Kanuni za Matumizi ya Fedha za Kigeni za Mwaka, 2025

Government Notice 198 of 2025

Kanuni za Matumizi ya Fedha za Kigeni za Mwaka, 2025

Tanzania
Bank of Tanzania Act, 2006

Kanuni za Matumizi ya Fedha za Kigeni za Mwaka, 2025

Tangazo la Serikali 198 ya 2025

[Sura 197; Zimetengenezwa chini ya kifungu cha 70]

1. Jina

Kanuni hizi zitajulikana kama Kanuni za Matumizi ya Fedha za Kigeni za mwaka 2025.

2. Matumizi ya shilingi

Bei zote za bidhaa na huduma nchini zitatangazwa kwa shilingi ya Tanzania.

3. Malipo kwa shilingi

(1)Mtu anapaswa kufanya muamala ndani ya nchi kwa kutumia shilingi ya Tanzania pekee.
(2)Kwa kuzingatia masharti ya kanuni ndogo ya (1), mtu anatenda kosa endapo atafanya yafiiatayo:
(a)atalazimisha, atashiriki, atasaidia au kuwezesha upangaji bei ya bidhaa au huduma yoyote nchini kwa kutumia fedha ya kigeni;
(b)atanukuu, atatangaza, atabainisha au kuchapisha bei ya bidhaa au huduma yoyote nchini kwa kutumia fedha ya kigeni;
(c)atalazimisha au kuwezesha malipo ya bidhaa au huduma yoyote nchini kufanyika kwa kutumia fedha ya kigeni;
(d)atakataa bidhaa au huduma yoyote nchini kulipiwa kwa kutumia shilingi ya Tanzania; au
(e)atapokea malipo ya bidhaa au huduma ndani ya nchi kwa kutumia fedha ya kigeni.
(3)Kwa madhumuni ya kanuni ndogo ya (1), “muamala” maana yake ni kunukuu, kutangaza, kubainisha, kuchapisha au kupanga bei au kulipa au kupokea malipo ya bidhaa au huduma ndani ya nchi.

4. Miamala inayoruhusiwa

(1)Miamala iliyoainishwa katika Jedwali inaweza kufanyika kwa kutumia fedha za kigeni.
(2)Waziri, baada ya mashauriano na Gavana, anaweza kuongeza au kupunguza orodha ya miamala ambayo inaweza kufanyika kwa kutumia fedha za kigeni.

5. Katazo kwa mikataba ya malipo kwa fedha ya kigeni

(1)Mtu yeyote hataruhusiwa kuingia mkataba wa bidhaa au huduma kwa malipo ya fedha ya kigeni ndani ya nchi, isipokuwa kwa mkataba unaohusisha malipo yaliyoruhusiwa kwa mujibu wa masharti ya kanuni ya 4.
(2)Bila kuathiri kanuni ndogo ya (1)—
(a)malipo kwa ajili ya wafanyakazi, huduma au bidhaa zitakazonunuliwa nchini wakati wa utekelezaji wa mkataba yatafanyika kwa kutumia shilingi ya Tanzania, isipokuwa kwa mikataba itakayoruhusiwa kwa mujibu wa kanuni ya 4;
(b)mkataba wowote wa utoaji wa bidhaa au huduma ndani ya nchi ulioingiwa kwa fedha ya kigeni kabla ya kuanza kutumika kwa Kanuni hizi utapaswa kufanyiwa marekebisho ndani ya muda wa mwaka mmoja tangu tarehe ya kutangazwa kwa Kanuni hizi.
(3)Mkataba ambao hautafanyiwa marekebisho ndani ya muda ulioainishwa katika kanuni ndogo ya (2)(b) utakuwa batili isipokuwa pale ambapo Waziri atatoa idhini ya kuongeza muda usiozidi muda wa mkataba ulioingiwa.

Jedwali (Limetengenezwa chini ya kanuni ya 4)

Orodha ya miamala inayoweza kufanyika kwa fedha ya kigeni

Na.Aina ya miamala
1.Michango ya uanachama inayolipwa na Serikali kwa taasisi za kikanda zilizopo nchini
2.Miamala inahusisha Balozi na mashirika ya kimataifa yaliyopo nchini
3.Mikopo ya fedha za kigeni inayotolewa na benki za biashara na taasisi za fedha zilizopo nchini
4.Malipo ya bidhaa katika maduka yasiyotoza ushuru
▲ To the top

History of this document

28 March 2025 this version
11 March 2025
Assented to