya Muungano.

2. Eneo la Jamhuri ya Muungano

(1)Eneo la Jamhuri ya Muungano ni eneo lote la Tanzania Bara na eneo lote la Tanzania Zanzibar, na ni pamoja na sehemu yake ya bahari ambayo Tanzania inapakana nayo.
(2)Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Rais aweza kuigawa Jamhuri ya Muungano katika mikoa, wilaya na maeneo mengineyo, kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria au kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge; isipokuwa kwamba Rais atashauriana kwanza na Rais wa Zanzibar kabla ya kuigawa Tanzania Zanzibar katika mikoa, wilaya au maeneo mengineyo.

3. Tangazo la nchi yenye mfumo wa Vyama Vingi

(1)Jamhuri ya Muungano ni nchi ya kidemokrasia na ya kijamaa, yenye kufuata mfumo wa vyama vingi vya siasa.
(2)Mambo yote yahusuyo uandikishaji na uendeshaji wa vyama vya siasa nchini yatasimamiwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na ya sheria iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo.

4. Utekelezaji wa shughuli za Mamlaka ya Nchi

(1)Shughuli zote za Mamlaka ya Nchi katika Jamhuri ya Muungano zitatekelezwa na kudhibitiwa na vyombo viwili vyenye mamlaka ya utendaji, vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki, na pia vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma.
(2)Vyombo vyenye mamlaka ya utendaji vitakuwa ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar; vyombo vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki vitakuwa ni Idara ya Mahakama ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Idara ya Mahakama ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na vyombo vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma vitakuwa ni Bunge na Baraza la Wawakilishi.
(3)Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za umma katika Jamhuri ya Muungano, na kwa ajili ya mgawanyo wa madaraka juu ya shughuli hizo baina ya vyombo vilivyotajwa katika ibara hii, kutakuwa na Mambo ya Muungano kama yalivyoorodheshwa katika Nyongeza ya Kwanza iliyoko mwishoni mwa Katiba hii, na pia kutakuwa na mambo yasiyo ya Muungano, ambayo ni mambo mengine yote yasiyo Mambo ya Muungano.
(4)Kila chombo kilichotajwa katika ibara hii kitaundwa na kutekeleza majukumu yake kwa kufuata masharti mengine yaliyomo katika Katiba hii.

5. Haki ya kupiga kura

(1)Kila raia wa Tanzania aliyetimiza umri wa miaka kumi na minane anayo haki ya kupiga kura katika uchaguzi unaofanywa Tanzania na wananchi. Na haki hii itatumiwa kwa kufuata masharti ya ibara ndogo ya (2) pamoja na masharti mengineyo ya Katiba hii na ya Sheria inayotumika nchini Tanzania kuhusu mambo ya uchaguzi.
(2)Bunge laweza kutunga sheria na kuweka masharti yanayoweza kuzuia raia asitumie haki ya kupiga kura kutokana na yoyote kati ya sababu zifuatazo, yaani raia huyo–
(a)kuwa na uraia wa nchi nyingine;
(b)kuwa na ugonjwa wa akili;
(c)kutiwa hatiani kwa makosa fulani ya jinai;
(d)kukosa au kushindwa kuthibitisha au kutoa kitambulisho cha umri, uraia au uandikishwaji kama mpiga kura,
mbali na sababu hizo hakuna sababu nyingine yoyote inayoweza kumzuia raia asitumie haki ya kupiga kura.
(3)Bunge litatunga Sheria ya Uchaguzi na kuweka masharti kuhusu mambo yafuatayo–
(a)kuanzisha Daftari la Kudumu la wapiga kura, na kuweka utaratibu wa kurekebisha yaliyomo katika Daftari hilo;
(b)kutaja sehemu na nyakati za kuandikisha wapiga kura na kupiga kura;
(c)utaratibu wa kumwezesha mpiga kura aliyejiandikisha sehemu moja kupiga kura sehemu nyingine na kutaja masharti ya utekelezaji wa utaratibu huo;
(d)kutaja kazi na shughuli za Tume ya Uchaguzi na utaratibu wa kila uchaguzi ambao utaendeshwa chini ya uongozi na usimamizi wa Tume ya Uchaguzi.

Sehemu ya Pili – Malengo muhimu na misingi ya mwelekeo wa shughuli za Serikali (Ib 6—11)

6. Tafsiri

Katika Sehemu hii ya Sura hii, isipokuwa kama maelezo yahitaji vinginevyo, neno "Serikali" maana yake ni pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, serikali za mitaa na pia mtu anayetekeleza madaraka au mamlaka yoyote kwa niaba ya Serikali yoyote.

7. Matumizi ya masharti ya Sehemu ya Pili

(1)Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (2), Serikali, vyombo vyake vyote na watu wote au mamlaka yoyote yenye kutekeleza madaraka ya utawala, madaraka ya kutunga sheria au madaraka ya utoaji haki, watakuwa na jukumu na wajibu wa kuzingatia, kutia maanani na kutekeleza masharti yote ya Sehemu hii ya Sura hii.
(2)Masharti ya Sehemu hii ya Sura hii hayatatiliwa nguvu ya kisheria na Mahakama yoyote. Mahakama yoyote nchini haitakuwa na uwezo wa kuamua juu ya suala kama kutenda au kukosa kutenda jambo kwa mtu au mahakama yoyote, au kama sheria, au hukumu yoyote, inaambatana na masharti ya Sehemu hii ya Sura hii.

8. Serikali na watu

(1)Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii, na kwa hiyo–
(a)wananchi ndio msingi wa mamlaka yote, na Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii;
(b)lengo kuu la Serikali litakuwa ni ustawi wa wananchi;
(c)Serikali itawajibika kwa wananchi;
(d)wananchi watashiriki katika shughuli za Serikali yao kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(2)Muundo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, au wa chochote kati ya vyombo vyake na uendeshaji wa shughuli zake utatekelezwa kwa kuzingatia umoja wa Jamhuri ya Muungano na haja ya kukuza umoja wa kitaifa na kudumisha heshima ya Taifa.

9. Ujenzi wa Ujamaa na Kujitegemea

Lengo la Katiba hii ni kuwezesha ujenzi wa Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar au wa chochote kati ya vyombo vyake na udugu na amani kutokana na kufuata siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, ambayo inasisitiza utekelezaji wa misingi ya kijamaa kwa kuzingatia mazingira yaliyomo katika Jamhuri ya Muungano. Kwa hiyo Mamlaka ya Nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha–
(a)kwamba utu na haki nyinginezo zote za binadamu zinaheshimiwa na kuthaminiwa;
(b)kwamba sheria za nchi zinalindwa na kutekelezwa;
(c)kwamba shughuli za Serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo zitahakikisha kwamba utajiri wa Taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote kwa jumla na pia kuzuia mtu kumnyonya mtu mwingine;
(d)kwamba maendeleo ya uchumi wa Taifa yanakuzwa na kupangwa kwa ulinganifu na kwa pamoja;
(e)kwamba kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi anafanya kazi, na kazi maana yake ni shughuli yoyote ya halali inayompatia mtu riziki yake;
(f)kwamba heshima ya binadamu inahifadhiwa na kudumishwa kwa kufuata Kanuni za Tangazo la Dunia kuhusu Haki za Binadamu;
(g)kwamba Serikali na vyombo vyake vyote vya umma vinatoa nafasi zilizo sawa kwa raia wote, wake kwa waume, bila ya kujali rangi, kabila, dini au hali ya mtu;
(h)kwamba aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini;
(i)kwamba matumizi ya utajiri wa Taifa yanatilia mkazo maendeleo ya wananchi na hasa zaidi yanaelekezwa kwenye jitihada ya kuondosha umaskini, ujinga na maradhi;
(j)kwamba shughuli za uchumi haziendeshwi kwa njia zinazoweza kusababisha ulimbikizaji wa mali au njia kuu za uchumi katika mamlaka ya watu wachache binafsi;
(k)kwamba nchi inatawaliwa kwa kufuata misingi ya demokrasia na ujamaa.

10. ***

[Imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ib. 10]

11. Haki ya kufanya kazi, kupata elimu na nyinginezo

(1)Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa haki ya mtu kufanya kazi, haki ya kujipatia elimu na haki ya kupata msaada kutoka kwa jamii wakati wa uzee, maradhi au hali ya ulemavu, na katika hali nyinginezo za mtu kuwa hajiwezi. Na bila ya kuathiri haki hizo, Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba kila mtu anaishi kwa jasho lake.
(2)Kila mtu anayo haki ya kujielimisha, na kila raia atakuwa huru kutafuta elimu katika fani anayopenda hadi kufikia upeo wowote kulingana na stahili na uwezo wake.
(3)Serikali itafanya jitihada kuhakikisha kwamba watu wote wanapata fursa sawa na za kutosha kuwawezesha kupata elimu na mafunzo ya ufundi katika ngazi zote za shule na vyuo vinginevyo vya mafunzo.

Sehemu ya Tatu – Haki na wajibu muhimu (Ib 12—32)

Haki ya Usawa (Ib 12—13)

12. Usawa wa binadamu

(1)Binadamu wote huzaliwa huru, na wote ni sawa.
(2)Kila mtu anastahili heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake.

13. Usawa mbele ya sheria

(1)Watu wote ni sawa mbele ya sheria na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria.
(2)Ni marufuku kwa sheria yoyote iliyotungwa na mamlaka yoyote katika Jamhuri ya Muungano kuweka sharti lolote ambalo ni la ubaguzi ama wa dhahiri au kwa taathira yake.
(3)Haki za raia, wajibu na maslahi ya kila mtu na jumuiya ya watu yatalindwa na kuamuliwa na Mahakama na vyombo vinginevyo vya Mamlaka ya Nchi vilivyowekwa na Sheria au kwa mujibu wa sheria.
(4)Ni marufuku kwa mtu yeyote kubaguliwa na mtu au mamlaka yoyote inayotekeleza madaraka yake chini ya sheria yoyote au katika utekelezaji wa kazi au shughuli yoyote ya Mamlaka ya Nchi.
(5)Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya ibara hii neno "kubagua" maana yake ni kutimiza haja, haki au mahitaji mengineyo kwa watu mbalimbali kwa kuzingatia utaifa wao, kabila, pahala walipotokea, maoni yao ya kisiasa, rangi, dini, jinsia au hali yao ya maisha kwa namna ambayo watu wa aina fulani wanafanywa au kuhesabiwa kuwa dhaifu au duni na kuwekewa vikwazo au masharti ya vipingamizi ambapo watu wa aina nyingine wanatendewa tofauti au wanapewa fursa au faida iliyoko nje ya masharti au sifa za lazima, isipokuwa kwamba neno "kubagua" halitafafanuliwa kwa namna ambayo itaizuia Serikali kuchukua hatua za makusudi zenye lengo la kurekebisha matatizo katika jamii.
(6)Kwa madhumuni ya kuhakikisha usawa mbele ya sheria, Mamlaka ya Nchi itaweka taratibu zinazofaa au zinazozingatia misingi kwamba–
(a)wakati haki na wajibu wa mtu yeyote vinahitaji kufanyiwa uamuzi wa mahakama au chombo kinginecho kinachohusika, basi mtu huyo atakuwa na haki ya kupewa fursa ya kusikilizwa kwa ukamilifu, na pia haki ya kukata rufaa au kupata nafuu nyingine ya kisheria kutokana na maamuzi ya mahakama au chombo hicho kinginecho kinachohusika;
(b)ni marufuku kwa mtu aliyeshtakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu mwenye kosa hilo mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo;
(c)ni marufuku kwa mtu kuadhibiwa kwa sababu ya kitendo chochote ambacho alipokitenda hakikuwa ni kosa chini ya sheria, na pia kwamba ni marufuku kwa adhabu kutolewa ambayo ni kubwa kuliko adhabu iliyokuwapo wakati kosa linalohusika lilipotendwa;
(d)kwa ajili ya kuhifadhi haki ya usawa wa binadamu, heshima ya mtu itatunzwa katika shughuli zote zinazohusu upelelezi na uendeshaji wa mambo ya jinai na katika shughuli nyinginezo ambazo mtu anakuwa chini ya ulinzi bila uhuru, au katika kuhakikisha utekelezaji wa adhabu;
(e)ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazomtweza au kumdhalilisha.

Haki ya Kuishi (Ib 14—17)

14. Haki ya kuwa hai

Kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka kwa jamii hifadhi ya maisha yake, kwa mujibu wa sheria.

15. Haki ya Uhuru wa mtu binafsi

(1)Kila mtu anayo haki ya kuwa huru na kuishi kama mtu huru.
(2)Kwa madhumuni ya kuhifadhi haki ya mtu kuwa huru na kuishi kwa uhuru, itakuwa ni marufuku kwa mtu yeyote kukamatwa, kufungwa, kufungiwa, kuwekwa kizuizini, kuhamishwa kwa nguvu au kunyang'anywa uhuru wake vinginevyo, isipokuwa tu–
(a)katika hali na kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria; au
(b)katika kutekeleza hukumu, amri au adhabu iliyotolewa na mahakama kutokana na shauri au na mtu kutiwa hatiani kwa kosa la jinai.

16. Haki ya faragha na ya usalama wa mtu

(1)Kila mtu anastahili kuheshimiwa na kupata hifadhi kwa nafsi yake, maisha yake binafsi na familia yake na unyumba wake, na pia heshima na hifadhi ya maskani yake na mawasiliano yake ya binafsi.
(2)Kwa madhumuni ya kuhifadhi haki ya mtu kwa mujibu wa ibara hii, Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu wa sheria kuhusu hali, namna na kiasi ambacho haki ya mtu ya faragha na ya usalama na nafsi yake, mali yake na maskani yake, yaweza kuingiliwa bila ya kuathiri ibara hii.

17. Uhuru wa mtu kwenda atakako

(1)Kila raia wa Jamhuri ya Muungano anayo haki ya kwenda kokote katika Jamhuri ya Muungano na kuishi katika sehemu yoyote, kutoka nje ya nchi na kuingia, na pia haki ya kutoshurutishwa kuhama au kufukuzwa kutoka katika Jamhuri ya Muungano.
(2)Kitendo chochote cha halali au sheria yoyote yenye madhumuni ya–
(a)kupunguza uhuru wa mtu kwenda atakako na kumweka chini ya ulinzi au kifungoni; au
(b)kuweka mipaka kwa matumizi ya uhuru wa mtu kwenda anakotaka ili–
(i)kutekeleza hukumu au amri ya mahakama; au
(ii)kumlazimisha mtu kutimiza kwanza wajibu wowote anaotakiwa na sheria nyingine kuutimiza; au
(iii)kulinda manufaa ya umma kwa jumla au kuhifadhi maslahi fulani mahususi au maslahi ya sehemu fulani ya umma, kitendo hicho hakitahesabiwa au sheria hiyo haitahesabiwa kuwa ni haramu au ni kinyume cha ibara hii.

Haki ya Uhuru wa Mawazo (Ib 18—21)

18. Uhuru wa Maoni

(1)Bila ya kuathiri sheria za nchi, kila mtu yuko huru kuwa na maoni yoyote na kutoa nje mawazo yake, na kutafuta, kupokea na kutoa habari na dhana zozote kupitia chombo chochote bila ya kujali mipaka ya nchi, na pia ana uhuru wa kutoingiliwa kati mawasiliano yake.
(2)Kila raia anayo haki ya kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali nchini na duniani kote ambayo ni muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi, na pia juu ya masuala muhimu kwa jamii.

19. Uhuru wa mtu kuamini dini atakayo

(1)Kila mtu anastahili kuwa na uhuru wa mawazo, imani na uchaguzi katika mambo ya dini, pamoja na uhuru wa mtu kubadilisha dini au imani yake.
(2)Bila ya kuathiri sheria zinazohusika za Jamhuri ya Muungano, kazi ya kutangaza dini, kufanya ibada na kueneza dini itakuwa ni huru na jambo la hiari la mtu binafsi; na shughuli na uendeshaji wa jumuiya za dini zitakuwa nje ya shughuli za mamlaka ya nchi.
(3)Kila palipotajwa neno "dini" katika ibara hii ifahamike kwamba maana yake ni pamoja na madhehebu ya dini, na maneno mengineyo yanayofanana au kuambatana na neno hilo nayo yatatafsiriwa kwa maana hiyo.

20. Uhuru wa mtu kushirikiana na wengine

(1)Kila mtu anastahili kuwa huru, bila kuathiri sheria za nchi, kukutana na watu wengine kwa hiari yake na kwa amani, kuchanganyika na kushirikiana na watu wengine, kutoa mawazo hadharani, na hasa zaidi kuanzisha au kujiunga na vyama au mashirika yaliyoanzishwa kwa madhumuni ya kuhifadhi au kuendeleza imani au maslahi yake au maslahi mengineyo.
(2)Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (1) haitakuwa halali kwa chombo chochote cha siasa kuandikishwa ambacho kutokana na Katiba au sera yake–
(a)kinakusudia kukuza au kupigania maslahi ya–
(i)imani au kundi lolote la dini;
(ii)kundi lolote la kikabila pahala watu watokeapo, rangi au jinsia;
(iii)eneo fulani tu katika sehemu yoyote ya Jamhuri ya Muungano;
(b)kinapigania kuvunjwa kwa Jamhuri ya Muungano;
(c)kinakubali au kupigania matumizi ya nguvu au mapambano kama njia za kufikia malengo yake ya kisiasa;
(d)kinapigania au kukusudia kuendesha shughuli zake za kisiasa katika sehemu moja tu ya Jamhuri ya Muungano;
(e)hakiruhusu uongozi wake kuchaguliwa kwa vipindi na kwa njia za kidemokrasia.
(3)Bunge laweza kutunga sheria inayoweka masharti yatakayohakikisha kuwa vyama vya siasa vinazingatia mipaka na vigezo vilivyowekwa na masharti ya ibara ndogo ya (2) kuhusu uhuru na haki ya watu kushirikiana na kujumuika.
(4)Bila ya kuathiri sheria za nchi zinazohusika ni marufuku kwa mtu yeyote kulazimishwa kujiunga na chama chochote au shirika lolote, au kwa chama chochote au cha siasa kukataliwa kusajiliwa kwa sababu tu ya itikadi au falsafa yake.

21. Uhuru wa kushiriki shughuli za umma

(1)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ya 5, ya 39 na ya 67 ya Katiba hii na ya sheria za nchi kuhusiana na masharti ya kuchagua na kuchaguliwa, au kuteua na kuteuliwa kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi, kila raia wa Jamhuri ya Muungano anayo haki ya kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi, ama moja kwa moja au kwa kupitia wawakilishi waliochaguliwa na wananchi kwa hiari yao, kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa na sheria au kwa mujibu wa sheria.
(2)Kila raia anayo haki na uhuru wa kushiriki kwa ukamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomhusu yeye, maisha yake au yanayolihusu Taifa.

Haki ya Kufanya Kazi (Ib. 22—24)

22. Haki ya kufanya kazi

(1)Kila mtu anayo haki ya kufanya kazi.
(2)Kila raia anastahili fursa na haki sawa, kwa masharti ya usawa, ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyo chini ya Mamlaka ya Nchi.

23. Haki ya kupata ujira wa haki

(1)Kila mtu, bila ya kuwapo ubaguzi wa aina yoyote, anayo haki ya kupata ujira unaolingana na kazi yake, na watu wote wanaofanya kazi kulingana na uwezo wao watapata malipo kulingana na kiasi na sifa za kazi wanayoifanya.
(2)Kila mtu anayefanya kazi anastahili kupata malipo ya haki.

24. Haki ya kumiliki mali

(1)Bila ya kuathiri masharti ya sheria za nchi zinazohusika, kila mtu anayo haki ya kumiliki mali, na haki ya hifadhi kwa mali yake aliyonayo kwa mujibu wa sheria.
(2)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), ni marufuku kwa mtu yeyote kunyang'anywa mali yake kwa madhumuni ya kuitaifisha au madhumuni mengineyo bila ya idhini ya sheria ambayo inaweka masharti ya kutoa fidia inayostahili.

Wajibu wa Jamii (Ib 25—28)

25. Wajibu wa kushiriki kazini

(1)Kazi pekee ndiyo huzaa utajiri wa mali katika jamii, ndilo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha utu. Kila mtu anao wajibu wa–
(a)kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji mali; na
(b)kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji ya binafsi na yale ya pamoja yanayotakiwa au yaliyowekwa na sheria.
(2)Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (1), hakutakuwapo na kazi ya shuruti katika Jamhuri ya Muungano.
(3)Kwa madhumuni ya ibara hii, na katika Katiba hii kwa jumla, ifahamike kwamba kazi yoyote haita hesabiwa kuwa ni kazi ya shuruti au kazi ya kikatili au ya kutweza endapo kazi hiyo, kwa mujibu wa sheria ni–
(a)kazi inayobidi ifanywe kutokana na hukumu au amri ya mahakama;
(b)kazi inayobidi ifanywe na askari wa jeshi lolote katika kutekeleza majukumu yao;
(c)kazi ambayo mtu yeyote inabidi aifanye kutokana na kuwapo hali ya hatari au baa lolote linalotishia uhai wa ustawi wa jamii;
(d)kazi au huduma yoyote ambayo ni sehemu ya–
(i)majukumu ya kawaida ya kuhakikisha ustawi wa jamii;
(ii)ujenzi wa taifa wa lazima kwa mujibu wa sheria;
(iii)jitihada za taifa za kutumia uwezo wa kila mtu kufanya kazi kwa ajili ya kuimarisha jamii na uchumi wa taifa na kuhakikisha maendeleo na tija ya kitaifa.

26. Wajibu wa kutii sheria za nchi

(1)Kila mtu ana wajibu wa kufuata na kutii Katiba hii na sheria za Jamhuri ya Muungano.
(2)Kila mtu ana haki, kwa kufuata utaratibu uliowekwa na sheria, kuchukua hatua za kisheria kuhakikisha hifadhi ya Katiba na sheria za nchi.

27. Kulinda mali ya Umma

(1)Kila mtu ana wajibu wa kulinda maliasilia ya Jamhuri ya Muungano, mali ya Mamlaka ya Nchi na mali yote inayomilikiwa kwa pamoja na wananchi, na pia kuiheshimu mali ya mtu mwingine.
(2)Watu wote watatakiwa na sheria kutunza vizuri mali ya Mamlaka ya Nchi na ya pamoja, kupiga vita aina zote za uharibifu na ubadhilifu, na kuendesha uchumi wa taifa kwa makini kama watu ambao ndio waamuzi wa hali ya baadaye ya taifa lao.

28. Ulinzi wa taifa

(1)Kila raia ana wajibu wa kulinda, kuhifadhi na kudumisha uhuru, mamlaka, ardhi na umoja wa taifa.
(2)Bunge laweza kutunga Sheria zinazofaa kwa ajili ya kuwawezesha wananchi kutumikia katika majeshi na katika ulinzi wa taifa.
(3)Mtu yeyote hatakuwa na haki ya kutia sahihi kwenye mkataba wa kukubali kushindwa vita na kulitoa taifa kwa mshindi, wala kuridhia au kutambua kitendo cha uvamizi au mgawanyiko wa Jamhuri ya Muungano au wa sehemu yoyote ya ardhi ya eneo la taifa na, bila ya kuathiri Katiba hii na sheria zilizowekwa, hakuna mtu atakayekuwa na haki ya kuwazuia raia wa Jamhuri ya Muungano kupigana vita dhidi ya adui yeyote anayeshambulia nchi.
(4)Uhaini kama unavyofafanuliwa na sheria utakuwa ni kosa la juu kabisa dhidi ya Jamhuri ya Muungano.

Masharti ya Jumla (Ib 29—30)

29. Haki na wajibu muhimu

(1)Kila mtu katika Jamhuri ya Muungano anayo haki ya kufaidi haki za msingi za binadamu, na matokeo ya kila mtu kutekeleza wajibu wake kwa jamii, kama zilivyofafanulia katika ibara ya 12 hadi ya 28 za Sehemu hii ya Sura hii ya Katiba.
(2)Kila mtu katika Jamhuri ya Muungano anayo haki ya kupata hifadhi sawa chini ya sheria za Jamhuri ya Muungano.
(3)Raia yeyote wa Jamhuri ya Muungano hatakuwa na haki, au cheo maalum kwa misingi ya nasaba, jadi au urithi wake.
(4)Ni marufuku kwa sheria yoyote kutoa haki, hadhi au cheo maalum kwa raia yeyote wa Jamhuri ya Muungano kwa msingi ya nasaba, jadi au urithi.
(5)Ili watu wote waweze kufaidi haki na uhuru vilivyotajwa na Katiba hii kila mtu ana wajibu wa kutenda na kuendesha shughuli zake kwa namna ambayo haitaingilia haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma.

30. Mipaka ya haki na Uhuru na hifadhi kwa haki na wajibu

(1)Haki na uhuru wa binadamu ambavyo misingi yake imeorodheshwa katika Katiba hii havitatumiwa na mtu mmoja kwa maana ambayo itasababisha kuingiliwa kati au kukatizwa kwa haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma.
(2)Ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika sehemu hii ya Katiba hii, yanayofafanua misingi ya haki, uhuru na wajibu wa binadamu, hayaharamishi sheria yoyote iliyotungwa wala kuzuia sheria yoyote kutungwa au jambo lolote halali kufanywa kwa mujibu wa sheria hiyo, kwa ajili ya–
(a)kuhakikisha kwamba haki na uhuru wa watu wengine au maslahi ya umma haviathiriwi na matumizi mabaya ya uhuru na haki za watu binafsi;
(b)kuhakikisha ulinzi, usalama wa jamii, amani katika jamii, maadili ya jamii, afya ya jamii, mipango ya maendeleo ya miji na vijiji, ukuzaji na matumizi ya madini au ukuzaji na uendelezaji wa mali au maslahi mengineyo yoyote kwa nia ya kukuza manufaa ya umma;
(c)kuhakikisha utekelezaji wa hukumu au amri ya mahakama iliyotolewa katika shauri lolote la madai au la jinai;
(d)kulinda sifa, haki na uhuru wa watu wengine au maisha binafsi ya watu wanohusika katika mashauri mahakamani; kuzuia kutoa habari za siri; kutunza heshima, mamlaka na uhuru wa mahakama;
(e)kuweka vizuizi, kusimamia na kudhibiti uanzishaji, uendeshaji na shughuli za vyama na mashirika ya watu binafsi nchini; au
(f)kuwezesha jambo jingine lolote kufanyika ambalo linastawisha au kuhifadhi maslahi ya taifa kwa jumla.
(3)Mtu yeyote anayedai kuwa sharti lolote katika Sehemu hii ya Sura hii au katika sheria yoyote inayohusu haki yake au wajibu kwake, limevunjwa, linavunjwa au inaelekea litavunjwa na mtu yeyote popote katika Jamhuri ya Muungano, anaweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu.
(4)Bila ya kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Katiba hii, Mahakama Kuu itakuwa na mamlaka ya kusikiliza kwa mara ya kwanza na kuamua shauri lolote lililoletwa mbele yake kwa kufuata ibara hii; na Mamlaka ya Nchi yaweza kuweka sheria kwa ajili ya–
(a)kusimamia utaratibu wa kufungua mashauri kwa mujibu wa ibara hii;
(b)kufafanua uwezo wa Mahakama Kuu katika kusikiliza mashauri yaliyofunguliwa chini ya ibara hii.
(c)kuhakikisha utekelezaji bora wa madaraka ya Mahakama Kuu, hifadhi na kutilia nguvu haki, uhuru na wajibu kwa mujibu wa Katiba hii;
(5)Endapo katika shauri lolote inadaiwa kwamba sheria yoyote iliyotungwa na hatua yoyote iliyochukuliwa na Serikali au mamlaka nyingine inafuta au inakatiza haki, uhuru na wajibu muhimu zitokanazo na ibara ya 12 hadi 29 za Katiba hii, na Mahakama Kuu inaridhika kwamba sheria au hatua inayohusika, kwa kiwango inachopingana na Katiba ni batili au kinyume cha Katiba basi Mahakama Kuu ikiona kuwa yafaa au hali au masilahi ya jamii yahitaji hivyo, badala ya kutamka kuwa sheria au hatua hiyo ni batili, itakuwa na uwezo wa kuamua kutoa fursa kwa ajili ya Serikali au mamlaka nyingine yoyote inayohusika kurekebisha hitilafu iliyopo katika sheria inayotuhumiwa au hatua inayohusika katika muda na kwa jinsi itakavyotajwa na Mahakama Kuu, na sheria hiyo au hatua inayohusika itaendelea kuhesabiwa kuwa ni halali hadi ama marekebisho yatakapofanywa au muda uliowekwa na Mahakama Kuu utakapokwisha, mradi muda mfupi zaidi ndio uzingatiwe.

Madaraka ya pekee ya Mamlaka ya Nchi (Ib. 31—32)

31. Ukiukaji wa haki na uhuru

(1)Mbali na masharti ya ibara ya 30(2), sheria yoyote iliyotungwa na Bunge haitakuwa haramu kwa sababu tu kwamba inawezesha hatua kuchukuliwa wakati wa hali ya hatari, au wakati wa hali ya kawaida kwa watu wanaoaminika kuwa wanafanya vitendo vinavyohatarisha au kudhuru usalama wa taifa, ambazo zinakiuka masharti ya ibara ya 14 na ya 15 za Katiba hii.
(2)Ni marufuku kwa hatua zilizotajwa katika ibara ndogo ya (1) ya ibara hii kuchukuliwa kwa mujibu wa sheria yoyote wakati wa hali ya hatari, au wakati wa hali ya kawaida kwa mtu yeyote, isipokuwa tu kwa kiasi ambacho ni lazima na halali kwa ajili ya kushughulikia hali iliyopo wakati wa hali ya hatari au wakati wa hali ya kawaida kushughulikia hali iliyosababishwa na mwenendo wa mtu anayehusika.
(3)Ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika ibara hii hayataidhinisha mtu kunyang'anywa haki yake ya kuwa hai isipokuwa tu kwa kifo kama matokeo ya vitendo vya kivita.
(4)Kwa madhumuni ya ibara hii na ibara zifuatazo za Sehemu hii "wakati wa hali ya hatari" maana yake ni kipindi chochote ambapo Tangazo la Hali ya Hatari, lililotolewa na Rais kwa kutumia uwezo aliopewa katika ibara ya 32, linatumika.

32. Madaraka ya kutangaza hali ya hatari

(1)Bila ya kuathiri Katiba hii, au sheria iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo, Rais aweza kutangaza hali ya hatari katika Jamhuri ya Muungano au katika sehemu yake yoyote.
(2)Rais aweza tu kutangaza kuwa kuna hali ya hatari iwapo–
(a)Jamhuri ya Muungano iko katika vita; au
(b)kuna hatari hasa kwamba Jamhuri ya Muungano inakaribia kuvamiwa au kuingia katika hali ya vita; au
(c)kuna hali halisi ya kuvurugika kwa amani ya jamii au kutoweka kwa usalama wa jamii katika Jamhuri ya Muungano au sehemu yake yoyote kiasi kwamba ni lazima kuchukua hatua za pekee ili kurejesha amani na usalama; au
(d)kuna hatari dhahiri na kubwa, kiasi kwamba amani ya jamii itavurugika na usalama wa raia kutoweka katika Jamhuri ya Muungano au sehemu yake yoyote ambayo haiwezi kuepukika isipokuwa kwa kutumia mamlaka ya pekee; au
(e)karibu kutatokea tukio la hatari au tukio la balaa au la baa ya kimazingira ambalo linatishia jamii au sehemu ya jamii katika Jamhuri ya Muungano; au
(f)kuna aina nyingineyo ya hatari ambayo kwa dhahiri ni tishio kwa nchi.
(3)Endapo inatangazwa kwamba kuna hali ya hatari katika Jamhuri ya Muungano nzima, au katika Tanzania Bara nzima au katika Tanzania Zanzibar nzima, Rais atatuma mara nakala ya tangazo hilo kwa Spika wa Bunge ambaye, baada ya kushauriana na Kiongozi wa shughuli za Serikali Bungeni, ataitisha mkutano wa Bunge ndani ya siku zisizozidi kumi na nne, ili kuitafakari hali ya mambo na kuamua kupitisha au kutopitisha azimio, litakaloungwa mkono na kura za wajumbe wasiopungua theluthi mbili ya wajumbe wote, la kuunga mkono tangazo la hali ya hatari lililotolewa na Rais.
(4)Bunge laweza kutunga sheria inayoweka masharti kuhusu nyakati na utaratibu ambao utawawezesha watu fulani wenye kusimamia utekelezaji wa mamlaka ya Serikali katika sehemu mahususi za Jamhuri ya Muungano kumuomba Rais kutumia madaraka aliyopewa na ibara hii kuhusiana na yoyote kati ya sehemu hizi endapo katika sehemu hizi kunatokea yoyote kati ya hali zilizotajwa katika aya ya (c), (d) na (e) za ibara ndogo ya (2) na hali hiyo haivuki mipaka ya sehemu hizo; na pia kwa ajili ya kufafanua utekelezaji wa mamlaka ya Serikali wakati wa hali ya hatari.
(5)Tangazo la hali ya hatari lililotolewa na Rais kwa mujibu wa ibara hii litakoma kutumika–
(a)iwapo litafutwa na Rais;
(b)endapo zitapita siku kumi na nne tangu tangazo lilipotolewa kabla ya kupitishwa azimio lililotajwa katika ibara ndogo ya (3);
(c)baada ya kupita muda wa miezi sita tangu tangazo hilo lilipotolewa; isipokuwa kwamba kikao cha Bunge chaweza, kabla ya muda wa miezi sita kupita, kuongeza mara kwa mara muda wa tangazo hilo kutumika kwa vipindi vya miezi mingine sita kwa azimio litakaloungwa mkono na kura za wajumbe wa kikao hicho wasiopungua theluthi mbili ya wajumbe wote;
(d)wakati wowote ambapo mkutano wa Bunge utalitangua tangazo hilo kwa azimio litakaloungwa mkono na kura za wajumbe wasiopungua theluthi mbili ya wajumbe wote.
(6)Kwa madhumuni ya kuondoa mashaka juu ya ufafanuzi au utekelezaji wa masharti ya ibara hii, masharti ya sheria iliyotungwa na Bunge na ya sheria nyingine yoyote, inayohusu utangazaji wa hali ya hatari kama ilivyotajwa katika ibara hii, yatatumika tu katika sehemu ya Jamhuri ya Muungano ambapo hali hiyo ya hatari imetangazwa.

Sura ya Pili
Serikali ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 33—61)

Sehemu ya Kwanza – Rais (Ib. 33—46B)

33. Rais wa Jamhuri ya Muungano

(1)Kutakuwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano.
(2)Rais atakuwa Mkuu wa Nchi, Kiongozi wa Serikali na Amiri Jeshi Mkuu.

34. Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Mamlaka yake

(1)Kutakuwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambayo itakuwa na mamlaka juu ya mambo yote ya Muungano katika Jamhuri ya Muungano, na pia juu ya mambo mengine yote yahusuyo Tanzania Bara.
(2)Mamlaka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano yatahusu utekelezaji na hifadhi ya Katiba hii na pia mambo mengineyo yote ambayo Bunge lina mamlaka ya kuyatungia sheria.
(3)Mamlaka yote ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano juu ya mambo yote ya Muungano katika Jamhuri ya Muungano, na pia juu ya mambo mengineyo yote yahusuyo Tanzania Bara, yatakuwa mikononi mwa Rais wa Jamhuri ya Muungano.
(4)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, madaraka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano yatatekelezwa ama na Rais mwenyewe moja kwa moja au kwa kukasimu madaraka hayo kwa watu wengine wenye madaraka katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(5)Ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika ibara hii hayatahesabiwa kwamba–
(a)yanahamishia kwa Rais madaraka yoyote ya kisheria yaliyowekwa na sheria mikononi mwa mtu au mamlaka yoyote ambayo si Rais; au
(b)yanalizuia Bunge kukabidhi madaraka yoyote ya kisheria mikononi mwa mtu au watu au mamlaka yoyote ambayo si Rais.

35. Utekelezaji wa shughuli za Serikali

(1)Shughuli zote za utendaji za Serikali ya Jamhuri ya Muungano zitatekelezwa na watumishi wa Serikali kwa niaba ya Rais.
(2)Amri na maagizo mengine yanayotolewa kwa madhumuni ya ibara hii yatathibitishwa kwa namna itakavyoelezwa katika kanuni zilizowekwa na Rais, kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii.

36. Mamlaka ya kuanzisha na kuwateua watu wa kushika nafasi za madaraka

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Katiba hii na ya sheria nyingine yoyote, Rais atakuwa na mamlaka ya kuanzisha na kufuta nafasi za madaraka ya namna mbalimbali katika utumishi wa Umma wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2)Rais atakuwa na madaraka ya kuteua watu wa kushika nafasi za madaraka ya viongozi wanaowajibika kuweka sera za idara na taasisi za Umma na watendaji wakuu wanaowajibika kusimamia utekelezaji wa sera za idara na taasisi hizo katika utumishi wa Umma wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, nafasi ambazo zimetajwa katika Katiba hii au katika sheria mbalimbali zilizotungwa na Bunge kwamba zitajazwa kwa uteuzi unaofanywa na Rais.
(3)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (2), masharti mengineyo yaliyomo katika Katiba hii na ya sheria yoyote inayohusika, mamlaka ya kuwateua watu wengine wote wasiokuwa viongozi wala watendaji wakuu, kushika nafasi za madaraka katika utumishi wa Umma wa Serikali ya Muungano, na pia mamlaka ya kuwapandisha vyeo watu hao, kuwaondoa katika madaraka, kuwafukuza kazi na mamlaka ya kudhibiti nidhamu ya watu waliokabidhiwa madaraka, yatakuwa mikononi mwa Tume za Utumishi na mamlaka mengineyo yaliyotajwa na kupewa madaraka kuhusu nafasi za madaraka kwa mujibu wa Katiba hii au kwa mujibu wa sheria yoyote inayohusika.
(4)Masharti ya ibara ndogo ya (2) na ya (3) hayatahesabiwa kuwa yanamzuia Rais kuchukua hatua za kudhibiti nidhamu ya watumishi na utumishi wa umma katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

37. Utekelezaji wa kazi na shughuli za Rais, n.k.3

3T. S. Na. ina maana Tangazo la Serikali namba 133 la 2001.
(1)Mbali na kuzingatia masharti yaliyomo katika Katiba hii na katika sheria za Jamhuri ya Muungano katika utendaji wa kazi na shughuli zake, Rais atakuwa huru na hatalazimika kufuata ushauri atakaopewa na mtu yeyote, isipokuwa tu pale anapotakiwa na Katiba hii au na sheria nyingine yoyote kufanya jambo lolote kulingana na ushauri anaopewa na mtu au mamlaka yoyote.
(2)Endapo Baraza la Mawaziri litaona kuwa Rais hawezi kumudu kazi zake kwa sababu ya maradhi ya mwili au ya akili, laweza kuwasilisha kwa Jaji Mkuu azimio la kumwomba Jaji Mkuu athibitishe kwamba Rais, kwa sababu ya maradhi ya mwili au akili, hawezi kumudu kazi zake. Baada ya kupokea azimio kama hilo, Jaji Mkuu atateua Bodi ya utabibu ya watu wasiopungua watatu atakaowateua kutoka miongoni mwa mabingwa wanaotambuliwa na sheria ya matabibu ya Tanzania, na Bodi hiyo itachunguza suala hilo na kumshauri Jaji Mkuu ipasavyo, naye aweza, baada ya kutafakari ushahidi wa kitabibu kuwasilisha kwa Spika hati ya kuthibitisha kwamba Rais, kutokana na maradhi ya mwili au ya akili, hamudu kazi zake; na iwapo Jaji Mkuu hatabatilisha tamko hilo ndani ya siku saba kutokana na Rais kupata nafuu na kurejea kazini, basi itahesabiwa kwamba kiti cha Rais ki wazi, na masharti yaliyomo katika ibara ndogo ya (3) yatatumika.
(3)Ikitokea kwamba kiti cha Rais ki wazi kutokana na masharti yaliyomo katika ibara ndogo ya (2), endapo kiti cha Rais ki wazi kutokana na sababu nyingine yoyote, na endapo Rais atakuwa hayupo katika Jamhuri ya Muungano, kazi na shughuli za Rais zitatekelezwa na mmojawapo wa wafuatao, kwa kufuata orodha kama ilivyopangwa, yaani–
(a)Makamu wa Rais au kama nafasi yake i wazi au kama naye hayupo au ni mgonjwa; basi
(b)Spika wa Bunge au, kama nafasi yake i wazi au kama naye hayupo au ni mgonjwa; basi
(c)Jaji Mkuu wa Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano.
(4)Endapo yeyote kati ya watu waliotajwa katika aya ya (b) na (c) za ibara ndogo ya (3) atatekeleza kazi na shughuli za Rais kutokana na sababu kwamba mtu mwingine anayemtangulia katika orodha hiyo hayupo, basi mtu huyo ataacha kutekeleza kazi na shughuli hizo mara tu mtu huyo mwingine anayemtangulia atakaporejea na akashika na kuanza kutekeleza kazi na shughuli za Rais.
(5)Endapo kiti cha Rais kitakuwa wazi kutokana na Rais kufariki dunia, kujiuzulu, kupoteza sifa za uchaguzi au kutomudu kazi zake kutokana na maradhi ya mwili au kushindwa kutekeleza kazi na shughuli za Rais, basi Makamu wa Rais ataapishwa na atakuwa Rais kwa muda uliobaki katika kipindi cha miaka mitano na kwa masharti yaliyoelezwa katika ibara ya 40, kisha baada ya kushauriana na chama cha siasa anachotoka Rais atapendekeza jina la mtu atakayekuwa Makamu wa Rais na uteuzi huo utathibitishwa na Bunge kwa kura zisizopungua asilimia hamsini ya Wabunge wote.
(6)Ifahamike kwamba kiti cha Rais hakitakuwa ki wazi na Rais hatahesabiwa kwamba hayuko katika Jamhuri ya Muungano endapo–
(a)atakuwa hayupo katika mji ambao ndio makao makuu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano;
(b)atakuwa hayupo katika Jamhuri ya Muungano kwa kipindi cha muda wa saa ishirini na nne; au
(c)atakuwa ni mgonjwa lakini anatumaini kuwa atapata nafuu baada ya muda si mrefu.
(7)Iwapo kutatokea lolote kati ya mambo yaliyotajwa katika ibara ndogo ya (6) na Rais akiona kuwa inafaa kuwakilisha madaraka yake kwa muda wa jambo hilo, basi aweza kutoa maagizo kwa maandishi ya kumteua yeyote kati ya watu waliotajwa katika aya ya (a) au ya (b) za ibara ndogo ya (3) ya ibara hii kwa ajili ya kutekeleza madaraka ya Rais wakati yeye hayupo au ni mgonjwa, na mtu huyo atakayeteuliwa atatekeleza madaraka hayo ya Rais kwa kufuata masharti yoyote yatakayowekwa na Rais; isipokuwa kwamba masharti yaliyomo katika ibara hii ndogo yafahamike kuwa hayapunguzi wala kuathiri uwezo wa Rais alionao kwa mujibu wa sheria nyingine yoyote wa kuwakilisha madaraka yake kwa mtu mwingine yeyote.
(8)Rais aweza, akiona inafaa kufanya hivyo, kumwagiza kwa maandishi Waziri yeyote kutekeleza kazi na shughuli zozote za Rais ambazo Rais atazitaja katika maagizo yake na Waziri aliyeagizwa hivyo kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo, atakuwa na mamlaka ya kutekeleza kazi na shughuli hizo kwa kufuata masharti yoyote yaliyowekwa na Rais, lakini bila ya kujali masharti ya sheria nyingine yoyote; isipokuwa kwamba–
(a)Rais hatakuwa na mamlaka ya kuwakilisha kwa Waziri kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo kazi yoyote ya Rais aliyokabidhiwa na sheria yoyote inayotokana na masharti ya mkataba wowote uliotiwa sahihi na Jamhuri ya Muungano iwapo kisheria Rais haruhusiwi kuwakilisha kazi hiyo kwa mtu mwingine yeyote;
(b)ifahamike kwamba maagizo yanayotolewa na Rais kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo, ya kumwagiza Waziri yeyote kutekeleza kazi yoyote ya Rais, hayatahesabiwa kwamba yanamzuia Rais kutekeleza kazi hiyo yeye mwenyewe.
(9)Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya ibara hii–
(a)Mkutano wa Baraza la Mawaziri uliofanywa kwa ajili ya kuwasilisha kwa Jaji Mkuu azimio kuhusu hali ya afya ya Rais utahesabiwa kuwa ni mkutano halali hata kama mjumbe yeyote wa Baraza hilo hayupo au kiti chake ki wazi, na itahesabiwa kuwa Baraza limepitisha azimio hilo ikiwa litaungwa mkono kwa kauli ya wajumbe walio wengi waliohudhuria mkutano na kupiga kura;
(b)Rais hatahesabiwa kuwa hayupo katika Jamhuri ya Muungano kwa sababu tu ya kupitia nje ya Tanzania wakati yuko safarini kutoka sehemu moja ya Tanzania kwenda sehemu nyingine, au kwa sababu kwamba ametoa maagizo kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (7) na maagizo hayo bado hayajabatilishwa.
(10)Bila ya kujali masharti yaliyoelezwa hapo awali katika ibara hii, mtu atakayetekeleza kazi na shughuli za Rais kwa mujibu wa ibara hii hatakuwa na mamlaka ya kulivunja Bunge, kumwondoa yeyote kati ya Mawaziri katika madaraka yake, au kufuta uteuzi wowote uliofanywa na Rais.
(11)Mtu yeyote atakayetekeleza kazi na shughuli za Rais kwa mujibu wa masharti ya ibara hii kama ni Mbunge hatapoteza kiti chake katika Bunge wala hatapoteza sifa zake za kuchaguliwa kuwa Mbunge kwa sababu tu ya kutekeleza kazi na shughuli za Rais kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.

38. Uchaguzi wa Rais

(1)Rais atachaguliwa na wananchi kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na kwa mujibu wa Sheria itakayoweka masharti kuhusu uchaguzi wa Rais ambayo itatungwa na Bunge kwa kufuata masharti ya Katiba hii.
(2)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, kiti cha Rais kitakuwa ki wazi na uchaguzi wa Rais utafanyika au nafasi hiyo itajazwa vinginevyo kwa mujibu wa Katiba hii, kadri itakavyokuwa, kila mara litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)baada ya Bunge kuvunjwa;
(b)baada ya Rais kujiuzulu bila ya kuvunja Bunge kwanza;
(c)baada ya Rais kupoteza sifa za kushika nafasi ya madaraka ya kuchaguliwa;
(d)baada ya Rais kushtakiwa Bungeni kwa mujibu wa Katiba hii, na kuondolewa katika madaraka;
(e)baada ya kuthibitishwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 37 ya Katiba hii kwamba Rais hawezi kumudu kazi na shughuli zake;
(f)baada ya Rais kufariki.
(3)Kiti cha Rais hakitahesabiwa kuwa ki wazi kwa sababu tu ya Bunge kupitisha hoja ya kutokuwa na imani kwa Waziri Mkuu.

39. Sifa za mtu kuchaguliwa kuwa Rais

(1)Mtu hatastahili kuchaguliwa kushika kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano isipokuwa tu kama–
(a)ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Sheria ya Uraia;
(b)ametimiza umri wa miaka arobaini;
(c)ni mwanachama, na mgombea aliyependekezwa na chama cha siasa;
(d)anazo sifa za kumwezesha kuwa Mbunge au Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi;
(e)katika kipindi cha miaka mitano kabla ya tarehe ya Uchaguzi Mkuu hajawahi kutiwa hatiani katika Mahakama yoyote kwa kosa lolote la kukwepa kulipa kodi yoyote ya Serikali.
(2)Bila ya kuingilia haki na uhuru wa mtu kuwa na maoni yake, kuamini dini atakayo, kushirikiana na wengine na kushiriki shughuli za umma kwa mujibu wa sheria za nchi, mtu yeyote hatakuwa na sifa za kuchaguliwa kushika kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano kama si mwanachama na mgombea aliyependekezwa na chama cha siasa.

40. Haki ya kuchaguliwa tena

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika ibara hii, mtu yeyote ambaye ni Rais anaweza kuchaguliwa tena kushika kiti hicho.
(2)Hakuna mtu atakayechaguliwa zaidi ya mara mbili kushika kiti cha Rais.
(3)Mtu aliyewahi kuwa Rais wa Zanzibar hatapoteza sifa za kuweza kuchaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa sababu tu kwamba aliwahi kushika madaraka ya Rais wa Zanzibar.
(4)Endapo Makamu wa Rais anashika kiti cha Rais kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 37(5) kwa kipindi kinachopungua miaka mitatu ataruhusiwa kugombea nafasi ya Rais mara mbili, lakini kama akishika kiti cha Rais kwa muda wa miaka mitatu au zaidi ataruhusiwa kugombea nafasi ya Rais mara moja tu.

41. Utaratibu wa uchaguzi wa Rais

(1)Baada ya Bunge kuvunjwa au kukitokea jambo jingine lolote lililotajwa katika ibara ndogo ya (2) ya ibara ya 38 na inalazimu uchaguzi wa Rais kufanyika, kila chama cha siasa kinachopenda kushiriki katika uchaguzi wa Rais kitawasilisha kwa Tume ya Uchaguzi, kwa mujibu wa sheria, jina la mwanachama wake mmoja kinayetaka asimame kama mgombea katika uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, na jina la mwanachama wake mwingine kinayempendekeza kwa nafasi ya Makamu wa Rais.
(2)Mapendekezo ya majina ya wagombea katika uchaguzi wa Rais yatawasilishwa kwa Tume ya Uchaguzi katika siku na saa itakayotajwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge, na mtu hatakuwa amependekezwa kwa halali isipokuwa tu kama kupendekezwa kwake kunaungwa mkono na wananchi wapiga kura kwa idadi na kwa namna itakayotajwa na sheria iliyotungwa na Bunge.
(3)Endapo inapofika saa na siku iliyotajwa kwa ajili ya kuwasilisha mapendekezo ya majina ya wagombea, ni mgombea mmoja tu ambaye anapendekezwa kwa halali, Tume itawasilisha jina lake kwa wananchi, nao watapiga kura ya kumkubali au kumkataa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii na ya sheria iliyotungwa na Bunge.
(4)Uchaguzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano utafanywa siku itakayoteuliwa na Tume ya Uchaguzi kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.
(5)Mambo mengine yote yahusuyo utaratibu wa uchaguzi wa Rais yatakuwa kama itakavyofafanuliwa katika sheria iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo.
(6)Mgombea yeyote wa kiti cha Rais atatangazwa kuwa amechaguliwa kuwa Rais iwapo tu amepata kura nyingi zaidi kuliko mgombea mwingine yeyote.
(7)Iwapo mgombea ametangazwa na Tume ya Uchaguzi kwamba amechaguliwa kuwa Rais kwa mujibu wa ibara hii, basi hakuna mahakama yoyote itakayokuwa na mamlaka ya kuchunguza kuchaguliwa kwake.

42. Wakati na muda wa kushika madaraka ya Rais

(1)Rais mteule atashika madaraka ya Rais mapema iwezekanavyo baada ya kutangazwa kwamba amechaguliwa kuwa Rais, lakini kwa hali yoyote itabidi ashike madaraka kabla ya kupita siku saba.
(2)Isipokuwa kama atajiuzulu au atafariki mapema zaidi mtu aliyechaguliwa kuwa Rais, bila ya kuathiri masharti yaliyo katika ibara ndogo ya (3), atashika kiti cha Rais kwa muda wa miaka mitano tangu siku alipochaguliwa kuwa Rais.
(3)Mtu aliyechaguliwa kuwa Rais atashika kiti cha Rais hadi–
(a)siku ambapo mtu atakayemfuatia katika kushika kiti hicho atakula kiapo cha Rais; au
(b)siku ambapo atafariki dunia akiwa katika madaraka; au
(c)siku atakapojiuzulu; au
(d)atakapoacha kushika kiti cha Rais kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(4)Iwapo Jamhuri ya Muungano inapigana vita dhidi ya adui na Rais anaona kuwa haiwezekani kufanya uchaguzi, Bunge laweza mara kwa mara kupitisha azimio la kuongeza muda wa miaka mitano uliotajwa katika ibara ndogo ya (2) ya ibara hii isipokuwa kwamba muda wowote utakaoongezwa kila mara hautazidi miezi sita.
(5)Kila Rais mteule na kila mtu atakayeshikilia kiti cha Rais, kabla ya kushika madaraka ya Rais, ataapa mbele ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano kiapo cha uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

43. Masharti ya kazi ya Rais

(1)Rais atalipwa mshahara na malipo mengineyo, na atakapostaafu atapokea malipo ya uzeeni, kiinua mgongo au posho, kadri itakavyoamuliwa na Bunge, na mshahara, malipo hayo mengineyo, malipo ya uzeeni na kiinua mgongo hicho, vyote vitatokana na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vitatolewa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(2)Mshahara na malipo mengineyo yote ya Rais havitapunguzwa wakati Rais atakapokuwa bado ameshika madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.

44. Madaraka ya kutangaza vita

(1)Bila ya kuathiri Katiba hii, au sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo, Rais aweza kutangaza kuwapo kwa hali ya vita kati ya Jamhuri ya Muungano na nchi yoyote.
(2)Baada ya kutoa tangazo, Rais atapeleka nakala ya tangazo hilo kwa Spika wa Bunge ambaye, baada ya kushauriana na Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni, ndani ya siku kumi na nne kuanzia tarehe ya tangazo, ataitisha mkutano wa Bunge ili kuitafakari hali ya mambo na kufikiria kupitisha au kutopitisha azimio la kuunga mkono tangazo la vita lililotolewa na Rais.

45. Uwezo wa kutoa msamaha

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika ibara hii, Rais anaweza kutenda lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)kutoa msamaha kwa mtu yeyote aliyepatikana na hatia mbele ya mahakama kwa kosa lolote, na aweza kutoa msamaha huo ama bila ya masharti au kwa masharti, kwa mujibu wa sheria;
(b)kumwachilia kabisa au kwa muda maalum mtu yeyote aliyehukumiwa kuadhibiwa kwa ajili ya kosa lolote ili mtu huyo asitimize kabisa adhabu hiyo au asitimize adhabu hiyo wakati wa muda huo maalum;
(c)kuibadilisha adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa kosa lolote iwe adhabu tahafifu;
(d)kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu yoyote aliyopewa mtu yeyote kwa ajili ya kosa lolote au kufuta adhabu yote au sehemu ya adhabu ya kutoza, au kuhozi (au kuchukua) kitu cha mtu mwenye hatia ambacho vinginevyo kingechukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2)Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka utaratibu utakaofuatwa na Rais katika utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa ibara hii.
(3)Masharti ya ibara hii yatatumika kwa watu waliohukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Zanzibar na kwa adhabu zilizotolewa Tanzania Zanzibar kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge inayotumika Tanzania Zanzibar, hali kadhalika, masharti hayo yatatumika kwa watu waliohukumiwa na kuadhibiwa Tanzania Bara kwa mujibu wa sheria.

46. Kinga dhidi ya mashtaka na madai

(1)Wakati wote Rais atakapokuwa bado ameshika madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii, itakuwa ni marufuku kumshtaki au kuendesha mashtaka ya aina yoyote juu yake mahakamani kwa ajili ya kosa lolote la jinai.
(2)Wakati wote Rais atakapokuwa bado ameshika madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii, haitaruhusiwa kufungua mahakamani shauri kuhusu jambo lolote alilolitenda au alilokosa kulitenda yeye binafsi kama raia wa kawaida ama kabla au baada ya kushika madaraka ya Rais, ila tu kama angalau siku thelathini kabla ya shauri kufunguliwa mahakamani, Rais atapewa au ametumiwa kwamba taarifa ya madai kwa maandishi kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge, na taarifa hiyo ikiwa inatoa maelezo kuhusu chanzo cha shauri hilo, kiini cha madai yenyewe, jina lake na anwani ya mahali anapoishi huyo mdai na jambo hasa analodai.
(3)Isipokuwa kama ataacha kushika madaraka ya Rais kutokana na masharti ya ibara ya 46A(10), itakuwa ni marufuku kumshtaki au kufungua mahakamani shauri lolote la jinai au la kumdai mtu aliyekuwa anashika madaraka ya Rais baada ya kuacha madaraka hayo kutokana na jambo lolote alilofanya yeye kama Rais wakati alipokuwa bado anashika madaraka ya Rais kwa mujibu wa Katiba hii.

46A. Bunge laweza kumshtaki Rais

(1)Bila ya kujali masharti ya ibara ya 46 ya Katiba hii, Bunge linaweza kupitisha azimio la kumuondoa Rais madarakani endapo itatolewa hoja ya kumshtaki Rais na ikapitishwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(2)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya ibara hii, hoja yoyote ya kumshtaki Rais haitatolewa isipokuwa tu kama inadaiwa kwamba Rais–
(a)ametenda vitendo ambavyo kwa jumla vinaivunja Katiba au sheria ya maadili ya Viongozi wa Umma;
(b)ametenda vitendo ambavyo vinakiuka maadili yanayohusu uandikishwaji wa vyama vya siasa yaliyotajwa katika ibara ya 20(2) ya Katiba; au
(c)amekuwa na mwenendo unaodhalilisha kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano, na haitatolewa hoja ya namna hiyo ndani ya miezi kumi na miwili tangu hoja kama hiyo ilipotolewa na ikakataliwa na Bunge.
(3)Bunge halitapitisha hoja ya kumshtaki Rais isipokuwa tu kama–
(a)taarifa ya maandishi, iliyotiwa sahihi na kuungwa mkono na Wabunge wasiopungua asilimia ishirini ya Wabunge wote itawasilishwa kwa Spika siku thelathini kabla ya kikao ambapo hoja hiyo inakusudiwa kutolewa Bungeni, ikifafanua makosa aliyoyatenda Rais, na ikipendekeza kuwa Kamati Maalum ya Uchunguzi iundwe ili ichunguze mashtaka yaliyowasilishwa dhidi ya Rais;
(b)wakati wowote baada ya Spika kupokea taarifa iliyotiwa sahihi na Wabunge na kujiridhisha kuwa masharti ya Katiba kwa ajili ya kuleta hoja yametimizwa, Spika atamruhusu mtoa hoja kuiwasilisha hoja hiyo, na kisha Spika atalitaka Bunge, bila ya kufanya majadiliano, lipige kura juu ya hoja ya kuunda Kamati Maalum ya Uchunguzi na kama ikiungwa mkono na Wabunge wasiopungua theluthi mbili ya Wabunge wote, atatangaza majina ya wajumbe wa Kamati Maalum ya Uchunguzi.
(4)Kamati Maalum ya Uchunguzi, kwa madhumuni ya ibara hii, itakuwa na wajumbe wafuatao, yaani–
(a)Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, ambaye atakuwa ndiye Mwenyekiti wa Kamati;
(b)Jaji Mkuu wa Tanzania Zanzibar; na
(c)Wabunge saba walioteuliwa na Spika kwa mujibu wa Kanuni za Bunge na kwa kuzingatia uwiano wa uwakilishi baina ya vyama vya siasa vinavyowakilishwa Bungeni.
(5)Endapo Bunge litapitisha hoja ya kuunda Kamati Maalum ya Uchunguzi, Rais atahesabiwa kuwa hayupo kazini, kisha kazi na madaraka ya Rais yatatekelezwa kwa mujibu wa masharti ya ibara 37(3) ya Katiba hii hadi Spika atakapomfahamisha Rais juu ya azimio la Bunge kuhusiana na mashtaka yaliyotolewa dhidi yake.
(6)Ndani ya siku saba baada ya Kamati Maalum ya Uchunguzi kuundwa, itakaa, ichunguze na kuchambua mashtaka dhidi ya Rais, pamoja na kumpatia Rais fursa ya kujieleza, kwa kufuata utaratibu uliowekwa na Kanuni za Bunge.
(7)Mapema iwezekanavyo, na kwa vyovyote vile katika muda usiozidi siku tisini, Kamati Maalum ya Uchunguzi itatoa taarifa yake kwa Spika.
(8)Baada ya Spika kupokea taarifa ya Kamati Maalum ya Uchunguzi, taarifa hiyo itawasilishwa Bungeni kwa kufuata utaratibu uliowekwa na Kanuni za Bunge.
(9)Baada ya taarifa ya Kamati Maalum ya Uchunguzi kuwasilishwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (8), Bunge litaijadili taarifa hiyo na litampa Rais fursa ya kujieleza, na kisha, kwa kura za Wabunge wasiopungua theluthi mbili ya Wabunge wote, Bunge litapitisha azimio ama kuwa mashtaka dhidi ya Rais yamethibitika, na kwamba hastahili kuendelea kushika kiti cha Rais, au kuwa mashtaka hayo hayakuthibitika.
(10)Endapo Bunge litapitisha azimio kuwa mashtaka dhidi ya Rais yamethibitika na kwamba hastahili kuendelea kushika kiti cha Rais, Spika atawafahamisha Rais na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi juu ya azimio la Bunge, na hapo Rais atawajibika kujiuzulu kabla ya kuisha kwa siku ya tatu tangu Bunge lilipopitisha azimio hilo.
(11)Endapo Rais ataacha kushika kiti cha Rais kutokana na mashtaka dhidi yake kuthibitika, hatakuwa na haki ya kupata malipo yoyote ya pensheni wala kupata haki au nafuu nyinginezo alizo nazo kwa mujibu wa Katiba au Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge.

46B. Wajibu wa viongozi Wakuu wa vyombo vya Mamlaka ya Utendaji kudumisha Muungano

(1)Bila ya kuathiri wajibu wa kila raia uliotajwa katika ibara ya 28 ya Katiba hii, viongozi wakuu wa vyombo vyenye mamlaka ya utendaji katika Jamhuri ya Muungano vilivyotajwa katika ibara ya 4 ya Katiba hii, watawajibika, kila mmoja wao katika kutekeleza madaraka aliyopewa kwa mujibu wa Katiba hii au Katiba ya Zanzibar, 1984, kuhakikisha kuwa analinda, kuimarisha na kudumisha umoja wa Jamhuri ya Muungano.
(2)Kwa madhumuni ya masharti ya ibara ndogo ya (1), kila mmojawapo wa viongozi wakuu wa vyombo vyenye mamlaka ya utendaji katika Jamhuri ya Muungano kabla ya kushika madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii ataapa kuitetea na kudumisha umoja wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Katiba hii.
(3)Viongozi wakuu wanaohusika na masharti ya ibara hii–
(a)Rais wa Jamhuri ya Muungano;
(b)Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano;
(c)Rais wa Zanzibar; na
(d)Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano.

Sehemu ya Pili – Makamu wa Rais (Ib 47—50)

47. Makamu mmoja wa Rais, kazi na mamlaka yake

(1)Kutakuwa na Makamu wa Rais ambaye ndiye msaidizi mkuu wa Rais kuhusu mambo ya Jamhuri ya Muungano kwa jumla, na hususan–
(a)atamsaidia Rais katika kufuatilia utekelezaji wa siku hata siku wa Mambo ya Muungano;
(b)atafanya kazi zote atakazoagizwa na Rais;
(c)atafanya kazi zote za Rais kama Rais hayupo kazini au yuko nje ya nchi.
(2)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ya 37(5), Makamu wa Rais atapatikana kwa kuchaguliwa katika uchaguzi ule ule kwa pamoja na Rais, baada ya kupendekezwa na chama chake wakati ule ule anapopendekezwa mgombea kiti cha Rais na watapigiwa kura kwa pamoja. Mgombea kiti cha Rais akichaguliwa basi na Makamu wa Rais atakuwa amechaguliwa.
(3)Mtu atateuliwa kugombea kiti cha Makamu wa Rais kwa kufuata kanuni kwamba endapo Rais wa Jamhuri ya Muungano atatoka sehemu moja ya Muungano, basi Makamu wa Rais atakuwa ni mtu anayetoka sehemu ya pili ya Muungano.
(4)Mtu hatateuliwa kugombea au kushika kiti cha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano isipokuwa tu kama–
(a)ni raia wa kuzaliwa wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa sheria ya Uraia;
(b)ametimiza umri wa miaka arobaini;
(c)ni mwanachama na mgombea aliyependekezwa na Chama cha Siasa;
(d)anazo sifa za kumwezesha kuwa Mbunge au Mjumbe wa Baraza la Wawakilishi;
(e)katika kipindi cha miaka mitano kabla ya tarehe uchaguzi hajawahi kutiwa hatiani katika Mahakama yoyote kwa kosa lolote la kukwepa kulipa kodi yoyote ya Serikali.
(5)Chama chochote hakitazuiwa kumpendekeza mtu yeyote kuwa mgombea kiti cha Makamu wa Rais kwa sababu tu kwamba mtu huyo kwa wakati huo ameshika kiti cha Rais wa Zanzibar au kiti cha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano.
(6)Makamu wa Rais hatakuwa kwa wakati huo huo Mbunge, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wala Rais wa Zanzibar.
(7)Endapo mtu ambaye ni Waziri Mkuu, au Rais wa Zanzibar atateuliwa au kuchaguliwa kuwa Makamu wa Rais ataacha kiti cha Waziri Mkuu, au cha Rais wa Zanzibar, kadri itakavyokuwa.
(8)Makamu wa Rais atatekeleza madaraka yake chini ya uongozi na usimamizi wa Rais, na ataongoza na kuwajibika kwa Rais kuhusu mambo au shughuli zozote atakazokabidhiwa na Rais.

48. Wakati wa Makamu wa Rais kushika madaraka

(1)Makamu wa Rais atashika madaraka ya Makamu wa Rais siku hiyo hiyo Rais anaposhika madaraka.
(2)Makamu wa Rais aliyeteuliwa kwa mujibu wa Ibara ya 50(3) ataapa na kushika madaraka yake baada ya uteuzi wake kuthibitishwa na Bunge.

49. Kiapo cha Makamu wa Rais

Makamu wa Rais, kabla ya kushika madaraka yake ataapishwa mbele ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, kiapo cha uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

50. Muda wa Makamu wa Rais kushika Madaraka

(1)Isipokuwa kama atajiuzulu atafariki mapema zaidi, mtu aliyechaguliwa, au kuteuliwa kwa mujibu wa ibara ya 37(5), kuwa Makamu wa Rais, bila ya kuathiri masharti mengine ya ibara hii, atashika kiti cha Makamu wa Rais kwa muda wa miaka mitano tangu alipochaguliwa kuwa Makamu wa Rais.
(2)Makamu wa Rais atashika kiti hicho hadi–
(a)muda wake utakapokwisha;
(b)akifariki dunia akiwa katika madaraka;
(c)atakapojiuzulu;
(d)atakapoapishwa kuwa Rais baada ya kiti cha Rais kuwa wazi;
(e)atakapotiwa hatiani kwa kosa la jinai linaloonyesha utovu wake wa uaminifu;
(f)atakapoapishwa Rais mwingine kushika nafasi ya Rais pamoja na Makamu wake;
(g)atakapoondolewa madarakani baada ya kushtakiwa Bungeni kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) ya Ibara hii;
(h)atakapoacha kushika kiti cha Makamu wa Rais vinginevyo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(3)Bunge litakuwa na madaraka ya kumuondoa Makamu wa Rais madarakani kama yale liliyonayo kuhusiana na Rais, isipokuwa kwamba hoja yoyote ya kumshtaki Makamu wa Rais itatolewa tu kama inadaiwa kwamba–
(a)Rais amewasilisha hati kwa Spika inayoeleza kwamba Makamu wa Rais ameacha au ameshindwa kutekeleza kazi za Makamu wa Rais;
(b)ametenda vitendo ambavyo kwa jumla vinaivunja Katiba au Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma;
(c)ametenda vitendo ambavyo vinakiuka maadili yanayohusu uandikishwaji wa vyama vya siasa yaliyotajwa katika ibara ya 20(2) ya Katiba;
(d)amekuwa na mwenendo unaodhalilisha kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano au kiti cha Makamu wa Rais, na haitatolewa hoja ya namna hiyo ndani ya miezi kumi na miwili tangu hoja hiyo ilipotolewa na ikakataliwa na Bunge.
(4)Ikitokea kwamba kiti cha Makamu wa Rais ki wazi kutokana na masharti yaliyomo katika ibara ndogo ya 50(3), kwa kutokana na kifo au kujiuzulu, basi mapema iwezekanavyo na kwa vyovyote ndani ya siku zisizozidi kumi na nne baada ya kiticha Makamu wa Rais kuwa wazi, Rais atamteua mtu atakayekuwa Makamu wa Rais kushika madaraka yake na uteuzi huo utathibitishwa na Bunge kwa kura za Wabunge walio wengi.
(5)Masharti mengine yote ya ibara ya 46A ya Katiba yatatumika pia kuhusiana na Makamu wa Rais isipokuwa tu kwamba Makamu wa Rais aliyeondolewa tena madarakani chini ya ibara ndogo ya (3) hatakuwa na sifa za kushika nafasi ya Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu wala Rais wa Zanzibar.

Sehemu ya Tatu – Waziri Mkuu, Baraza la Mawaziri na Serikali (Ib 51—61)

Waziri Mkuu (Ib 51—53A)

51. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano

(1)Kutakuwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano atakayeteuliwa na Rais kwa kufuata masharti ya ibara hii na ambaye kabla ya kushika madaraka yake, ataapa mbele ya Rais kwa kiapo kinachohusika na kiti cha Waziri Mkuu kitakachowekwa na Bunge.
(2)Mapema iwezekanavyo, na kwa vyovyote vile ndani ya siku kumi na nne, baada ya kushika madaraka yake, Rais atamteua Mbunge wa kuchaguliwa kutoka katika jimbo la uchaguzi anayetokana na chama cha siasa chenye Wabunge wengi zaidi Bungeni au, kama hakuna chama cha siasa chenye Wabunge wengi zaidi, anayeelekea kuungwa mkono na Wabunge walio wengi kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano, naye hatashika madaraka hayo mpaka kwanza uteuzi wake uwe umethibitishwa na Bunge kwa azimio litakaloungwa mkono na kura za Wabunge walio wengi.
(3)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, Waziri Mkuu atashika kiti cha Waziri Mkuu hadi–
(a)siku ambapo Rais mteule ataapa kushika kiti chake; au
(b)siku ambapo atafariki dunia akiwa katika madaraka; au
(c)siku atakapojiuzulu; au
(d)siku Rais atakapomteua Mbunge mwingine kuwa Waziri Mkuu; au
(e)atakapoacha kushika kiti cha Waziri Mkuu kwa mujibu wa masharti mengineyo ya Katiba hii.

52. Kazi na mamlaka ya Waziri Mkuu

(1)Waziri Mkuu atakuwa na madaraka juu ya udhibiti, usimamiaji, utekelezaji wa siku hata siku wa kazi na shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2)Waziri Mkuu atakuwa Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni.
(3)Katika utekelezaji wa madaraka yake, Waziri Mkuu atatekeleza au kusababisha utekelezaji wa jambo lolote au mambo yoyote ambayo Rais ataagiza kwamba yatekelezwe.

53. Uwajibikaji wa Serikali

(1)Bila ya kuathiri masharti ya Katiba hii, Waziri Mkuu atawajibika kwa Rais kuhusu utekelezaji wa madaraka yake.
(2)Serikali ya Jamhuri ya Muungano, chini ya mamlaka ya Rais, ndiyo itakuwa na uwezo wa kufanya maamuzi juu ya sera ya Serikali kwa jumla; na Mawaziri, chini ya uongozi wa Waziri Mkuu, watawajibika kwa pamoja Bungeni kuhusu utekelezaji wa shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

53A. Kura ya kutokuwa na imani

(1)Bila ya kujali masharti ya ibara ya 51 ya Katiba hii, Bunge linaweza kupitisha azimio la kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu endapo itatolewa hoja kupendekeza hivyo na ikapitishwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(2)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya ibara hii, hoja yoyote ya kutaka kupitisha kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu haitatolewa Bungeni endapo–
(a)haina uhusiano na utekelezaji wa majukumu ya Waziri Mkuu kwa mujibu wa ibara ya 52 ya Katiba hii, wala hakuna madai kwamba Waziri Mkuu amevunja sheria ya Maadili ya viongozi wa Umma;
(b)haijapita miezi sita tangu alipoteuliwa;
(c)haijapita miezi tisa tangu hoja ya namna hiyo ilipotolewa Bungeni na Bunge likakataa kuipitisha.
(3)Hoja ya kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu haitapitishwa na Bunge isipokuwa tu kama–
(a)taarifa ya maandishi, iliyotiwa sahihi na kuungwa mkono na Wabunge wasiopungua asilimia ishirini ya Wabunge wote itatolewa kwa Spika, siku angalau kumi na nne kabla ya siku inapokusudiwa kuwasilishwa Bungeni;
(b)Spika atajiridhisha kuwa masharti ya Katiba kwa ajili ya kuleta hoja yametimizwa.
(4)Hoja iliyotimiza masharti ya ibara hii itawasilishwa Bungeni mapema iwezekanavyo kwa mujibu wa Kanuni za Bunge.
(5)Hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu itapitishwa tu iwapo inaungwa mkono na Wabunge walio wengi.
(6)Endapo hoja ya kura ya kutokuwa na imani kwa Waziri Mkuu itaungwa mkono na Wabunge wengi, Spika atawasilisha azimio hilo kwa Rais, na mapema iwezekanavyo, na kwa vyovyote vile ndani ya siku mbili tangu Bunge lilipopitisha azimio la hoja ya kura ya kutokuwa na imani kwa Waziri Mkuu, Waziri Mkuu atatakiwa ajiuzulu, na Rais atamteua Mbunge mwingine kuwa Waziri Mkuu.

Baraza la Mawaziri na Serikali (Ib 54—61)

54. Baraza la Mawaziri

(1)Kutakuwa na Baraza la Mawaziri ambalo wajumbe wake watakuwa ni Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Rais wa Zanzibar na Mawaziri wote.
(2)Rais atahudhuria mikutano ya Baraza la Mawaziri na ndiye atakayeongoza mikutano hiyo. Na endapo Rais hayupo basi mikutano itaongozwa na Makamu wa Rais na kama wote wawili Rais na Makamu wa Rais hawapo, Waziri Mkuu ndiye ataongoza mikutano hiyo.
(3)Bila ya kuathiri masharti yaliyomo katika ibara ya 37(1) ya Katiba hii, Baraza la Mawaziri litakuwa ndicho chombo kikuu cha kumshauri Rais juu ya mambo yote yanayohusika na utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, na litamsaidia na kumshauri Rais juu ya jambo lolote litakalowasilishwa kwenye Baraza hilo kwa mujibu wa maagizo maalum au maagizo ya jumla yatakayotolewa na Rais.
(4)Mwanasheria Mkuu wa Serikali atahudhuria mikutano yote ya Baraza la Mawaziri na atakuwa na haki zote za mjumbe wa mikutano hiyo isipokuwa hatakuwa na haki ya kupiga kura katika mikutano hiyo.
(5)Suala kama ushauri wowote, na ni ushauri gani uliotolewa na Baraza la Mawaziri kwa Rais, halitachunguzwa katika mahakama yoyote.

55. Uteuzi wa Mawaziri

(1)Mawaziri wote ambao ni wajumbe wa Baraza la Mawaziri kwa mujibu wa ibara ya 58 watateuliwa na Rais baada ya kushauriana na Waziri Mkuu.
(2)Pamoja na Mawaziri waliotajwa katika ibara ndogo ya (1), Rais aweza, baada ya kushauriana na Waziri Mkuu, kuwateua Naibu Mawaziri. Naibu Mawaziri wote hawatakuwa wajumbe wa Baraza la Mawaziri.
(3)Rais aweza kuteua idadi yoyote ya Naibu Mawaziri ambao watawasaidia Mawaziri katika utekelezaji wa kazi na shughuli zao.
(4)Mawaziri na Naibu Mawaziri wote watateuliwa kutoka miongoni mwa Wabunge.
(5)Bila ya kujali masharti ya ibara ndogo ya (1) ikitokea kwamba Rais anahitajiwa kumteua Waziri au Naibu Waziri baada ya Bunge kuvunjwa, basi aweza kumteua mtu yeyote ambaye alikuwa Mbunge kabla ya Bunge kuvunjwa.

56. Kiapo cha Mawaziri na Naibu Mawaziri

Waziri au Naibu Waziri hatashika madaraka yake ila mpaka awe ameapa kwanza mbele ya Rais kiapo cha uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

57. Wakati wa muda wa Mawaziri kushika madaraka

(1)Muda wa kushika madaraka ya Waziri na Naibu Waziri utaanza tarehe atakapoteuliwa kushika madaraka hayo.
(2)Kiti cha Waziri au Naibu Waziri kitakuwa wazi litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)endapo mwenye madaraka atajiuzulu au kufariki dunia;
(b)ikiwa mwenye madaraka hayo atakoma kuwa Mbunge kwa sababu yoyote isiyohusika na kuvunjwa kwa Bunge;
(c)ikiwa Rais atafuta uteuzi na kumwondoa kazini mwenye madaraka hayo;
(d)iwapo atachaguliwa kuwa Spika;
(e)iwapo Waziri Mkuu atajiuzulu au kiti chake kikiwa wazi kwa sababu nyingine yoyote;
(f)ukiwadia wakati wa Rais mteule kushika madaraka ya Rais basi mara tu kabla Rais mteule hajashika madaraka hayo;
(g)iwapo Baraza la Maadili linatoa uamuzi unaothibitisha kwamba amevunja sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

58. Masharti ya kazi ya Mawaziri

Mawaziri na Naibu Mawaziri watashika madaraka yao kwa ridhaa ya Rais, na watalipwa mshahara, posho na malipo mengineyo kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

59. Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano

(1)Kutakuwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano ambaye katika ibara zifuatazo za Katiba hii atatajwa tu kwa kifupi kama "Mwanasheria Mkuu" ambaye atateuliwa na Rais.
(2)Mtu yeyote hatastahili kuteuliwa kushika au kutekeleza madaraka ya Mwanasheria Mkuu isipokuwa tu kama kwa mujibu wa Katiba hii ana sifa maalum, kama ilivyofafanuliwa katika ibara ya 109(8) zinazomwezesha kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar, na amekuwa na mojawapo ya hizo sifa maalum kwa muda usiopungua miaka mitano.
(3)Mwanasheria Mkuu atakuwa ndiye mshauri mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano juu ya mambo ya sheria na, kwa ajili hiyo, atawajibika kutoa ushauri kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhusu mambo yote ya kisheria, na kutekeleza shughuli nyinginezo zozote zenye asili ya au kuhusiana na sheria zitakazopelekwa kwake au atakazoagizwa na Rais kuzitekeleza, na pia kutekeleza kazi au shughuli nyinginezo zilizokabidhiwa kwake na Katiba hii au na sheria yoyote.
(4)Katika kutekeleza kazi na shughuli zake kwa mujibu wa ibara hii, Mwanasheria Mkuu atakuwa na haki ya kuhudhuria na kusikilizwa katika mahakama zote katika Jamhuri ya Muungano.
(5)Mwanasheria Mkuu atakuwa Mbunge kutokana na wadhifa wake, na atashika madaraka yake mpaka–
(a)uteuzi wake utakapofutwa na Rais; au
(b)mara tu kabla ya Rais mteule kushika madaraka ya Rais,
na atalipwa mshahara, posho na malipo mengine kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

60. Katibu wa Baraza la Mawaziri

Kutakuwa na Katibu wa Baraza la Mawaziri ambaye atakuwa ndiye mtendaji mkuu katika Ofisi ya Baraza la Mawaziri, na atatekeleza shughuli zifuatazo kwa kufuata maagizo ya jumla au maalum atakayopewa na Rais, yaani–
(a)kuanda ratiba ya mikutano ya Baraza na kutayarisha orodha ya shughuli za kila mkutano;
(b)kuandika na kuweka kumbukumbu za mikutano ya Baraza;
(c)kutoa taarifa na maelezo ya maamuzi ya Baraza kwa kila mtu au chombo cha umma kinachohusika na uamuzi wowote; na
(d)kutekeleza kazi na shughuli nyingine zozote atakazoagizwa mara kwa mara na Rais.

61. Wakuu wa Mikoa

(1)Kutakuwa na Mkuu wa Mkoa kwa kila Mkoa katika Jamhuri ya Muungano ambaye, bila ya kuathiri ibara ndogo ya (3), atakuwa ni kiongozi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2)Wakuu wa Mikoa katika Tanzania Bara watateuliwa na Rais baada ya kushauriana na Waziri Mkuu.
(3)Wakuu wa Mikoa katika Tanzania Zanzibar watateuliwa na Rais wa Zanzibar baada ya kushauriana na Rais.
(4)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (5), kila Mkuu wa Mkoa, atakuwa na wajibu wa kusimamia utekelezaji wa kazi na shughuli zote za Serikali ya Jamhuri ya Muungano katika Mkoa aliokabidhiwa; na kwa ajili hiyo, atatekeleza kazi na shughuli zote zilizotajwa na sheria, au kwa mujibu wa sheria kama ni kazi au shughuli za Mkuu wa Mkoa na atakuwa na madaraka yote yatakayotajwa na Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge.
(5)Pamoja na wajibu na madaraka yake yaliyotajwa kwenye masharti yaliyotangulia ya ibara hii, Mkuu wa Mkoa kwa Mkoa wowote katika Tanzania Zanzibar atatekeleza kazi na shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar atakazokabidhiwa na Rais wa Zanzibar, na kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar 1984 au sheria yoyote iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi.

Sura ya Tatu
Bunge la Jamhuri ya Muungano (Ib. 62—101)

Sehemu ya Kwanza – Bunge (Ib. 62—65)

62. Bunge

(1)Kutakuwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano ambalo litakuwa na sehemu mbili, yaani Rais na Wabunge.
(2)Bunge litakuwa na Wajumbe wa aina zote zilizotajwa katika ibara ya 66 ya Katiba hii ambao wote wataitwa Wabunge.
(3)Iwapo jambo lolote lahitaji kuamuliwa au kutekelezwa na sehemu zote mbili za Bunge kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au masharti ya sheria nyingine yoyote, basi jambo hilo halitahesabiwa kuwa limeamuliwa au limetekelezwa ipasavyo ila mpaka liwe limeamuliwa au limetekelezwa na Wabunge na vile vile na Rais, kwa mujibu wa madaraka yao kuhusu jambo hilo.

63. Madaraka ya Bunge

(1)Rais kama sehemu moja ya Bunge atatekeleza madaraka yote aliyokabidhiwa na Katiba hii kwa ajili hiyo.
(2)Sehemu ya pili ya Bunge itakuwa ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii.
(3)Kwa madhumuni ya utekelezaji wa madaraka yake Bunge laweza–
(a)kumuuliza Waziri yeyote swali lolote kuhusu mambo ya umma katika Jamhuri ya Muungano ambayo yako katika wajibu wake;
(b)kujadili utekelezaji wa kila Wizara wakati wa Mkutano wa Bunge wa kila mwaka wa bajeti;
(c)kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu au wa muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano, na kutunga sheria ya kusimamia utekelezaji wa mpango huo;
(d)kutunga sheria pale ambapo utekelezaji unahitaji kuwapo sheria;
(e)kujadili na kuridhia mikataba yote inayohusu Jamhuri ya Muungano na ambayo kwa masharti yake inahitaji kuridhiwa.

64. Madaraka ya kutunga Sheria

(1)Mamlaka yote ya kutunga sheria juu ya mambo yote ya Muungano katika Jamhuri ya Muungano, na pia juu ya mambo mengine yote yahusuyo Tanzania Bara, yatakuwa mikononi mwa Bunge.
(2)Mamlaka yote ya kutunga Sheria katika Tanzania Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo Mambo ya Muungano yatakuwa mikononi mwa Baraza la Wawakilishi.
(3)Endapo sheria yoyote iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi inahusu jambo lolote katika Tanzania Zanzibar ambalo liko chini ya mamlaka ya Bunge, sheria hiyo itakuwa batili na itatanguka na pia endapo sheria yoyote iliyotungwa na Bunge inahusu jambo lolote ambalo liko chini ya mamlaka ya Baraza la Wawakilishi, sheria hiyo itakuwa batili na itatanguka.
(4)Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kuhusu jambo lolote haitatumika Tanzania Zanzibar ila kwa mujibu wa masharti yafuatayo–
(a)Sheria hiyo iwe imetamka wazi kwamba itatumika Tanzania Bara na vile vile Tanzania Zanzibar au iwe inabadilisha, kurekebisha au kufuta sheria inayotumika Tanzania Zanzibar; au
(b)Sheria hiyo iwe inabadilisha au kurekebisha au kufuta sheria iliyokuwa inatumika tangu zamani Tanzania Bara ambayo ilikuwa inatumika pia Tanzania Zanzibar kwa mujibu wa Mapatano ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ya mwaka 1964, au kwa mujibu wa sheria yoyote ambayo ilitamka wazi kwamba itatumika Tanzania Bara na vile vile Tanzania Zanzibar; au
(c)Sheria hiyo iwe inahusu Mambo ya Muungano, na kila inapotajwa Tanzania katika sheria yoyote ifahamike kuwa sheria hiyo itatumika katika Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa ufafanuzi uliotolewa na masharti ya ibara hii.
(5)Bila ya kuathiri kutumika kwa Katiba ya Zanzibar kwa mujibu wa Katiba hii kuhusu mambo yote ya Tanzania Zanzibar yasiyo Mambo ya Muungano, Katiba hii itakuwa na nguvu ya sheria katika Jamhuri nzima ya Muungano na endapo sheria nyingine yoyote itakiuka masharti yaliyomo katika Katiba hii, Katiba ndiyo itakuwa na nguvu, na sheria hiyo nyingine, kwa kiasi inachokiuka Katiba, itakuwa batili.

65. Muda wa Bunge

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, maisha ya kila Bunge yatakuwa ni muda wa miaka mitano.
(2)Kwa madhumuni ya Katiba hii maneno "maisha ya Bunge" maana yake ni ule muda wote unaoanzia tarehe ambapo Bunge jipya limeitishwa kukutana kwa mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu na kuishia tarehe ya kuvunjwa kwa Bunge kwa ajili ya kuwezesha Uchaguzi Mkuu mwingine wa kawaida kufanyika.

Sehemu ya Pili – Wabunge, wilaya za uchaguzi na uchaguzi wa wabunge (Ib 66—83)

Wajumbe wa Bunge (Ib 66—73)

66. Wabunge

(1)Bila ya kuathiri masharti mengine ya ibara hii, kutakuwa na aina zifuatazo za Wabunge, yaani–
(a)Wabunge waliochaguliwa kuwakilisha majimbo ya uchaguzi;
(b)Wabunge wanawake wa idadi inayoongezeka, kuanzia asilimia ishirini ya Wabunge waliotajwa katika aya ya (a), (c) na (d), itakayotajwa mara kwa mara na Tume ya Uchaguzi kwa taarifa itakayochapishwa katika Gazeti la Serikali baada ya kupata kibali cha Rais, watakaochaguliwa na vyama vya siasa vinavyowakilishwa Bungeni, kwa mujibu wa ibara ya 78, na kwa kuzingatia masharti ya uwiano wa uwakilishi baina ya vyama hivyo;
(c)Wabunge watano waliochaguliwa na Baraza la Wawakilishi kutoka miongoni mwa wajumbe wake;
(d)Mwanasheria Mkuu;
(e)Wabunge wasiozidi kumi walioteuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye sifa kwa mujibu wa ibara ya 67, isipokuwa sifa iliyotajwa katika ibara ya 67(1)(b).
(2)Rais, Makamu wa Rais na Rais wa Zanzibar, kila mmojawao hatakuwa Mbunge.
(3)Endapo Mkuu wa Mkoa atachaguliwa kuwa Mbunge anayewakilisha wilaya ya uchaguzi au endapo Mbunge anayewakilisha wilaya ya uchaguzi atateuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa, Bunge litahesabiwa kuwa lina idadi ya Wabunge inayohitajika na shughuli zake zitakuwa halali ingawaje idadi ya jumla ya kawaida ya Wabunge kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, itakuwa imepungua kutokana na uchaguzi huo wa Mkuu wa Mkoa au uteuzi huo wa Mbunge anayewakilisha wilaya ya uchaguzi.

67. Sifa za mtu kuwa Mbunge

(1)Bila ya kuathiri masharti yaliyomo katika ibara hii, mtu yeyote atakuwa na sifa za kustahili kuchaguliwa au kuteuliwa kuwa Mbunge endapo–
(a)ni raia wa Jamhuri ya Muungano aliyetimiza umri wa miaka ishirini na moja, na ambaye anajua kusoma na kuandika katika Kiswahili au Kiingereza;
(b)ni mwanachama na ni mgombea aliyependekezwa na chama cha siasa;
(c)katika kipindi cha miaka mitano kabla ya tarehe ya uchaguzi hakuwahi kutiwa hatiani katika Mahakama yoyote kwa kosa la kukwepa kulipa kodi yoyote ya Serikali.
(2)Mtu hatakuwa na sifa za kustahili kuchaguliwa au kuteuliwa kuwa Mbunge–
(a)ikiwa mtu huyo anao au kwa hiari yake amejipatia uraia wa nchi nyingine yoyote; au
(b)ikiwa kwa mujibu wa Sheria inayotumika katika Jamhuri ya Muungano imethibitishwa rasmi kwamba mtu huyo ana ugonjwa wa akili; au
(c)ikiwa mtu huyo amehukumiwa na Mahakama yoyote katika Jamhuri ya Muungano na kupewa adhabu ya kifo au ya kufungwa gerezani kwa muda unaozidi miezi sita kwa kukutwa na hatia ya kosa lolote, vyovyote linavyoitwa, linaloambatana na utovu wa uaminifu; au
(d)ikiwa katika kipindi cha miaka mitano kabla ya tarehe ya Uchaguzi Mkuu amepata kuhukumiwa na kupewa adhabu ya kifungo kwa kosa linaloambatana na utovu wa uaminifu au kwa kuvunja Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma;
(e)bila ya kuingilia haki na uhuru wa mtu kuwa na maoni yake, kuamini dini atakayo, kushirikiana na wengine na kushiriki shughuli za umma kwa mujibu wa sheria za nchi, ikiwa mtu huyo si mwanachama na mgombea aliyependekezwa na chama cha siasa;
(f)ikiwa mtu huyo ana masilahi yoyote katika mkataba wa Serikali wa aina yoyote aliyowekewa miiko maalum kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge, na iwapo amekiuka miiko hiyo;
(g)ikiwa mtu huyo ameshika madaraka ya afisa mwandamizi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano isipokuwa madaraka ambayo Rais aweza au anatakiwa kukabidhi kwa Mbunge kwa mujibu wa Katiba hii au sheria iliyotungwa na Bunge;
(h)ikiwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge inayoshughulikia makosa yanayohusika na uchaguzi wa aina yoyote mtu huyo amezuiliwa kujiandikisha kama mpiga kura au kupiga kura katika uchaguzi wa Wabunge.
(3)Mtu hataweza kugombea uchaguzi kuwa Mbunge wa kuwakilisha jimbo la uchaguzi katika Uchaguzi Mkuu wowote ikiwa wakati huo yeye amesimama katika uchaguzi kugombea kiti cha Rais, wala hataweza kugombea uchaguzi kuwa Mbunge katika uchaguzi mdogo wowote ikiwa yeye ni Rais.
(4)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti yatakayomzuia mtu asichaguliwe kuwa Mbunge wa kuwakilisha jimbo la uchaguzi ikiwa mtu huyo ni mwenye madaraka yanayohusika na shughuli za kuongoza au kusimamia uchaguzi wa Wabunge au shughuli za uandikishaji wa wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi wa Wabunge; isipokuwa kwamba sheria kama hiyo haiwezi kuweka masharti yatakayomzuia Spika wa Bunge asichaguliwe kuwa Mbunge wa kuwakilisha wilaya ya uchaguzi, wala masharti yatakayosababisha mtu aliyechaguliwa kuwa Spika kupoteza kiti cha Spika au kiti chake cha kawaida katika Bunge.
(5)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti yatakayomzuia mtu asichaguliwe kuwa Mbunge wa kuwakilisha wilaya ya uchaguzi kwa muda wowote utakaotajwa na Bunge (ilimradi muda huo usizidi miaka mitano) ikiwa mtu huyo atapatikana na hatia mbele ya mahakama kwa ajili ya aina yoyote ya makosa yatakayotajwa katika Sheria hiyo yanayohusika na uchaguzi wa Wabunge.
(6)Kwa madhumuni ya kutoa fursa ya kukata rufaa kwa mujibu wa Sheria kwa mtu yeyote aliyethibitishwa rasmi kisheria kuwa ana ugonjwa wa akili au aliyehukumiwa na kupewa adhabu ya kifo au ya kufungwa gerezani au aliyepatikana na hatia ya kosa lolote lililotajwa katika Sheria kwa mujibu wa ibara ndogo ya (5) ya ibara hii, Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti yatakayoeleza kwamba hiyo hukumu inayopingwa na mtu huyo haitakuwa na nguvu kwa ajili ya utekelezaji wa masharti ya ibara ndogo ya (2) au ya (5) ya ibara hii mpaka upite kwanza muda utakaotajwa katika sheria hiyo.
(7)Kanuni zifuatazo zitatumika kwa ajili ya ufafanuzi wa aya ya (c), ya (d) na ya (e) za ibara ndogo ya (2) ya ibara hii, yaani–
(a)ikiwa mtu amepewa adhabu mbili au zaidi za kufungwa gerezani na ameamriwa afungwe kwa muda wa mfululizo, basi adhabu hizo zitahesabiwa kama ni adhabu mbali mbali iwapo muda uliotajwa katika kila moja ya adhabu hizo hauzidi miezi sita; lakini iwapo muda uliotajwa katika adhabu yoyote kati ya adhabu hizo unazidi miezi sita basi adhabu hizo zote zitahesabiwa kama ni adhabu moja;
(b)ikiwa mtu atapewa adhabu ya kufungwa gerezani ikifahamika kuwa adhabu hiyo ya kifungo imetolewa badala ya adhabu ya kutozwa faini au imetolewa kwa sababu mtu huyo ameshindwa kulipa faini aliyoamriwa kulipa, basi muda wa kifungo cha namna hiyo hautahesabiwa.
(8)Katika aya ya (f) ya ibara ndogo ya (2) ya ibara hii "mkataba wa Serikali" maana yake ni mapatano yoyote ya mkataba ambayo mmojawapo wa walioshiriki ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar au Idara yoyote ya Serikali au mtumishi yeyote wa Umma aliyeshiriki kwa niaba ya Serikali.
(9)[Ibara ndogo ya (9) imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ib. 19(d)]
(10)[Ibara ndogo ya (10) imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ib. 19(d)]
(11)[Ibara ndogo ya (11) imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ib. 19(d)]
(12)[Ibara ndogo ya (12) imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ib. 19(d)]
(13)Kwa ajili ya ufafanuzi wa maelezo kuhusu sifa za uchaguzi yaliyomo katika ibara zifuatazo, kila itakapotajwa katika Katiba hii kwamba utekelezaji wa jambo lolote wahitaji mtu mwenye sifa au uchaguzi au mtu ambaye hakupoteza sifa za uchaguzi, basi, isipokuwa kama maelezo yahitajia vinginevyo, ifahamike kuwa sifa zinazohusika ni zile zinazomwezesha mtu kuchaguliwa kuwa Mbunge wa kuwakilisha jimbo la uchaguzi kama ilivyoelezwa katika ibara ndogo ya (1) ya ibara hii.

68. Kiapo cha Wabunge

Kila Mbunge atatakiwa kuapishwa katika Bunge kiapo cha uaminifu kabla hajaanza kushiriki katika shughuli za Bunge; lakini Mbunge aweza kushiriki katika uchaguzi wa Spika hata kabla hajaapishwa.

69. Tamko rasmi la Wabunge kuhusu maadili ya Viongozi

(1)Kila Mbunge atatakiwa, kabla ya kumalizika siku thelathini tangu aapishwe kushika madaraka yake kama Mbunge kuwasilisha kwa Spika nakala mbili za tamko rasmi kwamba hajapoteza sifa za uchaguzi kwa mujibu wa masharti ya aya ya (d) ya ibara ndogo ya (2) ya ibara ya 67.
(2)Tamko rasmi linalotakiwa kuwasilishwa kwa Spika kwa mujibu wa masharti ya ibara hii litatolewa kwa kutumia fomu maalum itakayowekwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge.
(3)Spika atawasilisha kwa Kamishna wa Maadili nakala moja ya kila tamko rasmi lililowasilishwa kwake kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(4)Katika ibara hii na katika ibara ya 70 na ya 84 "Kamishna wa Maadili" maana yake ni Kamishna aliyeteuliwa kuwa kiongozi wa Sekretarieti ya Maadili iliyotajwa katika ibara ya 132 ya Katiba hii.

70. Wabunge kutoa taarifa ya mali

(1)Kila Mbunge atatakiwa kuwasilisha kwa Spika nakala mbili za taarifa rasmi ya maelezo ya mali yake na kadri itakavyokuwa, mali ya mke au mume wake. Taarifa itatolewa kwa kutumia fomu maalum itakayowekwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge na itatolewa mara kwa mara kama itakavyoagizwa na Sheria hiyo.
(2)Spika atawasilisha kwa Kamishna wa Maadili nakala moja ya kila taarifa rasmi iliyowasilishwa kwake kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(3)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti kwa makusudi ya kusimamia hifadhi ya taarifa ya mali iliyowasilishwa na Mbunge kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, na kuhakikisha kwamba watu wasioruhusiwa au wasiohusika hawapati nafasi ya kuona taarifa ya mali wala kujua yaliyomo katika taarifa ya mali.

71. Muda wa Wabunge kushika madaraka kama Wabunge

(1)Mbunge atakoma kuwa Mbunge na ataacha kiti chake katika Bunge litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)ikiwa litatokea jambo lolote ambalo, kama asingekuwa Mbunge lingemfanya asiwe na sifa za uchaguzi au apoteze sifa za uchaguzi au asiweze kuchaguliwa au kuteuliwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii;
(b)ikiwa Mbunge huyo atachaguliwa kuwa Rais;
(c)ikiwa Mbunge atakosa kuhudhuria vikao vya Mikutano ya Bunge mitatu mfululizo bila ya ruhusa ya Spika;
(d)ikiwa itathibitishwa kwamba amevunja masharti ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma;
(e)ikiwa Mbunge ataacha kuwa mwanachama wa chama alichokuwamo wakati alipochaguliwa au alipoteuliwa kuwa Mbunge;
(f)iwapo Mbunge anachaguliwa au anateuliwa kuwa Makamu wa Rais;
(g)kwa Mbunge ambaye anatakiwa kutoa taarifa rasmi ya mali kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 70, ikiwa atashindwa kutoa hilo tamko rasmi kwa mujibu wa masharti ya hiyo ibara ya 70 katika muda uliowekwa mahususi kwa ajili hiyo kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge, lakini iwapo Mbunge hatakoma kuwa Mbunge kwa mujibu wa jambo lolote kati ya mambo hayo yaliyotajwa na kama hatajiuzulu au kufariki mapema zaidi, basi Mbunge ataendelea kushika madaraka yake kama Mbunge mpaka wakati Bunge litakapovunjwa kwa mujibu wa ibara ya 90, bila ya kuathiri haki na stahili zinazotokana na ubunge wake.
(2)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti yatakayomwezesha Mbunge kukata rufaa, kwa mujibu wa Sheria kupinga hukumu ya kuthibitishwa kwake kuwa ni mtu mwenye ugonjwa wa akili au kupinga kukumu ya kifo au ya kufungwa gerezani, au kupinga kupatikana kwake na hatia kwa kosa la aina iliyotajwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (5) ya ibara ya 67 ya Katiba hii; na Sheria hiyo yaweza kueleza kwamba hiyo hukumu iliyopingwa na huyo Mbunge haitatiliwa nguvu kisheria mpaka umalizike kwanza muda utakaotajwa katika Sheria hiyo.

72. Watu wenye madaraka Serikalini kukoma utumishi wanapochaguliwa

Iwapo mtu yeyote mwenye madaraka katika utumishi wa Umma, madaraka ya aina iliyotajwa katika ibara ya 67(2)(g) ataamua–
(a)kuwa mgombea uchaguzi wa Rais au wa nafasi nyingine yoyote chini ya Katiba hii, au
(b)kugombea uongozi wa ngazi yoyote katika chama cha siasa kinyume na masharti ya ajira,
mtu huyo atahesabiwa kuwa utumishi wake umekoma tangu tarehe yake ya kuwa mgombea uchaguzi au ya kugombea uongozi katika chama cha siasa.

73. Masharti ya kazi ya Wabunge

Wabunge wote wa aina zote watashika madaraka yao kwa mujibu wa Katiba hii, na watalipwa mshahara, posho na malipo mengine kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

Tume ya Uchaguzi (Ib. 74)

74. Tume ya Uchaguzi

(1)Kutakuwa na Tume ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano ambayo itakuwa na wajumbe wafuatao watakaoteuliwa na Rais–
(a)Jaji wa Mahakama Kuu au Jaji wa Mahakama ya Rufani, ambaye atakuwa mwenyekiti;
(b)Makamu Mwenyekiti ambaye atakuwa ni mtu anayeshika, aliyewahi kushika au anayestahili kuteuliwa kushika madaraka ya Jaji wa Mahakama Kuu au Jaji wa Mahakama ya Rufani;
(c)Wajumbe wengine watakaotajwa na sheria iliyotungwa na Bunge.
(2)Rais atamteua Makamu wa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi kwa kufuata kanuni kwamba endapo Mwenyekiti ni mtu anayetoka sehemu moja ya Muungano, Makamu wake atakuwa ni mtu anayetoka sehemu ya pili ya Muungano.
(3)Watu wafuatao hawataweza kuteuliwa kuwa wajumbe wa Tume ya Uchaguzi yaani–
(a)Waziri au Naibu Waziri;
(b)mtu mwenye madaraka ya aina yoyote iliyotajwa mahususi na sheria iliyotungwa na Bunge kwamba ni mwiko kwa mtu mwenye madaraka hayo kuwa mjumbe wa Tume ya Uchaguzi;
(c)Mbunge, Diwani au mtu mwingine mwenye madaraka ya aina yaliyotajwa na sheria iliyotungwa na Bunge kwa mujibu wa masharti ya aya ya (g) ya ibara ndogo ya (2) ya ibara ya 67 ya Katiba hii;
(d)Kiongozi wa chama chochote cha siasa.
(4)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya ibara hii, Mjumbe wa Tume ya Uchaguzi atakoma kuwa Mjumbe litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)ukimalizika muda wa miaka mitano tangu alipoteuliwa; au
(b)ikiwa litatokea jambo lolote ambalo, kama asingekuwa Mjumbe wa Tume, lingemfanya asiweze kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Tume ya Uchaguzi.
(5)Rais aweza tu kumwondoa katika madaraka Mjumbe wa Tume ya Uchaguzi kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi zake, ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote, au kwa sababu ya tabia mbaya au kupoteza sifa za kuwa mjumbe.
(6)Majukumu ya Tume ya Uchaguzi yatakuwa ni–
(a)kusimamia na kuratibu uandikishaji wa wapiga kura katika uchaguzi wa Rais na Wabunge katika Jamhuri ya Muungano;
(b)kusimamia na kuratibu uendeshaji wa uchaguzi wa Rais na Wabunge;
(c)kuchunguza mipaka na kuigawa Jamhuri ya Muungano katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya uchaguzi wa Wabunge;
(d)kusimamia na kuratibu uandikishaji wa wapiga kura na uendeshaji wa uchaguzi wa madiwani; na
(e)kutekeleza majukumu mengine yoyote kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.
(7)Kwa madhumuni ya utekelezaji bora wa majukumu yake yaliyoainishwa katika ibara hii, Tume ya Uchaguzi itakuwa ni idara huru inayojitegemea, itafanya maamuzi yake rasmi kuhusu utekelezaji wa majukumu yake kwa vikao, na mtendaji mkuu wake atakuwa ni Mkurugenzi wa Uchaguzi ambaye atateuliwa na kufanya kazi kwa mujibu wa masharti ya sheria iliyotungwa na Bunge.
(8)Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti ya kuweka utaratibu wa kusimamia uchaguzi wa Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi.
(9)Tume ya Uchaguzi yaweza kutekeleza shughuli zake bila ya kujali kwamba kuna nafasi miongoni mwa viti vya wajumbe au kwamba mjumbe mmojawapo hayupo, lakini kila uamuzi wa Tume ya Uchaguzi ni lazima uungwe mkono na wajumbe walio wengi kati ya wajumbe wote wa Tume ya Uchaguzi.
(10)Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti ya kuweka utaratibu wa kuwateua Wajumbe wa kusimamia uchaguzi wa Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi na, bila ya kuathiri masharti ya Sheria kama hiyo au maagizo ya Tume ya Uchaguzi, madaraka ya Tume ya Uchaguzi ya kusimamia uchaguzi yaweza kutekelezwa na wajumbe hao.
(11)Katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, Tume ya Uchaguzi haitalazimika kufuata amri au maagizo ya mtu yeyote au idara yoyote ya Serikali, au maoni ya chama chochote cha siasa.
(12)Hakuna mahakama yoyote itakayokuwa na mamlaka ya kuchunguza jambo lolote lililotendwa na Tume ya Uchaguzi katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(13)Katika utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii, Tume ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Muungano itashauriana mara kwa mara na Tume ya Uchaguzi ya Tanzania Zanzibar.
(14)Itakuwa ni marufuku kwa watu wanaohusika na uchaguzi kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba kila mmoja wao atakuwa na haki ya kupiga kura iliyotajwa katika ibara ya 5 ya Katiba hii.
(15)Kwa madhumuni ya ibara ndogo ya (14) watu wanaohusika na uchaguzi ni–
(a)Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi;
(b)Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi;
(c)Wajumbe wote wa Tume ya Uchaguzi;
(d)Mkurugenzi wa Uchaguzi pamoja na watumishi wote wa Tume ya Uchaguzi;
(e)Wasimamizi wote wa Uchaguzi katika miji na wilaya zote.

Majimbo ya Uchaguzi (Ib 75)

75. Majimbo ya uchaguzi

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo yaliyo katika ibara hii, Jamhuri ya Muungano itagawanywa katika majimbo ya uchaguzi kwa idadi na kwa namna itakavyoamuliwa na Tume ya Uchaguzi baada ya kupata kibali cha Rais.
(2)Bila ya kuathiri sheria yoyote inayotumika kuhusu mambo hayo, Tume ya Uchaguzi, baada ya kupata kibali cha Rais itakuwa na mamlaka ya kuweka mipaka ya majimbo ya uchaguzi.
(3)Katika kuweka mipaka ya majimbo ya uchaguzi, Tume ya Uchaguzi itazingatia ipasavyo upatikanaji wa njia za mawasiliano, na pia hali ya kijiografia ya eneo linalokusudiwa kugawanywa katika majimbo ya uchaguzi.
(4)Bila ya kuathiri masharti ya Katiba hii na ya Sheria yoyote inayohusika na mgawanyo wa nchi katika majimbo ya uchaguzi, Tume ya Uchaguzi yaweza mara kwa mara, na angalao kila baada ya miaka kumi, kuchunguza mgawanyo wa Jamhuri ya Muungano katika majimbo ya uchaguzi, na yaweza kubadilisha majimbo ya uchaguzi kama matokeo ya uchunguzi huo au kutokana na matokeo ya hesabu ya watu wote katika Jamhuri ya Muungano.
(5)Endapo baada ya uchunguzi kufanywa kuhusu mgawanyo wa Jamhuri ya Muungano katika majimbo ya uchaguzi kunafanyika mabadiliko katika majimbo ya uchaguzi, au katika idadi ya Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi au mabadiliko kwa idadi ya majimbo ya uchaguzi au idadi ya Wabunge, basi mabadiliko yatakayotokea katika idadi ya Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi yataanza kutumika wakati Bunge litakapovunjwa tena baada ya kutokea mabadiliko hayo ya idadi ya majimbo au idadi ya Wabunge katika majimbo ya uchaguzi.
(6)Bila ya kujali masharti mengineyo ya ibara hii, hakuna mahakama yoyote itakayokuwa na mamlaka ya kuchunguza jambo lolote lililotendwa na Tume katika utekelezaji wake wa kugawa Jamhuri ya Muungano katika majimbo ya uchaguzi.

Uchaguzi na uteuzi wa Wabunge (Ib 76—83)

76. Uchaguzi katika Majimbo ya Uchaguzi

(1)Kila mara baada ya Bunge kuvunjwa, kutakuwa na uchaguzi wa Wabunge katika majimbo yote ya uchaguzi.
(2)Hali kadhalika, kutakuwa na uchaguzi wa Mbunge katika jimbo la uchaguzi, ikiwa kiti cha Mbunge yeyote aliyechaguliwa kuwakilisha jimbo hilo kitakuwa wazi kwa sababu nyingine yoyote isiyohusika na kuvunjwa kwa Bunge.
(3)Bila ya kujali masharti ya ibara hii yaliyotangulia, ifahamike kwamba ikiwa tarehe ya kuvunjwa Bunge imetangazwa au inafahamika kutokana na matukio yaliyoelezwa katika ibara ndogo ya (3) ya ibara ya 90, basi uchaguzi wa namna hiyo hautafanywa katika kipindi chote cha miezi kumi na miwili ya nyuma ikihesabiwa tangu tarehe hiyo.

77. Utaratibu wa Uchaguzi wa Wabunge wa Majimbo ya Uchaguzi

(1)Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi watachaguliwa na wananchi kwa kufuata masharti ya Katiba hii na vile vile masharti ya Sheria iliyotungwa na Bunge kwa mujibu wa Katiba hii inayoweka masharti kuhusu uchaguzi wa Wabunge wanaowakilisha majimbo ya uchaguzi.
(2)Isipokuwa pale ambapo Tume ya Uchaguzi, kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au Sheria iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo, itaagiza vinginevyo, kutachaguliwa Mbunge mmoja tu katika jimbo la uchaguzi.
(3)Wagombea uchaguzi katika jimbo la uchaguzi watatakiwa watimize masharti yafuatayo–
(a)wawe wamependekezwa mmoja mmoja, na chama cha siasa kinachoshiriki uchaguzi katika jimbo hilo;
(b)wamewasilisha majina yao kwa Tume ya Uchaguzi kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa na Sheria iliyotungwa na Bunge au uliofafanuliwa na Tume ya Uchaguzi kwa mujibu wa sheria.

78. Utaratibu wa Uchaguzi wa Wabunge Wanawake wa kuchaguliwa na Bunge

(1)Kwa madhumuni ya uchaguzi wa Wabunge Wanawake waliotajwa katika ibara ya 66 (1) (b), vyama vya siasa vilivyoshiriki uchaguzi, kwa kufuata utaratibu uliowekwa, vitapendekeza kwa Tume ya Uchaguzi majina ya wanawake kwa kuzingatia masharti ya uwiano wa uwakilishi baina ya vyama vilivyoshinda uchaguzi katika majimbo na kupata viti Bungeni. Tume ya Uchaguzi ikiridhika kuwa mtu yeyote aliyependekezwa anazo sifa za kuwa Mbunge itamtangaza kuwa amechaguliwa kuwa Mbunge, na masharti ya ibara ya 67 ya Katiba hii yatatumika kuhusu kuchaguliwa kwa mtu huyo kuwa Mbunge.
(2)Mtu yeyote hataweza kupendekezwa na chama chochote cha siasa kwa ajili ya uchaguzi kwa mujibu wa ibara hii ila tu iwapo anazo sifa za kustahili kuchaguliwa zilizotajwa na masharti ya ibara ya 67 ya Katiba hii.
(3)Majina ya watu waliopendekezwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya (1) na Tume ya Uchaguzi yatatangazwa kama matokeo ya uchaguzi baada ya Tume ya Uchaguzi kuridhika kwamba masharti ya Katiba na Sheria yanayohusika yamezingatiwa.
(4)Orodha ya majina ya wagombea wanawake iliyowasililshwa kwa Tume ya Uchaguzi na kila chama kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu ndiyo itakayotumiwa na Tume ya Uchaguzi baada ya kushauriana na chama kinachohusika, kwa madhumuni ya kujaza nafasi yoyote ya Mbunge wa aina hii inapotokea wakati wowote katika maisha ya Bunge.

79. Utaratibu wa Uchaguzi wa Wabunge wa kuchaguliwa na Baraza la Wawakilishi

Baraza la Wawakilishi litaweka utaratibu litakaoufuata kwa ajili ya kufanya uchaguzi wa Wabunge waliotajwa katika ibara ya 66(1)(c) ya Katiba hii.

80. ***

[Imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ib. 27.]

81. Utaratibu wa kupendekeza majina ya Wagombea uchaguzi wa Wabunge Wanawake

Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, Tume ya Uchaguzi yaweza kuweka masharti yanayofafanua utaratibu utakaotumiwa na vyama vya siasa kwa ajili ya kuchagua na kupendekeza majina ya Wabunge wa aina iliyotajwa katika ibara ya 66(1)(b).

82. ***

[Imefutwa na Sheria Na. 4 ya 1992 ibara ya 29]

83. Uamuzi wa suala kama mtu ni Mbunge au sivyo

(1)Kila shauri kwa ajili ya kupata uamuzi juu ya suala–
(a)kama uchaguzi au uteuzi wa mtu yeyote kuwa Mbunge ulikuwa halali au sivyo;
(b)kama Mbunge amekoma kuwa Mbunge na kiti chake katika Bunge ki wazi au hapana,
litafunguliwa na kusikilizwa kwanza katika Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (2) ya ibara hii.
(2)Lwapo Tume ya Uchaguzi katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 41(3) ya Katiba hii imemtangaza Mbunge yeyote kwamba amechaguliwa kuwa Rais basi hakuna mahakama wala chombo chochote kingine kitakachochunguza zaidi suala lolote linalohusu kiti cha Mbunge huyo kuwa wazi.
(3)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti kuhusu mambo yafuatayo–
(a)watu wanaoweza kufungua shauri katika Mahakama Kuu kwa ajili ya kupata uamuzi juu ya suala lolote kwa mujibu wa masharti ya ibara hii;
(b)sababu na nyakati za kufungua shauri la namna hiyo, utaratibu wa kufungua shauri na masharti yanayotakiwa yatimizwe kwa kila shauri kama hilo; na
(c)kutaja mamlaka ya Mahakama Kuu juu ya shauri kama hilo na kueleza utaratibu wa kusikiliza shauri lenyewe.
(4)Kutakuwa na haki ya kukata rufaa mbele ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu juu ya shauri lolote lililosikilizwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.

Sehemu ya Tatu – Utaratibu, madaraka na haki za bunge (Ib 84—101)

Spika na Naibu wa Spika (Ib 84—86)

84. Spika na mamlaka yake

(1)Kutakuwa na Spika wa Bunge ambaye atachaguliwa na Wabunge kutoka miongoni mwa watu ambao ni Wabunge au wenye sifa za kuwa Wabunge; atakuwa ndiye kiongozi wa Bunge na atawakilisha Bunge katika vyombo na vikao vingine vyote nje ya Bunge.
(2)Waziri, Naibu Waziri au mtu mwenye madaraka ya aina nyingine yoyote itakayotajwa na Sheria iliyotungwa na Bunge kwa madhumuni ya ibara hii, hataweza kuchaguliwa kuwa Spika.
(3)Mtu yeyote atakayechaguliwa kuwa Spika atatakiwa, kabla ya kumaliza siku kumi na tano tangu kuchaguliwa kwake, kuwasilisha kwa Rais tamko rasmi kwamba hajapoteza sifa za uchaguzi kwa mujibu wa masharti ya aya ya (d) ya ibara ndogo ya (2) ya ibara ya 67. Tamko hilo litatolewa kwa kutumia fomu maalum itakayowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.
(4)Rais atawasilisha kwa Kamishna wa Maadili nakala moja ya kila tamko rasmi lililowasilishwa kwake kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) ya ibara hii.
(5)Spika atatakiwa kuwasilisha kwa Rais nakala mbili za taarifa rasmi ya maelezo ya mali ya huyo Spika na, kadri itakavyokuwa mali ya mke au mume wake. Spika atatoa taarifa hiyo kwa kutumia fomu maalum iliyowekwa kwa ajili hiyo kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge na atatoa taarifa ya namna hiyo mara kwa mara kadri itakavyoagiza Sheria hiyo.
(6)Masharti ya ibara ndogo ya (2) na ya (3) ya ibara ya 70 yatatumika pia, kwa kadri itakavyowezekana, kwa taarifa ya mali yoyote itakayotolewa na Spika, kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(7)Spika atakoma kuwa Spika na ataacha kiti cha Spika litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)iwapo mtu huyo alichaguliwa kutoka miongoni mwa Wabunge, basi ikiwa atakoma kuwa Mbunge kwa sababu yoyote ambayo haihusiki na kuvunjwa Bunge; au
(b)ikiwa kutatokea jambo lolote ambalo, kama asingekuwa Spika lingemfanya mtu huyo asiwe na sifa za uchaguzi au apoteze sifa za uchaguzi wa Spika; au
(c)Bunge litakapokutana kwa mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanywa baada ya Bunge kuvunjwa, lakini masharti ya aya hii yatatumika bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (4) ya ibara ya 90 ya Katiba hii; au
(d)ikiwa mtu huyo ataondolewa kwenye madaraka ya Spika kwa azimio la Bunge lilioungwa mkono na Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote; au
(e)ikiwa mtu huyo atashindwa kuwasilisha kwa Rais tamko rasmi kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) ya ibara hii; au
(f)ikiwa mtu huyo atapatikana na hatia kwa kosa la kutoa habari za uongo, kwa kiapo kinyume cha sheria ya Kanuni ya Jinai, kuhusu tamko rasmi lolote lililotolewa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) ya ibara hii; au
(g)ikiwa mtu huyo huyo atashindwa kuwasilisha kwa Rais taarifa ya mali kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (5) ya ibara hii kabla ya kumalizika muda uliowekwa kwa ajili hiyo kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge;
(h)ikiwa itathibitika kuwa mtu huyo amevunja masharti ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
(8)Hakuna shughuli yoyote itakayotekelezwa katika Bunge (isipokuwa uchaguzi wa Spika) wakati wowote ambao kiti cha Spika kitakuwa ki wazi.
(9)Mtu yeyote ambaye si Mbunge atakayechaguliwa kuwa Spika, atatakiwa, kabla ya kuanza kutekeleza madaraka yake, kuapishwa katika Bunge kiapo cha uaminifu.

85. Naibu wa Spika

(1)Kutakuwa na Naibu wa Spika wa Bunge ambaye atachaguliwa na Wajumbe kutoka miongoni mwa Wabunge.
(2)Waziri, Naibu Waziri au mtu mwenye madaraka ya aina nyingine yoyote itakayotajwa na Sheria iliyotungwa na Bunge kwa madhumuni ya ibara hii, hataweza kuchaguliwa kuwa Naibu wa Spika.
(3)Wabunge watamchagua Naibu Spika, nyakati zifuatazo–
(a)Bunge litakapokutana kwa mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu au mapema iwezekanavyo baada ya wakati huo; na
(b)katika kikao cha kwanza cha Bunge baada ya kiti cha Naibu wa Spika kuwa wazi kwa sababu yoyote isiyohusika na Bunge kuvunjwa au mapema iwezekanavyo baada ya kikao hicho.
(4)Naibu wa Spika, atakoma kuwa Naibu wa Spika na ataacha kiti cha Naibu wa Spika, litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo–
(a)ikiwa mtu huyo atakoma kuwa Mbunge; au
(b)ikiwa kutatokea jambo lolote ambalo kama asingekuwa Naibu wa Spika, lingemfanya mtu huyo asiwe na sifa za uchaguzi au apoteze sifa za uchaguzi wa Naibu Spika; au
(c)ikiwa mtu huyo ataondolewa kwenye madaraka ya Naibu wa Spika kwa azimio la Bunge.

86. Utaratibu wa kumchagua Spika na Naibu wa Spika

(1)Kutakuwa na uchaguzi wa Spika katika kikao cha kwanza cha Mkutano wa Kwanza wa Bunge Jipya, na katika kikao cha kwanza chochote mara baada ya kutokea nafasi katika kiti cha Spika.
(2)Kutakuwa na uchaguzi wa Naibu wa Spika wakati wowote katika Mkutano wa Kwanza wa Bunge Jipya utakaoteuliwa na Bunge na vile vile katika kikao cha kwanza cha Bunge mara baada ya kutokea nafasi katika kiti cha Naibu wa Spika.
(3)Uchaguzi wa Spika, na vile vile uchaguzi wa Naibu wa Spika, utafanywa kwa kura ya siri, na utaendeshwa kwa kufuata utaratibu uliowekwa na Kanuni za Bunge.

Ofisi ya Bunge (Ib 87—88)

87. Katibu wa Bunge

(1)Kutakuwa na Katibu wa Bunge ambaye atateuliwa na Rais kutoka miongoni mwa watu wenye madaraka ya juu katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano.
(2)Katibu wa Bunge atakuwa ndiye mtendaji mkuu katika Ofisi ya Bunge na atawajibika kwa utendaji bora wa shughuli za Bunge kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii na ya sheria inayohusika.

88. Sekretarieti ya Bunge

(1)Kutakuwa na Sekretarieti ya Bunge itakayokuwa na nafasi za madaraka katika utumishi wa Umma kwa idadi atakayoagiza Rais.
(2)Sekretarieti ya Bunge itakuwa na watumishi kwa idadi na ngazi za utumishi itakavyoamuliwa mara kwa mara na Tume ya Utumishi inayohusika baada ya kushauriana na Katibu wa Bunge.
(3)Sekretarieti ya Bunge chini ya uongozi wa Katibu wa Bunge itaendeleza kazi na shughuli zote zilizowekwa au zitakazokuwa ni muhimu kwa ajili ya kuhakikisha utekelezaji bora wa Bunge na wa Wabunge wa madaraka ya Bunge chini ya Katiba hii.

Utaratibu wa shughuli Bungeni (Ib. 89—96)

89. Kanuni za Kudumu za Bunge

(1)Bila ya kuathiri masharti ya Katiba hii Bunge laweza kutunga Kanuni za Kudumu kwa ajili ya kuweka utaratibu wa kutekeleza shughuli zake.
(2)Kanuni za Kudumu zilizotungwa kwa mujibu wa ibara hii zaweza kuweka utaratibu wa kusimamia utekelezaji wa shughuli za Sekretarieti ya Bunge na pia utekelezaji wa shughuli za Bunge ndani ya Bunge na zile za kamati na kamati ndogo za Bunge.

90. Kuitishwa kwa Mikutano ya Bunge na kuvunjwa kwa Bunge

(1)Baada ya Uchaguzi Mkuu Rais ataitisha Mkutano wa Bunge Jipya ufanyike kabla ya kupita siku saba tangu kutangazwa matokeo ya huo Uchaguzi Mkuu katika majimbo ya uchaguzi yote isipokuwa katika majimbo yale ambako uchaguzi umefutwa na kufanywa upya.
(2)Rais hatakuwa na uwezo wa kulivunja Bunge wakati wowote, isipokuwa tu–
(a)kama Bunge limemaliza muda wa uhai wake kwa mujibu wa ibara ya 65 ya Katiba; au wakati wowote katika miezi kumi na miwili ya mwisho ya uhai wa Bunge, isipokuwa tu kama Spika amepokea taarifa rasmi inayopendekeza kuundwa kwa Kamati Maalum ya Uchunguzi kwa madhumuni ya kumuondoa Rais madarakani kwa mujibu wa ibara ya 46A ya Katiba hii;
(b)kama Bunge limekataa kupitisha Bajeti iliyopendekezwa na Serikali;
(c)kama Bunge limekataa kupitisha Muswada wa Sheria kwa mujibu wa ibara ya 97(4) ya Katiba;
(d)kama Bunge limekataa kupitisha hoja ambayo ni ya msingi katika sera za Serikali, na Rais anaona kwamba njia ya kuendelea kutoka hapo si kumteua Waziri Mkuu mwingine bali ni kuitisha Uchaguzi Mkuu;
(e)endapo, kutokana na uwiano wa uwakilishi wa Vyama vya Siasa katika Bunge, Rais anaona kwamba hakuna uhalali kwa Serikali iliyopo kuendelea kuwapo, na wala haiwezekani kuunda Serikali mpya.
(3)Muda wa maisha ya Bunge ukimalizika Bunge litahesabiwa kuwa limevunjwa; isipokuwa kwamba muda huo ukiisha wakati wowote ambapo Jamhuri ya Muungnao iko katika vita Bunge laweza mara kwa mara kuongeza muda huo uliotajwa katika ibara ya 65 ya Katiba hii kwa muda usiozidi miezi kumi na miwili mara kwa mara lakini maisha ya Bunge hayawezi kuongezwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo hii kwa muda unaozidi miaka mitano.
(4)Kukitokea hali ya hatari au kama kuna hali ya hatari ambayo Rais anaona inasababisha kuitisha Mkutano wa Bunge na iwapo wakati huo Bunge limevunjwa na matokeo ya kura zilizo nyingi za Uchaguzi Mkuu hayajatangazwa basi Rais aweza kutoa Taarifa Maalum ya kuitisha Mkutano wa Bunge na kuagiza kwamba Spika na watu wote waliokuwa Wabunge mara tu kabla Bunge halijavunjwa wahudhurie Mkutano huo wa Bunge na watu hao pamoja na huyo Spika, watahesabiwa kuwa ndio Wajumbe wa Bunge kwa madhumuni ya Mkutano huo na watahesabiwa hivyo mpaka usiku wa manane wa siku yatakapotangazwa matokeo ya kura zilizo nyingi za Uchaguzi Mkuu.

91. Rais aweza kulihutubia Bunge

(1)Rais atalihutubia Bunge Jipya katika Mkutano wake wa Kwanza na kulifungua rasmi Bunge hilo.
(2)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1), Rais aweza wakati wowote kulihutubia Bunge au kupeleka kwenye Bunge taarifa ambayo itasomwa na Waziri.

92. Mikutano ya Bunge

(1)Bunge litafanya Mikutano yake mahali ambapo ni desturi kufanya Mikutano hiyo au mahali pengine popote katika Jamhuri ya Muungano patakapotajwa na Rais kwa ajili hiyo.
(2)Mkutano wa kwanza wa Bunge katika Maisha ya Bunge utaanza siku ile ambayo Bunge limeitwa kukutana, na kila Mkutano ufuatao utaanza siku yoyote itakayopangwa na Bunge lenyewe au siku yoyote itakayopangwa kwa mujibu wa Kanuni za Bunge.
(3)Rais aweza kuitisha Mkutano wa Bunge wakati wowote.

93. Uongozi wa vikao vya Bunge

Kila kikao cha Bunge kitaongozwa na mmojawapo wa watu wafuatao, yaani–
(a)Spika; au
(b)ikiwa Spika hayupo, Naibu wa Spika; au
(c)ikiwa Spika na Naibu wa Spika wote hawapo, Mbunge yeyote aliyechaguliwa na Bunge kwa ajili hiyo, lakini Waziri, au Naibu Waziri au mtu mwenye madaraka ya aina nyingine yoyote yaliyotajwa na Sheria iliyotungwa na Bunge kwa madhumuni ya ibara hii hataweza kuchaguliwa kwa mujibu wa masharti ya aya hii.

94. Kiwango cha vikao vya Bunge

(1)Kiwango cha kila kikao cha Bunge ni nusu ya Wabunge wote.
(2)Isipokuwa kama imeelezwa vingine katika Katiba hii, kila swali litakalotolewa kwa ajili ya kupata uamuzi wa Bunge litaamuliwa kwa kufuata wingi wa kura za Wabunge waliohudhuria na kupiga kura.
(3)Spika, Naibu wa Spika au mtu mwingine atakayeongoza kikao cha Bunge, hatakuwa na kura ya kawaida bali atakuwa na kura ya uamuzi kukitokea usawa wa kura.
(4)Kanuni za Bunge zaweza kuweka masharti kwamba Mbunge yeyote atakayepiga kura juu ya jambo lolote ambalo yeye binafsi ana masilahi nalo atahesabiwa kuwa hakupiga kura.

95. Viti vilivyo wazi katika Bunge

Bunge laweza kutekeleza shughuli wakati wa vikao vyake bila ya kujali kwamba kuna kiti kilicho wazi miongoni mwa viti vya Wabunge (iwe kiti hicho kimekuwa wazi tangu Bunge lilipokutana kwa mara ya kwanza baada ya Uchaguzi Mkuu au kimekuwa wazi baada ya Mkutano huo wa kwanza) na iwapo katika shughuli hizo atashiriki mtu yeyote ambaye hana haki ya kushiriki au kama wakati wa shughuli hizo atakuwapo mtu yeyote ambaye hana haki ya kuwapo, basi kushiriki kwa mtu huyo au kuwapo kwake hakutabatilisha shughuli hizo.

96. Kamati za Kuduma za Bunge

(1)Bunge laweza kuunda Kamati za Bunge za namna mbalimbali kadri litakavyoona inafaa kwa ajili ya utekelezaji bora wa madaraka yake.
(2)Kanuni za Bunge zaweza kufafanua muundo na shughuli za Kamati za Bunge zitakazoundwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.

Utaratibu wa kutunga sheria (Ib. 97—99)

97. Namna ya kutumia madaraka ya kutunga sheria

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo yaliyomo katika Katiba hii, Bunge litatumia madaraka yake ya kutunga sheria kwa kufuata utaratibu wa kujadili na kupitisha Miswada ya Sheria ambayo hatimaye itabidi ipate kibali cha Rais, na Muswada hautakuwa Sheria mpaka uwe umepitishwa na Bunge na kukubaliwa na Rais kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.
(2)Baada ya Muswada kuwasilishwa kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali chake, Rais aweza kuukubali au kukataa kuukubali, na iwapo Rais atakataa kuukubali Muswada basi ataurudisha kwa Bunge pamoja na maelezo ya sababu zake za kukataa kuukubali Muswada huo.
(3)Baada ya Muswada kurudishwa kwa Bunge kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, hauwezi kupelekwa tena kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali chake kabla kumalizika muda wa miezi sita tangu uliporudishwa, isipokuwa kama katika hatua yake ya mwisho kwenye Bunge kabla haujapelekwa tena kwa Rais Muswada huo umeungwa mkono na Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote.
(4)Iwapo Muswada umerudishwa kwa Bunge na Rais, halafu ukaungwa mkono kwenye Bunge na Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote kama ilivyoelezwa katika ibara ndogo ya (3) na kupelekwa kwa Rais kwa ajili ya kupata kibali chake kwa mara ya pili kabla haujamalizika muda wa miezi sita tangu uliporudishwa, basi Rais atatakiwa kuukubali Muswada huo kabla ya kumalizika muda wa siku ishirini na moja tangu Muswada huo ulipowasilishwa kwake la sivyo basi itabidi alivunje Bunge.
(5)Masharti yaliyomo katika ibara hii au katika ibara ya 64 ya Katiba hii hayatalizuia Bunge kutunga Sheria na kuweka masharti ambayo yaweza kukabidhi kwa mtu yeyote au kwa idara yoyote ya Serikali madaraka ya kuweka Kanuni za nguvu ya kisheria au kuzipa nguvu ya kisheria Kanuni zozote zilizowekwa na mtu yeyote au idara yoyote ya Serikali.

98. Utaratibu wa kubadilisha Katiba hii na baadhi ya Sheria

(1)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii kwa kufuata Kanuni zifuatazo–
(a)Muswada wa Sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii (isipokuwa yale yanayohusika na aya ya (b) ya ibara hii ndogo) au masharti yoyote ya sheria yoyote iliyotajwa katika Orodha ya Kwanza kwenye Nyongeza ya Pili utaungwa mkono kwa kura za Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote;
(b)Muswada wa Sheria kwa ajili ya kubadilisha masharti yoyote ya Katiba hii au masharti yoyote ya Sheria yoyote yanayohusika na jambo lolote kati ya mambo yaliyotajwa katika Orodha ya Pili kwenye Nyongeza ya Pili iliyoko mwishoni mwa Katiba hii, utapitishwa tu iwapo utaungwa mkono kwa kura za Wabunge ambao idadi yao haipungui theluthi mbili ya Wabunge wote kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya Wabunge wote kutoka Tanzania Zanzibar.
(2)Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya ibara ndogo ya (1), kubadilisha masharti ya Katiba hii au masharti ya sheria maana yake ifahamike kuwa ni pamoja na kurekebisha au kusahihisha masharti hayo au kufuta na kuweka masharti mengine badala yake au kusisitiza au kubadilisha matumizi ya masharti hayo.

99. Utaratibu wa kutunga Sheria kuhusu mambo ya fedha

(1)Bunge halitashughulikia jambo lolote kati ya mambo yanayohusika na ibara hii isipokuwa kama Rais amependekeza kwamba jambo hilo lishughulikiwe na Bunge na pendekezo hilo la Rais liwe limewasilishwa kwenye Bunge na Waziri.
(2)Mambo yanayohusika na ibara hii ni haya yafuatayo:
(a)Muswada wa Sheria kwa ajili ya lolote kati ya mambo yafuatayo–
(i)kutoza kodi au kubadilisha kodi kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza;
(ii)kuagiza kwamba malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali au mfuko wa Serikali mwingine wowote au kubadilisha kiwango hicho kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza;
(iii)kuagiza kwamba malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali au mfuko wa Serikali mwingine wowote wakati ikifahamika kwamba fedha iliyomo katika mifuko hiyo haikupangiwa itolewe kwa ajili ya malipo au matumizi hayo, au kuagiza kwamba malipo au matumizi yanayofanywa kutokana na mifuko hiyo yaongezwe;
(iv)kufuta au kusamehe deni lolote linalotakiwa lilipwe kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano;
(b)hoja au mabadiliko yoyote ya Hoja kwa ajili ya lolote kati ya mambo yaliyoelezwa katika aya ya (a) ya ibara hii ndogo.
(3)Masharti ya ibara hii hayatatumika kwa muswada wowote uliowasilishwa kwenye Bunge au Hoja yoyote iliyotolewa katika Bunge na Waziri au Naibu Waziri.

Madaraka na Haki za Bunge (Ib. 100—101)

100. Uhuru wa majadiliano na utaratibu wa shughuli

(1)Kutakuwa na uhuru wa mawazo, majadiliano na utaratibu katika Bunge, na uhuru huo hautavunjwa wala kuhojiwa na chombo chochote katika Jamhuri ya Muungano, au katika mahakama au mahali penginepo nje ya Bunge.
(2)Bila ya kuathiri Katiba hii au masharti ya sheria nyingine yoyote inayohusika, Mbunge yeyote hatashtakiwa au kufunguliwa shauri la madai mahakamani kutokana na jambo lolote alilolisema au kulifanyw ndani ya Bunge au alilolileta Bungeni kwa njia ya maombi, muswada, hoja au vinginevyo.

101. Kuhifadhi na kutilia nguvu uhuru wa majadiliano na wa shughuli

Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti ya kuwezesha mahakama na sheria kuhifadhi na kutilia nguvu uhuru wa mawazo, majadiliano na utaratibu wa shughuli katika Bunge ambao kwa mujibu wa ibara ya 100 umedhaminiwa na Katiba hii.

Sura ya Nne
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Baraza la Mapinduzi la Zanzibar na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar (Ib. 102—107)

Sehemu ya Kwanza – Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Rais wa Zanzibar (Ib. 102—104)

102. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mamlaka yake

(1)Kutakuwa na Serikali ya Zanzibar itakayojulikana kama "Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar", ambayo itakuwa na mamlaka katika Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo mambo ya Muungano kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(2)Bila ya kuathiri masharti yaliyomo katika ibara hii na katika ibara zifuatazo katika Sura hii ya Katiba hii, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaundwa na itatekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na Katiba ya Zanzibar 1984.

103. Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na madaraka yake

(1)Kutakuwa na Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambaye ndiye atakuwa Rais wa Zanzibar na Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na vile vile Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi la Zanzibar.
(2)Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kabla ya kushika madaraka yake ataapa mbele ya Jaji Mkuu wa Zanzibar kiapo cha kuilinda na kuitetea Katiba ya Jamhuri ya Muungano, na kiapo kingine chochote kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar kinachohusika na utendaji wa kazi yake, kisha atashika na kutekeleza madaraka hayo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na Katiba ya Zanzibar, 1984.
(3)Pamoja na madaraka yake mengine kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ndiye atakayewateua na kuwakabidhi madaraka Mawaziri na Naibu Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

104. Uchaguzi wa Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar

(1)Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar atachaguliwa na wananchi katika Tanzania Zanzibar kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Zanzibar na kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar inayohusu uchaguzi kwa ujumla au uchaguzi wa Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
(2)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya Katiba hii, kiti cha Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kitakuwa ki wazi, na uchaguzi wa Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar utafanyika ili kujaza nafasi hiyo kila mara litokeapo lolote kati ya mambo yafuatayo:
(a)baada ya Baraza la Wawakilishi kuvunjwa;
(b)baada ya Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kujiuzulu bila ya kulivunja Baraza la Wawakilishi kwanza;
(c)baada ya Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupoteza sifa za kushika nafasi ya madaraka ya kuchaguliwa;
(d)baada ya Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kushtakiwa katika Baraza la Wawakilishi kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar 1984 na kuondolewa katika madaraka;
(e)baada ya kuthibitishwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar 1984 kwamba Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hawezi kumudu kazi na shughuli zake;
(f)baada ya Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufariki.

Sehemu ya Pili – Baraza la Mapinduzi la Zanzibar (Ib. 105)

105. Baraza la Mapinduzi la Zanzibar na kazi zake

(1)Kutakuwa na Baraza la Mapinduzi la Zanzibar litakalokuwa na wajumbe wafuatao:
(a)Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
(b)Waziri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;
(c)Mawaziri wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;
(d)Wajumbe wengine watakaoteuliwa na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Zanzibar.
(2)Bila ya kuyaingilia madaraka ya Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kama Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Baraza la Mapinduzi litakuwa ndicho chombo kikuu cha kumshauri Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar juu ya mambo yote yanayohusika na utekelezaji wa madaraka yake ya uongozi na usimamizi wa shughuli za Serikali ya Zanzibar na pia utekelezaji wa madaraka yake juu ya shughuli zote za Serikali kuhusu mambo yote yasiyo Mambo ya Muungano, kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na yale ya Katiba ya Zanzibar.

Sehemu ya Tatu – Baraza la Wawakilishi la Zanzibar (Ib. 106—107)

106. Baraza la Wawakilishi la Zanzibar na madaraka ya kutunga Sheria za Zanzibar

(1)Kutakuwa na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar. Baraza la Wawakilishi litakuwa na sehemu mbili; sehemu moja itakuwa ni ya Wajumbe wa Baraza hilo waliochaguliwa na kuteuliwa kwa namna itakavyoelezwa na masharti ya Katiba ya Zanzibar, ya mwaka 1984, na ambao watajulikana kama Wajumbe Wawakilishi; sehemu nyingine ya Baraza la wawakilishi itakuwa ni Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika utekelezaji wa madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na masharti ya Katiba ya Zanzibar, ya mwaka 1984.
(2)Iwapo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, masharti ya Katiba ya Zanzibar, ya mwaka 1984, au masharti ya Sheria yoyote iliyowekwa na inayotumika Zanzibar, jambo lolote lahitaji kuamuliwa au kutekelezwa na sehemu zote mbili za Baraza la Wawakilishi, basi jambo hilo halitahesabiwa kuwa limeamuliwa au limetekelezwa ipasavyo ila mpaka liwe limeamuliwa au limetekelezwa na Wajumbe Wawakilishi na vile vile Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa mujibu wa madaraka yao kuhusu jambo hilo.
(3)Madaraka yote ya kutunga Sheria katika Zanzibar juu ya mambo yote yasiyo Mambo ya Muungano yatakuwa mikononi mwa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar.

107. Madaraka ya Baraza la Wawakilishi

(1)Rais wa Zanzibar kama sehemu moja ya Baraza la Wawakilishi atatekeleza madaraka yote aliyokabidhiwa na Katiba hii na pia Katiba ya Zanzibar kwa ajili hiyo.
(2)Wajumbe Wawakilishi kama Baraza la Wawakilishi watakuwa ndicho chombo Kikuu cha Tanzania Zanzibar ambacho kitakuwa na madaraka kwa niaba ya wananchi wa Tanzania Zanzibar, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kwa mujibu wa Katiba hii na Katiba ya Zanzibar.
(3)Kwa madhumuni ya utekelezaji wa madaraka yake, Baraza la Wawakilishi laweza–
(a)kumuuliza Waziri yeyote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar swali lolote kuhusu mambo ya umma katika Tanzania Zanzibar yaliyomo katika wajibu wake;
(b)kujadili utekelezaji wa kila Wizara ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakati wa Mkutano wa Baraza la Wawakilishi wa kila mwaka wa bajeti;
(c)kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu au wa muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa Tanzania Zanzibar, na kutunga sheria ya kusimamia utekelezaji wa mpango huo;
(d)kutunga sheria pale ambapo utekelezaji unahitaji kuwapo sheria; na
(e)kutayarisha au kuagiza itayarishwe na kuwasilisha kwenye Chama chochote cha siasa taarifa kuhusu jambo lolote ambalo liko chini ya mamlaka ya Bunge.

Sura ya Tano
Utoaji Haki katika Jamhuri ya Muungano, Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano, Tume ya Kuajiri ya Mahakama ya Tanzania Bara, Mahakama Kuu ya Zanzibar, Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano na Mahakama Maalum ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 107A—128)

Sehemu ya Kwanza – Utoaji ahki katika Jamhuri ya Muungano (Ib. 107A—107B)

107A. Mamlaka ya utoaji haki

(1)Mamlaka ya utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano itakuwa mikononi mwa Idara ya Mahakama na Idara ya Mahakama ya Zanzibar, na kwa hiyo hakuna chombo cha Serikali wala cha Bunge au Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kitakachokuwa na kauli ya mwisho katika utoaji haki.
(2)Katika kutoa uamuzi wa mashauri ya madai na jinai kwa kuzingatia sheria, Mahakama zitafuata kanuni zifuatazo, yaani–
(a)kutenda haki kwa wote bila ya kujali hali ya mtu kijamii au kiuchumi;
(b)kutochelewesha haki bila sababu ya kimsingi;
(c)kutoa fidia ipasayo kwa watu wanaoathirika kutokana na makosa ya watu wengine, na kwa mujibu wa sheria mahususi iliyotungwa na Bunge;
(d)kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro.

107B. Uhuru wa Mahakama

Katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, Mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya Katiba na yale ya sheria za nchi.

Sehemu ya Pili – Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 108-111)

108. Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano na Mamlaka yake

(1)Kutakuwa na Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano (itakayojulikana kwa kifupi kama "Mahakama Kuu") ambayo mamlaka yake yatakuwa kama ilivyoelezwa katika Katiba hii au katika Sheria nyingine yoyote.
(2)Iwapo Katiba hii au Sheria nyingine yoyote haikutamka wazi kwamba shauri la aina iliyotajwa mahsusi litasikilizwa kwanza katika Mahakama ya ngazi iliyotajwa mahsusi kwa ajili hiyo, basi Mahakama Kuu itakuwa na mamlaka ya kusikiliza kila shauri la aina hiyo. Hali kadhalika, Mahakama Kuu itakuwa na uwezo wa kutekeleza shughuli yoyote ambayo kwa mujibu wa mila za kisheria zinazotumika Tanzania, shughuli ya aina hiyo kwa kawaida hutekelezwa na Mahakama Kuu.
Isipokuwa kwamba masharti ya ibara hii ndogo yatatumika bila ya kuathiri mamlaka ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania kama ilivyoelezwa katika Katiba hii au katika sheria nyingine yoyote.

109. Majaji wa Mahakama Kuu na uteuzi wao

(1)Kutakuwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu (ambaye katika ibara zifuatazo kwenye Katiba hii atatajwa tu kwa kifupi kama "Jaji Kiongozi") na Majaji wengine wa Mahakama Kuu wasiopungua kumi na watano.
(2)Jaji Kiongozi na Majaji wengineo wa Mahakama Kuu watateuliwa na Rais baada ya kushauriana na Tume ya Kuajiri ya Mahakama.
(3)Bila ya kuathiri masharti ya Katiba hii au sheria nyingine yoyote kuhusu madaraka ya Jaji Mkuu aliyetajwa katika ibara ya 118, Jaji Kiongozi atakuwa ndiye msaidizi maalum wa Jaji Mkuu katika utendaji wa kazi katika Mahakama Kuu na Mahakama nyinginezo zote za ngazi ya chini yake, na katika madaraka hayo Jaji Kiongozi atatekeleza kazi na shughuli atakazoagizwa au kuelekezwa mara kwa mara na Jaji Mkuu, na kwa madhumuni ya ibara hii, Jaji Kiongozi atajulikana pia kama Mkuu wa Mahakama Kuu.
(4)Mbali ya madaraka yake ya kawaida ya Jaji wa Mahakama Kuu kama Majaji wengine wote wa Mahakama Kuu, Jaji Kiongozi atakuwa pia na mamlaka ya kutekeleza kazi na shughuli zote zinazoambatana na mamlaka ya Mahakama Kuu ambazo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au ya sheria nyingine yoyote au kufuatana na mila za kisheria zinazotumika hutakiwa zitekelezwe na Mkuu wa Mahakama Kuu:Isipokuwa kwamba masharti ya ibara hii ndogo hayatatumika kwa ajili ya utekelezaji wa kazi au shughuli ambazo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au ya Sheria nyingine yoyote au kufuatana na mila za kisheria zinazotumika Tanzania zimetajwa mahsusi au zinafahamika kuwa ni kazi au shughuli zinazotakiwa kutekelezwa tu na Jaji Mkuu.
(5)Kwa madhumuni ya kuondoa mashaka juu ya ufafanuzi au utekelezaji wa masharti ya ibara ndogo ya (3) na ya (4) ya ibara hii, inatamkwa rasmi hapa kwamba isipokuwa kama masharti ya Katiba hii au ya sheria nyingine yoyote yameagiza vingine, Jaji Mkuu atakuwa na uwezo wa kutoa kwa Jaji Kiongozi mara kwa mara maagizo au maelekezo kuhusu utendaji wa kazi na shughuli zake kama Mkuu wa Mahakama Kuu; vile vile, Jaji Mkuu atakuwa na uwezo wa kuwakilisha kwa Jaji Kiongozi baadhi ya madaraka yake ya uongozi na usimamizi juu ya utekelezaji wa kazi katika Mahakama Kuu na Mahakama nyinginezo zote za ngazi ya chini yake, na kila inapohitajika, Jaji Mkuu anaweza kutekeleza yeye mwenyewe moja kwa moja madaraka yake yoyote aliyowakilisha kwa Jaji Kiongozi.
(6)Nafasi ya Jaji wa Mahakama Kuu haitafutwa wakati yupo mtu aliyeshika madaraka ya kiti cha Jaji.
(7)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (9) ya ibara hii, mtu aweza tu kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ikiwa ana sifa maalum, kama ilivyofafanuliwa katika ibara ndogo ya (8) ya ibara hii, na awe mtu ambaye amekuwa na mojawapo ya sifa maalum kwa muda usiopungua miaka mitano.
(8)Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa ibara ndogo ya (7), ya (9) na ya (11) ya ibara hii, "sifa maalum" maana yake ni sifa zilizotajwa katika Sheria ya Mawakili 4 (au Sheria nyingine yoyote inayobadilisha hiyo sheria ya Mawakili au inayotumika badala yake) ambazo ni lazima mtu awe nayo mojawapo ya sifa hizo ili aweze kukubaliwa kuandikishwa kama Wakili Tanzania Bara.4Sura ya 341
(9)Iwapo Rais atatosheka kwamba ijapokuwa mtu mwenye sifa mojawapo ya hizo sifa maalum hakuwa nayo sifa hiyo kwa muda usiopungua miaka mitano, lakini mtu huyo ana uwezo, ujuzi na kwa kila hali anafaa kukabidhiwa madaraka ya Jaji wa Mahakama Kuu na kuna sababu za kumfanya mtu huyo astahili kukabidhiwa madaraka hayo, basi Rais aweza kutangua lile sharti la kuwa na sifa maalum kwa muda usiopungua miaka mitano, na baada ya kushauriana na Tume ya Kuajiri ya Mahakama, Rais aweza kumteua mtu huyo kuwa Jaji wa Mahakama Kuu.
(10)Ikitokea kwamba kiti cha Jaji Kiongozi kinakuwa wazi au kwamba Jaji Kiongozi anashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, basi kazi hizo zitatekelezwa na Jaji mmojawapo atakayeteuliwa na Rais kwa ajili hiyo, na Jaji huyo atatekeleza kazi hizo mpaka atakapoteuliwa Jaji Kiongozi mwingine na kushika madaraka ya kiti cha Jaji Kiongozi au mpaka Jaji Kiongozi mwenyewe ambaye alikuwa hamudu kazi zake atakaporejea kazini.
(11)Ikitokea kwamba kiti cha Jaji yeyote kitakuwa wazi au ikiwa Jaji yeyote atateuliwa kuwa Kaimu Jaji Kiongozi au kama atashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, au kama Jaji Mkuu atamshauri Rais kuwa kazi za Mahakama Kuu zilivyo wakati huo zahitaji ateuliwe Kaimu Jaji, basi Rais aweza, baada ya kushauriana na Jaji Mkuu kama kawaida, kumteua Kaimu Jaji kutoka miongoni mwa watu wenye sifa maalum:Isipokuwa kwamba–
(a)mtu hatahesabiwa kuwa hastahili kuteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo kwa sababu tu kwamba ametimiza umri uliotajwa katika ibara ndogo ya (1) ya ibara ya 110 ya Katiba hii;
(b)kwa madhumuni ya kumteua Kaimu Jaji kwa mujibu wa masharti ya ibara hii ndogo, Rais aweza kutangua lile sharti la kuwa na sifa maalum kwa muda usiopungua miaka mitano kwa sababu kama zile zilizotajwa katika ibara ndogo ya (9) ya ibara hii.
(12)Mtu yeyote atakayeteuliwa kuwa Kaimu Jaji kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (11) ya ibara hii, ataendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji kwa muda wowote utakaotajwa wakati wa kuteuliwa kwake au, kama muda haukutajwa, mpaka uteuzi wake utakapofutwa na Rais, lakini bila ya kujali kwamba muda wake wa kazi umemalizika au kwamba uteuzi wake umefutwa, mtu huyo aweza kuendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwisha anza kuyasikiliza kabla muda wake wa kazi haujamalizika au kabla ya uteuzi wake haujafutwa.

110. Muda wa Majaji wa Mahakama Kuu kushika madaraka

(1)Kila Jaji wa Mahakama Kuu atalazimika kuacha kazi yake atakapotimiza umri wa miaka sitini, lakini masharti ya ibara hii ndogo yatatumika bila ya kuathiri masharti yafuatayo katika ibara hii.
(2)Jaji yeyote wa Mahakama Kuu aweza kujiuzulu kazi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano wakati wowote baada ya kutimiza umri wa miaka hamsini na tano, isipokuwa kama Rais ataagiza kwamba asijiuzulu na iwapo Rais ataagiza hivyo, basi huyo Jaji atakayehusika na maagizo hayo ya Rais hatakuwa na haki ya kujiuzulu mpaka upite kwanza muda wowote utakaotajwa na Rais kwa ajili hiyo.
(3)Iwapo Rais ataona kuwa kwa ajili ya manufaa ya Umma inafaa Jaji aliyetimiza umri wa miaka sitini aendelee kufanya kazi, na huyo Jaji mwenyewe anakubali kwa maandishi kuendelea kufanya kazi, basi Rais aweza kuagiza kuwa Jaji huyo aendelee kufanya kazi kwa muda wowote utakaotajwa na Rais.
(4)Bila ya kujali kwamba Jaji ametimiza umri ambao analazimika kuacha kazi kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, mtu anayefanya kazi ya Jaji wa Mahakama Kuu aweza kuendelea kufanya kazi baada ya kutimiza umri huo mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwisha anza kuyasikiliza kabla hajatimiza umri huo wa kuacha kazi.
(5)Jaji wa Mahakama Kuu aweza tu kuondolewa katika madaraka ya kazi ya Jaji kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi zake (ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote) au kwa sababu ya tabia mbaya inayoathiri Maadili ya Kazi ya Jaji au Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma; na hataweza kuondolewa kazini ila kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (7) ya ibara hii.
(6)Iwapo Rais anaona kuwa suala la kumwondoa Jaji kazini lahitaji kuchunguzwa, basi katika hali hiyo mambo yatakuwa ifuatavyo–
(a)Rais atateua Tume ambayo itakuwa na Mwenyekiti na Wajumbe wengine wasiopungua wawili. Na huyo Mwenyekiti na angalau nusu ya Wajumbe wengine wa Tume hiyo itabidi wawe watu ambao ni Majaji wa Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufani katika nchi yoyote iliyomo kwenye Jumuiya ya Madola;
(b)Tume hiyo itachunguza shauri lote halafu itatoa taarifa kwa Rais kuhusu maelezo ya shauri hilo lote na itamshauri Rais kama huyo Jaji anayehusika aondolewe kazini kwa mujibu wa masharti ya ibara hii kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi na sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya.
(7)Ikiwa Tume iliyoteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (6) itamshauri Rais kwamba Jaji ambaye habari zake zimechunguzwa na hiyo Tume aondolewe kazini kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya, basi Rais atamwondoa kazini Jaji huyo anayehusika.
(8)Ikiwa suala la kumwondoa Jaji kazini limepelekwa kwenye Tume kwa ajili ya uchunguzi kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (6) ya ibara hii, Rais aweza kumsimamisha kazi Jaji huyo anayehusika, na Rais aweza wakati wowote kufuta uamuzi huo wa kumsimamisha kazi Jaji huyo, na kwa hali yoyote uamuzi huo utabatilika ikiwa Tume itamshauri Rais kwamba Jaji huyo asiondolewe kazini.
(9)Masharti ya ibara hii yatatumika bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (12) ya ibara ya 109 ya Katiba hii.

111. Kiapo cha Majaji

Jaji wa Mahakama Kuu hatashika madaraka yake ila mpaka awe ameapishwa kwanza kiapo cha uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

Sehemu ya Tatu – Madaraka ya Kuajiri Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama za Tanzania Bara na Tume ya Kuajiri ya Mahakama (Ib. 112—113A)

112. Tume ya Kuajiri ya Mahakama

(1)Kutakuwa na Tume ya Kuajiri kwa ajili ya Mahakimu na Watumishi wengineo wa Mahakama za Tanzania Bara. Wajumbe wa Tume hiyo watakuwa hawa wafuatao–
(a)Jaji Mkuu ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b)Mwanasheria Mkuu;
(c)Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania ambaye atateuliwa kwa ajili hiyo na Rais baada ya kushauriana na Jaji Mkuu;
(d)Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu;
(e)Wajumbe wawili ambao watateuliwa na Rais.
(2)Mtu hataweza kuteuliwa kuwa mjumbe wa Tume kwa mujibu wa masharti ya aya ya (d) ya ibara ndogo ya (1) ya ibara hii ikiwa mtu huyo ni Mbunge au ni mtu mwenye madaraka ya aina nyingine yoyote iliyotajwa kwa ajili hiyo na sheria iliyotungwa na Bunge.

113. Madaraka ya kuajiri Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama

(1)Bila ya kuathiri masharti ya Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge inayohusika na suala la kuajiri Mahakimu na Watumishi wengineo wa Mahakama mgawanyo wa madaraka kwa ajili ya suala hilo utakuwa ifuatavyo–
(a)madaraka ya kuwaajiri watu wa kushika madaraka ya aina zilizotajwa katika ibara ndogo ya (2) ya ibara hii (pamoja na madaraka ya kuwathibitisha watu hao kazini na kuwapandisha vyeo) yatakuwa mikononi mwa Rais;
(b)madaraka ya kudhibiti nidhamu ya watu hao na madaraka ya kuwaondoa kazini yatakuwa mikononi mwa Tume ya Kuajiri iliyotajwa katika ibara ya 112 ya Katiba hii.
(2)Madaraka yanayohusika na masharti ya ibara hii ni madaraka ya Msajili wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania na Naibu wa Msajili huyo wa daraja lolote, madaraka ya Msajili wa Mahakama Kuu na Naibu wa Msajili huyo wa daraja lolote, madaraka ya Hakimu Mkazi na Hakimu wa aina nyingine yoyote, na madaraka ya aina nyingine yoyote yanayohusika na Mahakama yoyote (isipokuwa Mahakama ya Kijeshi) itakayotajwa na Sheria iliyotungwa na Bunge kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.

113A. Uanachama katika vyama vya siasa

Itakuwa ni marufuku kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Hakimu wa ngazi yoyote kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba atakuwa na haki ya kupiga kura iliyotajwa katika ibara ya 5 ya Katiba hii.

Sehemu ya Nne – Mahakama Kuu ya Zanzibar (Ib. 114—115)

114. Mahakama Kuu ya Zanzibar

Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa Sura hii ya Katiba hii, ifahamike kwamba masharti yaliyomo katika Sura hii hayazuii kuendelea kuwapo au kuanzishwa, kwa mujibu wa Sheria zinazotumika Zanzibar, kwa Mahakama Kuu ya Zanzibar au mahakama zilizo chini ya Mahakama Kuu ya Zanzibar.

115. Mamlaka ya Mahakama Kuu ya Zanzibar

(1)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ya 83 na 116 ya Katiba hii, mamlaka ya Mahakama Kuu ya Zanzibar yatakuwa kama itakavyoelezwa katika Sheria zinazotumika Zanzibar.
(2)Bila ya kuathiri masharti ya Katiba hii au sheria nyingine yoyote iliyotungwa na Bunge, iwapo sheria yoyote iliyotungwa na Bunge inayotumika Tanzania Bara na vile vile Tanzania Zanzibar imekabidhi madaraka yoyote kwa Mahakama Kuu, basi Mahakama Kuu ya Zanzibar yaweza kutekeleza madaraka hayo kwa kiasi kile kile inavyoweza kutekeleza Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano.

Sehemu ya Tano – Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 116—123)

116. Ufafanuzi

(1)Katika Sehemu hii ya Tano ya Sura hii ya Tano ya Katiba hii na katika sehemu nyingine za Katiba hii, ila iwapo maelezo yahitaji vinginevyo–"Idara ya Mahakama" maana yake ni Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano iliyotajwa katika ibara ya 117 ya Katiba hii (au kwa kifupi "Mahakama ya Rufani"), Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano iliyotajwa katika ibara ya 108 ya Katiba hii (ambayo itajulikana kwa kifupi kama "Mahakama Kuu") pamoja na Mahakama nyingine zozote za ngazi zilizo chini ya Mahakama Kuu;"Jaji Mkuu" maana yake ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Rufani na ni pamoja na Kaimu Jaji Mkuu au Jaji wa Rufani anayeshikilia au kutekeleza madaraka ya Jaji Mkuu;"Jaji wa Rufani" maana yake ni Jaji yoyote wa Mahakama ya Rufani.
(2)Bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (3), Jaji Mkuu hatakuwa na madaraka juu ya jambo lolote linalohusu muundo na uendeshaji wa shughuli za siku hadi siku za Mahakama zilizoundwa kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar au sheria yoyote ya Tanzania Zanzibar.
(3)Jaji Mkuu atashauriana mara kwa mara na Jaji Mkuu wa Zanzibar kuhusu uendeshaji wa shughuli za Mahakama ya Rufani kwa jumla, na pia kuhusu uteuzi wa Majaji wa Rufani.

117. Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano na Mamlaka yake

(1)Kutakuwa na Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano (itakayojulikana kwa kifupi kama "Mahakama ya Rufani") ambayo mamlaka yake yatakuwa kama ilivyoelezwa katika Katiba hii au katika Sheria nyingine yoyote.
(2)Mahakama ya Rufani haitakuwa na mamlaka yoyote kuhusu usuluhishi wa suala lolote litakaloshughulikiwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 126 ya Katiba hii ambayo inahusu ubishi kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
(3)Kazi ya Mahakama ya Rufani itakuwa ni kusikiliza na kutoa uamuzi juu ya kila rufaa inayoletwa mbele ya Mahakama ya Rufani kutokana na hukumu au uamuzi wa namna nyingine yoyote wa Mahakama Kuu au Mahakama ya yoyote ya chini iliyopewa Mamlaka maalum ya Mahakama Kuu.
(4)Sheria iliyotungwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na Bunge au na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar yaweza kuweka masharti yatakayoeleza utaratibu wa kupeleka rufaa mbele ya Mahakama ya Rufani, nyakati na sababu za kukata rufaa na namna ya kushughulikia rufaa hizo.

118. Majaji wa Mahakama ya Rufani na uteuzi wao

(1)Kutakuwa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Rufani (ambaye katika ibara zifuatazo kwenye Katiba hii atatajwa tu kwa kifupi kama "Jaji Mkuu") na Majaji wengine wa Mahakama ya Rufani wasiopungua wawili, isipokuwa kwamba kikao maalum cha Mahakama nzima kitakuwa kamili kukiwa na Majaji Rufani wasiopungua watano.
(2)Jaji Mkuu atateuliwa na Rais na atakuwa ndiye Kiongozi wa Mahakama ya Rufani na pia Mkuu wa Idara ya Mahakama kama ilivyofafanuliwa katika ibara ya 116 ya Katiba hii.
(3)Majaji wengineo wa Mahakama ya Rufani watateuliwa na Rais, baada ya kushauriana na Jaji Mkuu, kutoka miongoni mwa watu ambao wanaweza kuteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano kama ilivyoelezwa katika ibara ya 109 ya Katiba hii au kutoka miongoni mwa watu wanaoweza kuteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar kwa mujibu wa Sheria zinazotumika Zanzibar.
(4)Iwapo itatokea kwamba–
(a)kiti cha Jaji Mkuu kitakuwa wazi; au
(b)Jaji Mkuu hayupo Tanzania; au
(c)Jaji Mkuu atashindwa kutekeleza kazi yake kwa sababu yoyote, na Rais akiona kuwa kwa muda wa tukio lolote kati ya hayo matatu inafaa kumteua Kaimu Jaji Mkuu, basi Rais aweza kumteua Kaimu Jaji Mkuu kutoka miongoni mwa watu wenye sifa za kustahili kuteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani, na huyo Kaimu Jaji Mkuu atatekeleza kazi za Jaji Mkuu au mpaka atakapoteuliwa Jaji Mkuu au mpaka Jaji Mkuu mwingine ambaye alikuwa hayupo Tanzania au alikuwa hamudu kazi zake atakaporejea kazini.
(5)Ikitokea kwamba kiti cha Jaji yeyote wa Mahakama ya Rufani kitakuwa wazi au ikiwa Jaji yeyote wa Mahakama ya Rufani atateuliwa kuwa Kaimu Jaji Mkuu au kama atashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, au kama Jaji Mkuu atamshauri Rais kuwa kazi za Mahakama ya Rufani ilivyo wakati huo zahitaji ateuliwe Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani, basi Rais aweza, baada ya kushauriana na Jaji Mkuu kama kawaida, kumteua Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani kutoka miongoni mwa watu wanaoweza kuteuliwa kuwa Majaji wa Mahakama ya Rufani kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) ya ibara hii.
(6)Mtu yeyote atakayeteuliwa kuwa Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (5) ya ibara hii, ataendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa muda wowote utakaotajwa wakati wa kuteuliwa kwake, au kama muda haukutajwa, mpaka uteuzi wake utakapofutwa na Rais, lakini bila ya kujali kwamba muda wake wa kazi umemalizika au kwamba uteuzi wake umefutwa, mtu huyo aweza kuendelea kufanya kazi kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na rufaa au mashauri mengine yoyote ambayo alikwisha anza kuyasikiliza kabla muda wake wa kazi haujamalizika au kabla ya uteuzi wake haujafutwa.
(7)Kwa madhumuni ya kuondoa mashaka juu ya ufafanuzi wa masharti ya ibara ndogo ya (1) ya ibara ya 118 ya Katiba hii (inayotaja idadi ya Majaji wa kudumu wa Mahakama ya Rufani) na masharti ya ibara ya 119 ya Katiba hii (inayoeleza mamlaka ya Majaji wa Mahakama ya Rufani), inatamkwa rasmi hapa kwamba Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani aliyeteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (5) ya ibara hii atakuwa na mamlaka kamili ya Jaji wa Mahakama ya Rufani na kwamba atatekeleza kazi zake kama Kaimu Jaji wa Mahakama ya Rufani bila ya kujali kuwa kuteuliwa kwake kutakiuka idadi ya Majaji wa kudumu wa Mahakama ya Rufani iliyotajwa katika ibara ndogo ya (1) ya ibara ya 118 ya Katiba hii, lakini masharti ya ibara hii ndogo yatatumika bila ya kuathiri masharti ya ibara ya 122 ya Katiba hii kuhusu kiwango cha vikao vya Mahakama ya Rufani.
(8)Nafasi ya Jaji wa Mahakama ya Rufani haitafutwa wakati yupo mtu aliyeshika madaraka ya kiti cha Jaji wa Mahakama ya Rufani.

119. Mamlaka ya Majaji wa Mahakama ya Rufani

Jaji yeyote wa Mahakama ya Rufani hatakuwa na mamlaka ya kusikiliza shauri lolote katika Mahakama Kuu au katika Mahakama ya Hakimu ya ngazi yoyote:Isipokuwa kwamba iwapo Jaji yeyote wa Mahakama Kuu atateuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, basi hata baada ya kuteuliwa kwake kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji huyo aweza kuendelea kufanya kazi zake katika Mahakama Kuu mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwisha anza kuyasikiliza kabla hajateuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, na kwa ajili hiyo itakuwa halali kwake kutoa hukumu au uamuzi mwingine wowote unaohusika kwa kutumia na kutaja madaraka aliyoshika kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, lakini endapo hatimaye hukumu hiyo au uamuzi huo mwingine utapingwa kwa njia ya rufaa itakayofikishwa mbele ya Mahakama ya Rufani, basi katika hali hiyo Jaji huyo wa Mahakama ya Rufani, hatakuwa na mamlaka ya kusikiliza rufaa hiyo.

120. Muda wa Majaji wa Mahakama ya Rufani kushika madaraka

(1)Kila Jaji wa Mahakama ya Rufani atalazimika kuacha kazi yake atakapotimiza umri wa miaka sitini na tano, lakini masharti ya ibara hii ndogo yatatumika bila kuathiri masharti yafuatayo katika ibara hii.
(2)Jaji yeyote wa Mahakama ya Rufani aweza kujiuzulu kazi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano wakati wowote baada ya kutimiza umri wa miaka sitini, isipokuwa kama Rais ataagiza kwamba asijiuzulu, na iwapo Rais ataagiza hivyo, basi huyo Jaji wa Mahakama ya Rufani atakayehusika na maagizo hayo ya Rais hatakuwa na haki ya kujiuzulu mpaka upite kwanza muda wowote utakaotajwa na Rais kwa ajili hiyo.
(3)Iwapo Rais ataona kuwa kwa ajili ya manufaa ya Umma inafaa Jaji wa Mahakama ya Rufani aliyetimiza umri wa miaka sitini na tano aendelee kufanya kazi, na huyo Jaji mwenyewe wa Mahakama ya Rufani anakubali kwa maandishi kuendelea kufanya kazi; basi Rais aweza kuagiza kuwa Jaji huyo wa Mahakama ya Rufani aendelee kufanya kazi kwa muda wowote utakaotajwa na Rais.
(4)Bila ya kujali kwamba Jaji wa Mahakama ya Rufani ametimiza umri ambao analazimika kuacha kazi kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, mtu anayefanya kazi ya Jaji wa Mahakama ya Rufani aweza kuendelea kufanya kazi baada ya kutimiza umri huo mpaka amalize kutayarisha na kutoa hukumu au mpaka akamilishe shughuli nyingine yoyote inayohusika na mashauri ambayo alikwisha anza kuyasikiliza kabla hajatimiza umri huo wa kuacha kazi.
(5)Jaji wa Mahakama ya Rufani aweza tu kuondolewa katika madaraka ya kazi ya Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi zake (ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote) au kwa sababu ya tabia mbaya, na hataweza kuondolewa kazini ila kwa mujibu wa masharti ya utaratibu unaofanana na ule uliowekwa kwa ajili ya kumwondoa kazini Jaji wa Mahakama Kuu kama ilivyoelezwa katika ibara ndogo ya (6) na ya (7) ya ibara ya 110 ya Katiba hii, na kwa ajili hiyo masharti ya ibara ndogo ya (8) ya ibara hiyo ya 110 yatatumika kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani kwa namna ile ile yanavyotumika kwa Jaji wa Mahakama Kuu.
(6)Masharti ya ibara hii yatatumika bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (5) ya ibara ya 118 ya Katiba hii.

121. Kiapo cha Majaji wa Mahakama ya Rufani

Jaji wa Mahakama ya Rufani hatashika madaraka yake ila mpaka awe ameapishwa kiapo cha uaminifu na kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi kitakachowekwa kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

122. Kiwango cha vikao vya Mahakama ya Rufani

(1)Kiwango cha kila kikao cha Mahakama ya Rufani ni Majaji wa Mahakama ya Rufani wasiopungua watatu.
(2)Katika kila rufaa suala linalohitaji uamuzi wa Mahakama ya Rufani litaamuliwa kwa kufuata kauli ya walio wengi kati ya Majaji wa Mahakama ya Rufani waliosikiliza rufaa.

123. Mashauri yanayoweza kuamuliwa na Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani

Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani aweza kutekeleza madaraka yoyote ya Mahakama ya Rufani ambayo hayahusiki na kutoa uamuzi juu ya rufaa:Isipokuwa kwamba–
(a)Katika mashauri ya jinai, iwapo Jaji wa Mahakama ya Rufani aliyeombwa kutekeleza madaraka hayo atatoa uamuzi ambao mwombaji haridhiki nao, basi mwombaji atakuwa na haki kutaka maombi yake yaamuliwe na Mahakama ya Rufani;
(b)katika mashauri ya madai, Mahakama ya Rufani yaweza kubatilisha au kubadilisha amri, agizo au uamuzi wa namna nyingine wowote uliotolewa na Jaji mmoja wa Mahakama ya Rufani kwa mujibu wa masharti ya ibara hii.

Sehemu ya Sita – Utaratibu wa kupeleka hati za kutekeleza maagizo yaliyomo katika hati zilizotolewa na Mahakama (Ib. 124)

124. Utekelezaji wa maagizo ya Mahakama utafanywa nchini Tanzania kote

(1)Hati zenye maagizo yaliyotolewa na Mahakama za Tanzania Bara na Mahakama za Tanzania Zanzibar katika mashauri ya madai ya aina zote na mashauri ya jinai ya aina zote (pamoja na hati za kuamuru kukamatwa watu) zaweza kupelekwa mahali popote nchini Tanzania na maagizo hayo yaweza kutekelezwa mahali popote nchini Tanzania kwa kufuata masharti yafuatayo–
(a)iwapo Mahakama imetoa hati zenye maagizo yatakayotekelezwa mahali ambako mahakama hiyo haina mamlaka, basi hati hiyo itapelekwa huko na maagizo yaliyomo katika hati hiyo yatatekelezwa kwa mujibu wa utaratibu unaotumika huko kwa ajili ya kupeleka hati au kutekeleza maagizo yaliyomo katika hati iliyotolewa na Mahakama yenye mamlaka huko ilikopelekwa hati; na
(b)iwapo Sheria inayotumika huko ilikopelekwa hati imeweka masharti kwamba hati zilizotolewa na Mahakama ya mahali pengine ni lazima ithibitishwe kwanza na Mahakama yenye mamlaka mahali hapo inapotumika sheria hiyo, basi kila hati iliyotolewa na Mahakama ya mahali pengine itabidi ithibitishwe kwanza kwa mujibu wa sheria hiyo kabla maagizo yaliyomo katika hati hiyo hayajatekelezwa.
(2)Iwapo mtu amekamatwa mahali popote nchini Tanzania kwa mujibu wa hati ya kuamuru kukamatwa kwake iliyotolewa na Mahakama ambayo haina mamlaka mahali hapo alipokamatwa mtu huyo, basi mtu huyo atahesabiwa kuwa yuko chini ya ulinzi halali na aweza kufikishwa mbele ya Mahakama iliyotoa hati hiyo, lakini masharti haya yaliyomo katika ibara hii ndogo itabidi yatumiwe bila kuathiri masharti ya sheria inayotumika hapo mahali alipokamatwa mtu huyo.
(3)Masharti yaliyomo katika ibara hii hayatazuia sheria kuweka utaratibu kwa ajili ya kupeleka nje ya Tanzania hati zilizotolewa na Mahakama za Tanzania Bara au Mahakama za Tanzania Zanzibar.

Sehemu ya Saba – Mahakama Maalum ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 125—128)

125. Mahakama Maalum ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano

Kutakuwa na Mahakama Maalum ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ambayo mamlaka yake, muundo wake na utaratibu wa shughuli zake ni kama ilivyoelezwa katika ibara ya 126, 127 na 128 ya Katiba hii.

126. Mamlaka ya Mahakama Maalum ya Katiba

(1)Kazi pekee ya Mahakama Maalum ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ni kusikiliza shauri lililotolewa mbele yake, kutoa uamuzi wa usuluhishi, juu ya suala lolote linalohusika na tafsiri ya Katiba hii iwapo tafsiri hiyo au utekelezaji wake unabishaniwa kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
(2)Katika kutekeleza kazi yake kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, Mahakama Maalum ya Katiba haitakuwa na mamlaka ya kuchunguza au kubadilisha uamuzi wa Mahakama Kuu au uamuzi wa Mahakama ya Rufani uliotolewa kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 83 ya Katiba hii au uamuzi wa Mahakama ya Rufani uliotolewa kwa mujibu wa ibara ya 117 ya Katiba hii.
(3)Kila uamuzi wa usuluhishi utakaotolewa na Mahakama Maalum ya Katiba kwa mujibu wa ibara hii utakuwa ndio wa mwisho; hakutakuwa na haki ya kukata rufaa popote.

127. Muundo wa Mahakama Maalum ya Katiba

(1)Mahakama Maalum ya Katiba itakuwa na wajumbe ambao nusu ya jumla ya wajumbe wote watateuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano na nusu nyingine ya jumla hiyo watateuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
(2)Mtu anayeweza kuteuliwa kuwa Mjumbe wa Mahakama Maalum ya Katiba ni yule tu ambaye ni Jaji au aliyepata kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au wa Mahakama Kuu ya Zanzibar, au mtu mwenye uwezo na ujuzi wa kazi ya Jaji na anayestahili kuteuliwa kuwa Jaji au Kaimu Jaji kwa mujibu wa sheria inayotumika Tanzania Bara na sheria inayotumika Tanzania Zanzibar, kadri hali itakavyokuwa.
(3)Mtu aweza kuteuliwa kuwa mjumbe wa Mahakama Maalum ya Katiba ama kwa ajili ya kusikiliza shauri moja tu au mashauri mawili au zaidi kama yatatokea. Mjumbe ataendelea kutekeleza madaraka ya kazi yake kama Mjumbe wa Mahakama Maalum ya Katiba mpaka shauri analohusika nalo litakapokwisha au mpaka uteuzi wake utakapofutwa au mpaka atakaposhindwa kutekeleza kazi yake kama Mjumbe kwa sababu ya maradhi au sababu nyingine yoyote.

128. Utaratibu katika vikao vya Mahakama Maalum ya Katiba

(1)Mahakama Maalum ya Katiba itafanya vikao vyake wakati ule tu kunapokuwa na shauri la kusikiliza, na itafanya vikao vyake mahali popote patakapoamuliwa kwa utaratibu utakaotumika kwa ajili ya mashauri yatakayosikilizwa na Mahakama Maalum ya Katiba.
(2)Kiwango cha kila kikao cha Mahakama Maalum ya Katiba ni wajumbe wote, na iwapo mjumbe yeyote atakuwa hayupo au ikiwa kiti cha mjumbe yeyote kitakuwa wazi basi Serikali iliyomteua mjumbe huyo ambaye hayupo au ambaye kiti chake ki wazi itamteua mjumbe mwingine wa kushika mahali pake. Mjumbe wa muda aliyeteuliwa kwa mujibu wa ibara hii ndogo ataendelea kutekeleza kazi katika Mahakama Maalum ya Katiba mpaka mjumbe wa kawaida atakaporejea kazini au mpaka mtu atakapoteuliwa kujaza nafasi iliyo wazi au mpaka shauri litakapokwisha, kutegemea ni lipi kati ya mambo hayo litakalotokea mapema zaidi.
(3)Kila suala linalohitaji uamuzi wa Mahakama Maalum ya Katiba litaamuliwa kwa kufuata kauli ya theluthi mbili ya wajumbe kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya wajumbe kutoka Tanzania Zanzibar.
(4)Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti kuhusu utaratibu wa uchaguzi wa Mwenyekiti wa Mahakama Maalum ya Katiba, utaratibu wa kupeleka shauri mbele ya Mahakama hiyo, utaratibu wa kuendesha shauri katika Mahakama na utaratibu wa kuwasilisha Serikalini uamuzi wa Mahakama Maalum ya Katiba:
Isipokuwa kwamba iwapo shauri lolote litafikishwa mbele ya Mahakama Maalum ya Katiba wakati hakuna sheria yoyote ya aina iliyoelezwa katika ibara hii ndogo, basi shauri litasikilizwa na kuamuliwa kwa kufuata utaratibu utakaowekwa na Mahakama yenyewe kabla ya kuanza kusikiliza shauri, au iwapo Wajumbe wa Mahakama watashindwa kukubaliana juu ya utaratibu huo, basi shauri litasikilizwa na kuamuliwa kwa kufuata utaratibu utakaoamuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Sura ya Sita
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma (Ib. 129—132)

Sehemu ya Kwanza – Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (Ib. 129—131)

129. Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora

(1)Kutakuwa na Tume itakayoitwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, ambayo majukumu yake yatakuwa kama ilivyoelezwa katika ibara ya 130 ya Katiba hii.
(2)Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora itakuwa na Makamishna wafuatao:
(a)Mwenyekiti, ambaye atakuwa ni mtu mwenye sifa ya kuweza kuteuliwa kuwa Jaji;
(b)Makamu Mwenyekiti, ambaye atateuliwa kwa kuzingatia kanuni kwamba endapo Mwenyekiti ni mtu anayetoka upande mmoja wa Jamhuri ya Muungano, yeye atakuwa ni mtu wa kutoka upande mwingine wa Jamhuri ya Muungano;
(c)Makamishna wengine wasiozidi watano watakaoteuliwa kutoka miongoni mwa watu wenye ujuzi, uzoefu na upeo mkubwa katika mambo ya haki za binadamu, sheria, utawala, siasa au mambo ya jamii;
(d)Makamishna Wasaidizi.
(3)Makamishna na Makamishna Wasaidizi wote watateuliwa na Rais baada ya kushauriana na Kamati ya Uteuzi.
(4)Kutakuwa na Kamati ya Uteuzi kwa madhumuni ya ibara hii ambayo itakuwa na wajumbe wafuatao:
(a)Jaji Mkuu wa Mahakama ya Rufani;
(b)Spika wa Bunge;
(c)Jaji Mkuu wa Zanzibar;
(d)Spika wa Baraza la Wawakilishi; na
(e)Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ambaye atakuwa ndiye Katibu wa Kamati hii.
(5)Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wengine wote kila mmoja atashika madaraka yake kwa kipindi cha miaka mitatu na anaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine kimoja tu cha miaka mitatu.
(6)Kwa madhumuni ya kuwakinga Makamishna kutokana na migongano ya kimasilahi, mtu yeyote akiteuliwa kuwa Kamishna wa Tume atalazimika kuacha mara moja madaraka yoyote katika chama chochote cha siasa au madaraka ya aina nyingine yoyote yatakayotajwa kwa ajili hiyo na sheria iliyotungwa na Bunge.
(7)Kamishna au Kamishna Msaidizi wa Tume aweza tu kuondolewa katika madaraka ya kazi yake katika Tume kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi yake, ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote, au kwa sababu ya tabia mbaya inayoathiri maadili ya kazi ya Kamishna.
(8)Tume yaweza kutekeleza shughuli zake bila ya kujali kwamba kuna nafasi iliyo wazi miongoni mwa viti vya wajumbe au kwamba mjumbe mmojawapo hayupo.

130. Majukumu ya Tume na taratibu za utekelezaji

(1)Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora itatekeleza majukumu yafuatayo:
(a)kuhamasisha nchini hifadhi ya haki za binadamu na wajibu kwa jamii kwa mujibu wa Katiba na sheria za nchi;
(b)kufanya shughuli za kupokea malalamiko ya uvunjaji wa haki za binadamu kwa jumla;
(c)kufanya uchunguzi juu ya mambo yanayohusu uvunjaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya Utawala Bora;
(d)kufanya utafiti, kutoa na kueneza nchini elimu kwa umma kuhusu haki za binadamu na Utawala Bora;
(e)kama ikibidi, kufungua mashauri mahakamani ili kuzuia vitendo vya uvunjaji wa haki za binadamu au kurekebisha haki inayotokana na uvunjwaji huo wa haki za binadamu, au ukiukwaji wa misingi ya Utawala Bora;
(f)kuchunguza mwenendo wa mtu yeyote anayehusika au taasisi yoyote inayohusika na masharti ya ibara hii katika utekelezaji wa kawaida wa madaraka ya kazi au majukumu yake au utekelezaji unaokiuka madaraka hayo;
(g)kutoa ushauri kwa Serikali na vyombo vingine vya umma na vya sekta ya binafsi kuhusu haki za binadamu na Utawala Bora;
(h)kuchukua hatua zipasazo kwa ajili ya kukuza na kuendeleza usuluhishi na suluhu miongoni mwa watu na taasisi mbalimbali wanaofika au kufikishwa mbele ya Tume.
(2)Tume itakuwa ni idara inayojitegemea, na bila ya kuathiri masharti mengineyo ya ibara hii, katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii, Tume haitalazimika kufuata maagizo au amri ya mtu yeyote au idara yoyote ya Serikali au maoni ya chama chochote cha siasa au ya taasisi nyingine yoyote ya umma au ya sekta binafsi.
(3)Masharti ya ibara ndogo ya (2) yasihesabiwe kuwa yanamzuia Rais kutoa maagizo au amri kwa Tume, wala hayatoi haki kwa Tume kutofuata maagizo au amri, endapo Rais ataona kuwa, kuhusiana na jambo lolote au hali yoyote, masilahi ya taifa yahitajia hivyo.
(4)Tume itafanya uchunguzi kwa kufuata masharti ya ibara hii na masharti ya sheria iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo, na itafanya uchunguzi juu ya mtu yeyote anayehusika au taasisi yoyote inayohusika kila itakapoagizwa na Rais kufanya uchunguzi, vilevile, isipokuwa kama Rais ameagiza Tume isifanye uchunguzi, Tume yaweza kufanya uchunguzi wakati wowote inapoona inafaa kuchunguza mwenendo wa mtu yeyote anayehusika, au taasisi yoyote inayohusika, na masharti ya ibara hii anayetuhumiwa au inayotuhumiwa kwa kukiuka madaraka ya kazi yake, kutumia vibaya madaraka ya kazi yake au majukumu ya taasisi hiyo au kwa uvunjaji wa haki za binadamu au misingi ya Utawala Bora.
(5)Tume haitakuwa na mamlaka yoyote, ama kwa mujibu wa masharti ya ibara hii au masharti ya sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kwa madhumuni ya Sura hii ya Katiba hii ya kuchunguza uamuzi wa Jaji yeyote, Hakimu yeyote au wa Mahakama iwapo uamuzi huo ameutoa katika kutekeleza madaraka ya kazi yake; vile vile Tume haitakuwa na mamlaka ya kuchunguza uamuzi wowote uliotolewa na chombo chochote chenye asili ya Mahakama kilichoanzishwa kwa mujibu wa sheria iwapo uamuzi huo umetolewa katika kutekeleza mamlaka yake.
(6)Masharti ya ibara hii yatatumika kwa watumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano na wale wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, watumishi na viongozi wa vyama vya siasa wanaoshughulikia mambo ya umma, wajumbe na watumishi wa Tume zote za Serikali ya Jamhuri ya Muungano na za Serikali hizo, mashirika ya umma na vyombo vingine vya binafsi, kama ni kampuni, jumuiya, ushirika, wadhamini au muundo mwingine wowote, kadri itakavyoelezwa katika sheria iliyotungwa na Bunge; lakini masharti haya hayatatumika kwa Rais wala kwa Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar isipokuwa tu kwa kuzingatia masharti ya ibara ya 46 ya Katiba hii au ibara ya 36 ya Katiba ya Zanzibar, ya 1984.

131. Mamlaka ya Tume na utaratibu wa shughuli zake

(1)Bila ya kuathiri masharti mengineyo ya ibara hii, Bunge laweza kutunga sheria kwa mujibu wa masharti ya Sura hii ya Katiba hii kwa ajili ya kuweka masharti kuhusu mamlaka ya Tume, utaratibu wa kuendesha shughuli zake na kuhusu kinga za kisheria watakazokuwa nazo Makamishna na watumishi wa Tume kwa makusudi ya kuwawezesha kutekeleza kazi zao bila ya matatizo ya kisheria.
(2)Tume haitachunguza mambo yafuatayo, kwa madhumuni ya kutekeleza majukumu yake, yaani–
(a)jambo lolote ambalo liko mbele ya Mahakama au chombo kinginecho cha kimahakama;
(b)jambo lolote linalohusu uhusiano au mashirikiano kati ya Serikali na Serikali ya nchi yoyote ya nje au shirika la kimataifa;
(c)jambo linalohusu madaraka ya Rais kutoa msamaha;
(d)jambo jingine lolote lililotajwa na sheria yoyote.
(3)Kila mwaka wa fedha Tume itatayarisha na kuwasilisha kwa Waziri anayesimamia haki za binadamu taarifa kuhusu–
(a)shughuli za Tume katika mwaka uliotangulia;
(b)hali ya utekelezaji wa hifadhi ya haki za binadamu katika Jamhuri ya Muungano,
na Waziri atawasilisha mbele ya Bunge kila taarifa iliyowasilishwa kwake na Tume mapema iwezekanavyo baada ya kuipokea.
(4)Masharti ya ibara ndogo ya (3) hayatahesabiwa kuwa yanaizuia Tume kuwasilisha taarifa nyingine yoyote kwa mtu mwingine au mamlaka nyingine yoyote.

Sehemu ya Pili – Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma (Ib. 132)

132. Sekretarieti ya Maadili

(1)Kutakuwa na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ambayo itakuwa na mamlaka ya kuchunguza tabia na mwenendo wa kiongozi wa umma yeyote kwa madhumuni ya kuhakikisha kwamba masharti ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma yanazingatiwa ipasavyo.
(2)Kwa madhumuni ya ibara hii, maana ya kiongozi wa umma na masharti ya maadili ya viongozi wa umma itabidi ifahamike kwa mujibu wa masharti ya sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma au masharti ya sheria nyingine yoyote iliyotungwa na Bunge kwa kadri masharti hayo yanavyohusika na suala la uongozi na ufafanuzi wake.
(3)Sekretarieti ya Maadili itakuwa na Kamishna wa Maadili na wafanyakazi wengine ambao idadi yao itatajwa na sheria iliyotungwa na Bunge.
(4)Bunge litatunga Sheria itakayoainisha misingi ya Maadili ya Viongozi wa Umma itakayozingatiwa na watu wote wanaoshika nafasi za madaraka zitakazotajwa na Bunge.
(5)Misingi ya Maadili ya Viongozi wa Umma–
(a)itafafanua nafasi za madaraka ambazo watu wenye kushika nafasi hizo watahusika nayo;
(b)itawataka watu wanaoshika nafasi fulani za madaraka kutoa mara kwa mara maelezo rasmi kuhusu mapato, rasilimali na madeni yao;
(c)itapiga marufuku mienendo na tabia inayopelekea kiongozi kuonekana hana uaminifu, anapendelea au si muadilifu au inaelekea kukuza au kuchochea rushwa katika shughuli za umma au anahatarisha maslahi au ustawi wa jamii;
(d)itafafanua adhabu zinazoweza kutolewa kwa kuvunja misingi ya maadili;
(e)itaelekeza taratibu, madaraka na desturi zitakazofuatwa ili kuhakikisha utekelezaji wa maadili;
(f)itaweka masharti mengine yoyote yanayofaa na ambayo ni muhimu kwa madhumuni ya kukuza na kudumisha uaminifu, uwazi, kutopendelea na uadilifu katika shughuli za umma na kwa ajili ya kulinda fedha na mali nyinginezo za umma.
(6)Bunge laweza kwa sheria kuweka masharti ya mtu kufukuzwa au kuondolewa kazini kutokana na kuvunja maadili ya viongozi, bila ya kujali kama kazi hiyo ni ya kuchaguliwa au kuteuliwa.

Sura ya Saba
Masharti kuhusu Mchango wa Serikali na mambo mengineyo ya fedha zinazoingia katika Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 133—144)

Sehemu ya Kwanza – Mchango na Mgawanyo wa Mapato ya Jamhuri ya Muungano (Ib. 133—134)

133. Akaunti ya Fedha ya Pamoja

Serikali ya Jamhuri ya Muungano itatunza akaunti maalum itakayoitwa "Akaunti ya Fedha ya Pamoja", na ambayo itakuwa ni sehemu ya Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, ambamo kutawekwa fedha yote itakayochangwa na Serikali mbili kwa kiasi kitakachoamuliwa na Tume ya Pamoja ya Fedha kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge, kwa madhumuni ya shughuli za Jamhuri ya Muungano kwa Mambo ya Muungano.

134. Tume ya Fedha ya Pamoja

(1)Kutakuwa na Tume ya Pamoja ya Fedha yenye wajumbe wasiozidi saba ambao watateuliwa na Rais kwa mujibu wa ibara hii na masharti ya sheria iliyotungwa na Bunge.
(2)Majukumu ya Tume yatakuwa ni–
(a)kuchambua mapato na matumizi yanayotokana na, au yanayohusu utekelezaji wa Mambo ya Muungano, na kutoa mapendekezo kwa Serikali mbili kuhusu mchango na mgawo wa kila mojawapo ya Serikali hizo;
(b)kuchunguza kwa wakati wote mfumo wa shughuli za fedha wa Jamhuri ya Muungano na pia uhusiano katika mambo ya kifedha kati ya Serikali mbili;
(c)kutekeleza majukumu mengine ambayo Rais ataipatia Tume au kama Rais atakavyoagiza, na kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

Sehemu ya Pili – Mfuko Mkuu wa Hazina na Fedha za Jamhuri ya Muungano (Ib. 135—144)

135. Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano

(1)Fedha zote zitakazopatikana kwa njia mbalimbali kwa ajili ya matumizi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, isipokuwa fedha za aina iliyotajwa katika ibara ndogo ya (2) ya ibara hii, zitawekwa katika mfuko mmoja maalum ambao utaitwa Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali.
(2)Fedha ambazo hazitawekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ni zile zote ambazo zimetajwa na Sheria kwamba zitumike kwa shughuli maalum au ziwekwe katika mfuko mwingine kwa ajili ya matumizi maalum.

136. Masharti ya kutoa fedha za matumizi kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali

(1)Fedha hazitatolewa kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali kwa ajili ya matumizi ila kwa mujibu wa masharti yafuatayo–
(a)fedha hizo ziwe kwa ajili ya matumizi ambayo yameidhinishwa yatokane na fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali na idhini hiyo iwe imetolewa na Katiba hii au sheria yingine yoyote;
(b)fedha hizo ziwe kwa ajili ya matumizi ambayo yameidhinishwa ama na sheria ya Matumizi ya Serikali iliyotungwa mahususi na Bunge au sheria iliyotungwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 140 ya Katiba hii.
(2)Fedha zilizomo katika mfuko maalum wowote wa Serikali, ukiachilia mbali Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali, hazitatolewa kutoka mfuko huo kwa ajili ya matumizi ila mpaka matumizi hayo yawe yameidhinishwa na sheria.
(3)Fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali hazitatolewa kutoka Mfuko huo kwa ajili ya matumizi ila mpaka matumizi hayo yawe yameidhinishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na pia kwa sharti kwamba fedha hizo ziwe zimetolewa kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa ajili hiyo kwa mujibu wa sheria iliyotungwa na Bunge.

137. Utaratibu wa kuidhinisha matumizi ya fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali

(1)Rais atatoa maagizo kwa watu wanaohusika kwamba watengeneze na kuwasilisha kwenye Bunge katika kila mwaka wa fedha wa Serikali, Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya kipindi cha mwaka wa fedha unaofuata.
(2)Baada ya Bunge kuyakubali Makadirio ya Matumizi (mbali na matumizi ambayo yameidhinishwa ama na Katiba hii au sheria nyingine yoyote kuwa yatokane na fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali) kutawasilishwa kwenye Bunge Muswada ambao utaitwa Muswada wa sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali, kwa ajili ya kuidhinisha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali, na fedha hizo zitatolewa kulipa gharama za shughuli mbalimbali za Serikali zinazohusika na Makadirio hayo.
(3)Ikiwa katika mwaka wa fedha wowote inaonekana kwamba–
(a)fedha za matumizi zilizoidhinishwa na sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali kwa ajili ya shughuli fulani hazitoshi au kwamba imekuwa lazima kulipa gharama za shughuli ambayo haikupangiwa fedha za matumizi kwa mujibu wa sheria; au
(b)kuna fedha ambazo zimetumiwa kwa ajili ya shughuli fulani kwa kiasi kinachozidi kiwango cha matumizi yaliyoidhinishwa na sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali kuhusu shughuli hiyo au kwamba fedha zimetumiwa kulipia gharama za shughuli ambayo haikupangiwa fedha za matumizi kwa mujibu wa Sheria, kutawasilishwa kwenye Bunge Makadirio ya Matumizi ya Nyongeza au, kadri itakavyokuwa, Maelezo ya Matumizi ya Ziada, na baada ya Bunge kuyakubali hayo Makadirio ya Matumizi ya Nyongeza au Maelezo ya Matumizi ya Ziada, kutawasilishwa kwenye Bunge Muswada wa Sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali kwa ajili ya kuidhinisha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali, na fedha hizo zitatumiwa kulipia gharama za shughuli zinazohusika na hayo Makadirio au Maelezo.

138. Masharti ya kutoza kodi

(1)Hakuna Kodi ya aina yoyote itakayotozwa isipokuwa kwa mujibu wa Sheria iliyotungwa na Bunge au kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa kisheria na uliotiliwa nguvu ya kisheria na sheria iliyotungwa na Bunge.
(2)Masharti yaliyomo katika ibara ndogo ya (1) ya ibara hii hayatalizuia Baraza la Mapinduzi la Zanzibar kutumia mamlaka yake ya kutoza kodi ya aina yoyote kwa mujibu wa madaraka ya Baraza hilo.

139. Utaratibu wa kuidhinisha matumizi ya fedha kabla ya Sheria za Matumizi kuanza kutumika

(1)Bunge laweza kutunga sheria kwa ajili ya kuweka masharti ya kuidhinisha matumizi ya fedha kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali kwa kufuata utaratibu ulioelezwa katika ibara ndogo ya (2) ya ibara hii.
(2)Iwapo mwaka wa fedha wa Serikali umeanza na Sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali inayohusika na mwaka huo haijaanza kutumika, basi Rais aweza kuidhinisha fedha itolewe kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali kwa ajili ya kulipia gharama za lazima za shughuli za Serikali, na fedha hizo zitatumiwa mpaka ipite miezi minne tangu mwanzo wa mwaka wa fedha au mpaka Sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali itakapoanza kutumika, kutegemea ni lipi kati ya mambo hayo litakalotokea mapema zaidi.

140. Mfuko wa Matumizi ya dharura

(1)Bunge laweza kutunga Sheria kwa ajili ya kuweka masharti kuhusu mambo yafuatayo–
(a)kuanzisha Mfuko wa Matumizi ya Dharura na kumwezesha Rais au Waziri aliyeteuliwa na Rais kwa ajili hiyo kuazima fedha kutoka mfuko huo kulipia gharama za jambo la haraka na la dharura ambalo halikutazamiwa kutokea na ambalo halikupangiwa fedha zozote za matumizi; na
(b)kumwezesha Rais au Waziri aliyeteuliwa na Rais kwa ajili hiyo kutumia fedha zilizotengwa mahsusi kwa ajili ya shughuli fulani kulipia gharama za jambo la haraka na la dharura kama ilivyoelezwa katika aya ya (a) ya ibara hii ndogo.
(2)Iwapo fedha zimeazimwa kutoka Mfuko wa Matumizi ya Dharura au fedha zilitengwa mahsusi kwa ajili ya shughuli fulani zimetumiwa kulipia gharama za jambo la haraka na la dharura, basi kutawasilishwa kwenye Bunge Makadirio ya Matumizi ya Nyongeza, na baada ya Bunge kuyakubali Makadirio hayo Muswada wa Sheria ya Matumizi ya Fedha za Serikali utakaowasilishwa kwenye Bunge kwa ajili ya kuidhinisha Matumizi hayo ya nyongeza utahakikisha kwamba fedha zozote zilizoazimwa kutoka Mfuko wa Matumizi ya Dharura zitarudishwa kwenye Mfuko huo kutokana na fedha za matumizi yatakayoidhinishwa na Muswada huo.

141. Deni la Taifa

(1)Deni la Taifa litadhaminiwa na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
(2)Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa ibara hii deni la Taifa maana yake ni deni lenyewe na pia faida inayolipwa juu ya deni hilo, fedha zinazowekwa akiba kwa ajili ya kulipa deni pole pole na gharama zote zinazoambatana na usimamizi wa deni hilo.

142. Mishahara ya watumishi fulani wa Umma kudhaminiwa na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali

(1)Watumishi wa Umma wanaohusika na masharti ya ibara hii watalipwa mishahara na posho kama itakavyoelezwa na Sheria iliyotungwa na Bunge.
(2)Fedha za malipo ya mishahara na posho za watumishi wa Umma wanaohusika na masharti ya ibara hii pamoja na fedha za malipo ya uzeeni na kiinua mgongo kwa wale wanaostahili malipo hayo miongoni mwa watumishi hao zitatolewa kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali.
(3)Mshahara anaolipwa mtumishi wa Umma anayehusika na masharti ya ibara hii pamoja na masharti yake ya kazi havitabadilishwa, baada ya mtumishi huyo kuteuliwa, kwa jinsi ambayo itapunguza masilahi ya mtumishi huyo, lakini maelezo haya hayahusiki na posho anayolipwa mtumishi huyo.
(4)Iwapo mtumishi wa Umma anayehusika na masharti ya ibara hii ana hiari ya kuchagua kima cha mshahara au aina ya masharti ya kazi, basi kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya ibara ndogo ya (3) ya ibara hii, mshahara wa kima hicho atakachochagua na aina hiyo ya masharti ya kazi atakayochagua vitahesabiwa kuwa vina masilahi zaidi kwake kuliko kima cha mshahara kingine chochote angalichoweza kuchagua au aina ya masharti ya kazi nyingine yoyote angaliyoweza kuchagua.
(5)Masharti ya ibara hii yatatumika kwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano, Mwenyekiti na kila Mjumbe wa Haki za Binadamu na Utawala Bora na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Jamhuri ya Muungano.

143. Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano

(1)Kutakuwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali wa Jamhuri ya Muungano.
(2)Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu atakuwa na jukumu juu ya mambo yafuatayo:
(a)kuhakikisha kwamba fedha zozote zinazokusudiwa kutolewa kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali matumizi yake yameidhinishwa na kwamba zitatolewa kwa mujibu wa masharti ya ibara ya 136 ya Katiba hii, na iwapo atatosheka kwamba masharti hayo yatatekelezwa ipasavyo, basi ataidhinisha fedha hizo zitolewe;
(b)kuhakikisha kwamba fedha zote ambazo matumizi yake yameidhinishwa yatokane na fedha zilizomo katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali au fedha ambazo matumizi yake yameidhinishwa na Sheria iliyotungwa na Bunge, na ambazo zimetumika, zimetumiwa kwa ajili ya shughuli zilizohusika na matumizi ya fedha hizo na kwamba matumizi hayo yamefanywa kwa kufuata idhini iliyotolewa kuhusu matumizi hayo; na
(c)angalau mara moja kila mwaka kufanya ukaguzi na kutoa taarifa juu ya ukaguzi wa hesabu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano, hesabu zinazosimamiwa na watumishi wote wa Umma wa Jamhuri ya Muungano na hesabu za Mahakama zote za Jamhuri ya Muungano na hesabu zinazosimamiwa na Katibu wa Bunge.
(3)Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu na kila mtumishi wa Umma aliyeruhusiwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu atakuwa na haki ya kuchunguza vitabu, kumbukumbu, hati nyinginezo zote zinazohusika na hesabu za aina yoyote iliyotajwa katika ibara ndogo ya (2) ya ibara hii.
(4)Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu atawasilisha kwa Rais kila taarifa atakayotoa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2) ya ibara hii. Baada ya kupokea taarifa hiyo Rais atawaagiza watu wanaohusika wawasilishe taarifa hiyo kwenye kikao cha kwanza cha Bunge kitakachofanyika baada ya Rais kupokea taarifa hiyo na itabidi iwasilishwe katika kikao hicho kabla ya kupita siku saba tangu siku ile kilipoanza kikao hicho. Iwapo Rais hatachukua hatua za kuwasilisha taarifa hiyo kwa Spika wa Bunge (au Naibu wa Spika ikiwa kiti cha Spika ki wazi wakati huo au ikiwa kwa sababu yoyote Spika hawezi kutekeleza shughuli za kazi yake) ambaye atawasilisha taarifa hiyo kwenye Bunge.
(5)Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu atakuwa pia na jukumu la kutekeleza kazi na shughuli nyingine, na atakuwa na madaraka mengine ya namna mbalimbali, kama itakavyoelezwa na Sheria, kuhusu hesabu za Serikali ya Jamhuri ya Muungano au hesabu za vyombo vya Umma au hesabu za mashirika.
(6)Katika kutekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2), (3) na (4) ya ibara hii, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu hatalazimika kufuata amri au maagizo ya mtu mwingine yeyote au idara yoyote ya Serikali, lakini maelezo hayo ya ibara hii ndogo hayataizuia Mahakama nayo kutumia madaraka yake kwa ajili ya kuchunguza kama Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu ametekeleza madaraka yake kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii au sivyo.

144. Kumwondoa kazini Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali

(1)Bila ya kuathiri masharti mengine yaliyomo katika ibara hii, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu wa Jamhuri ya Muungano atalazimika kuacha kazi yake atakapotimiza umri wa miaka sitini au umri mwingine wowote utakaotajwa na sheria iliyotungwa na Bunge.
(2)Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu aweza tu kuondolewa katika madaraka ya kazi yake kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi zake (ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote) au kwa sababu ya tabia mbaya, au kwa kuvunja masharti ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, na hataweza kuondolewa kazini ila kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (4) ya ibara hii.
(3)Iwapo Rais anaona kwamba suala la kumwondoa kazini Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu kwa mujibu wa masharti ya ibara hii lahitaji kuchunguzwa, basi katika hali hiyo mambo yatakuwa ifuatavyo:
(a)Rais atateua Tume Maalum ambayo itakuwa na Mwenyekiti na Wajumbe wengine wasiopungua wawili. Huyo Mwenyekiti na angalau nusu ya wajumbe wengine wa Tume hiyo itabidi wawe watu ambao ni Majaji au watu waliopata kuwa Majaji wa Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufani katika nchi yoyote iliyomo kwenye Jumuiya ya Madola;
(b)Tume hiyo itachunguza shauri lote halafu itatoa taarifa kwa Rais kuhusu maelezo ya shauri lote na itamshauri Rais kama huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu aondolewe kazini kwa mujibu wa masharti ya ibara hii kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya.
(4)Ikiwa Tume iliyoteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (3) itamshauri Rais kwamba huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu aondolewe kazini kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya, basi Rais atamwondoa kazini.
(5)Ikiwa suala la kumwondoa kazini Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu limepelekwa kwenye Tume kwa ajili ya uchunguzi kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, Rais aweza kumsimamisha kazi huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu, na Rais aweza wakati wowote kufuta uamuzi huo wa kumsimamisha kazi, na kwa hali yoyote uamuzi huo utabatilika ikiwa Tume itamshauri Rais kwamba huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu asiondolewe kazini.
(6)Mtu ambaye ni Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu au aliyepata kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu hawezi kuteuliwa kushika au kushikilia madaraka ya kazi nyingine yoyote katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano.
(7)Masharti ya ibara hii hayatatumika kwa mtu yeyote aliyeteuliwa kuwa Kaimu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu.

Sura ya Nane
Madaraka ya Umma (Ib. 145—146)

145. Serikali za Mitaa

(1)Kutakuwa na vyombo vya Serikali za Mitaa katika kila mkoa, wilaya, mji na kijiji, katika Jamhuri ya Muungano, ambavyo vitakuwa vya aina na majina yatakayowekwa na sheria iliyotungwa na Bunge au na Baraza la Wawakilishi.
(2)Bunge au Baraza la Wawakilishi, kadri itakavyokuwa, litatunga sheria itakayofafanua utaratibu wa kuanzisha vyombo vya Serikali za Mitaa, miundo na wajumbe wake, njia za mapato na utaratibu wa utekelezaji wa shughuli za vyombo hivyo.

146. Kazi za Serikali za Mitaa

(1)Madhumuni ya kuwapo Serikali za Mitaa ni kupeleka madaraka kwa wananchi. Vyombo vya Serikali za Mitaa vitakuwa na haki na mamlaka ya kushiriki na kuwashirikisha wananchi katika mipango na shughuli za utekelezaji wa maendeleo katika sehemu zao na nchini kote kwa jumla.
(2)Bila ya kuathiri maelezo ya jumla yaliyomo katika ibara ndogo ya (1) ya ibara hii, kila chombo cha Serikali za Mitaa, kwa kuzingatia masharti ya sheria iliyokianzisha, kitahusika na shughuli zifuatazo–
(a)kutekeleza kazi za Serikali za Mitaa katika eneo lake;
(b)kuhakikisha utekelezaji wa sheria na ulinzi wa wananchi; na
(c)kuimarisha demokrasia katika eneo lake na kuitumia demokrasia kuharakisha maendeleo ya wananchi.

Sura ya Tisa
Majeshi ya ulinzi (Ib. 147—148)

147. Marufuku kuunda majeshi ya ulinzi yasiyo majeshi ya Ulinzi ya Umma

(1)Ni marufuku kwa mtu yeyote au shirika lolote au kikundi chochote cha watu, isipokuwa Serikali, kuunda au kuweka Tanzania Jeshi la aina yoyote.
(2)Serikali ya Jamhuri ya Muungano yaweza, kwa mujibu wa Sheria, kuunda au kuweka Tanzania majeshi ya aina mbalimbali kwa ajili ya ulinzi na usalama wa nchi na wananchi wa Tanzania.
(3)Itakuwa ni marufuku kwa mwanajeshi yeyote kujiunga na chama chochote cha siasa, isipokuwa tu kwamba atakuwa na haki ya kupiga kura iliyotajwa katika ibara ya 5 ya Katiba hii.
(4)Kwa madhumuni ya ibara hii, "mwanajeshi" maana yake ni askari aliyeajiriwa kwa masharti ya muda au ya kudumu katika Jeshi la Ulinzi, Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza au Jeshi la Kujenga Taifa.

148. Madaraka ya Amiri Jeshi Mkuu

(1)Bila ya kuathiri masharti yatakayowekwa na Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge, miongoni mwa madaraka ya Rais akiwa kama Amiri Jeshi Mkuu ni kuyaamuru majeshi ya nchi yatende mambo yanayohusika na vita vya ulinzi wa Jamhuri ya Muungano, mambo ya kuokoa maisha na mali ya watu katika hali ya hatari na mambo mengineyo ambayo Amiri Jeshi Mkuu ataona yahitajika, na kwa ajili hiyo Amiri Jeshi Mkuu aweza kuyaamuru hayo majeshi yatende mambo hayo ama ndani au nje ya Tanzania.
(2)Bila ya kuathiri masharti yatakayowekwa na Sheria iliyotungwa na Bunge, madaraka juu ya mambo yafuatayo yatakuwa mikononi mwa Amiri Jeshi Mkuu, yaani–
(a)madaraka ya kuwateua viongozi katika Majeshi ya Ulinzi ya Jamhuri ya Muungano;
(b)madaraka ya kuwateua watu watakaojiunga na Majeshi ya Ulinzi na madaraka ya kuwaondoa jeshini wanajeshi;
(c)madaraka ya kuwateua wanajeshi watakaoongoza vikosi mbalimbali vya Majeshi ya Ulinzi; na
(d)madaraka ya kumwamuru mwanajeshi yeyote asitumie madaraka yoyote aliyokabidhiwa na ambayo yanaambatana na kuwa kwake mwanajeshi.
(3)Jambo lolote atakalotenda mwanajeshi yeyote kinyume cha amri iliyotolewa na Amiri Jeshi Mkuu kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (1) na (2) ya ibara hii litakuwa batilifu.

Sura ya Kumi
Mengineyo (Ib. 149—152)

149. Maelezo ya mambo yanayohusika na madaraka ya kazi mbalimbali zilizoanzishwa na Katiba hii

(1)Mtu yeyote mwenye dhamana ya kazi yoyote iliyoanzishwa na Katiba hii (pamoja na kazi ya Waziri, Naibu Waziri au Mbunge, isipokuwa Mbunge ambaye ni Mbunge kwa mujibu wa madaraka ya kazi yake), aweza kujiuzulu kwa kutoa taarifa iliyoandikwa na kutiliwa sahihi kwa mkono wake, kwa kufuata masharti yafuatayo:
(a)iwapo mtu huyo aliteuliwa au alichaguliwa na mtu mmoja, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu atawasilisha kwa mtu huyo aliyemteua au kumchagua, au iwapo aliteuliwa au alichaguliwa na kikao cha watu, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwenye kikao hicho;
(b)iwapo mtu huyo ni Rais, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa Spika;
(c)iwapo mtu huyo ni Spika au Naibu Spika wa Bunge, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwenye Bunge; na
(d)iwapo mtu huyo ni Mbunge, basi taarifa hiyo ya kujiuzulu ataiwasilisha kwa Spika.
(2)Mtu aliyetoa taarifa ya kujiuzulu kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (1) ya ibara hii, atahesabiwa kuwa amejiuzulu tangu siku ile ambayo taarifa yake ya kujiuzulu itakapopokelewa na mtu anayehusika au kikao kinachohusika au itakapopokelewa na mtu yeyote aliyeruhusiwa kuipokea taarifa hiyo na mtu anayehusika au kikao kinachohusika, lakini kama taarifa hiyo ya kujiuzulu imeeleza kwamba mtu huyo atajiuzulu tangu siku nyingine baada ya taarifa hiyo kupokelewa na mtu anayehusika au kikao kinachohusika, basi mtu huyo atahesabiwa kuwa amejiuzulu tangu siku hiyo nyingine ya baadaye.
(3)Iwapo mtu yeyote mwenye dhamana ya kazi yoyote iliyoanzishwa na Katiba hii (pamoja na kazi ya Waziri, Naibu Waziri au Mbunge, isipokuwa Mbunge ambaye ni Mbunge kwa mujibu wa madaraka ya kazi yake) amejiuzulu, basi ikiwa anazo sifa zote zinazohitajika na kwa kila hali anastahili, aweza kuteuliwa au kuchaguliwa tena kushika madaraka ya kazi hiyo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii.
(4)Masharti yaliyomo katika ibara ndogo ya (3) ya ibara hii hayatamzuia mtu ambaye ni Rais kuchaguliwa tena kuwa Rais wakati bado ameshika madaraka ya kazi ya Rais.

150. Maelezo kuhusu utaratibu wa kukabidhi madaraka ya kazi katika Utumishi wa Umma

(1)Kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya Katiba hii kuhusu utaratibu wa kukabidhi madaraka ya kazi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano, ifahamike kuwa mtu yeyote mwenye mamlaka, kwa mujibu wa Katiba hii, ya kumteua au kumchagua mtu mwingine kushika madaraka ya kazi fulani anao pia uwezo wa kumteua au kumchagua Kaimu au mtu ambaye atashikilia kwa muda na kutekeleza madaraka ya kazi hiyo:Isipokuwa kwamba maelezo hayo hayatatumika kwa madaraka ya kazi ya Waziri, Naibu Waziri, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu, Mjumbe wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora au Mjumbe wa Tume ya Uchaguzi.
(2)Kanuni zifuatazo zitatumika pia kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya Katiba hii kuhusu utaratibu wa kukabidhiana madaraka ya kazi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano, yaani–
(a)iwapo kuna mtu mwenye madaraka ya kazi fulani aliyokabidhiwa kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii na mtu huyo yupo likizoni na wakati huo huo anangojea kuacha kazi hiyo, basi anaweza kuteuliwa mtu mwingine na kukabidhiwa madaraka ya kazi hiyo, bila ya kujali kuwapo kwa yule mtu anayengojea kuacha kazi hiyo;
(b)iwapo kuna watu wawili au zaidi ambao kwa wakati mmoja wote wanashika madaraka ya kazi fulani kutokana na uteuzi wao uliofanywa kwa mujibu wa Kanuni iliyoelezwa katika aya ya (a) ya ibara hii ndogo, basi katika hali hiyo kukitokea haja ya kutekeleza shughuli yoyote inayohusika na madaraka ya kazi hiyo yule mtu wa mwisho kuteuliwa ndiye atakayehesabiwa kuwa mtu pekee mwenye dhamana ya kazi hiyo;
(c)iwapo mtu ameteuliwa, kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii, kuwa Kaimu au kushikilia madaraka ya kazi fulani wakati mtu maalum aliyeteuliwa kushika madaraka ya kazi hiyo anashindwa kutekeleza shughuli zinazohusika na kazi hiyo, basi haitaruhusiwa kufanya uchunguzi wowote au kutoa hoja yoyote juu ya uteuzi wa huyo Kaimu eti kwa sababu kwamba huyo mtu maalum aliyeteuliwa kushika madaraka ya kazi hiyo anashindwa kutekeleza shughuli zinazohusika na kazi hiyo.

151. Ufafanuzi

(1)Katika Katiba hii, ila iwapo maelezo yahitaji vinginevyo–"amri ya jeshi" maana yake ni sheria au amri iliyotolewa kwa mujibu wa sheria, ya kusimamia nidhamu katika jeshi;"askari" likitumika kuhusiana na jeshi lolote maana yake ni pamoja na askari yeyote ambaye kwa mujibu wa amri ya jeshi hilo ni mtu anayewajibika kinidhamu;"Baraza la Wawakilishi" maana yake ni Baraza la Wawakilishi la Zanzibar lililotajwa katika ibara ya 106 ya Katiba hii na linalotekeleza madaraka yake kwa mujibu wa Katiba hii na Katiba ya Zanzibar, 1984;"Bunge" maana yake ni Bunge la Jamhuri ya Muungano lililotajwa katika ibara ya 62 ya Katiba hii;"Chama cha Siasa" maana yake ni chama cha siasa kilichoandikishwa kikamilifu kwa mujibu wa Sheria ya Vyama vya Siasa ya mwaka 1992; 55Sura ya 258"Idara ya Mahakama" maana yake ni kama ilivyofafanuliwa katika ibara ndogo ya (1) ya ibara ya 116 ya Katiba hii;"Idara ya Mahakama ya Zanzibar" maana yake ni Idara ya Mahakama inayojumlisha mahakama zote ambazo ziko katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar;"Jaji Mkuu" maana yake ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Rufani aliyetajwa katika ibara ndogo ya (1) ya ibara ya 118 ya Katiba hii ambaye ameteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (2) ya ibara hiyo ya 118 au iwapo Jaji Mkuu hayupo au anashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, Kaimu Jaji Mkuu aliyeteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (4) ya ibara hiyo ya 118 ya Katiba hii, na kama Kaimu Jaji Mkuu naye hayupo au anashindwa kutekeleza kazi za Jaji Mkuu, Jaji wa Mahakama ya Rufani aliyepo kazini kwa wakati huo na ambaye yuko kwenye daraja la juu zaidi la madaraka kupita Majaji wote wa Rufani waliopo;"Jaji Mkuu wa Zanzibar" maana yake ni Jaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Zanzibar ambaye, kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar 1984, ndiye Mkuu wa Idara ya Mahakama ya Zanzibar;"Jeshi" maana yake ni jeshi lolote kati ya majeshi ya ulinzi na ni pamoja na jeshi lolote jingine lilioundwa na Katiba hii au kwa mujibu wa sheria na linalotawaliwa kwa amri ya jeshi;"Jumuiya ya Madola" maana yake ni jumuiya ambayo wanachama wake ni Jamhuri ya Muungano, Uingereza na kila nchi ambayo iliwahi kutawaliwa na Uingereza;"kiapo" maana yake itabidi ifahamike kwa maana ya kawaida ya neno hilo na ni pamoja na tamko rasmi la namna yoyote linaloruhusiwa kisheria kutumiwa badala ya kiapo;"kiapo cha uaminifu" maana yake ni kiapo cha kuwa mwaminifu kwa Nchi na kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano;"Maadili ya Kazi ya Jaji" maana yake ni masharti ya kimaadili yanayoongoza mwenendo wa watu wafanyao kazi ya Jaji au ya Hakimu;"madaraka ya kazi katika utumishi wa Umma Jamhuri ya Muungano" maana yake itabidi ifahamike kwa mujibu wa maana ya kawaida na maneno hayo na ni pamoja na utumishi katika Majeshi ya Ulinzi ya Jamhuri ya Muungano na katika Jeshi la Polisi au jeshi linginelo lilioundwa kwa mujibu wa Sheria;"mahakama" maana yake ni mahakama yoyote yenye mamlaka katika Jamhuri ya Muungano isipokuwa mahakama iliyoundwa kwa amri ya jeshi; lakini kwa ajili ya ibara ya 13, ya 14 na ya 15 za Katiba hii, itakuwa ni pamoja na mahakama iliyoundwa kwa amri ya jeshi;"Mahakama Kuu" maana yake ni Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano au Mahakama Kuu ya Zanzibar;"Mambo ya Muungano" maana yake ni mambo yote ya umma ambayo yametajwa na ibara ya 4 ya Katiba hii kuwa ni Mambo ya Muungano;"Mamlaka ya Nchi" ni pamoja na Serikali na Bunge la Jamhuri ya Muungano, pamoja na Serikali na Baraza la Wawakilishi la Zanzibar;"Mwanasheria Mkuu" maana yake ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano aliyetajwa katika ibara ya 59;"Serikali" maana yake ni pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar au Halmashauri ya Wilaya au ya Mji, na pia mtu yeyote anayetekeleza madaraka au mamlaka yoyote kwa niaba ya Serikali au Halmashauri;"Serikali za Mitaa" maana yake ni vyombo vya kiserikali vilivyoundwa kwa mujibu wa ibara ya 145 ya Katiba hii kwa madhumuni ya kutekeleza madaraka ya umma;"Tanzania Bara" maana yake ni eneo lote la Jamhuri ya Muungnao ambalo zamani lilikuwa eneo la Jamhuri ya Tanganyika;"Tanzania Zanzibar" maana yake ni eneo lote la Jamhuri ya Muungano ambalo zamani lilikuwa eneo la Jamhuri ya Watu wa Zanzibar na ambalo kabla ya Sheria hii kutungwa liliitwa Tanzania Visiwani;"Uchaguzi Mkuu" au "uchaguzi unaofanywa na wananchi" maana yake ni uchaguzi wa Rais na uchaguzi wa Wabunge wanaowakilisha wilaya za uchaguzi unaofanywa baada ya Bunge kuvunjwa;"Ujamaa" au "Ujamaa na Kujitegemea" maana yake ni misingi ya maisha ya jamii ya kujenga Taifa linalozingatia demokrasia, kujitegemea, uhuru, haki, usawa, udugu na umoja wa wananchi wa Jamhuri ya Muungano;"Waziri" maana yake ni Mbunge aliyekabidhiwa madaraka ya kazi ya Waziri, isipokuwa Naibu Waziri, na maana hiyo itatumika pia kwa Makamu wote wa Rais;"Zanzibar" maana yake ni sawa na maana ya Tanzania Zanzibar.
(2)Kanuni zifuatazo zitatumika kwa madhumuni ya ufafanuzi wa masharti ya Katiba, yaani–
(a)kila yanapotajwa madaraka ya Rais, ifahamike kuwa madaraka yanayohusika ni pamoja na mamlaka ya kutekeleza shughuli na kazi mbalimbali na vile vile wajibu wa kutekeleza shughuli na kazi mbali mbali kama Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, na pia mamlaka mengine kama hayo au wajibu mwingine kama huo ikiwa imeelezwa katika Katiba hii au katika sheria nyingine yoyote kwamba mamlaka hayo mengine ni ya Rais au kwamba wajibu huo mwingine ni wa Rais;
(b)kila yanapotajwa madaraka ya kazi katika utumishi wa Umma, ifahamike kuwa kazi inayohusika ni kazi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano isipokuwa kama imeelezwa vingine, na kila inapotajwa idara ya Serikali ifahamike kuwa idara inayohusika ni idara ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano, isipokuwa kama imeelezwa vingine;
(c)iwapo kwa mujibu wa masharti ya Katiba hii kuna jambo lolote linalotakiwa litekelezwe au lishughulikiwe na chama chochote cha siasa, basi, jambo hilo litatekelezwa au litashughulikiwa na chama hicho kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa na chama hicho kwa ajili hiyo, na pia kwa kuzingatia masharti ya Katiba hii au sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kwa ajili hiyo;
(d)kwa madhumuni ya Katiba hii, mtu hatahesabiwa kuwa ana madaraka ya kazi katika utumishi wa Umma wa Jamhuri ya Muungano kwa sababu tu kwamba anapokea malipo ya uzeeni au malipo mengine ya aina hiyo kwa ajili ya utumishi wake wa zamani katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano au katika Serikali yoyote ya zamani ya Tanzania Bara au katika Jeshi la Ulinzi au la Polisi la Serikali ya Jamhuri ya Muungano au Serikali ya zamani ya Tanzania Bara au ya Tanzania Zanzibar;
(e)katika Katiba hii, ila iwapo maelezo yahitaji vingine, kila anapotajwa mtu mwenye dhamana ya kazi fulani kwa kutaja madaraka ya kazi yake, ifahamike kuwa mtu anayehusika ni pamoja na mtu yeyote ambaye ni Kaimu au aliyeteuliwa kwa njia ya halali kushikilia dhamana ya kazi hiyo;
(f)katika Katiba hii, kila yalipotajwa mamlaka ya kumwondoa mtu katika madaraka ya kazi katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, ifahamike kuwa mamlaka yanayohusika ni pamoja na mamlaka yaliyotolewa kwa mujibu wa masharti ya Sheria yoyote yanayomtaka mtu huyo au yanayomruhusu mtu huyo kustaafu:Isipokuwa kwamba maelezo ya Kanuni hii yasifahamike kuwa yanampa mtu yeyote mamlaka ya kumtaka Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji wa Mahakama Kuu au Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu astaafu;
(g)katika Katiba hii, kila ilipotajwa sheria ambayo inabadilisha au kufuta sheria nyingine, ifahamike kuwa sheria inayohusika ni pamoja na sheria ambayo inarekebisha sheria hiyo nyingine au ambayo inaendeleza kutumika kwa hiyo sheria nyingine, ama bila mabadiliko au baada ya kubadilishwa au kurekebishwa, au sheria ambayo inaweka masharti mapya katika sheria nyingine.

152. Jina Kamili la Katiba, tarehe ya kuanza kutumika na matumizi ya Katiba hii

(1)Jina kamili la Katiba hii ni Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya mwaka 1977.
(2)[Imefutwa na Sura ya 4.]
(3)Katiba hii itatumika Tanzania Bara na vile vile Tanzania Zanzibar.

Nyongeza ya Kwanza (Imetajwa katika ibara ya 4)

Mambo ya Muungano

1.Katiba ya Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
2.Mambo ya Nchi za Nje.
3.Ulinzi na Usalama.
4.Polisi.
5.Mamlaka juu ya mambo yanayohusika na hali ya hatari.
6.Uraia.
7.Uhamiaji.
8.Mikopo na Biashara ya Nchi za Nje.
9.Utumishi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
10.Kodi ya Mapato inayolipwa na watu binafsi na mashirika, ushuru wa forodha na ushuru wa bidhaa zinazotengenezwa nchini Tanzania unaosimamiwa na Idara ya Forodha.
11.Bandari, mambo yanayohusika na usafiri wa anga, posta na simu.
12.Mambo yote yanayohusika na sarafu na fedha kwa ajili ya malipo yote halali (pamoja na noti); mabenki (pamoja na mabenki ya kuweka akiba) na shughuli zote za mabenki; fedha za kigeni na usimamizi juu ya mambo yanayohusika na fedha za kigeni.
13.Leseni ya viwanda na takwimu.
14.Elimu ya juu.
15.Maliasili ya mafuta, pamoja na mafuta yasiyochujwa ya motokaa na mafuta ya aina ya petroli na aina nyinginezo za mafuta au bidhaa, na gesi asilia.
16.Baraza la Taifa la Mitihani la Tanzania na mambo yote yanayohusika na kazi za Baraza hilo.
17.Usafiri na usafirishaji wa anga.
18.Utafiti.
19.Utafiti wa Hali ya Hewa.
20.Takwimu.
21.Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano.
22.Uandikishaji wa vyama vya siasa na mambo mengine yanayohusiana navyo.

Nyongeza ya Pili (Sheria ambazo mabadiliko yake yahitaji kuungwa mkono na theluthi mbili ya Wabunge wote)

Orodha ya Kwanza (Imetajwa katika ibara 98(1)(a))

Sura ya 500, R.L. Sheria ya Kultiibitisha TanganyikaKuwa Jamhuri ya Mwaka 1962
Sura ya 298, Sheria ya Utumishi SerikaliniIbara ya 22, 23 na 24.
Sura ya 237, Sheria ya Utumishi katika Idara ya MahakamaIbara ya 22, 23 na 24
Sura ya 357, Sheria ya UraiaSheria yote.
Kiambatisho B kwa Sura ya 2;
Sheria ya Kuthibitisha Mapatano ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, ya mwaka 1964Sheria yoyote.

Orodha ya Pili (Imetajwa katika ibara 98(1)(b))

Mambo ambayo mabadiliko yake yahitaji kuungwa mkono na theluthi mbili ya Wabunge wote kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya Wabunge wote kutoka Tanzania Visiwani.
1.Kuwapo kwa Jamhuri ya Muungano.
2.Kuwapo kwa Ofisi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano.
3.Madaraka ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.
4.Kuwapo kwa Bunge la Jamhuri ya Muungano.
5.Madaraka ya Serikali ya Zanzibar.
6.Mahakama Kuu ya Zanzibar.
7.Orodha ya Mambo ya Muungano.
8.Idadi ya Wabunge kutoka Zanzibar.
▲ To the top

History of this document

31 July 2002 this version
Consolidation
26 April 1977
Commenced

Cited documents 0

Documents citing this one 861

Judgment 833
1. Attorney General vs Tanzania Ports Authority & Another (Civil Application No. 87 of 2016) [2016] TZCA 897 (12 October 2016) 114 citations
2. Mohamed Enterprises T. Limited vs Masoud Mohamed Nasser (Civil Application 33 of 2012) [2012] TZCA 219 (27 August 2012) 94 citations
3. Chama Cha Walimu Tanzania vs The Attorney General (Civil Application 151 of 2008) [2008] TZCA 23 (11 November 2008) 77 citations
4. Director of Public Prosecutions vs Dodoli Kapufi & Another (Criminal Application 11 of 2008) [2011] TZCA 46 (6 May 2011) 69 citations
5. Galus Kitaya vs Republic (Criminal Appeal No. 196 of 2015) [2016] TZCA 301 (15 April 2016) 67 citations
6. Director of Publication Prosecutions vs ACP Abdallah Zombe & Others (Criminal Appeal No. 254 of 2009) [2013] TZCA 497 (8 May 2013) 61 citations
7. Zuberi Mussa vs Shinyanga Town Council (Civil Application 100 of 2004) [2007] TZCA 181 (16 March 2007) 61 citations
8. Blueline Enterprises Limited vs East African Development Bank (Civil Application No. 21 of 2012) [2013] TZCA 171 (16 May 2013) 47 citations
9. Nkanga Daudi Nkanga vs Republic (Criminal Appeal No. 316 of 2013) [2014] TZCA 213 (21 October 2014) 44 citations
10. Murtaza Ally Mangungu vs Returning Officer for Kilwa North & Others (Civil Application No 80 of 2016) [2016] TZCA 2056 (6 June 2016) 41 citations
11. M/s Tanzania - China Friendship vs Our Lady of The Usambara Sisters (Civil Appeal 84 of 2002) [2005] TZCA 104 (19 October 2005) 40 citations
12. Anthony Kinanila & Another vs Republic (Criminal Appeal 83 of 2021) [2022] TZCA 356 (16 June 2022) 39 citations
13. Kulwa Makomelo and 2 Others vs The Republic (Criminal Appeal No. 15 of 2014) [2015] TZCA 559 (9 October 2015) 38 citations
14. Independent Power Tanzania Ltd & Standard Charterd Bank (hong Kong) Ltd (Civil Revision 1 of 2009) [2009] TZCA 17 (9 April 2009) 34 citations
15. Christina Mrimi vs Cocacola Kwanza Bottlers Ltd (Civil Appeal 112 of 2008) [2009] TZCA 33 (19 February 2009) 29 citations
16. Ahmed Mbaraka vs Mwananchi Engineering & Contracting Co. Ltd (Civil Application No. 229 of 2014) [2016] TZCA 747 (15 February 2016) 24 citations
17. Edson Osward Mbogoro vs Dr. Emmanuel John Nchimbi & Another (Civil Appeal 140 of 2006) [2007] TZCA 15 (20 September 2007) 24 citations
18. Honourable Attorney General vs Reverend Christopher Mtikila (Civil Appeal 20 of 2007) [2008] TZCA 57 (15 May 2008) 24 citations
19. Tanzania Breweries Limited vs Anthony Nyingi (Civil Appeal No. 119 of 2014) [2015] TZCA 580 (25 March 2015) 24 citations
20. Tanzania Cigarette Company Ltd vs The Fair Competition Commission & Another (Misc. Civil Cause 31 of 2010) [2012] TZHC 31 (28 September 2012) 24 citations
21. National Housing Corporation vs Etienes Hotel (Civil Application 10 of 2005) [2005] TZCA 82 (16 December 2005) 22 citations
22. Nico s/o Mhando & Others vs Republic (Criminal Appeal 332 of 2008) [2012] TZCA 102 (26 March 2012) 22 citations
23. African Marble Company Limited (amc) vs Tanzania Saruji Corporation (tsc) (Civil Application 132 of 2005) [2005] TZCA 79 (7 December 2005) 21 citations
24. Mechmar Corporation (malaysia) Berhard vs Vip Engineering & Marketing Ltd (Civil Application 9 of 2011) [2011] TZCA 3 (16 June 2011) 20 citations
25. P.9219 Abdon Edward Rwegasira vs The Judge Advocate General (Criminal Application No. 5 of 2011) [2016] TZCA 969 (2 December 2016) 20 citations
26. Gideon Wasonga & Others vs The Attorney General & Others (Civil Appeal 37 of 2018) [2021] TZCA 3534 (23 December 2021) 19 citations
27. Kweka & Another vs Ngorika Bus Services & Transport Company Limited (Civil Appeal 129 of 2002) [2006] TZCA 10 (4 October 2006) 19 citations
28. Pride Tanzania Limited vs Mwanzani Kasatu Kasamia (Misc. Commercial Cause No. 230 of 2015) [2016] TZHC 2235 (30 June 2016) 18 citations
29. David Mushi vs Abdallah Msham Kitwanga (Civil Appeal 286 of 2016) [2022] TZCA 535 (2 August 2022) 17 citations
30. Raphael Mhando vs Republic (Criminal Appeal No. 54 of 2017) [2019] TZCA 19 (1 March 2019) 17 citations
31. Attorney General vs Jeremia Mtobesya (Civil Appeal 65 of 2016) [2018] TZCA 347 (2 February 2018) 16 citations
32. Eustace Kubalyenda vs Venancia Daud (Civil Appeal 70 of 2011) [2012] TZCA 173 (29 May 2012) 16 citations
33. Judge Incharge High Court Arusha & Another vs Nin Munuo Ng'uni (Civil Appeal 45 of 1998) [2002] TZCA 12 (5 March 2002) 16 citations
34. Sarbjit Singh Bharya & Another vs Nic Bank Tanzania Ltd & Another (Civil Appeal 94 of 2017) [2021] TZCA 212 (25 May 2021) 15 citations
35. Chacha Nyikongoro vs Ndege Kiseke (Misc. Land Appeal 145 of 2020) [2021] TZHC 2830 (27 April 2021) 14 citations
36. Margwe Error & Others vs Moshi Bahalulu (Civil Appeal No. 111 of 2014) [2015] TZCA 282 (25 February 2015) 14 citations
37. Masalu Kayeye vs Republic (Criminal Appeal No. 120 of 2017) [2020] TZCA 302 (17 June 2020) 14 citations
38. Director of Public Prosecutions vs Farid Hadi Ahmed & Others (Criminal Appeal No. 96 of 2013) [2013] TZCA 260 (20 November 2013) 13 citations
39. Peter s/o Nhonda & Another vs Republic (Misc. Criminal Application 25 of 2007) [2007] TZHC 128 (14 November 2007) 13 citations
40. Tanzania Heart Institute vs Board of Trustees of N.S.S.F. (Civil Application 109 of 2008) [2008] TZCA 29 (15 August 2008) 13 citations
41. Fadhil Yussuf Hamid vs Director of Public Prosecution (Criminal Appeal No 129 of 2016) [2016] TZCA 2033 (6 December 2016) 12 citations
42. Hamis Said Mkuki vs Fatuma Ally (Civil Appeal No. 147 of 2017) [2018] TZCA 341 (19 November 2018) 12 citations
43. Honourable Attorney General vs Reverend Christopher Mtikila (Civil Appeal 45 of 2009) [2010] TZCA 162 (17 June 2010) 12 citations
44. Rizali Rajabu vs Republic (Criminal Application 4 of 2011) [2013] TZCA 452 (25 March 2013) 12 citations
45. Freeman Aikael Mbowe & Another vs Alex O. Lema (Civil Appeal 84 of 2001) [2001] TZCA 6 (20 September 2001) 11 citations
46. Fweda Mwanajoma & Another vs Republic (Criminal Appeal 174 of 2008) [2010] TZCA 96 (23 March 2010) 11 citations
47. M/s Bulk Distributors Limited vs Happyness William Mollel (Civil Application 4 of 2008) [2013] TZCA 370 (18 June 2013) 11 citations
48. Paul Dioniz vs Republic (Criminal Appeal 171 of 2018) [2020] TZCA 1840 (2 November 2020) 11 citations
49. Òysterbay Properties Ltd & Another vs Kinondoni Municipal Council & Others (Civil Revision 4 of 2011) [2011] TZCA 167 (18 November 2011) 11 citations
50. Afriscan Group (T) Limited vs Said Msangi (Commercial Case 87 of 2013) [2015] TZHCComD 20 (14 May 2015) 10 citations
51. Director of Public Prosecutions vs Said Saleh Ali (Criminal Appeal No. 476 of 2017) [2018] TZCA 328 (13 December 2018) 10 citations
52. Htt Infranco Limited vs Juliano Charles Mikongomi (Administrator of the estate of the late Charles Mikongomi), Mic Tanzania Ltd t/a Tigo Ltd and Alice Boaz (Misc. Civil Application 24 of 2020) [2022] TZHC 10467 (15 June 2022) 10 citations
53. Mbeya-rukwa Autoparts & Transport Ltd. vs Jestina George Mwakyoma (Civil Appeal 45 of 2001) [2001] TZCA 14 (9 August 2001) 10 citations
54. Eliester Philemon Lipangahela (Civil Appeal 139 of 2002) [2005] TZHC 191 (25 February 2005) 9 citations
55. Magoiga Magutu @ Wansima vs Republic (Criminal Appeal No. 65 of 2015) [2016] TZCA 608 (25 May 2016) 9 citations
56. Mapuji Mtogwashinge vs Republic (Criminal Appeal No. 162 of 2015) [2015] TZCA 398 (2 December 2015) 9 citations
57. Moses Mayanja @ Msoke vs Republic (Criminal Appeal 56 of 2009) [2012] TZCA 222 (17 May 2012) 9 citations
58. Zito Zuberi Kabwe (MP) vs Board of Trustees Chama Cha Democrasia na Maendeleo & another (Civil Case No. 270 of 2013) [2014] TZHC 2360 (3 January 2014) 9 citations
59. Charles Mushatshi vs Nyamiyaga Village Council and Another (Land Case 8 of 2016) [2020] TZHC 4156 (9 November 2020) 8 citations
60. Emmanuel Bakundukize and 9 Others vs Aloysius Benedictor Rutaihwa (Land Case Appeal 26 of 2020) [2021] TZHC 2634 (6 April 2021) 8 citations
61. Juma Mganga Lukobora and Others vs Tanzania Medicine and Medical Devices Authority (tmda) and Others (Misc. Civil Application 642 of 2020) [2021] TZHC 5890 (3 September 2021) 8 citations
62. Msafiri Hassan Masimba vs Republic (Criminal Appeal No. 425 of 2007) [2013] TZCA 377 (5 June 2013) 8 citations
63. Mwanza City Council vs Alfred Wambura (Civil Appeal) [2022] TZHC 55 (27 January 2022) 8 citations
64. Oscar Justinian Burugu vs Republic (Criminal Appeal 33 of 2017) [2020] TZCA 1873 (25 November 2020) 8 citations
65. Registered Trustees of Pentecoste Church In Tanzania vs Magreth Mukama (Civil Appeal 45 of 2015) [2016] TZHC 2 (15 December 2016) 8 citations
66. Tanzania Electric Supply Co. Ltd vs Jumanne Masanja (DC Civil Appeal 3 of 2011) [2014] TZHC 1 (8 September 2014) 8 citations
67. Agast Green Mwamanda vs Jena Martin (Misc. Land Appeal 40 of 2019) [2020] TZHC 2478 (27 August 2020) 7 citations
68. Bahati Matimba vs Jagro Enterprises Limited (Misc. Civil Application 5 of 2022) [2022] TZHC 13496 (6 October 2022) 7 citations
69. Francis Davis Mchacky and 10 Others vs Republic (Criminal Application 14 of 2022) [2022] TZHC 391 (4 March 2022) 7 citations
70. Judicate Rumishael Shoo & Others vs The Guardian Limited (Civil Application No. 43 of 2016) [2016] TZCA 2023 (13 October 2016) 7 citations
71. Julius Ishengoma Francis Ndyanabo vs The Attorney General (Civil Appeal 64 of 2001) [2002] TZCA 14 (14 February 2002) 7 citations
72. Legal and Human Rights Centre (LHRC) & Others vs Attorney General (Misc. Civil Cause 77 of 2005) [2006] TZHC 66 (30 June 2006) 7 citations
73. Alex Maganga vs Awadhi Mohamed Gessan & Another (Civil Appeal 13 of 2009) [2014] TZHC 2034 (29 August 2014) 6 citations
74. Charles Kalungu & Another vs Republic (Criminal Appeal 96 of 2015) [2016] TZCA 287 (12 April 2016) 6 citations
75. Eliasvitus Ndimbo & Another vs Republic (Criminal Appeal 272 of 2007) [2012] TZCA 169 (28 March 2012) 6 citations
76. Elly Millinga vs Republic (Criminal Appeal 268 of 2014) [2015] TZCA 480 (25 August 2015) 6 citations
77. Hamisi Rajabu Dibagula vs Republic (Criminal Appeal 53 of 2001) [2003] TZCA 1 (14 March 2003) 6 citations
78. Jeremia Mtobesya vs Attorney General (Misc. Civil Cause 29 of 2015) [2015] TZHC 2126 (22 December 2015) 6 citations
79. John Dongo & Others vs Lepasi Mbokoso (Civil Application 14 of 2018) [2019] TZCA 165 (9 April 2019) 6 citations
80. Manjit Singh Sandhu & Others vs Robiri R. Robiri (Civil Appeal No. 121 of 2014) [2015] TZCA 375 (11 December 2015) 6 citations
81. Manyonyi Weswa vs Malibha Njoya (Land Appeal 34 of 2022) [2022] TZHC 14729 (22 November 2022) 6 citations
82. Mapuji Mtogwashinge vs Republic (Criminal Appeal No. 162 of 2015) [2015] TZCA 123 (2 December 2015) 6 citations
83. Mohamed Enterprises (T) Limited Vd Masoud Mohamed Nasser (Civil Application 33 of 2012) [2012] TZCA 67 (23 August 2012) 6 citations
84. Naftal Joseph Kalalu vs Anjela Mashirima (P.C. Civil Appeal No. 145 of 2001) [2002] TZHC 2055 (26 July 2002) 6 citations
85. Onesmo Olengurumwa vs Attorney General (Misc. Civil Cause 36 of 2019) [2020] TZHC 3363 (21 October 2020) 6 citations
86. George David Gordon vs Reliance Insurance Company T. Limited (Commercial Case 102 of 2005) [2007] TZHCComD 30 (27 March 2007) 5 citations
87. Ng'waja Joseph Serengeta @ Matako Meupe vs Republic (Criminal Appeal 417 of 2018) [2021] TZCA 341 (2 August 2021) 5 citations
88. Paul Revocatus Kaunda vs the Speaker of National Assembly and Others (Misc. Civil Cause 10 of 2020) [2020] TZHC 4758 (3 June 2020) 5 citations
89. Philip Samson Chigulu T/a Philip Samson Chigulu Agent vs Judge of the High Court of Tanzania and Others. (Misc. Civil Cause 23 of 2021) [2021] TZHC 6648 (19 October 2021) 5 citations
90. Ruvu Gemstone Mining CO. Limited vs Reliance Insurance Company (T) Ltd (Misc. Commercial Cause 21 of 2016) [2016] TZHCComD 2047 (1 October 2016) 5 citations
91. Salehe Said Nahdi vs National Microfinance Bank PLC and Another (Commercial Case 1 of 2015) [2017] TZHCComD 22 (21 February 2017) 5 citations
92. Simon Kiles Samwel @ K and Two Others vs Republic (Criminal Session Case 50 of 2022) [2022] TZHC 11003 (3 August 2022) 5 citations
93. Zakaria Kamwela & Others vs The Minister of Education & Vocational Training & Another (Civil Appeal 3 of 2012) [2013] TZCA 256 (12 July 2013) 5 citations
94. African Barrick Gold Mine Plc vs Commissioner Genral (TRA) (Civil Appeal No. 77 of 2016) [2016] TZCA 875 (20 September 2016) 4 citations
95. Attorney General vs The Board Trustees of The Cashewnut Industry Development Trust Fund & Another (Civil Application 73 of 2015) [2015] TZCA 356 (27 November 2015) 4 citations
96. Attorney General vs The Board of Trustees of The Cashewnut Industry Development Trust Fund & Another (Civil Application No. 73 of 2015) [2015] TZCA 80 (27 November 2015) 4 citations
97. Benson Ndaro Makulile & Another vs Rose Makenge Ruge (Land Revision 8 of 2023) [2023] TZHC 19139 (21 July 2023) 4 citations
98. Betty Mbapa vs Dipak Vassa & Another (Civil Appeal 48 of 2010) [2011] TZCA 34 (8 July 2011) 4 citations
99. CRDB Bank PLC vs Intersystem Holdings Ltd & Another (Commercial Case No. 107 of 2009) [2011] TZHCComD 2057 (26 May 2011) 4 citations
100. Damiano Qadwe vs Republic (Criminal Appeal No. 317 of 2016) [2019] TZCA 37 (12 April 2019) 4 citations
101. Director of Public Prosecutions vs Mussa Lyamhelo @ Seba Akujiwe & Another (Criminal Appeal 156 of 2015) [2016] TZCA 240 (8 April 2016) 4 citations
102. Educational Books Publishers Ltd vs Hasham Kassam & Sons & 3 Others (Commercial Case No. 5 of 2011) [2015] TZHCComD 2185 (4 June 2015) 4 citations
103. Elidhiaha Fadhili vs The Executive Director Mbeya District Council (Civil Appeal No. 24 of 2014) [2014] TZCA 186 (28 October 2014) 4 citations
104. Emmanuel Richard @ Humbe vs Republic (Criminal Appeal 369 of 2018) [2021] TZCA 111 (14 April 2021) 4 citations
105. Erney Gasper Asenga vs Republic (Criminal Appeal 238 of 2007) [2010] TZCA 89 (23 February 2010) 4 citations
106. Gwabo Mwansasu and Others vs Tanzania National Roads Agency and Another (Land Case 8 of 2020) [2021] TZHC 4289 (27 July 2021) 4 citations
107. Hon. Andrew John Chenge vs The Public Leaders' Ethics Secretariat and 2 Others (Misc. Civil Cause 18 of 2015) [2015] TZHC 2069 (26 June 2015) 4 citations
108. Juma Juma Mohamed vs The Director of Public Prosecutions (Criminal Appeal 243 of 2011) [2011] TZCA 124 (12 December 2011) 4 citations
109. Kassim Salum Mnyukwa vs Republic (Criminal Appeal No.405 of 2019) [2022] TZCA 93 (4 March 2022) 4 citations
110. Katani A. Katani vs The Returning Officer Tandahima District & Others (Civil Appeal 115 of 2011) [2011] TZCA 186 (22 June 2011) 4 citations
111. Manjit Singh Sandhu & Others vs Robibi R. Robibi (Civil Appeal No. 121 of 2014) [2015] TZCA 103 (11 December 2015) 4 citations
112. Mashaka Juma Ntalula vs Republic (Criminal Appeal No. 159 of 2015) [2015] TZCA 570 (7 December 2015) 4 citations
113. Mayongera Mayunga @ Mayongera vs Republic (Criminal Appeal 134 of 2021) [2022] TZHC 9616 (20 May 2022) 4 citations
114. Melkizedeki Mkuta vs Republic (Criminal Appeal 17 of 2006) [2010] TZCA 47 (6 May 2010) 4 citations
115. Mwanaidi Nyahori and Kichere Wambura Nyahori vs Republic (Criminal Application 2 of 2022) [2022] TZHC 124 (4 February 2022) 4 citations
116. National Microfinance Bank PLC vs Elizabeth Alfred Khairo (Civil Appeal No.398 of 2020) [2023] TZCA 17490 (10 August 2023) 4 citations
117. Ramadhani Athumani Mohamed vs Republic (Criminal Appeal No. 456 of 2015) [2016] TZCA 722 (29 June 2016) 4 citations
118. Republic vs Mokiri Wambura @ Makuru (Criminal Session Case 70 of 2022) [2022] TZHC 14147 (12 October 2022) 4 citations
119. Said Shabani vs Republic (Criminal Application 7 of 2011) [2013] TZCA 423 (25 March 2013) 4 citations
120. Shaban Said Mganda vs Finca Tanzania Ltd (Misc. Civil Application No. 21 of 2022) [2023] TZHC 291 (17 February 2023) 4 citations
121. Tanzania Electric Supply Company Limited vs Mrisho Abdallah and 4 Others (Labour Revision 27 of 2020) [2021] TZHC 4194 (16 July 2021) 4 citations
122. Ugumba Igembe & Another vs Trustees of Tanzania National Parks & Another (Misc. Civil Application 1 of 2021) [2021] TZHC 2043 (18 January 2021) 4 citations
123. Yusuph s/o Mbululo vs Republic (Criminal Appeal 405 of 2018) [2021] TZCA 140 (28 April 2021) 4 citations
124. Zella Adam Abraham & Others vs The Hon. Attorney General & Others (Consolidated Civil Revision No. 1 of 2016) [2016] TZCA 971 (5 May 2016) 4 citations
125. Zitto Zuberi Kabwe vs President of the United Republic of Tanzania and Others (Misc. Civil Cause 1 of 2020) [2020] TZHC 1961 (18 March 2020) 4 citations
126. Abraham Israel Shomo Muro vs National Institute for Medical Research and Another (Civil Appeal No. 52 of 2017) [2017] TZCA 280 (8 December 2017) 3 citations
127. Alistides A. Kashasira vs Anna Kajumulo Tibaijuka & Others (Misc. Civil Application 44 of 2015) [2015] TZHC 2019 (15 December 2015) 3 citations
128. Anatolia J. Mgeni vs Njocoba & Others (Civil Appeal No. 291 of 2021) [2023] TZCA 17987 (15 December 2023) 3 citations
129. Baven Hamis & Others vs Republic (Criminal Appeal No. 99 of 2014) [2016] TZCA 312 (6 June 2016) 3 citations
130. Charles Christopher Humphrey Kombe t/a Kombe Building Materials vs Kinondoni Municipal Council (Civil Appeal No. 19 of 2017) [2022] TZCA 205 (14 April 2022) 3 citations
131. Charles Mayunga @ Chizi vs Republic (Criminal Appeal No. 493 of 2015) [2017] TZCA 152 (24 August 2017) 3 citations
132. Chenge Magwega Chenge vs Specioza Mochubi (Land Appeal 13 of 2023) [2023] TZHC 22230 (31 October 2023) 3 citations
133. Chiriko Harun David vs Kangi Alphaxad Lugora & Others (Civil Appeal No. 36 of 2013) [2013] TZCA 189 (31 May 2013) 3 citations
134. Elisha Ezron Misigaro vs Mukalehe Village Council (Misc. Land Case Application 17 of 2019) [2021] TZHC 2385 (8 March 2021) 3 citations
135. Emmanuel Jackson Kamwela vs Republic (Criminal Appeal No. 482 of 2015) [2016] TZCA 682 (29 July 2016) 3 citations
136. Emmanuel Mwakibinga vs Kelvin Mwampasi and Another (Land Appeal 9 of 2019) [2021] TZHC 4174 (12 July 2021) 3 citations
137. Emmanuel Nguka @ Anditi vs Republic (Misc. Criminal Application 25 of 2023) [2023] TZHC 21943 (20 October 2023) 3 citations
138. Ginai Bangiri vs. Kisibiri Warioba & Another (Land Appeal 63 of 2022) [2023] TZHC 17668 (1 June 2023) 3 citations
139. Godfery Nzowa vs Seleman Kova (Civil Appeal No 3 of 2015) [2016] TZCA 2072 (26 February 2016) 3 citations
140. Jared Nyakila & Another vs Shanti Shah & 3 Others (Commercial Case No. 40 of 2008) [2011] TZHCComD 2037 (15 March 2011) 3 citations
141. Jeremiah Madar Kerenge & Another vs Republic (Misc. Economic Cause 1 of 2016) [2016] TZHCCED 3 (14 November 2016) 3 citations
142. Joseph Kasawa Benson vs Mary Charles Thomas (Misc. Criminal Application No. 60 of 2022) [2023] TZHC 16159 (20 March 2023) 3 citations
143. Kantibhai M. Patel vs Dahyabhai F. Mistry (Civil Appeal 58 of 1997) [2001] TZCA 20 (19 November 2001) 3 citations
144. Martha A. Mwakinyali and Another vs Hamis Mitogwa (Misc. Land Appeal 13 of 2013) [2020] TZHC 2477 (27 August 2020) 3 citations
145. Maryam Nassoro vs Abla Estate Developers and 3 Others (Land Case 140 of 2020) [2021] TZHCLandD 797 (9 November 2021) 3 citations
146. Mazher Limited vs Wajidali Ramzanali Jiwa Hirji (Civil Appeal No. 64 of 2010) [2017] TZCA 220 (21 February 2017) 3 citations
147. Mirambo Limited vs Commissioner General,Tanzania Revenue Authority and Another (Misc. Civil Application 57 of 2020) [2021] TZHC 3047 (30 April 2021) 3 citations
148. Muhammad Rafik & Others vs The AD HOC Committee, Sunni Muslim Jamaat Dar es Salaam (Civil Case 119 of 2012) [2012] TZHC 22 (16 June 2012) 3 citations
149. Nathan Baguma @ Rushejela vs Republic (Criminal Appeal No. 166 of 2015) [2015] TZCA 401 (8 December 2015) 3 citations
150. National Bank of Commerce Limited vs Millo Construction Company Limited & others (Misc. Commercial Application No. 102 of 2015) [2016] TZHC 2234 (16 December 2016) 3 citations
151. Oscar Josiah vs Republic (Criminal Appeal 441 of 2015) [2016] TZCA 671 (26 February 2016) 3 citations
152. Ramadhani Mlindwa vs Republic (Criminal Appeal No. 158 of 2015) [2015] TZCA 405 (4 December 2015) 3 citations
153. Rebeca Z. Gyumi vs Attorney General (Misc. Civil Cause 5 of 2016) [2016] TZHC 2023 (3 March 2016) 3 citations
154. Registered Trustees, Cashewnut Industry Development Fund vs Cashewnut Board of Tanzania (Civil Appeal 18 of 2001) [2006] TZCA 25 (1 December 2006) 3 citations
155. Saed Kubena vs Attorney General (Misc. Civil Cause No. 28 of 2014) [2014] TZHC 2339 (7 October 2014) 3 citations
156. Said Kahana Rwaki vs Nsanda Mabhari Sarigre and Kisoku Mabhari Sagire (Misc. Appeal 3 of 2022) [2022] TZHC 9675 (25 May 2022) 3 citations
157. Samwel Gitau Saitoti @ Saimoo @ Jose & Others vs The Director of Public Prosecutions (Criminal Application 73 of 2020) [2021] TZCA 554 (1 October 2021) 3 citations
158. Sudi Abdi Athumani vs National Microfinance Bank Plc Bukoba Branch (Land Appeal 47 of 2018) [2020] TZHC 3294 (27 October 2020) 3 citations
159. Sweetbert Ndebea vs Nestory Tigwera (Civil Application 3 of 2019) [2020] TZHC 4153 (27 November 2020) 3 citations
160. Victor Nzagi vs Josephina Magwala (Misc. Appeal 29 of 2022) [2022] TZHC 11765 (17 August 2022) 3 citations
161. Waziri Hussein Isore vs Sokoine Mseti & 2 Others (Misc. Land Appeal 38 of 2022) [2022] TZHC 14753 (24 November 2022) 3 citations
162. Zebadia Wanchara Chacha & 21 Others vs North Mara Gold Mine Limited (Land Case 27 of 2022) [2023] TZHC 20308 (22 August 2023) 3 citations
163. Abdallah Said Akilimali vs Republic (Criminal Appeal No. 203 of 2015) [2015] TZCA 268 (12 October 2015) 2 citations
164. Ahmed Shilla Mkumbo vs The Director of Public Prosecutions (Criminal Appeal 235 of 2010) [2010] TZCA 18 (25 November 2010) 2 citations
165. Andrew John Chenge vs Public Leaders’ Ethics Secretariat (Misc. Civil Cause 18 of 2015) [2015] TZHC 5 (26 June 2015) 2 citations
166. Apolinary Zachwa vs Frola Katalaiya (Land Case Appeal 6 of 2020) [2021] TZHC 3545 (8 June 2021) 2 citations
167. Atuwonekye vs Hezron Manguta (Misc. Land Aplication 5 of 2020) [2022] TZHC 525 (22 March 2022) 2 citations
168. Ayubu Simkoko vs Zela Robert (Misc. Criminal Appl. 77 of 2020) [2021] TZHC 2591 (16 March 2021) 2 citations
169. Baddi Twaha Ally vs Crdb Bank Plc & Another (LAND CASE NO. 175 OF 2023) [2023] TZHCLandD 17011 (25 September 2023) 2 citations
170. Benjamin Mpilimi & Others vs Republic (Criminal Application No. 1 of 2011) [2013] TZCA 244 (15 March 2013) 2 citations
171. Bernard Makondo Gambachara vs Republic (Misc. Application 25 of 2022) [2022] TZHC 10745 (16 June 2022) 2 citations
172. Elias Tibendelana vs Inspector General of Police (Civil Appeal No. 115 of 2008) [2013] TZCA 317 (17 April 2013) 2 citations
173. Erasto Kamala Mwambuse vs Jubilee Insurance Co. Tz. Ltd and Another (Civil Appeal 13 of 2020) [2020] TZHC 4408 (14 December 2020) 2 citations
174. Federation of Mines Associations of Tanzania & Others vs M/S Africa Gem Resources (AFGEM) & Others (Misc. Civil Case 23 of 2001) [2001] TZHC 30 (22 August 2001) 2 citations
175. Florentina Philbert vs Verdiana Protace Mujwahuzi (Misc. Land Application 75 of 2020) [2021] TZHC 4034 (6 July 2021) 2 citations
176. Guardian Ltd & Another vs Justin Nyari (Civil Application No. 2 of 2015) [2016] TZCA 917 (24 May 2016) 2 citations
177. Haji A. Ukwaju t/a Wajenzi Enter vs The National Micro Finance Bank & Another (Commercial Case No. 27 of 2003) [2003] TZHCComD 29 (13 May 2003) 2 citations
178. Hassan Amiri Hemedi & Others vs Lake Oil Limited (T) & Another (Land Case 84 of 2020) [2022] TZHCLandD 12564 (2 November 2022) 2 citations
179. Hassan Kibasa vs Angelesia Chang'a (Civil Application 405 of 2018) [2021] TZCA 148 (30 April 2021) 2 citations
180. Hussein Malulu @ Elias Hussein & Others vs Republic (Criminal Appeal No. 263 of 2021) [2023] TZCA 17939 (13 December 2023) 2 citations
181. In the Matter of Rectification of Register of Members of Buyuni Company Limited. Ashura Said Ndundu and Another vs Buyuni Company Limited (Misc. Civil Cause 508 of 2020) [2020] TZHC 4643 (23 December 2020) 2 citations
182. Issa Dihando @ Makusekuse & Another vs Republic (Criminal Appeal 265 of 2005) [2010] TZCA 63 (5 October 2010) 2 citations
183. Jackson S/O Ole Nemeteni @Ole Saibul @Mdosi @Mjomba Mjomba & others vs Attorney General (Misc. Civil Cause No. 117 of 2004) [2007] TZHC 494 (13 July 2007) 2 citations
184. Kaheme Manyemela @ Manoni vs Republic (Criminal Appeal No. 212 of 2014) [2015] TZCA 371 (8 December 2015) 2 citations
185. Leonidas Karani Kitambi vs Gregory Mushaijaki (Misc. Land Case Application 38 of 2021) [2021] TZHC 7279 (25 October 2021) 2 citations
186. Luchalamila Mawanga vs Republic (Criminal Appeal 319 of 2007) [2010] TZCA 36 (7 June 2010) 2 citations
187. Luxury Appartments Limited vs Edward Wilson Ngwale & Others (Misc. Land Aplication 59 of 2013) [2014] TZHC 2278 (8 July 2014) 2 citations
188. Magambazi Mines Company Ltd & Others vs Kidee Mining T. Limited (Civil Appeals No. 238 & 239 of 2018) [2022] TZCA 814 (7 December 2022) 2 citations
189. Maheshkumar Raojibhai Patel vs Karim Shamshuddin Suleman (Commercial Case 80 of 2015) [2016] TZHCComD 15 (18 February 2016) 2 citations
190. Maruru Zabron vs The Republic (Misc. Criminal Application 24 of 2023) [2023] TZHC 22060 (27 October 2023) 2 citations
191. Mroni Garden Construction Ltd vs Ether Nicholas Matiko (Civil Appeal No. 9 of 2022) [2023] TZHC 15870 (3 March 2023) 2 citations
192. Mwita Juma @ Machango vs Republic (Misc. Application 31 of 2022) [2022] TZHC 10678 (15 July 2022) 2 citations
193. National Microfinance Bank PLC & Another vs Bwire Nyamwero & 5 Others (Misc. Land Application 96 of 2023) [2024] TZHC 1268 (4 April 2024) 2 citations
194. National Microfinance Bank vs Beatrice Mbasha (Civil Appeal No. 25 of 2012) [2014] TZHC 2398 (10 July 2014) 2 citations
195. Ngesela Keya Joseph @ Ismail & Others vs Republic (Criminal Appeal 116 of 2021) [2022] TZCA 449 (19 July 2022) 2 citations
196. Nile Healthcare Limited t/a Uhuru vs Filbert John Mpogoro (Labour Revision 7 of 2022) [2022] TZHC 14593 (11 November 2022) 2 citations
197. North Mara Gold Mine Limited vs Commissioner General (TRA) (Civil Appeal 78 of 2015) [2016] TZCA 781 (1 March 2016) 2 citations
198. Pangea Minerals Ltd vs Petrofuel (T) Ltd & 2 Others (Misc. Commercial Cause No. 194 of 2015) [2015] TZHCComD 2260 (28 September 2015) 2 citations
199. Peter Sagadege Kashuma vs Republic (Criminal Appeal 219 of 2019) [2021] TZCA 754 (14 December 2021) 2 citations
200. Petro Manhyakuwalwa vs Republic (Criminal Appeal No. 561 of 2015) [2018] TZCA 594 (28 September 2018) 2 citations
201. Pyrethrum Company of Tanzania vs Rehema Chioko (Labour Revision 6 of 2019) [2022] TZHC 11137 (16 May 2022) 2 citations
202. Rajabu Juma Mwasegera vs Mariam Hassan (PC Civil Appeal No. 13 of 2014) [2015] TZHC 2184 (22 September 2015) 2 citations
203. Registered Trustees of Evangelistic assemblies of God Tanzania & 4 Others vs Peter Charles Kaswiza (vice Bishop) Tabora South Province Eagt Church (Civil Appeal 17 of 2020) [2022] TZHC 729 (25 March 2022) 2 citations
204. Registrar of Societies & Others vs Baraza La Wanawake Tanzania & Others (Civil Appeal 82 of 1999) [2001] TZCA 11 (25 April 2001) 2 citations
205. Sabas William Kiwango vs The Attorney General (Misc. Civil Application 17 of 2011) [2011] TZHC 2067 (15 March 2011) 2 citations
206. Sirasi Wambura Chacha Mtoki vs. Julius Wambura Nyigesa & Another (Land Revision 3 of 2023) [2023] TZHC 17639 (2 June 2023) 2 citations
207. Steven Ngoloka vs Ponsian Nkwama (Misc. Land Application 8 of 2019) [2020] TZHC 65 (27 February 2020) 2 citations
208. Tanganyika Law Society vs Attorney General (Misc. Civil Cause No. 31 of 2014) [2014] TZHC 2303 (22 September 2014) 2 citations
209. Tanzania Breweries Limited vs Mohamed Kazingumbe (Civil Appeal 53 of 2008) [2009] TZCA 19 (9 October 2009) 2 citations
210. Tofiki Juma vs Republic (Criminal Appeal 418 of 2015) [2015] TZCA 135 (24 November 2015) 2 citations
211. Trustees of the Tanzania National Parks vs Ernatus I. Aron (Labour Rev. Application 19 of 2021) [2022] TZHC 292 (24 February 2022) 2 citations
212. Valerian Chrispin Mlay vs Kagera Tea Company Ltd (Misc. Labour Application 10 of 2019) [2020] TZHC 3285 (19 October 2020) 2 citations
213. Vodacom Tanzania Public Ltd. Co. vs the Commissioner General (tra) and Another (Misc. Civil Cause 33 of 2020) [2020] TZHC 4593 (10 December 2020) 2 citations
214. Zepherine Galeba vs The Attorney General (Misc. Civil Application 21 of 2013) [2016] TZHC 2019 (2 June 2016) 2 citations
215. Zitto Zuberi Kabwe vs the President of the United Republic of Tanzania and Others (Misc. Civil Cause 1 of 2020) [2020] TZHC 72 (18 March 2020) 2 citations
216. Zuberi Mussa vs Shimyanga Town Council (Civil Application 100 of 2004) [2007] TZCA 153 (16 March 2007) 2 citations
217. Abdi Ally vs Republic (Criminal Appeal No. 398 of 2013) [2014] TZCA 217 (25 September 2014) 1 citation
218. Ace Distributors (T) Ltd vs Khalid Said Kengabo (Commercial Case No. 46 of 2012) [2012] TZHCComD 68 (22 November 2012) 1 citation
219. Adelaida Chrisant vs Laurent Alexanda (Land Case Appeal 8 of 2019) [2021] TZHC 2387 (5 March 2021) 1 citation
220. Ahmed Mohamed Siwji vs NBC Ltd & Another (Commercial Case No. 96 of 2010) [2011] TZHCComD 2073 (5 August 2011) 1 citation
221. Alaf Limited vs Asulwisye Mwalupani (Revision No. 282 of 2014) [2016] TZHC 2300 (29 July 2016) 1 citation
222. Amos Wilson @ Sankara Ntiboneka vs Republic (Criminal Appeal No. 164 of 2015) [2015] TZCA 111 (7 December 2015) 1 citation
223. Anna Itagata & Another vs Geofrey Kajigili (Probate Appeal 9 of 2020) [2021] TZHC 2595 (4 March 2021) 1 citation
224. Aroni Mathew Kikoti vs Republic (Criminal Appeal No. 206 of 2013) [2013] TZCA 315 (3 December 2013) 1 citation
225. Atupakisye Mwakikuti vs Sekela Mwakikuti and Another (Misc. Land Application 48 of 2018) [2020] TZHC 1988 (22 July 2020) 1 citation
226. Barclays Bank Tanzania Limited vs Adam Mhagama and 4 Others (Labor Revision 18 of 2020) [2022] TZHC 11966 (24 August 2022) 1 citation
227. Barton Mwambola vs Stevene Mwaikasu (Misc. Land Appeal 16 of 2020) [2021] TZHC 3373 (25 May 2021) 1 citation
228. Basil Boay Surumbu vs Republic (Criminal Appeal 82 of 2017) [2020] TZHC 1984 (3 November 2020) 1 citation
229. Bernard Makondo Gambachara vs Republic (Misc. Application 25 of 2022) [2022] TZHC 10041 (14 June 2022) 1 citation
230. Board of Trustees of The National Social Security Fund (NSSF) vs Grace Lumelezi (Civil Appeal No. 38 of 2015) [2016] TZCA 258 (21 October 2016) 1 citation
231. Chacha Mago vs Dr James Kilaza (Misc. Appeal 57 of 2021) [2022] TZHC 191 (22 February 2022) 1 citation
232. Charles Sugwa vs Daniel Lucas (Commercial Case 10 of 2015) [2016] TZHCComD 5 (21 April 2016) 1 citation
233. Christina John Mwita vs Paschal Maganga (Land Case Appeal 50 of 2021) [2022] TZHC 295 (28 February 2022) 1 citation
234. Computers & Programs Africa, PTY Ltd (T) Electric Supply Co. Ltd (Commercial Case No. 129 of 2005) [2006] TZHCComD 47 (2 June 2006) 1 citation
235. Cornel Naiman Materu vs Cordian Matei Akaro (Civil Appeal No. 115 of 2021) [2024] TZCA 162 (5 March 2024) 1 citation
236. D.P.P vs Aidan Tangasi Mgonela and 2 Others (Misc. Criminal Application 81 of 2010) [2011] TZHC 2127 (21 September 2011) 1 citation
237. David Gerald Mhanga vs Republic (DC Criminal Appeal 22 of 2022) [2022] TZHC 14501 (7 November 2022) 1 citation
238. Dickson Chacha @Manyori & Another vs The Republic (Misc. Criminal Application 17 of 2023) [2023] TZHC 19793 (3 August 2023) 1 citation
239. Dyana Mwanangwa vs Mandela Samson and 2 Others (Misc. Land Application 44 of 2020) [2021] TZHC 2242 (18 February 2021) 1 citation
240. Editha Nababi vs Kemebos English Medium Boarding Primary School (Misc. Labour Application 8 of 2020) [2021] TZHC 4033 (5 July 2021) 1 citation
241. Eliadhiaha Fadhil vs The Executive Director of Mbeya District Counsel (Civil Appeal No. 24 of 2014) [2014] TZCA 278 (28 October 2014) 1 citation
242. Elias Kashagama vs theobard Bonephace Tibihikaho (Land Case Appeal 71 of 2019) [2021] TZHC 4158 (6 July 2021) 1 citation
243. Eliester Philemon Lipangahela vs Daud Makuhana (Civil Appeal 139 of 2002) [2005] TZHC 147 (25 February 2005) 1 citation
244. Eustace Kubalyenda vs Venancia Daud (Civil Appeal 70 of 2011) [2012] TZCA 89 (29 May 2012) 1 citation
245. Ex D. 1995 Pc Ahmed vs Republic (Criminal Appeal No. 207 of 2014) [2015] TZCA 92 (3 December 2015) 1 citation
246. Fredrick Anthony Mboma vs The Attorney General (Miscellaneous Civil Cause No. 08 of 2013) [2023] TZHC 20190 (17 August 2023) 1 citation
247. Fredrick Anthony Mboma vs The Attorney General [2023] TZHC 20188 (17 August 2023) 1 citation
248. Gamba Gibe Mondela vs Bamboo Rock Drilling (Labour Revision 2 of 2022) [2022] TZHC 12271 (30 August 2022) 1 citation
249. Geofrey Kisha vs Republic (Criminal Appeal No. 69 of 2015) [2016] TZCA 2100 (22 April 2016) 1 citation
250. Geofrey Watson Mwakasege vs Tanganyika Law Society and the Attorney General (Misc. Civil Cause 23 of 2021) [2022] TZHC 11064 (19 July 2022) 1 citation
251. George Katabi Mtasha & Another vs Mashauri Willson Ntizu (Civil Appeal 17 of 2021) [2022] TZHC 11581 (28 June 2022) 1 citation
252. Godwin Edinshen Sanga vs Emmanuel Ilomo (Land Appeal 44 of 2019) [2021] TZHC 3901 (5 May 2021) 1 citation
253. Halima James Mdee and 2 others vs Job Yustino Ndugai, The Speaker of the National Assembly of the United Republic of Tanzania (Misc. Civil Application No. 27 of 2017) [2017] TZHC 2245 (10 July 2017) 1 citation
254. Helena Mgini Kulimbi vs Revocatus Kuboja (Misc. Appeal 20 of 2022) [2022] TZHC 11766 (17 August 2022) 1 citation
255. Hussein Raphael & Others vs Republic (Criminal Appeal No.280 of 2008) [2013] TZCA 310 (4 March 2013) 1 citation
256. Ibrahim Wambura Wanchoke vs Daniel Paschal Kiusi (Misc. Appeal 17 of 2022) [2022] TZHC 10125 (15 June 2022) 1 citation
257. In Re: Constitution of the United Republic of Tanzania, 1977 (Misc. Civil Cause 77 of 2005) [2006] TZHC 4 (24 April 2006) 1 citation
258. Jackson Matandu & Others vs Republic (Consolidated Misc. Economic Causes 8 of 2018) [2018] TZHCCED 30 (4 July 2018) 1 citation
259. Jackson Ole Nemeteni & Others vs Attorney General (Misc. Civil Cause No. 117 of 2004) [2007] TZHC 486 (13 July 2007) 1 citation
260. Jared Nyakila & Another vs Shanti Shah & Others (Commercial Case No. 40 of 2008) [2011] TZHC 2178 (15 March 2011) 1 citation
261. Jayantkumar Chandubay Patel @ Jeetu Patel & Others (Misc. Civil Case 30 of 2009) [2011] TZHC 2044 (25 October 2011) 1 citation
262. Jayantkumar Chandubhai Patel @ Jeetu Patel & Others vs The Attorney General & Others (Civil Appeal No. 59 of 2012) [2016] TZCA 796 (15 April 2016) 1 citation
263. Johnson Amir Garuma vs Attorney General & Others (Misc. Civil Cause No. 11 of 2017) [2018] TZHC 123 (22 June 2018) 1 citation
264. Jonathan Ernest Mgongoro vs Judicial Officers Ethics Committee & Others (Civil Appeal No. 26 of 2021) [2022] TZCA 397 (21 March 2022) 1 citation
265. Joseph Jacob Kahungwa vs Rhobi Kikaro and Seven (7) Others (Misc. Application 104 of 2021) [2022] TZHC 9863 (31 May 2022) 1 citation
266. Joseph M. Mutashobya vs M/s Kibo Match Group Limited (Civil Appeal 53 of 2001) [2003] TZCA 21 (11 June 2003) 1 citation
267. Joseph Raphael Maruma vs Republic (Criminal Appeal No. 287 of 2015) [2016] TZCA 624 (21 July 2016) 1 citation
268. Joseph Siagi Singwe vs Boniphace Marwa Wang'anyi (Misc. Land Appeal 111 of 2021) [2022] TZHC 10228 (21 June 2022) 1 citation
269. Judge Advocate General vs P. 9219 Lt. Abdon Edward Rwegasira (Criminal Revision 3 of 2010) [2011] TZCA 122 (24 February 2011) 1 citation
270. Juma Limbu @ Tembo vs Republic (Criminal Appeal 168 of 2006) [2010] TZCA 79 (6 October 2010) 1 citation
271. Justine Nyari vs Guardian Limited & Another (Civil Application 3 of 2009) [2010] TZCA 82 (26 February 2010) 1 citation
272. Kachukura Nshekanabo @ Kakobeka (Criminal Appeal No. 314 of 2015) [2016] TZCA 666 (24 February 2016) 1 citation
273. Karege Pius Makunda vs John Mabhai Makunja and Nyang'ando John Makunja (Misc. Appeal 95 of 2021) [2022] TZHC 293 (23 February 2022) 1 citation
274. Karunde Mnubi vs Luti Jeje Mnubi (Land Appeal 92 of 2021) [2022] TZHC 10124 (16 June 2022) 1 citation
275. Kigundu Francis & Another vs Republic (Criminal Appeal 314 of 201) [2011] TZCA 71 (28 November 2011) 1 citation
276. Lalago Cotton Ginney & Oil Mills Co. Limited vs The Loans & Advances Realization Trust (lart) (Civil Appeal 51 of 2002) [2004] TZCA 48 (20 January 2004) 1 citation
277. Lazarus Mirisho Mafie and M/S Shidolya Tours & Safaris vs Odilo Gasper Kilenga Alias Moiso Gasper (Commercial Case 10 of 2008) [2010] TZHCComD 1 (10 January 2010) 1 citation
278. Legal and Human Rights Centre (LHRC) & Others vs Attorney General (2) (Massati, J.) (Misc. Civil Case 77 of 2006) [2006] TZHC 2 (24 April 2006) 1 citation
279. Luponya vs Republic (Criminal Appeal 129 of 2015) [2016] TZCA 129 (25 October 2016) 1 citation
280. Luxury Appartments Limited vs Edward Wilson Ngwale and 3 Others (Misc. Land Application 59 of 2013) [2014] TZHC 2184 (8 July 2014) 1 citation
281. Mahesh Kumar Raojibhai Patel vs Karim Shamshuddin Suleman (Commercial Case No. 80 of 2015) [2016] TZHCComD 2126 (18 February 2016) 1 citation
282. Makaranga Swea Limbe vs Republic (Misc. Criminal Application 21 of 2021) [2022] TZHC 9969 (6 June 2022) 1 citation
283. Mameck Matagache @ Kigoro and 2 Others vs Republic (Criminal Appeal 19 of 2022) [2022] TZHC 10756 (25 July 2022) 1 citation
284. Mariki and Others vs Republic (Criminal Appeal No. 289 of 2015) [2016] TZCA 70 (28 October 2016) 1 citation
285. Masalu Luponya vs Republic (Criminal Appeal No. 129 of 2015) [2016] TZCA 2097 (26 October 2016) 1 citation
286. Mkurugenzi Wa Nelis vs Eliab Cassius (Land Appeal 73 of 2010) [2012] TZHCLandD 7 (2 November 2012) 1 citation
287. Mohamed Enterprises(Tanzania) Limited vs Adili Auction Mart Limited & 2 Others (Land Case 54 of 2023) [2023] TZHCLandD 16827 (19 June 2023) 1 citation
288. Mohamed Said Hersy vs Ally Hersy (PC Civil Appeal 38 of 2021) [2022] TZHC 10629 (14 July 2022) 1 citation
289. Mohammadi Woodworks Ltd vs Honest Logistics Ltd (Misc. Commercial Cause No. 159 of 2023) [2024] TZHCComD 35 (22 March 2024) 1 citation
290. Moremi Mang'ango Moremi vs Suzan Mahimbo and 2 Others (Misc. Appeal 57 of 2021) [2022] TZHC 471 (15 March 2022) 1 citation
291. Moses Mayanja @ Msoke vs Republic (Criminal Appeal 56 of 2009) [2012] TZCA 70 (16 May 2012) 1 citation
292. Mselem Ali Mselem & Others vs Honourable Attorney General (Misc. Civil Cause No. 25 of 2017) [2018] TZHC 111 (17 August 2018) 1 citation
293. Mufindi Tea & Coffee Limited vs Valerian Joseph assey (Misc. Labour Application) [2022] TZHC 13592 (7 October 2022) 1 citation
294. Mugeta Torokoko and Another vs Ministry of Lands, Housing and Human Settlement and Another (Civil Case 12 of 2019) [2020] TZHC 656 (29 April 2020) 1 citation
295. Mwanaisha Mohamed Ngochele vs Mohamed Salum & Others (Land Case Appeal 99 of 2011) [2012] TZHCLandD 1 (11 December 2012) 1 citation
296. Nehemia Jacobo vs Murukulazo Village Council (Misc. Land Case Application 48 of 2020) [2021] TZHC 2630 (6 April 2021) 1 citation
297. Obadia Mwakasitu vs Tanzania Local Government Workers Union (talgwuhu) (Misc. Cause 3 of 2021) [2021] TZHC 5845 (27 August 2021) 1 citation
298. Onesmo Olengurumwa vs Attorney General (Misc. Civil Cause 9 of 2021) [2022] TZHC 17011 (15 February 2022) 1 citation
299. Paul John Muhozya vs Attorney General (Misc. Criminal Cause 2 of 2023) [2023] TZHC 20355 (18 August 2023) 1 citation
300. Penina Mhere Wangwe & 31 Others vs North Mara Gold Mine Limited (Land Case 19 of 2022) [2023] TZHC 20674 (4 September 2023) 1 citation
301. Pride (T) Ltd vs Mwazani Kasatu Kasamia (Misc. Commercial Cause No. 230 of 2015) [2016] TZHCComD 2138 (30 June 2016) 1 citation
302. Ramadhani Hussein vs Imelda Abdallah and Another (Misc. Land Application 1 of 2020) [2020] TZHC 3288 (6 October 2020) 1 citation
303. Ramadhani Mlindwa vs Republic (Criminal Appeal 158 of 2015) [2015] TZCA 131 (3 December 2015) 1 citation
304. Rashid Ahmed Kilindo vs Attorney General (Misc. Civil Cause 30 of 2018) [2020] TZHC 3261 (31 August 2020) 1 citation
305. Rashid Awami Njowoka vs Fatuma Mustapha (Misc. Civil Application 136 of 2021) [2022] TZHC 15069 (21 February 2022) 1 citation
306. Republic vs G 2573 PC Pacificus S/O Cleophance Simon (Criminal Session Case No. 45 of 2013) [2016] TZHC 2309 (22 June 2016) 1 citation
307. Said Nassor Zahor & Others vs Nassor Zahor Abdallah El Nabahany & Another (Civil Application No 278, 15 of 2016) [2017] TZCA 317 (8 March 2017) 1 citation
308. Samson Haruni Bina vs Nmb Bank (Land Appeal 114 of 2016) [2018] TZHC 2963 (16 March 2018) 1 citation
309. Sebastian Abdallah Msola vs Njombe Regional Manager, TANROADS (Civil Case No. 3 of 2014) [2014] TZHC 2305 (16 April 2014) 1 citation
310. Serikali ya Kijiji cha Bugoji vs Zephania Mahindi Lan (Land Appeal 91 of 2020) [2021] TZHC 9192 (3 December 2021) 1 citation
311. Shariff Ahmed Salim vs Kullaten Abdalla Khamis (Znz Civil Application 3 of 2006) [2006] TZCA 29 (17 November 2006) 1 citation
312. Sibonike Anyingisye Mwasalemba vs Teofilo Kisanji University (teku) (Misc. Civil Appeal 2 of 2020) [2020] TZHC 4075 (25 November 2020) 1 citation
313. Sigaye and Others vs Tanzania Revenue Authority (Civil Appeal 185 of 2002) [2008] TZHC 7 (10 June 2008) 1 citation
314. Stanbic Bank Tanzania Limited vs Abercrombie & Kent (T) Limited (Civil Appeal 21 of 2001) [2006] TZCA 86 (3 August 2006) 1 citation
315. Taher H. Muccadam vs Director, Urban and Rural Planning, Ministry of Lands, Housing and Urban Development and Another (Misc. Cause 12 of 2023) [2023] TZHC 17249 (12 May 2023) 1 citation
316. Tanzania Electricity Company Ltd (TANESCO) vs Mufungo Leonard Majura & Others (Civil Revision No. 5 of 2016) [2016] TZCA 933 (30 November 2016) 1 citation
317. Tanzania Heart Institute vs The Board of Trustees of N.S.S.F (Civil Application 109 of 2008) [2008] TZCA 59 (15 August 2008) 1 citation
318. Tanzania National Roads Agency (TANROADS) vs Prismo/Badr JV Partnership (Civil Appeal No. 241 of 2019) [2024] TZCA 479 (19 June 2024) 1 citation
319. The Hon. Attorney General & 3 Others vs Nobert Yamsebo (Consolidated Appeals No. 1 of 2013) [2013] TZCA 393 (6 May 2013) 1 citation
320. Thobias Nungu vs Deus Kyabana (Misc. Application 85 of 2021) [2022] TZHC 9571 (23 May 2022) 1 citation
321. Tito Elia Magoti & Another vs National Electoral Commission & 3 Others (Misc. Civil Cause 3 of 2022) [2022] TZHC 15383 (19 December 2022) 1 citation
322. Uitdager Consultancy & Business Investment Limited Tanzania Posts Corporation & 2 Others (Misc. Land Application 43 of 2022) [2022] TZHCLandD 543 (10 June 2022) 1 citation
323. VIP Engineering and Marketing Ltd vs Independent Power Tanzania Ltd & Others (Misc. Civil Cause 254 of 2003) [2008] TZHC 212 (5 February 2008) 1 citation
324. Veronica Mbai vs Kikundi Cha Ebeneza and Another (PC Civil Appeal 4 of 2023) [2023] TZHC 17146 (4 May 2023) 1 citation
325. Vicent Damian vs Republic (Criminal Application No. 1 of 2014) [2016] TZCA 934 (20 May 2016) 1 citation
326. Walhad Ngoli and Others vs Aida Adamson Kalinga (Misc. Land Application 85 of 2018) [2020] TZHC 1339 (18 June 2020) 1 citation
327. Wilfed Lwakatare & Another vs Republic (Misc. Criminal Application 14 of 2013) [2013] TZHC 2102 (3 May 2013) 1 citation
328. William Kisanga vs Republic (Criminal Appeal No. 90 of 2017) [2020] TZCA 279 (28 May 2020) 1 citation
329. Yokobeti Simon Sanga vs Yohana Sanga (Matrimonia Appeal 1 of 2010) [2010] TZHC 201 (30 September 2010) 1 citation
330. Zakaria Kamwela & Others vs Minister of Education & Vocational Training & Another (Civil Appeal 3 of 2012) [2013] TZCA 167 (5 July 2013) 1 citation
331. Zilipa Makondoro v Republic (Criminal Sessions Case 63 of 2023) [2023] TZHC 22865 (24 November 2023) 1 citation
332. (T) Breweries Ltd vs Josaka Investments Ltd (Misc. Commercial Application No. 124 of 2014) [2015] TZHCComD 2150 (17 April 2015)
333. (T) Sugar Producer Association vs The Ministry of Finance of The United Republic of (T)& Another (Misc. Civil Case No. 25 of 2003) [2003] TZHCComD 37 (2 August 2003)
334. Abbas Antony Kilumule & Another vs Felomena Peter Mawata @ Taliyamale (Misc. Land Application 14 of 2022) [2022] TZHC 14817 (23 November 2022)
335. Abbas Muhidini Mwira vs Col Elmon A. Mahawa (Civil Case No. 1 of 2005) [2007] TZHC 425 (23 August 2007)
336. Abdallah Omary Kilondomala vs Joseph Paul Zenda (Misc. Land Case Application No. 5 of 2011) [2013] TZHC 2236 (28 May 2013)
337. Abdallah Yahya @ Masjid Hadha & 4 Others vs Registration Insolvency & Trusteeship Agency (RITA) (Land Appeal No.176 of 2023) [2023] TZHCLandD 16927 (27 September 2023)
338. Abdi Omari vs Masinda Ng'arita (Misc. Land Appication 87 of 2021) [2022] TZHC 10272 (27 June 2022)
339. Abdul Ramadhan vs Republic (Misc. Appeal 58 of 2021) [2022] TZHC 9570 (19 May 2022)
340. Adelaida Lwekorama & Another vs Republic (Criminal Appeal 120 of 2013) [2014] TZHC 2227 (11 August 2014)
341. Adelina R. Kitare vs Audax Eustace Kaijage andanother (Land Case Appeal 95 of 2020) [2021] TZHC 3882 (18 June 2021)
342. Adoyo Nandori Kakoyo vs Adriano Development Microfinace (Misc. Civil Application 46 of 2022) [2023] TZHC 16635 (12 April 2023)
343. African Development Bank & Others vs M/s East African & Another (Consolidated Civil Application 84 of 2010) [2012] TZCA 131 (19 March 2012)
344. African Development Bank Eastern & Southern African Trade vs M/s East African Development Bank & Another (Consolidated Civil Application 84 of 2010) [2012] TZCA 117 (19 March 2012)
345. African's Sec School vs Halima Hamdan and 2 Others (Labour Revision No. 375 of 2022) [2023] TZHCLD 1149 (14 February 2023)
346. Afriscan Group T. Limited vs Said Msangi (Commercial Case 87 of 2013) [2015] TZHCComD 12 (14 May 2015)
347. Agnes Samwel Mollel & Another vs Tanzania Breweries Ltd (Civil Case 4 of 2008) [2009] TZHC 134 (29 September 2009)
348. Alaf Limited vs Asulwisye Mwalupani (Revision No. 282 of 2014) [2016] TZHC 2299 (29 July 2016)
349. Alex Chuma Kapama vs Registered Trustees of Jumuiya ya Maendeleo KIJICO and Others (Misc. Civil Application No. 38 of 2023) [2023] TZHC 23121 (5 December 2023)
350. Alex Loid Mgani (Administrator of the estate of the late Patrick Loid Mgani) vs Jenifa Paul Chambala (Land Appeal 5 of 2021) [2022] TZHC 11141 (19 April 2022)
351. Alfred Lucas and another vs Yusuf Manji (Misc. Criminal Application No. 71 of 2011) [2012] TZHC 155 (8 October 2012)
352. Alhaji Shaban Mintanga Kondo vs Republic (Misc. Criminal Application 38 of 2008) [2008] TZHC 167 (8 October 2008)
353. Alicheraus Mwesiga & Others vs Tanzania Portland Cement Comapny LTD & Others (Civil Case No. 175 of 2013) [2014] TZHC 2377 (4 June 2014)
354. Alliance Media (T) Ltd vs Monier 2000 Ltd (Commercial Case No. 45 of 2005) [2005] TZHCComD 37 (16 August 2005)
355. Ally Abdallah Sule vs Mariam Hamis Hussein (Misc. Land Aplication 299 of 2022) [2022] TZHCLandD 677 (15 July 2022)
356. Ally Mkombozi vs Republic (Criminal Application 3 of 2010) [2011] TZCA 191 (28 September 2011)
357. Ally Mohamed Makong'o vs Somoe Said Mtaka (Civil Appeal No. 178 of 2016) [2017] TZHC 2160 (20 March 2017)
358. Ally Said Ahmed & Others vs Republic (Misc. Economic Cause 3 of 2016) [2016] TZHC 2120 (23 December 2016)
359. Ally Saidi Ahmed & Others vs Republic (Misc. Economic Cause 3 of 2016) [2016] TZHCCED 1 (23 December 2016)
360. Amandus Lyimo vs Kudra Idd Mushi (Misc. Criminal Application 12 of 2019) [2020] TZHC 2226 (10 August 2020)
361. Amandus Ziky Masinde vs Nyamsera Marumba (HC Civil Appeal 88 of 2016) [2018] TZHC 2950 (24 April 2018)
362. Amaniel Rwegoshora Bubelwa (Legal Attorney of Peragia Bubelwa) vs Godfrey Bubelwa (Misc. Land Aplication 85 of 2022) [2022] TZHCLandD 370 (31 May 2022)
363. Ambakisye M. Mwakabana vs the Chief Secretary and Another (Misc. Civil Cause 1 of 2020) [2021] TZHC 5589 (13 August 2021)
364. Amir Athuman vs Republic (Criminal Application 5 of 2010) [2011] TZCA 192 (28 September 2011)
365. Amos Wilson @ Sanakara Ntiboneka vs Republic (Criminal Appeal No. 164 of 2015) [2015] TZCA 386 (7 December 2015)
366. Amy P. Kibatala vs Attorney General & Another (Misc. Civil Cause 37 of 2015) [2015] TZHC 4 (27 October 2015)
367. Anastazia @nyambura Magoto vs Sera Matembera (Misc. Land Appeal 101 of 2008) [2011] TZHCLandD 2150 (7 June 2011)
368. Andrew Ambrose vs Republic (Criminal Application No. 6 of 2009) [2015] TZCA 60 (16 June 2015)
369. Andrew Ambrose vs Republic (Criminal Application No. 6 of 2009) [2015] TZCA 337 (16 July 2015)
370. Andrew John Chenge vs Public Leaders' Ethics Secretariat & Others (Misc. Civil Cause 18 of 2015) [2015] TZHC 2107 (26 June 2015)
371. Anyimike Ngoloke vs Tabu Kanyamale (Misc. Land Appeal 14 of 2020) [2021] TZHC 3371 (25 May 2021)
372. Aqwilina Onesphory Silayo T/A Maliasili Pharmacy vs DCB Commercial Bank Plc & Another (Land Appeal No. 419 of 2023) [2024] TZHCLandD 404 (24 May 2024)
373. Arcopar (o.M) S.A vs Harbert Mawrwa & Family Investment Co. Ltd & Others (Civil Application No. 94 of 2013) [2015] TZCA 270 (15 May 2015)
374. Asaeli Ndossi vs Elisifa Jackson Ndossi (PC. Civil Appeal No. 56 of 2001) [2002] TZHC 2059 (13 February 2002)
375. Ashura Masengo vs Selina Sanga (Misc. Land Case Appeal No. 16 of 2015) [2016] TZHC 2242 (12 April 2016)
376. Ashura Said Ndundu and Another vs Buyuni Company Limited (Misc. Civil Application 508 of 2020) [2020] TZHC 4633 (23 December 2020)
377. Asimna Juma Ponela vs Jafari Kayombo (Civil Appeal No. 12 of 2023) [2023] TZHC 21410 (29 September 2023)
378. Atanas Mkaima & Others vs Deogratius Mselele January (PC Civil Appeal 1 of 2023) [2023] TZHC 17371 (24 May 2023)
379. Attorney General & Another vs Ngu'ni (Civil Appeal 45 of 1998) [2002] TZHC 2 (5 March 2002)
380. Attorney General & Others vs Valerian Bamanya t/a Tanzania Associated Merchandise (Civil Application 119 of 2004) [2005] TZCA 48 (8 September 2005)
381. Attorney General vs The Board of Trustees of The Cashewnut Industry Develepment Trust Fund & Another (Civil Application No. 73 of 2015) [2015] TZCA 536 (27 November 2015)
382. Augustino Mkalimoto vs Cosmas Mdesa (Misc. Land Case Appeal 13 of 2016) [2016] TZHC 2073 (4 November 2016)
383. Ayugi vs Ayugi and Others (Civil Revision 184 of 2002) [2005] TZHC 27 (9 May 2005)
384. Baddi Twaha Ally vs Crdb Bank Plc & Another [2023] TZHCLandD 16922 (25 September 2023)
385. Bakari Alli Lusaka & Another vs Republic (Dc Criminsl Appeal No. 3 of 2016) [2016] TZHC 2171 (4 April 2016)
386. Balbir Singh Ruprai vs MIC Tanzania Ltd & Another (Civil Case 117 of 2007) [2011] TZHC 2019 (23 May 2011)
387. Balozi A. Ibrahim & another vs M/S Benandy's Limited (Misc. Civil Revision No. 2 of 2005) [2005] TZHC 269 (12 May 2005)
388. Bank of Africa (T) Limited vs Intersales Tanzania Limited & Others (Commercial Case 61 of 2015) [2015] TZHCComD 2088 (12 November 2015)
389. Bank of Africa (T) Limited vs Intersales Tanzania Limited & Others (Commercial Case 61 of 2015) [2015] TZHCComD 3 (12 November 2015)
390. Bank of Africa (T) Ltd vs Intersales (T) Ltd & 2 Others (Commercial Case No. 61of 2015) [2015] TZHCComD 2164 (12 November 2015)
391. Bartazary Wambura Thomas vs Ayubu Joseph (Civil Appeal Case 4 of 2022) [2022] TZHC 14755 (23 November 2022)
392. Baven Hams & Others vs Republic (Criminal Appeal No. 99 of 2014) [2016] TZCA 639 (6 June 2016)
393. Beltida Bengesi & 2 Others vs The Attorney General (Misc. Civil Cause No. 16 of 2022) [2023] TZHC 23997 (16 June 2023)
394. Benedicto Ichulangula vs Johanes Mutayoba and Another (Misc. Land Application 8 of 2018) [2020] TZHC 3291 (30 October 2020)
395. Benedicto Mutachoka Mutungurehi vs Innocent Sebba Bilakwate & Others (Misc. Civil Application 43 of 2015) [2015] TZHC 1 (16 December 2015)
396. Benezeth Martin vs Apolonia Mbagala (PC Criminal Appeal 16 of 2020) [2021] TZHC 3511 (3 June 2021)
397. Benson Ndaro Makulile & Another vs Rose Makenge Ruge (Land Revision 8 of 2023) [2023] TZHC 19138 (21 July 2023)
398. Bernard Kiheri Maro and 2 Others vs Verediana Chacha (Misc. Civil Application 26 of 2020) [2022] TZHC 13354 (4 October 2022)
399. Bertha Israel Behile vs Zakaria Israel Kidava (Matrimonial Appeal No. 2 of 2015) [2016] TZHC 2230 (29 March 2016)
400. Bibiti Ginneries Ltd vs (T) Railways Corporation & Another (Misc. Civil Application No. 44 of 2006) [2007] TZHCComD 38 (10 May 2007)
401. Bidco Oil and Soap Ltd vs Saving and finance Comm Bank & Another (Commercial Case No. 84 of 2006) [2010] TZHCComD 15 (28 June 2010)
402. Bishop John Lupaa vs. Chenaviola Swenya (DC Civil 46 of 2022) [2023] TZHC 22602 (14 November 2023)
403. Boay Ahay vs Republic (Criminal Appeal 66 of 2010) [2013] TZCA 246 (19 June 2013)
404. Bombaga Asilile vs Philipo Mwansasu and Another (Land Reference 8 of 2020) [2021] TZHC 6488 (21 September 2021)
405. Bulyanhulu Gold Mine LTD vs Fortunatus John Nzoih (Cons. Revision Application No. 12 of 2016) [2016] TZHC 2168 (22 March 2016)
406. Bwire Mtundi vs Masatu Ekonjo (Misc. Application 12 of 2022) [2022] TZHC 10046 (15 June 2022)
407. Charles Bakebuki vs Everista andanother (Land Case Appeal 92 of 2020) [2021] TZHC 3385 (28 May 2021)
408. Charles Rondo Mago vs Daniel Akuno Oudu (Misc. Land Appeal 18 of 2022) [2022] TZHC 3235 (17 May 2022)
409. Chedi Mchomba Chikira vs Attorney General (Misc. Civil Cause No. 58 of 2002) [2006] TZHC 298 (20 March 2006)
410. Chief Court Administrator & another vs Johnson Joliga Tanda (Revision No. 52 of 2016) [2016] TZHC 2197 (25 November 2016)
411. Chongquing Foreign Trade & Economic Cooperation Co. Ltd vs Zakayo M. Msengi (Misc. Land Aplication 17 of 2016) [2016] TZHC 2071 (12 March 2016)
412. Christina Y. Kimale vs Principal Secretary Ministry of Finance & another (Civil Case No. 15 of 2002) [2008] TZHC 335 (14 February 2008)
413. Christina Y. Kimale vs Principal Secretary Ministry of Finance & another (Civil Case No. 15 of 2002) [2008] TZHC 336 (14 February 2008)
414. Christopher Mtikila vs Attorney General (Misc. Civil Cause 10 of 2005) [2006] TZHC 126 (5 May 2006)
415. Chrizant John vs Republic (Criminal Appeal 313 of 2015) [2016] TZCA 654 (24 February 2016)
416. Cosmas Mwaifwani vs Editor of Dira ya Mtanzania & another (Misc. Civil Application No. 90 of 2013) [2014] TZHC 2364 (29 December 2014)
417. Cyridion Rweyendera Mpambo vs Rodrick Rudengera Tryphone (Probate and Administration Appeal 10 of 2020) [2021] TZHC 3878 (16 June 2021)
418. D 7762 Sgt Mtuli Ndege @ Mgonya vs Republic (Criminal Application 126 of 2021) [2022] TZHC 11005 (3 August 2022)
419. DPP vs Owden Kasanja (Criminal Appeal 305 of 2009) [2011] TZCA 50 (18 November 2011)
420. DPP vs Owden Kassanja & Others (Criminal Appeal 305 of 2009) [2011] TZCA 170 (18 November 2011)
421. Daikin (T) Ltd vs Daikin Industries Ltd & Another (Commercial Case No. 115of 2015) [2015] TZHCComD 2177 (7 December 2015)
422. Damian Kahamba and Another vs Ashura Abdallah and Another (Land Case Appeal 68 of 2018) [2020] TZHC 3292 (30 October 2020)
423. Damiano Qwade vs Republic (Criminal Appeal No 317 of 2016) [2019] TZCA 581 (12 April 2019)
424. Daniel Mshana vs Republic (Criminal Revision 11 of 2021) [2022] TZHC 9750 (20 May 2022)
425. David T. Mbunda vs NMB Mbinga Branch (Civil Case No. 2 of 2012) [2013] TZHC 2128 (12 December 2013)
426. Denwill Mining Services Ltd vs Ally Msami & Others (Misc. Land Case Application 52 of 2013) [2014] TZHCLandD 43 (7 February 2014)
427. Deogratius S/O Philipo & Another vs Republic (Criminal Appeal 70 of 2012) [2014] TZHC 2095 (15 September 2014)
428. Devotha Mathew Minja vs Tito Saimon Haule & Others (Civil Appeal No. 336 of 2022) [2024] TZCA 418 (7 June 2024)
429. Diocese of Ruvuma Anglican Church vs Adelhlm Titus Gama (DC Civil Appeal No. 14 of 2007) [2008] TZHC 303 (24 July 2008)
430. Director Kahama Town Council & Another vs Vumilia Producers and Shopping Centre Co. Ltd (Misc. Land Aplication 15 of 2015) [2015] TZHCLandD 21 (21 September 2015)
431. Director Korosho (T) vs Kigumi (Civil Appeal 19 of 2002) [2009] TZHC 4 (28 May 2009)
432. Director of Public Prosecution vs Farid Hadi Ahmed & Others (Criminal Appeal No. 148 of 2014) [2015] TZCA 142 (14 December 2015)
433. Director of Public Prosecution vs Farid Hadi Ahmed & Others (Criminal Appeal No. 148 of 2014) [2015] TZCA 416 (14 December 2015)
434. Director of Public Prosecution vs Raymond James Kimario (Criminal Appeal 6 of 2015) [2015] TZHC 2104 (27 May 2015)
435. Director of Public Prosecutions vs Abdallah Sauzi and 3 Others (Criminal Appeal No. 113 of 2016) [2017] TZCA 276 (19 September 2017)
436. Director of Public Prosecutions vs Justine Kakuru Kasusura @John Laizer (Criminal Appeal 107 of 2004) [2004] TZHC 25 (11 October 2004)
437. Director of Public Prosecutions vs Prof. Dr. Costa Mahalu & Another (Criminal Appeal 135 of 2012) [2014] TZHC 2101 (9 May 2014)
438. Director of public Prosecutions vs Justine Kakuru Kasusura @John Laizer (Criminal Appeal 107 of 2004) [2004] TZHC 47 (11 October 2004)
439. Dominion Tanzania Limited vs Commissioner General (TRA) (Civil Appeal 159 of 2021) [2022] TZCA 398 (28 June 2022)
440. Donatus Christoms & Others vs Board of Trustees of NSSF (Civil Case 175 of 2009) [2011] TZHC 2028 (21 February 2011)
441. Doza Electronical Technology Services Limited v. Mary Charles Mwingira & 2 Others (Civil Case No. 150 of 2023) [2024] TZHC 6329 (4 July 2024)
442. Dr. Aman Walid Kaborou and The Attorney General and Another (Civil Appeal 26 of 1997) [2007] TZCA 152 (19 June 2007)
443. Dr. Gabriel Michael Muhagama vs Salum Abass Salum & Others (Civil Appeal 86 of 2006) [2006] TZCA 20 (17 November 2006)
444. Edgar Elias @ Sharo vs Republic (DC Criminal Appeal 16 of 2022) [2022] TZHC 15049 (5 December 2022)
445. Edgar Mugisha Augustine vs Domina Projestus (Misc. Land Case Appeal 29 of 2020) [2021] TZHC 3879 (29 June 2021)
446. Edson Osward Mbogoro vs Dr. Emmanuel John Nchimbi & Another (Civil Appeal Case 140 of 2006) [2007] TZCA 156 (20 September 2007)
447. Edson Swahili Mhele vs Republic (Misc (HC) Criminal Appl. No. 123 of 2004) [2007] TZHC 406 (5 September 2007)
448. Educational Books Publishers Ltd. vs Hasham Kassam & Sons Ltd and Others (Commercial Case 5 of 2011) [2015] TZHC 2022 (4 June 2015)
449. Edwin Denge and 3 Others vs Republic (Criminal Session Case 107 of 2022) [2022] TZHC 11006 (3 August 2022)
450. Electrical Transmission and Distribution Construction and Maintenance Company Limited (etdco) vs Isamilo Supplies Limited (DC Civil Appeal 20 of 2022) [2022] TZHC 15403 (19 December 2022)
451. Elias Kamokyo vs Jasson Kasaizi and Others (Misc. Land Application 32 of 2020) [2021] TZHC 3194 (17 May 2021)
452. Eliasvitus Ndimbo & Another vs Republic (Criminal Appeal 272 of 2007) [2012] TZCA 86 (28 March 2012)
453. Eligius Anord vs Laeli Sinyangwe (Misc. Civil Application No. 4 of 2006) [2007] TZHC 383 (20 December 2007)
454. Elisante Zuberi Challambo vs Mary Alex Kyara & another ((DC) Civil Appeal No. 2 of 2003) [2007] TZHC 463 (6 November 2007)
455. Elizabeth Donald Magazi & 3 Others vs Cosmas John Mdongo (PC Civil Appeal 53 of 2021) [2022] TZHC 10368 (30 June 2022)
456. Elizabeth Kintu vs William Francis (PC Civil Appeal 1 of 2020) [2021] TZHC 4154 (6 July 2021)
457. Elly Millinga vs Republic (Criminal Appeal 268 of 2014) [2015] TZCA 199 (24 August 2015)
458. Emmanuel Bernard Thadeo vs Republic (Criminal Appeal 150 of 2019) [2020] TZHC 2476 (25 August 2020)
459. Emmanuel Chindoma vs Phares Mchali (PC Criminal Appeal 12 of 2016) [2016] TZHC 2101 (12 August 2016)
460. Emmanuel Kalebi (Administrator of Estate of Late Kalebi Mpuku) and Another vs Issa Omari Sumbi and Another (Land Reference No. 2504 of 2024) [2024] TZHC 5619 (11 June 2024)
461. Erick Chanafi vs Republic (RM Criminal Appeal 58 of 2021) [2022] TZHC 11088 (25 July 2022)
462. Ernest Ojode Amuom vs Ezekiel Mosso Nelson (Land Appeal No. 35 of 2022) [2023] TZHC 15713 (28 February 2023)
463. Esrom Petro vs Republic (Criminal Appeal No. 167 of 2015) [2015] TZCA 115 (7 December 2015)
464. Ester Ndechela vs D.P.P (Misc. Criminal Application No. 11 of 2013) [2013] TZHC 2179 (20 November 2013)
465. Esterziah Ayugi vs Joseph Odundo Elijah Ayugi & Others (Civil Revision 184 of 2002) [2005] TZHC 149 (9 May 2005)
466. Esterziah Ayugi vs Joseph Odundo Elijah Ayugi & Others (Civil Revision 184 of 2002) [2005] TZHC 193 (9 May 2005)
467. Estone Eliza vs Nason Rugemalira (Land Case Revision 10 of 2019) [2021] TZHC 2643 (12 March 2021)
468. Eva Mhando vs Republic (Criminal Appeal No. 14 of 2014) [2014] TZHC 2330 (24 November 2014)
469. Ex D. 1995 Pc Ahmed vs Republic (Criminal Appeal No. 207 of 2014) [2015] TZCA 365 (3 December 2015)
470. Executive Director Golden Sands Hotel Ltd Zanzibar vs The Attorney General Zanzibar & Another (Civil Appeal No. 119 of 2015) [2015] TZCA 144 (11 December 2015)
471. Executive Director Golden Sands Hotel Ltd Zanzibar vs The Attorney General Zanzibar & Another (Civil Appeal No. 119 of 2015) [2015] TZCA 418 (11 December 2015)
472. Export Trading Commodities Limited vs Mohamed Enterprises (Tanzania) Limited (Civil Appeal 58 of 2022) [2022] TZHC 15703 (19 December 2022)
473. Ezekia Kalonge vs Schola Kinunda (PC Civil Appeal 34 of 2019) [2020] TZHC 4073 (26 November 2020)
474. Ezekiah T. Oluoch vs Permanent Secretary, President's office Public Service Management & 4 Others (Misc. Civil Case No. 18 of 2017) [2018] TZHC 1465 (12 April 2018)
475. Ezekiah T. Oluoch vs Permanent Secretary, President's office Public Service Managent (Misc. Civil Case No. 18 of 2017) [2018] TZHC 2521 (12 April 2018)
476. Ezrom Petro vs Republic (Criminal Appeal No. 167 of 2015) [2015] TZCA 390 (7 December 2015)
477. Fabiano Luhangano @ Mpwaga vs Republic (RM Criminal Appeal 71 of 2021) [2022] TZHC 14505 (7 November 2022)
478. Farija Athumani Mugaye vs Manager of National Microfinance Bank Ltd (nmb) Bukoba Branch (Land Case Appeal 17 of 2018) [2020] TZHC 957 (21 May 2020)
479. Fatuma Ally Khatibu & Another vs Hussein Bakari Mindia (Misc. Land Appeal 16 of 2019) [2020] TZHC 3803 (13 November 2020)
480. Fatuma Ally Khatibu & Another vs Hussein Bakari Mindia (Misc. Land Appeal 16 of 2019) [2020] TZHC 3804 (13 November 2020)
481. Fatuma Ally Khatibu vs Hussein Bakari Mindia (Land Case 4 of 2017) [2020] TZHC 3801 (13 November 2020)
482. Fayaz Shamji vs the Registered Trustees of Khoja Shia Ithna- Asheri Jamaat Mwanza (Application for Review 2 of 2021) [2021] TZHC 6429 (28 September 2021)
483. Federation of Mines Association of Tanzania & Others vs M/s Africa Gem Resources (AFGEM) & Others (Misc. Civil Case 23 of 2001) [2001] TZHC 7 (22 August 2001)
484. Felix Deogratias andanother vs Detrick Deogratias (Misc. Land Case Appeal 44 of 2019) [2021] TZHC 3388 (31 May 2021)
485. Festo Andrea v. The Republic (Misc. Criminal Application No.43 of 2023) [2023] TZHC 17935 (15 June 2023)
486. Finca Microfinance Bank Ltd v Jalala Hussein (Labour Revision No. 28234 of 2023) [2024] TZHC 1086 (26 March 2024)
487. Fortunatus Nyigama Paul vs Permanent Secretary Ministry of Public and Security & Others (Misc. Civil Cause 27 of 2006) [2009] TZHC 117 (24 July 2009)
488. France Tibenda vs Adija Simon and Others (Misc. Land Application 34 of 2019) [2021] TZHC 3655 (15 June 2021)
489. Francis Alex vs Republic (Criminal Appeal No. 374 of 2013) [2016] TZCA 188 (29 July 2016)
490. Francis Alex vs Republic (Criminal Appeal No. 374 of 2013) [2016] TZCA 822 (11 July 2016)
491. Frank Muneja and Athumani Sabuni vs Republic (Misc. Criminal Economic Application 17 of 2020) [2020] TZHC 968 (11 May 2020)
492. Fransis Alphonce Namilo vs Penina Benjamin Warioba (Land Revision No. 1 of 2022) [2022] TZHC 39 (27 January 2022)
493. Fred Tungu Mpendazoe vs The Attorney General & Others (Misc. Civil Application 98 of 2010) [2011] TZHC 2034 (16 September 2011)
494. Frederick Philemon Kyambile & 80 others vs Omari Kadri & 2 others (Application for Revision 12 of 2023) [2023] TZHCLandD 16557 (13 June 2023)
495. Fredy Jovin @ Sibiye Ngoti vs Republic (Criminal Session Case 47 of 2022) [2022] TZHC 11007 (3 August 2022)
496. Frida Andrew Kaiza vs Vedasto Mugyabuso Kujwalire & Another (Probate & Administration Cause 60 of 2007) [2014] TZHC 2156 (24 July 2014)
497. Gabriel Aplinaly vs. The Republic (Criminal appeal No. 36 0f 2022) [2023] TZHC 17800 (2 June 2023)
498. Ganga Mtemi @ Lutandula vs Republic (Misc. Application 6 of 2022) [2022] TZHC 360 (1 March 2022)
499. Gasaya Bwana @ Chacha vs Republic (Misc. Criminal Application 54 of 2022) [2022] TZHC 9970 (6 June 2022)
500. General Manager Nyanza Bottling co.LTD vs Liberatus N. Tibaitirwa (Civil Revision 1 of 2013) [2014] TZHC 2171 (2 October 2014)
501. Geofrey Kabaka Vs. Farida Hamza & Another (Misc. Land Application No. 104 of 2023) [2023] TZHC 23072 (22 November 2023)
502. George M. Kilindu vs C.R.D.B. (1996) LTD & another (Misc. Civil Cause No. 37 of 1998) [2000] TZHC 41 (7 June 2000)
503. Gervas John vs Leonce Leringo & Others (Civil Case 10 of 2015) [2016] TZHC 2128 (20 June 2016)
504. Gidion Mandesi vs Charles John Mkanga (Misc. Land Application 354 of 2021) [2021] TZHCLandD 857 (23 November 2021)
505. Ginai Bangiri vs. Kisibiri Warioba & Another (Land Appeal 63 of 2022) [2023] TZHC 17667 (1 June 2023)
506. Godfrey Malassy & Another vs Prosper Rweyendera (Misc. Land Application 433 of 2016) [2016] TZHCLandD 2 (27 June 2016)
507. Godfrey Mbilinyi vs Republic (Criminal Appeal 93 of 2020) [2020] TZHC 4409 (1 December 2020)
508. Godfrey Michael Mwamvongo vs. G&B Soap Industries Ltd & 2 Others (Civil Case No. 64 of 2023) [2024] TZHC 6052 (21 June 2024)
509. Godfrey Orango vs Dani Lisubi (Misc Civil Application 43 of 2022) [2023] TZHC 18028 (16 June 2023)
510. Godson Kiranga vs Republic (Criminal Appeal 72 of 2004) [2004] TZCA 61 (4 October 2004)
511. Gozbert Henerico vs Republic (Criminal Appeal 114 of 2015) [2016] TZCA 659 (26 February 2016)
512. Grand Regency Hotel Limited vs Pazi Ally (Civil Application 368 of 2019) [2022] TZCA 539 (6 September 2022)
513. Gulya Mohamed vs Ahmed Makamo (Civil Appeal No. 45 of 2001) [2001] TZHC 34 (8 June 2001)
514. Gumari Kimelezi vs Matyoko John Manyasi (Administrator of the estates of the late Juma Kakwaya Kisanya) (PC Probate Appeal 9 of 2022) [2022] TZHC 9980 (7 June 2022)
515. Gunda Samwel vs Elia Ernest Mpinga (Misc. Civil Application 30 of 2022) [2022] TZHC 15406 (9 November 2022)
516. Halfani Hamadi Kimaro vs Hai District Council ((DC) Civil Appeal No. 1 of 2006) [2007] TZHC 366 (30 May 2007)
517. Halid Maulid vs Republic (Criminal Appeal No. 94 of 2011) [2021] TZCA 225 (4 June 2021)
518. Halmashauri Ya Wilaya Ya Mwabegere vs Hamisi (shaban) Msambaa & Others (Civil Appeal 53 of 2010) [2012] TZCA 181 (2 February 2012)
519. Hamadi s/o Amri vs Republic (Misc. Criminal Application 34 of 2021) [2022] TZHC 334 (28 February 2022)
520. Hamisi Rajabu Dibagula vs Republic (Criminal Appeal 53 of 2001) [2003] TZCA 35 (14 March 2003)
521. Hassan Juma Mtungi vs North Mara Gold Mine (Labour Revision 12 of 2023) [2023] TZHC 22419 (8 November 2023)
522. Hassan Sadick Mloto vs Knight Support (T) LTD (Labour Revision No. 266 of 2013) [2014] TZHC 2387 (16 May 2014)
523. Henrick Willem Timmer vs Anna Kemilembe Bahigana (Civil Revision 22 of 2021) [2022] TZHC 10910 (20 July 2022)
524. Hima Investments Limited vs F.K. Motors Limited (Commercial Case 33 of 2003) [2003] TZHCComD 1 (20 May 2003)
525. Hima Investments Ltd vs F.K. Motors Ltd (Commercial Case No. 33 of 2003) [2003] TZHCComD 30 (20 May 2003)
526. Honoratha Stephano Nkuwi vs Albino Theodory Ghumpi (Land Appeal No. 32 of 2023) [2024] TZHC 446 (26 February 2024)
527. Hussein Raphael & Others vs Republic (Criminal Appeal No. 280 of 2008) [2013] TZCA 346 (4 March 2013)
528. Ibrahim Bakifu Mwanjala vs Florina Pius Mwanjala (Civil Appeal 47 of 2009) [2010] TZHC 7 (3 May 2010)
529. Idd Lugoye vs Republic (PC Criminal Appeal 131 of 2019) [2020] TZHC 685 (3 April 2020)
530. Ipyana Mwambete vs Republic (Criminal Appeal 103 of 2020) [2021] TZHC 2249 (15 February 2021)
531. Islam Saleh Nahdi Ltd vs The Commissioner General (T) Revenue Authority & 2 Others (Commercial Case No. 19 of 2009) [2009] TZHCComD 18 (14 December 2009)
532. Issa Brown Samson vs Republic (Criminal Appeal 102 of 2021) [2022] TZHC 10104 (20 May 2022)
533. Issa Juma @ Issaya Juma vs Republic (Misc. Criminal Application 44 of 2011) [2011] TZHC 2041 (24 November 2011)
534. Issa Maulid Mangara & another vs Tanzania Railways LTD (Revision No. 13 of 2014) [2015] TZHC 2180 (18 March 2015)
535. Issa Omary Sombi and Another v. Emmanuel Kalebi ( Administrator of estates of the late Kalebi Mpuku) and Another (Land Appeal No. 52 of 2022) [2023] TZHC 17782 (13 March 2023)
536. Italfood Limited vs Attorney General Zanzibar & others (Civil Case No. 66 of 2014) [2016] TZHC 2280 (23 August 2016)
537. J. 4020 PC Eustack Julius Manyoriv vs Republic (Misc. Criminal Application 16474 of 2024) [2024] TZHC 6006 (27 June 2024)
538. JCR Enterprises Ltd vs Tanganyika Investment Oil and Transport Co. Ltd & Another (Commercial Case No. 77 of 2007) [2011] TZHCComD 2033 (5 July 2011)
539. Jabiri Hamisi Bakari vs Republic (Criminal Appeal No.5 of 2023) [2023] TZHC 19893 (31 July 2023)
540. Jackson Mwaipopo vs Abdul Berege (Land Appeal 36 of 2022) [2022] TZHC 15502 (19 December 2022)
541. Jackson S-O Ole Nemeteni@ Ole Saibul @ Mdosi @ Mjomba Mjomba & 19 Others vs Attorney General (Misc. Civil Cause 117 of 2004) [2007] TZHC 38 (13 July 2007)
542. Jackson s/o Ole Nemeteni @ Ole Saibul @ Ndosi @ Mjomba Mjomba & Another vs The Attorney General (Misc. Civil Cause 117 of 2004) [2007] TZHC 197 (13 July 2007)
543. Jacquline Westring & Others vs The Attorney General & Another (Misc. Civil Cause No.13 of 2022) [2023] TZHC 19122 (11 July 2023)
544. Jafari Lazima Binamu vs Hassan Chionda & Others (Land Appeal 16 of 2015) [2016] TZHC 14 (28 July 2016)
545. Jaffer Noah vs Charles Cintika (Land Appeal 42 of 2021) [2022] TZHC 15405 (7 November 2022)
546. Jaku Hashim Ayoub vs Executive Secretary Commission of Land ZanzibarZanzibar (Civil Appeal No. 22 of 2016) [2016] TZHC 2166 (15 August 2016)
547. Japhet Ngw'andu vs Republic (Criminal Appeal No. 22 of 2007) [2008] TZHC 274 (21 April 2008)
548. Jasmine Bahasha Salugole vs Michael Ndongo Ngudungu (Civil Appeal No. 7655 of 2024) [2004] TZHC 65 (4 July 2004)
549. Jemima Masimba v. Jeni Mwamila (Land Revision No.8 of 2022) [2023] TZHC 17853 (7 June 2023)
550. Jitu Joram Maiga vs Labani Masatu Mafuru (Misc. Land Appeal 81 of 2022) [2023] TZHC 20210 (14 August 2023)
551. Johari Selemani and Another v. Blas Sebastian Elias (Misc. Land Application No. 90 of 2022) [2023] TZHC 17780 (14 March 2023)
552. John Kirongochi Marwa vs Bunda Town Council & Another (Misc. Civil Application 6253 of 2024) [2024] TZHC 2350 (29 May 2024)
553. John Paul Shibuda & Another vs Nordox Industrier As (Civil Application No. 171 of 2015) [2015] TZCA 540 (23 November 2015)
554. John Paul Shibuda & Another vs Nordox Industrier As (Civil Application 171 of 2015) [2015] TZCA 83 (17 November 2015)
555. John Paul Shibuda & Others vs Nordox Industries (Civil Application 171 of 2015) [2015] TZCA 359 (23 December 2015)
556. John Petro Malima vs Joseph Mataruma Makuri (Land Appeal No. 8 of 2023) [2023] TZHC 15924 (9 March 2023)
557. John Steven & Another vs Republic (Criminal Appeal No. 292 of 2013) [2014] TZCA 223 (23 September 2014)
558. John s/o Boniface Tulla vs Republic (Criminal Appeal 150 of 2020) [2022] TZHC 9753 (27 May 2022)
559. Joram Mwakansope vs Mary Mwanjelwa (DC Civil Appeal 19 of 2022) [2022] TZHC 15404 (2 November 2022)
560. Joseph Ntogwisangu & Others vs The Minister Secretary Ministry of Finance & Another (Consolidated Civil Appeals No. 82 of 2015) [2016] TZCA 926 (5 December 2016)
561. Joseph Nyakiha Daud vs Republic (Criminal Application No. 70 of 2020) [2021] TZCA 309 (16 July 2021)
562. Joseph Tigusaine vs Furgence Ichuchuza and Another (Land Case Revision 4 of 2019) [2021] TZHC 2377 (11 March 2021)
563. Josephat Jones Mwaipopo vs Attorney General & Another (Misc. Civil Cause 52 of 2008) [2011] TZHC 2154 (13 December 2011)
564. Josephat Ludago (as Administrator of the estate of the late Francis Ludago) vs Evaristo Mwipopo (as Administrator of the estate of the late Sadiki Kihalaga) (Land Appeal 9 of 2022) [2022] TZHC 13085 (21 September 2022)
565. Josiah Nsangira vs Anesius K. Stewart and2 Others (Civil Revision 20 of 2021) [2021] TZHC 2384 (11 March 2021)
566. Joyce Buriga & James Mang'erere vs Bwire Nyamwero (PC Civil Appeal 28 of 2021) [2022] TZHC 9622 (25 March 2022)
567. Judith Namangaya vs Straight Auction Mart and Court Brokers 7 Another (Land Appeal 10 of 2012) [2015] TZHC 2038 (14 July 2015)
568. Julias Yapwana Mwapule vs Selfina Co. Ltd (said Hamis) (PC. Civil Appeal 11 of 2019) [2021] TZHC 2245 (10 February 2021)
569. Julius Ishengoma Francis Ndyanabo vs Attorney General (Misc. Civil Cause No. 2 of 2001) [2001] TZHC 44 (28 June 2001)
570. Juma Kuziwa vs Bishop Diocese of Victoria Registered (Land Appeal 1 of 2007) [2007] TZHC 119 (2 October 2007)
571. Juma Ramadhani Hakumu vs Juma Athumani Kilinja and Another (Land Appeal No. 26967 of 2023) [2024] TZHC 2359 (28 May 2024)
572. Juma Swalehe vs Republic (Criminal Application 5 of 2011) [2012] TZCA 198 (20 September 2012)
573. Juma Swalehe vs Republic (Criminal Application 5 of 2011) [2012] TZCA 55 (19 September 2012)
574. Juma Wambura vs Republic (Criminal Appeal 30 of 2020) [2020] TZHC 1740 (24 July 2020)
575. Juma Wambura vs Republic (Criminal Appeal 30 of 2020) [2020] TZHC 2445 (24 July 2020)
576. Kaare Willaim Bulenga vs Manyama Makene (Misc. Appeal 78 of 2021) [2022] TZHC 761 (30 March 2022)
577. Kagwa Luoga and Others vs Attorney General and Another (Misc. Civil Cause 14 of 2020) [2021] TZHC 2620 (19 March 2021)
578. Kaheme Manyemela @ Manoni vs Republic (Criminal Appeal No. 212 of 2014) [2015] TZCA 98 (8 December 2015)
579. Kaltire Mining Group (T) Ltd vs John Kadutu (Commercial Case No. 129 of 2014) [2015] TZHCComD 2219 (12 June 2015)
580. Kashindye Bundala and Another vs The Republic (Criminal Appeal No. 349 of 2009) [2015] TZCA 566 (22 April 2015)
581. Kasi Margwe vs Republic (Criminal Appeal 110 of 2014) [2015] TZHC 2048 (20 August 2015)
582. Kassim Hassan Said @BEDUI vs Republic (Misc. Economic Cause 6 of 2016) [2016] TZHCCED 4 (3 January 2016)
583. Kassim Mwinshehe Mayoli vs Dar es salaam Water Sewarage Authority and 3 Others (Misc. Civil Application No. 15 of 2023) [2023] TZHC 17568 (31 May 2023)
584. Katani A. Katani vs The Returning Officer Tandahima & Others (Civil Appeal 115 of 2011) [2012] TZCA 8 (2 July 2012)
585. Katherina Makore vs Onjack Sospiter (Land Appeal 79 of 2021) [2022] TZHC 9864 (1 June 2022)
586. Kelvin Rajabu Ungele & Others vs Republic (Consolidated Misc. Economic Crimes Applications 1 of 2017) [2017] TZHC 2034 (6 March 2017)
587. Kerem Benjamin @ Jasasu vs Republic (Criminal Appeal No. 389 of 2015) [2016] TZCA 716 (29 June 2016)
588. Kidanile Fungo & others vs Alimu Haji Ngapona (Land Appeal No. 14 of 2013) [2014] TZHC 2363 (18 February 2014)
589. Kiswaga Mitwango vs Republic (Criminal Appeal No. 217 of 2014) [2015] TZCA 372 (11 December 2015)
590. Kiswaga Mitwango vs Republic (Criminal Appeal No. 217 of 2014) [2015] TZCA 99 (11 December 2015)
591. Kiswaga Mitwango vs Republic (Criminal Appeal No. 217 of 2014) [2015] TZCA 100 (9 December 2015)
592. Kolman Msoka vs Aun Said Msangi and Another (Land Case Revision 2 of 2018) [2020] TZHC 3438 (15 October 2020)
593. Kulwa Kulya vs Isaack Mlela (Misc. Land Application 37 of 2017) [2020] TZHC 708 (24 April 2020)
594. Kuruthum Omary Kahiba and Another vs Mwajuma Omary Kahiba (Misc. Civil Cause 4 of 2018) [2020] TZHC 3597 (29 September 2020)
595. Laban Airo vs Olwero Obonyo (Misc. Appeal 107 of 2021) [2022] TZHC 393 (7 March 2022)
596. Laurean Rugambwa vs Tanzania Red Cross Society & Another (Misc. Civil Cause 3 of 2013) [2014] TZHC 2271 (26 March 2014)
597. Laureno Mseya vs Republic (Criminal Application 2 of 2009) [2013] TZCA 362 (27 June 2013)
598. Laurent Chacha vs Twiga Bancorp Ltd (Civil Case 66 of 2007) [2008] TZHC 84 (5 February 2008)
599. Laurent Rugambwa vs Tanzania Red Cross Society and Another (Misc. Civil Cause 3 of 2013) [2014] TZHC 2183 (26 March 2014)
600. Lazarus Mirisho Mafie & Another vs Odilo Gasper Kilenga & Another (Commercial Case 10 of 2008) [2010] TZHCComD 3 (1 October 2010)
601. Legal and Human Rights Center (LHRC) & Others vs Attorney General (Misc. Civil Cause 77 of 2005) [2005] TZHC 159 (1 December 2005)
602. Legal and Human Rights Centre (LHRC) & Others vs Attornery General (Misc. Civil Cause 77 of 2005) [2006] TZHC 76 (5 May 2006)
603. Legal and Human Rights Centre (LHRC) & Others vs Attorney General (1) (Misc. Civil Case 77 of 2005) [2006] TZHC 1 (24 April 2006)
604. Legal and Human Rights Centre (LHRC) & Others vs Attorney General (3) (Mihayo, J.) (Misc. Civil Case 77 of 2007) [2006] TZHC 3 (24 April 2006)
605. Legal and Human Rights Centre (LHRC) & Others vs Attorney General (Misc. Civil Cause 77 of 2005) [2006] TZHC 67 (30 June 2006)
606. Leila Sheikh vs Helman Lupogo & others (Civil Case No. 71 of 2005) [2013] TZHC 2246 (18 February 2013)
607. Leiyan Meshikoki vs The Director of Public Prosecutions (Criminal Appeal 31 of 2009) [2011] TZCA 76 (22 November 2011)
608. Lemi Dhandi @ Makindi vs Republic (Misc. Application 13 of 2022) [2022] TZHC 356 (4 March 2022)
609. Leonard E. Mtepa vs The International Social Security Fund (NSSF) (Civil Appeal 137 of 2012) [2014] TZHC 2059 (18 August 2014)
610. Leonard Savel @ Tweve vs Republic (Criminal Appeal 153 of 2012) [2016] TZCA 690 (5 August 2016)
611. Leonidas Machumi & Others vs Yono Auction Mart & Another (Land Case 160 of 2007) [2013] TZHC 2078 (11 April 2013)
612. Lessa Msigwa vs Republic (DC Criminal Appeal 21 of 2006) [2007] TZHC 151 (19 April 2007)
613. Lipangahela vs Makuhana (Civil Appeal 139 of 2002) [2005] TZHC 15 (25 February 2005)
614. Logolie Lengaisa vs Philipo Levoos (Land Appeal 44 of 2011) [2014] TZHC 2149 (6 March 2014)
615. Lucas Vicent Lwiza vs Republic (Criminal Appeal 13 of 2015) [2015] TZHC 2105 (25 July 2015)
616. Lucia Benedicto vs Salvatory Benedicto and2 Others (Land Case Appeal 106 of 2020) [2021] TZHC 3892 (28 June 2021)
617. Lucy Bismark vs Octavian Rwechungura (PC Criminal Appeal 4 of 2020) [2021] TZHC 3269 (26 May 2021)
618. Lucy Nyagawa vs Nelson Mhoka & 9 Others (Land Appeal 23 of 2020) [2022] TZHC 14609 (14 November 2022)
619. Lukololo Kilosa & Another vs Attorney General & Another (Civil Case 14 of 2015) [2016] TZHC 2165 (27 September 2016)
620. Lwidiko Ramadhani Mbembati vs Mafinga Town Council & 2 Others (Land Case 4 of 2021) [2021] TZHC 9252 (16 December 2021)
621. MS E & A Construction vs Permanent secretary, Ministry of Planning Economy & Empowerment & Another (Misc. Commercial Cause No. 13 of 2007) [2008] TZHCComD 11 (15 August 2008)
622. MS Kalambo Contractors LTD vs Weston Sahawela (Misc. Civil Appeal No. 4 of 2013) [2015] TZHC 2263 (13 August 2015)
623. Mafuru Mwesa vs Wandaga Keya and Another (Civil Appeal 17 of 2021) [2021] TZHC 5846 (31 August 2021)
624. Magambo J. Masato & Others vs Ester Amos Bulaya & Others (Civil Appeal No. 49 of 2016) [2016] TZCA 823 (12 July 2016)
625. Magdalena Aminiel Koka vs.Galila Ramadhani Wabanhu (Civil Appeal No. 04 of 2023) [2023] TZHC 4 (3 August 2023)
626. Mahadhy Mmoto,ahamdad Issa Bilal,ramadhani Mohamed Chikawe,fadhil Slim Akram,rashid Said Kaukutu,martin David Kanangu,marko Makoye Mpina,salum Mohamed Jabu,salum Mohamed Pahi,ally Salum Liomenge and Shaban Sylvestor Mkane vs Republic (Misc. Criminal Application 43 of 2020) [2020] TZHC 4445 (10 December 2020)
627. Majulisho s/o Makombe vs Republic (DC Criminal Appeal 27 of 2022) [2022] TZHC 15051 (5 December 2022)
628. Makoye Kintoki vs Amos Maganga (Misc. Civil Application No. 64 of 2014) [2016] TZHC 2274 (21 June 2016)
629. Makumira Filling Station & 2 Others vs FBME bank ltd (Misc. Commercial Cause No. 24 of 2014) [2015] TZHCComD 2227 (19 February 2015)
630. Maliki Abubakar(The Lawful Attorney and Administrator of the Estate of the Late Hawa Hamisi Mtande) vs Zawadi Rwezaula & others (Misc. Land Application No. 21 of 2015) [2015] TZHC 2158 (10 September 2015)
631. Marco Lushona Sukuma vs Republic (Criminal Appeal No. 307 of 2012) [2014] TZCA 270 (4 March 2014)
632. Mariam Mashaka Faustine & Others vs Attorney General & Another (Consolidated Misc. Civil Cause 88 of 2010) [2011] TZHC 2050 (15 December 2011)
633. Mariam Mashaka Faustine & Others vs Attorney General & Others (Consolidated Misc. Civil Cause 88 of 2010) [2011] TZHC 2024 (15 December 2011)
634. Mariam Nyika vs Apolonia Ivo (Misc. Land Appeal 34 of 2020) [2021] TZHC 4155 (6 July 2021)
635. Martha Emmanuely Shayo vs Jesca Gordon Elias Karlo and Another (Civil Application 171 of 2021) [2023] TZCA 186 (11 April 2023)
636. Mary Asangalwisye Mwatonoka Vs Denkis Mariko & Another (Land Revision No. 3470 of 2024) [2024] TZHCLandD 451 (28 June 2024)
637. Masalu Luponya vs Republic (Criminal Appeal No. 129 of 2015) [2016] TZCA 273 (26 October 2016)
638. Mashaka Juma Ntalula vs Republic (Criminal Appeal No. 159 of 2015) [2015] TZCA 124 (7 December 2015)
639. Masinda Ng'arita vs Abdi Omari (Land Appeal 35 of 2021) [2023] TZHCLandD 146 (17 March 2023)
640. Masunga Charles @ Mulelema @ Nyamatoke vs The Republic (Criminal Revision No. 05 of 2023) [2023] TZHC 18710 (30 June 2023)
641. Matheo Paulo & Another vs Republic (Criminal Appeal No. 398 of 2016) [2019] TZCA 394 (6 November 2019)
642. Mathias Njile Bubinza vs Agricultural Imputes Trust Fund & Others (Civil Case 7 of 2013) [2016] TZHC 2046 (23 June 2016)
643. Mathiasi Njile Bubinza vs Agricultural Imputes Trust Fund & others (Civil Case No. 7 of 2013) [2016] TZHC 2316 (23 June 2016)
644. Mbasa Chitata vs Mosi Waryoba (Misc. Appeal 86 of 2021) [2022] TZHC 491 (16 March 2022)
645. Mechmar Corporation (malaysia) Berhard vs Vip Engineering & Marketing Ltd (Civil Application 9 of 2011) [2011] TZCA 224 (2 June 2011)
646. Meczedeck Maganya vs the Attorney General & Others (Miscellaneous Civil Cause No. 09 of 2023) [2023] TZHC 21704 (2 October 2023)
647. Mengi Machele Mumwi (as Administrator of the late Machele Mumwi Mugeta) vs Simion Jakob (Land Appeal 102 of 2021) [2022] TZHC 10038 (13 June 2022)
648. Mgore Miraji Kigera vs Chuki Mussa (Civil Case 20 of 2023) [2023] TZHC 21265 (29 September 2023)
649. Mgweno Mnyagato & Others vs Republic (Misc. Criminal Application 174 of 2019) [2019] TZHC 22 (16 October 2019)
650. Michael s/o Chaula vs Republic. (Criminal Appeal 81 of 2019) [2020] TZHC 1865 (2 June 2020)
651. Mika Mtweve vs Republic (Criminal Appeal 133 of 2020) [2021] TZHC 2248 (22 February 2021)
652. Mitras International Trading LLC. vs Dodsal Hydrocarbons and Power (T) PVT Ltd and 2 Others (Commercial Case 56 of 2014) [2014] TZHCComD 3 (8 May 2014)
653. Mnanka Sari Matiko @bisare and Sarya Sarya @ Matiko vs Republic (Consolidate Criminal Appeals 45 of 2022; Consolidated Criminal Appl. 44 of 2022) [2022] TZHC 123 (7 February 2022)
654. Mohamed Abdallah Mkuwili vs Republic (Criminal Appeal 235 of 2012) [2016] TZCA 765 (1 March 2016)
655. Mohamed Omari Mwinyi v. Romani Doo (Misc. Land Application 119 of 2022) [2023] TZHC 17776 (10 March 2023)
656. Mordikae Moseti Phanuel vs Republic (Criminal Appeal Case 28 of 2022) [2022] TZHC 14387 (4 November 2022)
657. Morities Corporation Limited vs Crdb Plc & Another (Land Case No. 12 of 2023) [2023] TZHC 23380 (1 December 2023)
658. Moses Francis Kongola vs Nema Richard Sendwa (Legal Representative of the Estate of the Late Richard Magawa Sendwa) and 3Others (Misc. Land Application No. 46 of 2023) [2023] TZHC 21563 (26 September 2023)
659. Mtikila vs Attorney General (Misc. Civil Cause 10 of 2005) [2006] TZHC 5 (5 May 2006)
660. Murtaza Mohamed Viran vs Mehboob Hassanali Versi (Civil Application 266 of 2016) [2020] TZCA 192 (20 April 2020)
661. Mustafa Songambele vs Republic (Criminal Application No. 16 of 2014) [2015] TZCA 287 (18 August 2015)
662. Muzzammil Mussa Kalokola and Others vs Mzumbe Mussa Kalokola (Misc. Probate Application 2 of 2019) [2020] TZHC 971 (19 May 2020)
663. Mwajuma Mohamed Njopeka vs Juma Said Mkorogoro (P.C. Civil Appeal No. 6 of 2001) [2001] TZHC 32 (13 July 2001)
664. Mwanza City Radiators City Company Limited vs Bunda Town Council & Another (Misc. Civil Application 4715 of 2024) [2024] TZHC 2348 (30 May 2024)
665. Mwidewe Madafu vs Elizabeth Barehemana (Application for Reference 2 of 2021) [2022] TZHC 14821 (23 November 2022)
666. Mwigamba Fidson Sosthenes vs National Microfinance Bank (NMB) (Civil Case No. 9 of 2014) [2016] TZHC 2279 (17 June 2016)
667. Nathan Baguma @ Rushejela vs Republic (Criminal Appeal No. 166 of 2015) [2015] TZCA 127 (8 December 2015)
668. National Bank of Commerce Limited vs Millo Construction Company Limited & Others (Misc. Commercial Application 102 of 2015) [2016] TZHCComD 2058 (16 December 2016)
669. National Bank of Commerce Limited vs Millo Construction Company Limited & Others (Misc. Commercial Application 102 of 2015) [2016] TZHCComD 25 (16 December 2016)
670. National Bank of Commerce Ltd vs Attorney General & Others (Misc. Civil Appeal 10 of 2007) [2007] TZHC 192 (29 June 2007)
671. National Bank of Commerce Ltd vs Attorney General & Others (Misc. Civil Application 10 of 2007) [2007] TZHC 122 (29 June 2007)
672. National Bankl Copmmerce Limited vs Pav Investment Limited and 3 Others (Commercial Case 59 of 2011) [2016] TZHCComD 2019 (16 December 2016)
673. National Oil (T) Ltd & Another vs Standard Chartered Bank (T) Ltd (Commercial Case No. 95 of 2005) [2006] TZHCComD 49 (9 February 2006)
674. Nautilus Limited vs Ametan Contractors Limited (Misc. Commercial Cause 11 of 2013) [2016] TZHCComD 2030 (17 October 2016)
675. Nazareno Kihaga vs Republic (Criminal Appeal 12 of 2012) [2016] TZCA 696 (4 August 2016)
676. Nestory Paulo Rugarabamu vs Lageka Company Limited and 4 Others (Land Case Appeal 55 of 2019) [2021] TZHC 3873 (28 June 2021)
677. Ng'weina Matare vs Masyaga Marwa (Misc. Land Appeal Case No. 118 of 2021) [2023] TZHC 19662 (17 January 2023)
678. Nkwabi Shing’oma Lume vs Secretary General, Chama Cha Mapinduzi (Civil Appeal No. 59 of 2022) [2023] TZHC 18579 (30 June 2023)
679. Noela Medard Wambura vs Juma Masagati Mabere (Civil Revision 86814 of 2023) [2024] TZHC 1323 (8 April 2024)
680. Noela Medard Wambura vs Juma Masagati Mabere (Civil Revision 86814 of 2023) [2024] TZHC 380 (22 February 2024)
681. North Mara Gold Mine Limited vs Commissioner General (TRA) (Civil Appeal 78 of 2015) [2016] TZCA 751 (1 March 2016)
682. North Mara Gold Mine vs John Milindi Makoko (Labor Revision 14 of 2023) [2023] TZHC 20526 (31 August 2023)
683. Novat theonest vs Adventina Petro and Another (Misc. Land Application 84 of 2020) [2021] TZHC 2286 (23 February 2021)
684. Numet - North Mara Gold Mine Branch vs North Mara Gold Mine Ltd (Labour Application 28 of 2021) [2022] TZHC 10122 (16 June 2022)
685. Nyaimano Ghati Marwa vs. Republic (Misc. Criminal Application 11 of 2023) [2023] TZHC 17436 (26 May 2023)
686. Nyamhanga Mrimi @ Limo and Merry Onyango @omuga @ Mugesi Mwita @ Magoyo vs Republic (Criminal Appeal 18 of 2022) [2022] TZHC 10754 (25 July 2022)
687. Nyarufunjo Kirongo vs Nyanyama Magesa Mafure (Misc. Appeal) [2022] TZHC 467 (9 March 2022)
688. Nzobarinda Salivatory and 4 Others vs Republic (Criminal Appeal 14 of 2022) [2022] TZHC 12836 (14 September 2022)
689. Odero Charles Odero vs Attorney General of Tanzania & Another (Misc Civil cause No 15 of 2023) [2024] TZHC 698 (4 March 2024)
690. Omary Rashid @ Makoti vs Republic (Criminal Appeal 67 of 2015) [2016] TZCA 235 (12 April 2016)
691. Onesmo Mpinzile vs Tanganyika Law Society & Another (Misc. Civil Cause 3 of 2017) [2017] TZHC 2038 (16 March 2017)
692. Onesmo Olengurumwa vs Attorney General (Misc. Civil Cause 36 of 2019) [2020] TZHC 3664 (21 October 2020)
693. Otieno Oselo Mangasa @Japunda vs The Republic (Misc. Criminal Application 18 of 2023) [2023] TZHC 20313 (21 August 2023)
694. Ottu & Others vs Ubungo Garments (Civil Appeal 194 of 2005) [2008] TZHC 56 (19 June 2008)
695. PATRICK PAUL ITULE VERSUS JANETH ISACK WAITHAKA (Land Appeal No. 552 of 2024) [2024] TZHCLandD 267 (29 April 2024)
696. Pamela Robert @ Raphael vs Republic (Misc. Economic Cause 18 of 2022) [2022] TZHC 9596 (25 May 2022)
697. Parmanent Secretary (establishments) & Another vs Hila Hamed Rashid & Others (Civil Appeal 64 of 2002) [2004] TZCA 54 (4 October 2004)
698. Paschal Maelele and Another vs Nyang'ubha Sibora (Land Revision 9 of 2022) [2022] TZHC 14375 (31 October 2022)
699. Paul Emmanuel Kilasa Kisabo vs Attorney General (Misc. Cause 9 of 2022) [2022] TZHC 12605 (7 September 2022)
700. Paul Juma vs Diesel & Auto Electrict Service (DAS) Ltd & 2 Others (Commercial Case No. 34 of 2005) [2005] TZHCComD 46 (11 July 2005)
701. Paulo Gadye vs Republic (Criminal Appeal No. 199 of 2015) [2015] TZCA 323 (13 October 2015)
702. Paulo Gadye vs Republic (Criminal Appeal No. 199 of 2015) [2015] TZCA 44 (13 October 2015)
703. Permanent Secretary Ministry of Justice and Constitutional Affairs vs K'S Builders Ltd (Misc. Commercial Application No. 6 of 2012) [2012] TZHCComD 74 (28 November 2012)
704. Peter Babeere & others vs Chacha Zakayo Wangwe & another (Misc. Civil Cause No. 03 of 2005) [2006] TZHC 281 (31 August 2006)
705. Peter Claver Bakilana (The liqudatior) TRI- TEL (T) Ltd (In Liqudation) vs Citibank (T) Ltd (Misc. Commercial Cause No. 6 of 2003) [2005] TZHCComD 14 (30 June 2005)
706. Peter Mziray Kuga vs Anne Kilango Malecela & others (Misc. Civil Appl. No. 3 of 2006) [2006] TZHC 187 (20 January 2006)
707. Peter Onesmo vs Republic (DC Criminal Appeal 64 of 2016) [2016] TZHC 2052 (18 November 2016)
708. Petro Chacha @kichere vs Republic (Criminal Appeal 145 of 2021) [2022] TZHC 1132 (11 April 2022)
709. Petro Nyasa & Others vs Simon Domela & Others (Civil Case No. 4 of 2007) [2009] TZHC 271 (9 July 2009)
710. Power and Network Back Up Ltd vs Faraji Iddi (Labour Revision 2 of 2020) [2022] TZHC 11140 (25 April 2022)
711. Pride Tanzania Limited vs Mwanzani Kasatu Kasamia (Misc. Commercial Cause 230 of 2015) [2016] TZHCComD 30 (30 June 2016)
712. Pride Tanzania Limited vs Mwanzani Sakatu Kasamia (Misc. Commercial Cause No. 230 of 2015) [2016] TZHC 2269 (30 June 2016)
713. Prisca Masatu Wajere vs Madaraka Mnada & Another (PC Civil Appeal Case 36 of 2021) [2022] TZHC 9920 (2 June 2022)
714. Priscah Mathias vs Rusalina On'wen (Misc. Appeal 70 of 2021) [2022] TZHC 175 (15 February 2022)
715. Protace Magombo vs Attorney General & Another (Civil Case 197 of 2005) [2010] TZHC 284 (16 September 2010)
716. Rahel Kayanda vs Sofia Byarugaba ((HC) Civil Revision No. 2 of 2002) [2006] TZHC 299 (10 February 2006)
717. Rahma Nyamisango Muzigaba vs Allan Abubakar Makame (Civil Appeal 189 of 2020) [2022] TZHC 11794 (3 June 2022)
718. Rajabu Kassimu vs Republic (Misc. Criminal Application 12 of 2021) [2021] TZHC 4195 (23 July 2021)
719. Ramadhani Hussein vs Imelda Abdallah (Land Case Revision 1 of 2018) [2021] TZHC 2383 (11 March 2021)
720. Ramadhani Mlindwa vs Republic (Criminal Appeal No. 158 of 2015) [2015] TZCA 575 (4 December 2015)
721. Ramadhani Mriri and 2 Others vs Mbati Gari Ouno (Land Case Revision 41 of 2010) [2013] TZHCLandD 5 (27 March 2013)
722. Raphael James Mwinuka & 4 Others vs Republic (Misc. Criminal Application 154 of 2015) [2018] TZHC 2560 (13 April 2018)
723. Raphael Matiko Makolom vs Merengo Gesewani (Misc. Land Appeal 15 of 2023) [2024] TZHC 332 (21 February 2024)
724. Rashid Awami Njowoka vs Fatuma Mustapha (Misc. Civil Application 136 of 2021) [2022] TZHC 15023 (21 February 2022)
725. Rashid Mbedule & Others vs Republic (Consolidate Criminal Appeals 12 of 2022) [2022] TZHC 13087 (21 September 2022)
726. Rashid Salum Adiy vs Minister of Constitution and Legal Affairs and Another (Misc. Civil Cause 30 of 2015) [2017] TZHC 2028 (3 February 2017)
727. Registered Trustees of International Gospel of God vs John Masebo & Another (Land Appeal 24 of 2021) [2022] TZHC 11586 (11 February 2022)
728. Registered Trustees of Redeemed Assembles of God in Tanzania (RAGT) vs Obed Heziron Sichembe & Another (Misc. Land Aplication 20 of 2015) [2016] TZHC 2149 (9 May 2016)
729. Registered Trustees of the Anglican Church of Tanzania vs Reverend Canon Dr. Mecka Okoth Ogunde (Labor Revision 14 of 2022) [2022] TZHC 15431 (27 December 2022)
730. Registereed Trustees of Manyema Mosque vs Africarriers Ltd (Civil Appeal 71 of 2005) [2007] TZHC 49 (26 June 2007)
731. Rehema Emmanuel & Another vs Alois Boniface (Misc. Land Application 8 of 2014) [2014] TZHC 2141 (19 June 2014)
732. Rejoice Ndalima vs The Board of Trustee Pentecostal Holiness Mission (187 of 2021) [2022] TZHCLandD 189 (31 March 2022)
733. Republic vs Abednego s/o Meshack (Criminal Case 42 of 2003) [2008] TZHC 27 (27 February 2008)
734. Republic vs Bisege Mwasomola (Criminal Session Case 3 of 2006) [2007] TZHC 176 (11 September 2007)
735. Republic vs Bisege Mwasomola (Criminal Session Case 3 of 2006) [2007] TZHC 189 (11 September 2007)
736. Republic vs Elvans s/o Cyprian Luvundu (Criminal Session Case 48 of 2003) [2005] TZHC 171 (15 April 2005)
737. Republic vs Media Boastice Mwale & Others (Criminal Appeal No. 2 of 2016) [2016] TZCA 677 (15 September 2016)
738. Republic vs Mwita Koroso Mwita Johanes and Others (Criminal Session Case 28 of 2019) [2020] TZHC 462 (6 March 2020)
739. Rev. Isack Richaed vs. Bishop Solomo Rukumaye & 3 Others (Civil Appeal 31 of 2022) [2023] TZHC 18372 (22 May 2023)
740. Rev. Isack Richard vs. Bishop Solomon Rukumaye & 3 Others (Civil Appeal 31 of 2022) [2023] TZHC 18371 (22 May 2023)
741. Rhobi Isaya Ryoba vs Isaya Ryoba (Misc Civil Application 5 of 2023) [2024] TZHC 812 (14 March 2024)
742. Rhoda Anthony vs Severian X-avery andOthers (Misc. Land Case Appeal 49 of 2019) [2021] TZHC 3654 (18 June 2021)
743. Rikanga vs the republic (Criminal Appeal 72 of 2004) [2004] TZCA 17 (4 October 2004)
744. Robbo Joachim Thobius & 78 Others vs Tanzania National Roads Agency & Another (Misc. Case Appeal 23 of 2022) [2022] TZHCLandD 377 (23 May 2022)
745. Robert John Maitland vs Republic & Others (Criminal Revision No. 13 of 2010) [2016] TZCA 673 (12 February 2016)
746. Rogers Adrian vs Family Planning Association of Tanzania (Misc. Labour Revision No. 4 of 2024) [2024] TZHC 2012 (13 May 2024)
747. Romwald William vs Republic (Criminal Appeal 315 of 2015) [2016] TZCA 674 (26 February 2016)
748. Rozalia Charles vs Charles Kahutu (Misc. Civil Application 25 of 2020) [2021] TZHC 4153 (6 July 2021)
749. Ruvu Gemstone Mining Ltd vs Reliance Insurance Co. Ltd (Misc. Commercial Cause No. 21 of 2016) [2016] TZHCComD 2141 (20 June 2016)
750. SISI Enterprises LTD vs Minister for Lands Human Settlements Development & others (Civil Case No. 47 of 2001) [2003] TZHC 101 (16 October 2003)
751. Saasaba Malembo Matage vs Elias Joshua Mganda (PC Probate Appeal 10 of 2022) [2022] TZHC 3236 (18 May 2022)
752. Sabasaba Enosi vs Republic (Criminal Appeal No 135 of 2015) [2016] TZCA 2086 (26 October 2016)
753. Sadam Ramadhani vs. The Republic (DC Criminal Appeal No. 80 of 2023) [2023] TZHC 22598 (10 November 2023)
754. Sadick Japhary @ Masunzu vs Republic (Criminal Appeal 44 of 2019) [2022] TZCA 675 (7 November 2022)
755. Sagati Wanjara vs Republic (Misc. Criminal Application 39176 of 2023) [2024] TZHC 1317 (8 April 2024)
756. Said Abdallah Nombo vs Republic (Criminal Appeal 142 of 2010) [2011] TZHC 2068 (9 November 2011)
757. Said Thomas Mhombe & Another vs Republic (Consolidated Criminal Appeals 469 of 2019) [2019] TZCA 340 (30 September 2019)
758. Saidi vs Registered Trustees of Manyema Masjid (Civil Appeal 33 of 2004) [2004] TZCA 2 (3 May 2004)
759. Salaam Health Centre vs Mary Kajeba & another (Misc. Labour Application No. 144 of 2014) [2014] TZHC 2323 (19 September 2014)
760. Salem Constrcution Co. Ltd vs B.H. Ladwa Ltd (Misc. Commercial Case No. 12 of 2010) [2011] TZHCComD 2087 (26 September 2011)
761. Salma Mohamed & Others vs Fidda Hussein & Co. Ltd (Misc. Application No. 61 of 2017) [2018] TZHCLD 31 (6 April 2018)
762. Salum Kayanda Kakulu and 1 Another vs Republic (Misc. Criminal Application 40 of 2020) [2020] TZHC 4318 (15 December 2020)
763. Samson S. S. Rumende vs Chief Justice of Tanznaia & Another (Misc. Civil Cause 75 of 2005) [2007] TZHC 53 (18 July 2007)
764. Samwel Apollo Odiero vs Temeke Municipal Council (Misc. Land Application 87 of 2017) [2018] TZHCLandD 83 (13 April 2018)
765. Samwel Muhulo vs. Zebio Real Estate (Application for Revision no. 9 of 2023) [2023] TZHC 17802 (19 May 2023)
766. Saraphina Mbinge vs Salehe Juma and 7 Others (Land Case 123 of 2019) [2021] TZHCLandD 795 (2 November 2021)
767. Selemani David @ Shaban & Others vs The Republic (Criminal Revision No. 03 of 2022) [2023] TZHC 19235 (21 July 2023)
768. Severine Shirima vs. Tanesco (Misc. Civil Application No. 57 of 2022) [2023] TZHC 22579 (13 November 2023)
769. Shaaban Fundi & 5 others vs Attorney General (Misc. Civil Cause 18 of 2022) [2023] TZHC 19068 (20 July 2023)
770. Shaabani Fundi & Others vs The Attorney General (Misc. Civil Cause No.18 of 2022) [2023] TZHC 19120 (20 July 2023)
771. Shabani Issa @ Msongoni vs Republic (Misc. Economic Cause 19 of 2022) [2022] TZHC 9595 (25 May 2022)
772. Shakiru Mohamed vs Jamira Juma (Land Appeal 5 of 2020) [2021] TZHC 3894 (28 June 2021)
773. Shana General Store vs EcoBank Tanzania LTD & Others (Civil Case 36 of 2013) [2014] TZHC 2168 (19 September 2014)
774. Siana John Angasirini vs. Godbless Eliushu Kimaro (Land Appeal 11 of 2020) [2020] TZHC 4586 (11 December 2020)
775. Sida Madirisha vs Republic (Criminal Appeal 62 of 2021) [2021] TZHC 6513 (16 September 2021)
776. Simbinda Kasimbili vs Joseph Mwasibula (Misc. Land Application 37 of 2019) [2020] TZHC 3574 (1 October 2020)
777. Simon Kayoyo Mwalemba vs Republic (Criminal Appeal No. 114 of 2014) [2015] TZCA 522 (1 September 2015)
778. Simon Kayoyo Mwalemba vs Republic (Criminal Appeal 114 of 2014) [2015] TZCA 241 (31 August 2015)
779. Simon Masasi vs Mwashona Village Council and 2 Others (Misc. Land Application 11 of 2020) [2020] TZHC 4412 (14 December 2020)
780. Solomon Mwakatundu vs Kyela District Council & others (Misc. Land Appeal No. 35 of 2013) [2015] TZHC 2270 (19 March 2015)
781. Sospeter Obuye Okey vs D.P.P (Criminal Appl No. 03 of 2014) [2014] TZHC 2332 (27 August 2014)
782. Sospeter Ramadhani and Two others vs. Mchiwa Chedego (Misc. Land Appeal No. 37 of 2023) [2023] TZHC 22767 (20 November 2023)
783. Spedito Pascal Twange vs Republic (DC Criminal Appeal 66 of 2021) [2022] TZHC 11055 (25 July 2022)
784. Star General Insurance (T) Ltd vs Rai Suleiman and Another (Civil Appeal 18 of 2019) [2021] TZHC 3359 (17 May 2021)
785. Steven Amandus Ngonyani vs Amos Ruben (Land Appeal 25 of 2022) [2022] TZHCLandD 12394 (4 October 2022)
786. Steven G. Malipula & Another vs Tanzania Revenue Authority (Civil Appeal No. 50 of 2008) [2014] TZCA 239 (26 September 2014)
787. Stewart Kimambo s/o Kimambo & Others vs Republic (Misc. Criminal Appeal No. 23 of 2007) [2007] TZHC 324 (6 November 2007)
788. Stick s/o Kinzaand Another vs Republic. (Criminal Appeal 106 of 2019) [2020] TZHC 1866 (5 June 2020)
789. Swala Solutions vs Ally Nasib (Labour Revision 8 of 2023) [2023] TZHC 22120 (26 October 2023)
790. TRIACT East Africa Ltd vs Labour Commissioner (Labour Revision No. 03 of 2023) [2023] TZHC 18143 (16 June 2023)
791. Tanganyika Sisal Spinning CO.Ltd vs Attorney General & Another (Misc. Civil Cause 52 of 2006) [2010] TZHC 250 (24 March 2010)
792. Tanzania Cigarette Company Limited vs Elizabeth Kipuyo (Revision No. 326 of 2015) [2016] TZHC 2243 (28 October 2016)
793. Tanzania Heart Institute vs Board of Trustees of N.S.S.F. (Civil Application 109 of 2008) [2008] TZCA 79 (15 August 2008)
794. Tanzania International Container Services Limited vs Abdullahi Hassan Wardere (Civil Appeal 86 of 2012) [2014] TZHC 2055 (29 August 2014)
795. Tanzania Local Government Workers Union (TALGWU) & another vs Attorney General & another (Misc. Labour Application No. 247 of 2014) [2015] TZHC 2198 (4 June 2015)
796. Tenende s. Mwakagile vs Edward Japhet Mbangala & Another (Land Appeal 9 of 2013) [2015] TZHC 2076 (13 February 2015)
797. The Director of Public Prosecutions (Criminal Application 8 of 2023) [2023] TZHC 19946 (7 August 2023)
798. The Registered Trustees of National Convention for Construction and Reform (NCCR MAGEUZI) vs James Francis Mbatia (Misc. Civil Application No. 17 of 2023) [2023] TZHC 17795 (12 June 2023)
799. The Registered Trustees of The Anglican Church of Tanzania vs Paschal Kamuzora & Another (Land Case Appeal 73 of 2019) [2002] TZHC 2003 (30 June 2002)
800. Thomas Mwita Marwa vs Republic (Misc. Criminal Application 10 of 2020) [2020] TZHC 2426 (3 August 2020)
801. Tib Development Bank Limited vs Space & Development Company Limited and 4 Others (Civil Case 167 of 2018) [2022] TZHC 13488 (22 March 2022)
802. Tiluhumula Pima vs Malogoi Muhoyi Hc. Land Revision No. 168 0f 2021 (Land Case Revision 168 of 2021) [2022] TZHC 695 (25 March 2022)
803. Timothy Daniel Kilumile Co. Ltd vs Hillary Patrice Otaiga t/a Nyankanga Filling Service Station (Commercial Case No. 22 of 2014) [2015] TZHCComD 2276 (16 April 2015)
804. Tito Mwang'ombe vs Republic (Criminal Appeal No. 208 of 2014) [2015] TZCA 378 (8 December 2015)
805. Trezia Mwashinga vs Hamis Maisha (PC Civil Appeal No. 5 of 2014) [2016] TZHC 2250 (16 February 2016)
806. Tumaini S. Habimana vs Bulyanhulu Gold Mine Limited (Civil Case 159 of 2011) [2012] TZHC 33 (3 May 2012)
807. VICTOR LAURENT MUSHI VS. REPUBLIC (Misc. Criminal Application No. 6 of 2023) [2023] TZHC 16007 (13 March 2023)
808. Valance Matunda Vs The Assistant Registrar of Titles & 5 Others (Misc. Land Appeal No. 43 of 2023) [2024] TZHCLandD 471 (4 July 2024)
809. Valentine Evarist vs. Jofarin Eneriko (Civil appeal No. 2 of 2022) [2023] TZHC 19812 (31 July 2023)
810. Valerian C. Mlay vs Nathan Alex(Advocate) (Hc Civil Appeal No. 39 of 2016) [2018] TZHC 2692 (10 August 2018)
811. Varentino Augustine Rahisi & Another vs Republic (Consolidated Economic Application 1 of 2006) [2007] TZHC 136 (6 December 2007)
812. Victorino Fidelis Masika vs Oliver Fidelis Masika & Another (Civil Appeal No. 246 of 2021) [2024] TZCA 429 (11 June 2024)
813. Virginia Rukunda Mafuko vs the Commissioner General of Immigration and Another (Misc. Civil Cause 1 of 2020) [2021] TZHC 4036 (5 July 2021)
814. Vitus Kasike vs Elizabeth Hindi (Misc. Land Case Appeal 17 of 2010) [2013] TZHCLandD 7 (29 November 2013)
815. Vitus Yamola and 10 Others vs Republic (Consolidated Misc. Criminal Economic Application 2 of 2020) [2021] TZHC 2937 (12 April 2021)
816. Wambura Sawa and Two Others vs Kagina Noti Zongori and Another (PC Civil Appeal 41 of 2021) [2022] TZHC 10746 (21 April 2022)
817. Watere Waryoba vs Republic (Criminal Application No 64,01 of 2016) [2020] TZCA 1943 (16 March 2020)
818. Wellworth Hotels & Lodges Limited and Another vs Enterprise (Tanzania) Ltd. (Misc. Land Cause 2 of 2010) [2012] TZHCLandD 24 (12 September 2012)
819. Wernery Method Kilowoko vs Republic (Misc. Criminal Application No. 8 of 2013) [2013] TZHC 2206 (20 November 2013)
820. Wikama Nyabusani vs Robert Kituho Waing'ari (Land Appeal 60 of 2021) [2022] TZHC 3014 (27 April 2022)
821. Willium Vincent Maeda vs Happiness Patrick (suing Through Her Next Friend Leokadia Gasper Charahani) (Misc. Land Application 39 of 2017) [2020] TZHC 175 (14 February 2020)
822. Yahaya Athumani Mwaliko (Criminal Appeal 48 of 2012) [2014] TZHC 2092 (23 June 2014)
823. Yahaya Sharif vs Republic (Criminal Application No. 1 of 2015) [2015] TZCA 86 (16 December 2015)
824. Yahaya Sharif vs Republic (Criminal Application No. 1 of 2015) [2015] TZCA 473 (16 December 2015)
825. Yahaya Sharif vs Republic (Criminal Application No. 1 of 2015) [2015] TZCA 745 (16 December 2015)
826. Yusufu Kassim Yusuf (mohamed Mafanya) vs Mohamed Eidha Awadh & 5 Others (Land Application 459 of 2022) [2022] TZHCLandD 12393 (26 September 2022)
827. Yusufu Zziwa vs Tanzania International Container & Others (Civil Appeal 76 of 2008) [2014] TZCA 303 (2 October 2014)
828. Yusuph Mohamed Kastel vs Republic (Misc. Civil Application No. 9 of 2016) [2016] TZHC 2203 (20 Aprili 2016)
829. Zainab Malale vs The Registered Board of Trustees of Muslim Society (Misc. Land Application 40 of 2023) [2023] TZHC 22645 (15 November 2023)
830. Zakaria Kamwela & Others vs The Minister of Education & Vocational Training & Another (Civil Appeal 3 of 2012) [2013] TZCA 448 (12 July 2013)
831. Zanzibar Petroleum Limited vs Hussein J. Kilongo (Revision No. 313 of 2013) [2014] TZHC 2367 (31 July 2014)
832. Zitto Zuberi Kabwe vs President of the United Republic of Tanzania (Misc. Civil Cause 8 of 2022) [2022] TZHC 15339 (5 December 2022)
833. andrew Michael Ulungi and Another vs Registrar of Cooperatives and Others (Misc. Civil Application 31 of 2020) [2022] TZHC 11094 (26 July 2022)
Gazette 13
1. Tanzania Government Gazette dated 2010-01-29 number 5
2. Tanzania Government Gazette dated 2011-12-02 number 48
3. Tanzania Government Gazette dated 2013-03-15 number 11
4. Tanzania Government Gazette dated 2013-03-15 number 94
5. Tanzania Government Gazette dated 2014-12-05 number 49
6. Tanzania Government Gazette dated 2015-09-25 number 39
7. Tanzania Government Gazette dated 2016-01-22 number 4
8. Tanzania Government Gazette dated 2016-04-22 number 17
9. Tanzania Government Gazette supplement number 10 dated 2007-03-09 number 10
10. Tanzania Government Gazette supplement number 15 dated 2017-02-09 number 6
11. Tanzania Government Gazette supplement number 26 dated 2010-07-09 number 28
12. Tanzania Government Gazette supplement number 34 dated 2014-08-29 number 35
13. Tanzania Government Gazette supplement number 5 dated 2010-01-29 number 5
Legislation 10
1. Law Reform (Fatal Accidents and Miscellaneous Provisions) Act 226 citations
2. Public Officers (Salaries and Allowances) Act 13 citations
3. Public Finance Act 12 citations
4. Local Authorities (Elections) Act, 1979 8 citations
5. Disqualification (National Assembly and Miscellaneous Offices) Act 1 citation
6. Parliamentary Services Commission Act 1 citation
7. Tanzania Intelligence and Security Service Act 1 citation
8. Election Complaints Rules, 1990
9. Joint Finance Commission Act
10. Tanzania Court of Appeal Rules, 1979
JOT Documents and Guidelines 3
1. Bail Guidelines
2. Gender Bench Book On Women’s Rights
3. The Tanzania Sentencing Guidelines, 2023
Guidelines 1
1. Asset Forfeiture, Recovery and Management Guidelines
Law Reform Report 1
1. Report on the Review of the Legal Framework on Social Welfare Services in Mainland Tanzania