Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya Mwaka 2022

Chapter 38

Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya Mwaka 2022
This is the latest version of this Act.
Ask AI
Ask questions and understand this document faster using AI.

Tanzania

Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya Mwaka 2022

Chapter 38

  1. [Iliyorekebishwa na Written Laws (Miscellaneous Amendments) Act, 2024 (Tenda 4 ya 2024) hadi 22 Machi 2024]
Sheria ya kuweka masharti ya uwekezaji Tanzania, kuweka masharti ya mazingira bora kwa wawekezaji, kuweka mfumo wa kitaasisi kwa ajili ya uratibu, ulinzi, uvutiaji, uhamasishaji na uwezeshaji wa uwekezaji nchini, kufuta Sheria ya Uwekezaji Tanzania, 1997 na masuala yanayohusiana na hayo.IMETUNGWA na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Sehemu ya kwanza – Masharti ya utangulizi

1. Jina la Sheria na kuanza kutumika

Sheria hii itajulikana kama Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya Mwaka 2022 na itaanza kutumika tarehe ambayo Waziri atateua kupitia tangazo katika Gazeti la Serikali.

2. Matumizi

(1)Kwa kuzingatia kifungu hiki, Sheria hii itatumika kwa taasisi yoyote ya kibiashara iliyokidhi matakwa yaliyoainishwa katika kifungu kidogo cha (2) isipokuwa—
(a)taasisi ya kibiashara iliyoidhinishwa kufanya shughuli za utafiti au uchimbaji wa madini chini ya Sheria ya Madini au inayoomba idhini ya kufanya shughuli nyingine zozote kama hizo;[Sura ya 123]
(b)taasisi ya kibiashara iliyoidhinishwa kufanya shughuli za utafiti au uzalishaji mafuta au kujenga au kuendesha bomba la mafuta chini ya Sheria ya Petroli au inayoomba idhini ya kufanya shughuli nyingine zozote kama hizo; na[Sura ya 392]
(c)taasisi ya kibiashara ambayo inajishughulisha na utengenezaji, utafutaji wa masoko au usambazaji wa kemikali hatarishi, silaha au aina yoyote ya milipuko.
(2)Biashara iliyoainishwa kwa madhumuni ya kifungu hiki ambayo inaweza kupata manufaa na kinga inayotolewa chini ya Sheria hii ni ile ambayo—
(a)ikiwa yote inamilikiwa na mwekezaji wa kigeni au ikiwa ni ubia, kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji si chini ya shilingi za Tanzania sawa na dola laki tano za Marekani (US$ 500,000); au
(b)ikiwa inamilikiwa na Mtanzania, kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji si chini ya shilingi za Tanzania sawa na dola za Marekani elfu hamsini (US$ 50,000).
(3)Bila kujali masharti ya kifungu kidogo cha (1)(a) na (b), masharti ya kifungu cha 28 yanayohusiana na dhamana ya uhamishaji wa mtaji, faida na gawio na kifungu cha 29 kinachohusiana na dhamana dhidi ya utaifishaji yatatumika kwa taasisi yoyote ya kibiashara ambayo ina haki ya madini iliyotolewa chini ya Sheria ya Madini au leseni iliyotolewa chini ya Sheria ya Petroli kana kwamba mmiliki kwa madhumuni ya masharti hayo amepewa cheti cha vivutio na kinga.[Sura ya 123; Sura ya 392]
(4)Hakuna chochote katika kifungu cha 29 kinachohusiana na utaifishaji kitasomwa au kutafsiriwa kuwa kinapunguza au kuongeza haki ya Waziri au Kamishna chini ya au kwa mujibu wa Sheria ya Petroli au Sheria ya Madini kufuta leseni iliyotolewa chini ya sheria hizo.[Sura ya 123; Sura ya 392]
(5)Bila kujali kifungu kidogo cha (1), Kituo kitawahudumia wawekezaji wote, bila kujali kuwa Sheria hii inawahusu au la, na kuwasaidia kupata vibali, idhini, usajili, ridhaa, leseni na suala lolote linalohitajika kisheria kwa mtu kuanzisha na kuendesha shughuli za uwekezaji.

3. Tafsiri

Katika Sheria hii, isipokuwa kama muktadha utahitaji vinginevyo—Bodi” maana yake ni Bodi ya Wakurugenzi ya Kituo iliyoteuliwa chini ya kifungu cha 9;cheti” maana yake ni cheti cha vivutio kilichotolewa chini ya kifungu cha 19(1);Kituo” maana yake ni Kituo cha Uwekezaji Tanzania kilichoanzishwa chini ya kifungu cha 4;manufaa” inajumuisha nyenzo na vivutio vinavyotolewa na au kwa mujibu wa Sheria hii;mtaji” inajumuisha mchango wa fedha taslimu, mitambo, mashine, vifaa, majengo, vipuri, ardhi, hakimiliki na mali nyingine za biashara tofauti na hadhi ambazo hazitumiki katika shughuli za kawaida za biashara na zinazoweza kudumu kwa zaidi ya miezi kumi na mbili;mtaji wa kigeni” inajumuisha fedha zinazoweza kubadilishwa, mtambo, mashine, vifaa, vipuri, malighafi na mali nyinginezo za biashara tofauti na hadhi zinazoingia Tanzania bila malipo ya awali ya fedha za kigeni na zinazokusudiwa kuzalisha bidhaa na huduma zinazohusiana na biashara ambayo Sheria hii inatumika;mwekezaji wa kigeni” ikiwa ni mtu binafsi maana yake ni mtu ambaye si raia wa Tanzania, na ikiwa ni kampuni, maana yake ni kampuni iliyosajiliwa chini ya sheria za nchi yoyote tofauti na Tanzania, kampuni iliyosajiliwa chini ya sheria za Tanzania ambapo zaidi ya asilimia hamsini ya hisa zinamilikiwa na mtu ambaye si raia wa Tanzania, na ikiwa ni ubia, maana yake ni ubia ambapo maslahi makubwa yanamilikiwa na mtu ambaye si raia wa Tanzania;mwekezaji wa ndani” maana yake ni mtu binafsi ambaye ni raia wa Tanzania, kampuni iliyosajiliwa chini ya sheria za Tanzania ambapo hisa nyingi zinamilikiwa na mtu ambaye ni raia wa Tanzania, au ubia ambao maslahi makubwa yanamilikiwa na mtu ambaye ni raia wa Tanzania;nyenzo” zinajumuisha leseni, idhini na vibali vinavyohitajika kwa ajili ya kuanzisha biashara ambazo mwekezaji atapaswa kupata kwa madhumuni ya Sheria hii;taasisi ya kibiashara” maana yake ni kiwanda, mradi, shughuli au biashara ambayo Sheria hii inatumika au upanuzi, urekebishaji, ukarabati au uboreshaji wa kiufundi wa kiwanda, mradi, shughuli au biashara au sehemu yoyote ya biashara, ili mradi taasisi hiyo ya biashara inaendeshwa kwa madhumuni ya kupata faida na kwa misingi ya kibiashara;uwekezaji” maana yake ni uanzishaji au umiliki wa mali mpya za biashara na inajumuisha upanuzi, urekebishaji au ukarabati wa biashara iliyopo;vivutio” maana yake ni nafuu za kikodi, viwango vya kodi vya masharti nafuu au manufaa mengine yoyote anayoweza kupata mwekezaji chini ya sheria yoyote inayotumika kwa wakati huo; naWaziri” maana yake ni Waziri mwenye dhamana ya uwekezaji.

Sehemu ya pili – Kituo cha Uwekezaji na majukumu yake

4. Kuendelea kuwepo kwa Kituo na malengo

(1)Kutaendelea kuwepo na chombo kitakachojulikana kama Kituo cha Uwekezaji Tanzania.
(2)Kituo kitakuwa Wakala wa Serikali na kitakuwa chini ya usimamizi wa jumla wa Waziri.
(3)Kituo kitakuwa taasisi nafsi chenye urithishano endelevu na lakiri na kwa jina lake kitakuwa na uwezo wa—
(a)kumiliki mali inayohamishika na isiyohamishika, kuuza mali na kuingia mkataba au shughuli nyingine yoyote;
(b)kushtaki na kushitakiwa; na
(c)kufanya mambo mengine yoyote ambayo taasisi nafsi inaweza kufanya kwa mujibu wa sheria, kwa ajili ya utekelezaji bora wa majukumu yake chini ya Sheria hii.
(4)Kituo kitakuwa sehemu ya huduma mahala pamoja kwa wawekezaji na kitakuwa ndicho chombo kikuu cha Serikali cha kuratibu, kuhimiza, kuhamasisha na kuwezesha uwekezaji Tanzania na kuishauri Serikali kuhusu sera ya uwekezaji na masuala yanayohusiana na hayo.

5. Kamati ya Taifa ya Uwekezaji

(1)Kwa madhumuni ya kuhamasisha, kuwezesha na kutekeleza kwa ufanisi miradi ya uwekezaji Tanzania, kutakuwa na Kamati ya Taifa ya Uwekezaji itakayokuwa na wajumbe wafuatao:
(a)Waziri Mkuu ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b)Waziri mwenye dhamana ya uwekezaji, ambaye atakuwa Makamu Mwenyekiti;
(c)Mwanasheria Mkuu wa Serikali;
(d)Waziri mwenye dhamana ya mambo ya nje;
(e)Waziri mwenye dhamana ya fedha;
(f)Waziri mwenye dhamana ya ardhi;
(g)Waziri mwenye dhamana ya katiba na sheria;
(h)Waziri mwenye dhamana ya serikali za mitaa;
(i)Waziri mwenye dhamana ya sera na uratibu;
(j)Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
(k)Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania;
(l)Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania, ambaye pia atakuwa Katibu wa Kamati; na
(m)mtu mwingine yeyote atakayealikwa na Waziri kadri itakavyohitajika baada ya kushauriana na Mwenyekiti.
(2)Kamati ya Taifa ya Uwekezaji, miongoni mwa mambo mengine—
(a)itahakikisha kuwa mazingira mazuri kwa uwekezaji katika sekta binafsi na miradi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi yanaendelezwa na kudumishwa;
(b)itaongoza sera ya uwekezaji na kutoa mwelekeo wa pamoja kuhusu Mpango wa Taifa wa Uwekezaji;
(c)itaidhinisha vivutio kwa wawekezaji wa kimkakati na wawekezaji maalum wa kimkakati; na
(d)itasimamia miradi mikubwa yenye matokeo makubwa kitaifa kulingana na ukubwa, mtaji, manufaa ya kiteknolojia na ajira.
(3)Kwa madhumuni ya kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya Kamati ya Taifa ya Uwekezaji, kutakuwa na Kamati ya Wataalam itakayoundwa na wajumbe kutoka katika taasisi za Serikali zinazohusika na uwekezaji kama itakavyoainishwa kwenye Kanuni.
(4)Waziri, baada ya kushauriwa na Bodi, atatengeneza kanuni kwa ajili ya kuweka utaratibu wa utekelezaji wa majukumu ya Kamati ya Taifa ya Uwekezaji na Kamati ya Wataalam.

6. Majukumu ya Kituo

(1)Kwa madhumuni ya kifungu cha 5, Kituo
(a)kitakuwa taasisi kuu itakayotekeleza na kuratibu uimarishaji wa taswira na rajamu ya nchi katika uwekezaji na uhamasishaji wa uwekezaji nchini;
(b)kitaanzisha na kusaidia hatua zitakazoboresha mazingira ya uwekezaji nchini kwa wawekezaji wa ndani na nje;
(c)kitakusanya, kupanga, kuchambua na kusambaza taarifa kuhusu fursa za uwekezaji na vyanzo vya mitaji ya uwekezaji, na pale kitakapoombwa kitatoa ushauri kwa wawekezaji kuhusu upatikanaji na uchaguzi wa wabia wanaofaa katika miradi ya ubia;
(d)kitahamasisha ushiriki wa sekta binafsi katika utoaji wa huduma kwa umma kupitia ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi;
(e)kwa kushauriana na taasisi na wakala za Serikali, kitaainisha maeneo ya uwekezaji, mashamba au ardhi pamoja na huduma zinazohusiana na maeneo, mashamba au ardhi yoyote kwa madhumuni ya wawekezaji na uwekezaji kwa ujumla;
(f)kitawahudumia wawekezaji wote, ikiwa ni pamoja na wale ambao hawafungwi na masharti ya Sheria hii, na kuwasaidia kupata vibali, leseni, ridhaa, idhini, ruhusa, usajili na masuala mengine yanayohitajika kisheria kwa mtu kuanzisha na kuendesha shughuli za uwekezaji na kuwezesha vyeti vinavyotolewa na Kituo kutumika kikamilifu;
(g)kitatunza taarifa kuhusu wawekezaji wote na uwekezaji kwa ujumla;
(h)kitatoa, kuendeleza, kujenga, kubadilisha, ili kuendana na mahitaji, kudumisha na kusimamia maeneo ya uwekezaji, mashamba au ardhi pamoja na nyenzo zinazohusiana na maeneo, mashamba, ardhi hizo na kwa kuzingatia sheria husika, uanzishaji na usimamizi wa maeneo ya uzalishaji kwa mauzo ya nje;
(i)kitaanzisha na kutunza kanzidata ya uwekezaji wa Watanzania nje ya nchi;
(j)kitatoa na kusambaza taarifa zinazoendana na wakati kuhusu manufaa au vivutio vilivyopo kwa ajili ya wawekezaji;
(k)kitashughulikia malalamiko yanayohusiana na uwekezaji;
(l)kitafanya ufuatiliaji na tathmini ya miradi ya uwekezaji iliyo chini ya mamlaka yake;
(m)kitatekeleza na kusaidia shughuli za uhamasishaji wa uwekezaji wa ndani ambazo ni muhimu katika kuhimiza na kuwezesha ongezeko la uwekezaji wa ndani, ikiwa ni pamoja na programu za maendeleo ya ujasiriamali; na
(n)kitatekeleza majukumu mengine yoyote kwa ajili ya kufikiwa kwa malengo ya Sheria hii.
(2)Kwa madhumuni ya utekelezaji wa jukumu lililoainishwa katika kifungu kidogo cha (1)(g), Kituo kwa kushirikiana na mamlaka nyingine zinazosimamia uwekezaji, kitaanzisha mfumo utakaowezesha upatikanaji wa taarifa muhimu za wawekezaji nchini.
(3)Waziri kwa kushirikiana na mawaziri wenye dhamana ya mamlaka nyingine zinazosimamia uwekezaji, atatengeneza kanuni zitakazoainisha namna ya upatikanaji wa taarifa za wawekezaji na wajibu wa kila mamlaka.

7. Fursa za uwekezaji

Kituo kitabainisha fursa za uwekezaji zilizopo nchini na namna ya kuzifikia kwa kushirikiana na mamlaka nyingine zinazohusika.

8. Mfumo unganishi wa kielektroniki

(1)Kituo kitaanzisha mfumo unganishi wa kielektroniki kwa ajili ya uwezeshaji na uhamasishaji wa uwekezaji.
(2)Mfumo unganishi utakaoanzishwa kwa mujibu wa kifungu hiki utaunganisha mamlaka zote muhimu zinazohusika na utoaji wa leseni, vibali, idhini na ridhaa anazohitaji mwekezaji.

9. Bodi

(1)Inaanzishwa Bodi ya Kituo ambayo itawajibika na utekelezaji wa majukumu ya Kituo.
(2)Bodi itakuwa na wajumbe tisa kama ifuatavyo:
(a)Mwenyekiti ambaye atateuliwa na Rais;
(b)wajumbe wawili kutoka sekta binafsi;
(c)wajumbe wanne watakaoteuliwa kutoka—
(i)Wizara yenye dhamana ya fedha;
(ii)Wizara yenye dhamana ya ardhi;
(iii)Wizara yenye dhamana ya mamlaka za serikali za mitaa; na
(iv)Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali; na
(d)wajumbe wengine wawili wenye ujuzi na uzoefu wa kutosha katika masuala ya uwekezaji na usimamizi katika sekta ya umma au binafsi.
(3)Wajumbe waliotajwa katika kifungu kidogo cha (2)(b) hadi (d) watateuliwa na Waziri.
(4)Muda wa wajumbe wa Bodi kushika nafasi utakuwa kama ifuatavyo:
(a)Mwenyekiti - miaka minne; na
(b)wajumbe wengine - miaka mitatu.
(5)Kila mjumbe anaweza kuteuliwa tena kwa muhula mmoja zaidi na baada ya muhula huo kuisha, hatastahili kuteuliwa tena.
(6)Bodi inaweza kumwalika mtu yeyote mwenye utaalam au ujuzi katika suala lolote ambalo Bodi inajadili katika kikao chake, isipokuwa kwamba mtu huyo hatakuwa na haki ya kupiga kura.
(7)Mkurugenzi Mtendaji atakuwa Katibu wa Bodi.
(8)Mjumbe yeyote wa Bodi anaweza kujiuzulu kwa kuitaarifu kimaandishi mamlaka yake ya uteuzi.
(9)Wajumbe wa Bodi watalipwa posho kwa mujibu wa taratibu na miongozo iliyowekwa.
(10)Kwa kawaida Bodi itakutana mara moja kila baada ya miezi mitatu na inaweza kukutana katika kikao cha dharura pale itakapobidi.

10. Mwenendo wa uendeshaji wa Bodi

Kwa kuzingatia masharti ya Sheria hii, Bodi itajiwekea utaratibu wa kuitisha na kuendesha vikao vyake.

11. Kamati za Bodi

(1)Kwa madhumuni ya utekelezaji wa majukumu ya Kituo, Bodi inaweza kuteua Kamati za Bodi zinazojumuisha wajumbe wa Bodi na inaweza kuwapangia majukumu yoyote ambayo Bodi inaweza kuamua.
(2)Kamati ya Bodi inaweza kumwalika mtu yeyote mwenye utaalam au ujuzi katika suala lolote ambalo Kamati inajadili katika kikao chake, isipokuwa kwamba mtu huyo hatakuwa na haki ya kupiga kura.

12. Mkurugenzi Mtendaji

(1)Kutakuwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo ambaye atateuliwa na Rais kwa mapendekezo ya Waziri kuhudumu—
(a)kwa kipindi cha miaka mitano na anaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine cha miaka mitano ambacho hakitaongezwa; na
(b)kwa vigezo na masharti yaliyoainishwa katika hati ya uteuzi wake au kama Bodi inavyoweza kuamua.
(2)Kwa kuzingatia maelekezo ya jumla ambayo Bodi inaweza kutoa, Mkurugenzi Mtendaji atawajibika kwa usimamizi wa kila siku wa Kituo na utekelezaji wa maamuzi ya Bodi.

13. Maafisa na wafanyakazi wengine wa Kituo

(1)Kwa kuzingatia masharti ya sheria zinazosimamia utumishi wa umma, Bodi itaajiri maafisa na wafanyakazi wengine wa Kituo kwa idadi na ngazi mbalimbali kama itakavyohitajika kwa ajili ya utekelezaji bora wa majukumu ya Kituo na kwa vigezo na masharti kama itakavyoamuliwa na Bodi.
(2)Kituo kitaanzisha ofisi za kanda zenye idadi na mgawanyo wa maafisa na wafanyakazi kama Bodi inavyoweza kuamua.
(3)Bodi inaweza kukasimu baadhi ya mamlaka yake chini ya kifungu kidogo cha (1) kwa Mkurugenzi Mtendaji kwa ajili ya uteuzi wa wafanyakazi katika ngazi yoyote inayoweza kuamua.

14. Ukomo wa uwajibikaji kwa wajumbe wa Bodi na wafanyakazi

Mjumbe, afisa au mfanyakazi mwingine wa Kituo hatawajibika kwa nafasi yake binafsi katika mashauri ya madai, kuhusiana na chochote alichotenda au kutotenda kwa nia njema katika utekelezaji wa majukumu yake chini ya Sheria hii.

15. Fedha za Kituo

(1)Fedha kwa ajili ya kukiwezesha Kituo kutekeleza majukumu yake chini ya Sheria hii zitajumuisha—
(a)fedha zitakazoidhinishwa na Bunge kwa ajili hiyo;
(b)ada na tozo zinazotozwa kwa utoaji huduma kwa wawekezaji na wahusika wengine kuhusiana na majukumu ya Kituo chini ya Sheria hii; na
(c)fedha nyingine zozote zitakazopokelewa na Kituo kwa madhumuni ya kutekeleza majukumu yake chini ya Sheria hii.
(2)Ndani ya miezi mitatu kabla ya mwisho wa kila mwaka wa fedha, Kituo kitaandaa na kuwasilisha kwa Bodi kwa ajili ya kuidhinishwa makadirio ya mapato na matumizi ya Kituo kwa mwaka unaofuata na kinaweza, wakati wowote kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha, kuandaa na kuwasilisha kwa Bodi kwa ajili ya idhini makadirio yoyote ya ziada ya mwaka husika.
(3)Kwa kuzingatia maelekezo mengine yoyote ya Bodi, hakuna matumizi yatakayofanywa kwa fedha za Kituo isipokuwa kama matumizi hayo ni sehemu ya matumizi yaliyoidhinishwa na Bodi chini ya makadirio ya mwaka wa fedha ambapo matumizi hayo yatafanyika au katika makadirio ya ziada.
(4)Kwa idhini ya Bodi, Kituo kinaweza kuwekeza fedha zozote zisizohitajika kwa matumizi ya haraka kadri kitakavyoona inafaa.

16. Mwaka wa fedha wa Kituo

Mwaka wa fedha wa Kituo utakuwa kipindi cha mwaka mmoja utakaoishia tarehe 30 Juni.

17. Hesabu, ukaguzi na taarifa

(1)Hesabu za Kituo zitaandaliwa kwa mujibu wa viwango vya hesabu vilivyoidhinishwa na zitakaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ndani ya miezi mitatu baada ya kumalizika kwa mwaka wa fedha.
(2)Mara baada ya hesabu za Kituo kukaguliwa na kwa vyovyote vile si zaidi ya miezi minne baada ya kumalizika kwa mwaka wa fedha, Bodi itawasilisha kwa Waziri nakala ya taarifa ya hesabu zilizokaguliwa pamoja na nakala ya taarifa iliyotolewa na mkaguzi kuhusu hesabu za Kituo.
(3)Ndani ya miezi mitano baada ya kumalizika kwa mwaka wa fedha, Kituo kitaandaa na kuwasilisha kwa Waziri taarifa inayohusu shughuli na uendeshaji wa Kituo katika mwaka husika pamoja na—
(a)nakala ya hesabu za Kituo zilizokaguliwa;
(b)nakala ya taarifa ya mkaguzi kuhusu hesabu; na
(c)taarifa nyingine yoyote ambayo Waziri anaweza kuelekeza.
(4)Ndani ya muda usiozidi miezi mitatu baada ya kupokea hesabu na taarifa ya Kituo, Waziri ataziwasilisha Bungeni.

Sehemu ya tatu – Masharti yanayohusu uwekezaji

18. Kituo cha Huduma Mahala Pamoja

(1)Kwa madhumuni ya kukifanya Kituo kuwa Kituo cha Huduma Mahala Pamoja, idara za Serikali, wakala za Serikali na taasisi nyingine za umma zitashirikiana kikamilifu na Kituo katika utekelezaji wa majukumu chini ya Sheria hii.
(2)Waziri anaweza, baada ya kushauriwa na Bodi kimaandishi, kumuomba Waziri husika kuweka katika ofisi za Kituo maafisa wowote watakaoainishwa na maombi hayo yatatekelezwa.
(3)Bila kujali kifungu kidogo cha (1), endapo leseni au idhini zinahitajika na mwekezaji, Kituo kitawasiliana kwa maandishi na mamlaka husika ili kuhakikisha leseni na idhini zinazohitajika zinapatikana.
(4)Mamlaka husika itakayopokea maombi chini ya kifungu kidogo cha (3) itatoa leseni au idhini inayohitajika au mrejesho kimaandishi wa ushughulikiaji wa maombi husika ndani ya siku saba za kazi baada ya kupokea maombi hayo.
(5)Endapo Kituo hakitapata mrejesho wa ushughulikiaji wa maombi kutoka kwa mamlaka husika ndani ya muda ulioainishwa chini ya kifungu kidogo cha (4), leseni au idhini husika itachukuliwa kuwa imetolewa.
(6)Endapo maombi ya kibali au idhini yatakataliwa na mamlaka husika, mwekezaji anaweza kukata rufaa kwa Waziri mwenye dhamana ya lcscni au idhini husika kwa mujibu wa sheria inayosimamia utoaji wa leseni au idhini hiyo.

19. Maombi ya cheti na usajili

(1)Maombi yote ya vyeti vya vivutio chini ya Sheria hii yatawasilishwa kwenye Kituo na Kituo kitatoa vyeti kwa utaratibu utakaoainishwa kwenye Kanuni.[kifungu kidogo cha (1) kimerekebishwa na kifungu cha 27 cha Act 4 of 2024]
(2)Endapo maombi ni ya uwekezaji mpya, yatakuwa na—
(a)jina na anwani ya taasisi ya kibiashara inayopendekezwa, hadhi yake kisheria, taarifa za benki, majina na anwani za kila mkurugenzi au mbia na jina, anwani, utaifa na umiliki wa hisa kwa kila mwanahisa;
(b)sifa, uzoefu na maelezo mengine muhimu ya wasimamizi wa mradi;
(c)aina ya shughuli ya kibiashara inayopendekezwa na eneo linalopendekezwa ambapo shughuli hiyo itafanyika;
(d)mchanganuo wa mtaji unaopendekezwa au kiasi cha uwekezaji na makadirio ya ukuaji katika kipindi cha miaka mitano ijayo;
(e)taarifa ya namna uwekezaji utakavyofadhiliwa;
(f)uthibitisho wa mtaji wa kutosha unaopatikana kwa uwekezaji; na
(g)ahadi kwamba mradi utatekelezwa kama ilivyooneshwa katika makadirio ya mradi.
(3)Endapo maombi ni kwa ajili ya kukarabati au kupanua biashara iliyopo au vyote kwa pamoja, yatakuwa na—
(a)jina la biashara iliyopo na Katiba yake;
(b)sifa za wasimamizi wa mradi;
(c)taarifa ya hesabu zilizokaguliwa kwa miaka mitatu iliyopita au kipindi kingine chochote kitakachoainishwa kwa biashara ambayo haijatimiza miaka mitatu tangu kuanzishwa;
(d)aina ya ukarabati au upanuzi;
(e)mchanganuo wa mtaji na makadirio ya ukuaji katika kipindi cha miaka mitano ijayo;
(f)ufadhili wa mradi wa ukarabati au upanuzi, pamoja na uthibitisho wa upatikanaji wa fedha; na
(g)ahadi kwamba upanuzi au ukarabati utatekelezwa kama ilivyooneshwa kwenye makadirio.
(4)Kituo kitatunza rejesta ya taasisi za kibiashara zote zilizothibitishwa itakayokuwa na taarifa kadri Bodi itakavyoamua.
(5)Cheti cha vivutio hakitahamishwa au kurekebishwa bila idhini ya Kituo.
(6)Endapo kwa sababu yoyote ile mmiliki wa cheti ataacha kufanya uwekezaji ulioainishwa kwenye cheti, atakitaarifu Kituo kwa maandishi na atastahili kupata haki zote na atakuwa na wajibu chini ya Sheria hii hadi tarehe ambayo aliacha kufanya uwekezaji na kwa tarehe hiyo cheti chake kitachukuliwa kuwa kimeisha muda wake.
(7)Mmiliki wa cheti atakitaarifu Kituo kwa maandishi pale ambapo—
(a)mtu mwingine tofauti na mmiliki wa cheti amerithi uwekezaji;
(b)jina au taarifa za biashara zimebadilika; au
(c)uwekezaji umeongezeka au kuna mabadiliko makubwa katika uwekezaji.
(8)Bila kujali masharti ya kifungu kidogo cha (5), mtu tofauti na mmiliki wa cheti ambaye ameathiriwa na au ana maslahi katika mabadiliko chini ya kifungu kidogo cha (7), anaweza kukitaarifu Kituo ikiwa mmiliki wa cheti atashindwa kukitaarifu Kituo ndani ya muda muafaka.

20. Uhai na kufutwa kwa cheti cha vivutio

(1)Cheti cha vivutio kilichotolewa chini ya Sheria hii—
(a)kuhusiana na vivutio vya kifedha, kitakuwa hai kwa muda usiozidi miaka mitano kuanzia tarehe ya kutolewa; na
(b)kuhusiana na vivutio visivyo vya kifedha, kitakuwa hai kwa kipindi chote cha utekelezaji wa mradi.
(2)Bila kuathiri masharti ya kifungu kidogo cha (1)(a), uhai wa cheti cha vivutio unaweza kuongezwa kwa kipindi kingine kadri itakavyoamuliwa na Kituo baada ya kuwasilisha maombi na sababu za msingi.
(3)Cheti cha vivutio kitafutwa endapo Kituo kitaridhika kwamba—
(a)cheti kilipatikana kwa njia ya udanganyifu au kwa kutoa taarifa za uongo;
(b)mmiliki wa cheti amekiuka masharti ya utoaji wa vivutio;
(c)cheti kimehamishwa kwa mtu au uwekezaji mwingine bila idhini ya Kituo;
(d)mmiliki wa cheti ameshindwa kutimiza wajibu ulioainishwa katika kifungu cha 26;
(e)mmiliki wa cheti hajaanza kutekeleza mradi ndani ya miaka miwili ya kwanza tangu kutolewa kwa cheti bila sababu za msingi; au
(f)mmiliki wa cheti hajawasilisha taarifa za mwaka za utekelezaji na maendeleo ya mradi wa uwekezaji kwa miaka miwili mfululizo.
(4)Utaratibu wa kufuta cheti cha vivutio na masuala mengine kuhusu ukomo wa cheti cha vivutio kwa kuzingatia aina na umuhimu wa mradi wa uwekezaji utakuwa kama itakavyoainishwa kwenye kanuni.

21. Uratibu wa uanzishwaji wa taasisi za kibiashara

Kituo kitaratibu uanzishaji wa taasisi za kibiashara zinazosimamiwa na Sheria hii ikiwa ni pamoja na—
(a)usajili wa taasisi za kibiashara chini ya Sheria ya Makampuni au sheria nyingine yoyote inayohusika na uanzishaji wa biashara; na
(b)kuwezesha wawekezaji kupata leseni, vibali, nyenzo au huduma muhimu.
[Sura ya 212]

22. Manufaa

(1)Taasisi ya kibiashara iliyopewa cheti chini ya Sheria hii itakuwa na haki ya kupata manufaa yanayoendana na biashara hiyo chini ya masharti ya Sheria ya Kodi ya Mapato, Sheria ya Ushuru wa Forodha, Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani au sheria nyingine yoyote inayotumika kwa wakati huo.
(2)Manufaa chini ya kifungu kidogo cha (1) hayatahusisha—
(a)gari lisilotumika moja kwa moja kwenye mradi lililoainishwa chini ya Namba za Utambuzi 8702.10.19, 8702.90.19 na Sura Na. 8703 katika mfumo wa kimataifa wa utambuzi wa bidhaa ili mradi zuio lililowekwa halitahusisha mwekezaji ambaye cheti chake cha vivutio kilitolewa kabla ya au tarehe 30 Juni, 2006;
(b)trela iliyoagizwa kutoka nje ya nchi iliyoainishwa chini ya Namba za Utambuzi 8716.31.90 na 8716.40.90 katika mfumo wa kimataifa wa utambuzi wa bidhaa;
(c)gari lililotengenezwa zaidi ya miaka nane kabla ya kuingizwa nchini;
(d)vifaa vya ofisi, shajara, samani, sukari, vinywaji baridi, pombe kali, vigae, magari yasiyotumika moja kwa moja kwenye mradi, vyombo vya chakula, viyoyozi, majokofu, matandiko, saruji, nondo, mabati, PVC na mabomba ya HDPE yenye Namba za Utambuzi 3917.23.00 na 3917.21.00 katika mfumo wa kimataifa wa utambuzi wa bidhaa mtawalia, matrela na vifaa vya kielektroniki vilivyoagizwa kutoka nje ya nchi;
(e)mawasiliano ya simu, isipokuwa bidhaa za mtaji kwa ajili ya usimikaji wa minara ya mawasiliano ya simu.
(3)Bila kujali masharti ya kifungu kidogo cha (1), msamaha wa ushuru wa forodha utakaotolewa kwa bidhaa za mtaji usio asili utatolewa kwa asilimia 75 ambapo mwckezaji atalipa asilimia 25 ya ushuru unaopaswa kulipwa.

23. Manufaa kwa uwekezaji wa kimkakati au uwekezaji maalum wa kimkakati

(1)Uwekezaji maalum wa kimkakati na uwekezaji wa kimkakati utatambuliwa na kupata vivutio vya ziada kwa mujibu wa masharti ya kifungu hiki.
(2)Bila kujali kifungu cha 2(2), taasisi ya kibiashara itachukuliwa kuwa uwekezaji wa kimkakati ikiwa-
(a)kwabiashara—
(i)inayomilikiwa na Mtanzania, kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji si chini ya shilingi za Tanzania sawa na dola za Marekani milioni ishirini (US$ 20,000,000); na
(ii)inayomilikiwa yote na mwekezaji wa kigeni au kwa ubia, kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji si chini ya shilingi za Kitanzania sawa na dola za Marekani milioni hamsini (US$ 50,000,000);
(b)inazalisha angalau ajira za ndani elfu moja zenye idadi ya kutosha ya nafasi za juu kwenye miradi isiyohitaji teknolojia ya hali ya juu na ya kisasa;
(c)ina uwezo wa kuongeza mauzo ya nje angalau kwa asilimia hamsini ya bidhaa zinazozalishwa au kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje;
(d)ina uwezo wa kuchochea uzalishaji kwa kuanzisha kongani za kiuchumi katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi;
(e)inaongeza ujuzi wa kiufundi kwa kuhaulisha teknolojia mpya kwa watanzania; au
(f)ina uwezo wa kuzalisha bidhaa au kutoa huduma muhimu kwa maendeleo katika sekta za kijamii na kiuchumi kwa kuzingatia vipaumbele kwa wakati huo.
(3)Serikali inaweza kubainisha miradi na kuipa hadhi ya uwekezaji maalum wa kimkakati.
(4)Hadhi ya uwekezaji maalum wa kimkakati inaweza kutolewa kwa mradi unaokidhi vigezo vifuatavyo—
(a)kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji usiopungua shilingi za Tanzania sawa na dola za Marekani milioni mia tatu (US$ 300,000,000); na
(b)miamala ya fedha za mtaji wa uwekezaji inafanywa kupitia taasisi za ndani za kifedha na bima zilizosajiliwa;
(c)angalau ajira za ndani elfu moja na mia tano za moja kwa moja zenye idadi ya kutosha ya nafasi za juu zinazalishwa kwenye miradi isiyohitaji teknolojia ya hali ya juu na ya kisasa; au
(d)uwezo wa kuzalisha kwa kiasi kikubwa mapato ya fedha za kigeni, kuzalisha bidhaa muhimu zitakazopunguza kiwango cha uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi au usambazaji wa nyenzo muhimu zinazohitajika kwa maendeleo katika sekta ya kijamii, kiuchumi au kifedha.
(5)Baada ya mradi kupewa hadhi ya uwekezaji wa kimkakati au uwekezaji maalum wa kimkakati, Waziri atapendekeza kwa Kamati ya Taifa ya Uwekezaji vivutio maalum vya ziada.
(6)Bila kujali mamlaka ya Waziri chini ya kifungu kidogo cha (5), vivutio vitakavyopendekezwa havitahusisha vivutio katika vifaa vya ofisi, shajara, samani, sukari, vinywaji baridi, pombe kali, vigae, magari yasiyotumika moja kwa moja kwenye mradi, vyombo, viyoyozi, jokofu, matandiko, saruji, nondo, mabati, PVC na mabomba ya HDPE yenye Namba ya Utambuzi 3917.23.00 na Namba ya Utambuzi 3917.21.00 katika mfumo wa kimataifa wa utambuzi wa bidhaa mtawalia, matrela yaliyoagizwa kutoka nje ya nchi yenye Namba ya Utambuzi 8716.31.90 na vifaa vya kielektroniki vyenye Namba ya Utambuzi 8716.40.90 katika mfumo wa kimataifa wa utambuzi wa bidhaa.
(7)Endapo Kamati ya Taifa ya Uwekezaji itaidhinisha vivutio maalum vya ziada, vivutio hivyo vitatolewa kwa mujibu wa sheria husika.
(8)Kamati ya Taifa ya Uwekezaji inaweza kupitia kila mradi uliopewa vivutio maalum vya ziada kuhusiana na uzingatiaji wa masharti ya vivutio vilivyotolewa na kuishauri Serikali kuhusu kuendelea kutoa au kusitisha vivutio hivyo.

24. Manufaa na vivutio vinavyosimamiwa na sheria nyingine

Endapo mtu anastahili manufaa au vivutio vya kifedha au visivyo vya kifedha chini ya Sheria hii na manufaa au vivutio hivyo vinasimamiwa na sheria nyingine, manufaa au vivutio hivyo vitatolewa kwa mujibu wa masharti ya sheria husika.

Sehemu ya nne – Haki na Wajibu wa Serikali na Wawekezaji

25. Haki ya kusimamia uwekezaji

Serikali itakuwa na haki ya kuchukua hatua zote za kusimamia uwekezaji ili kuhakikisha kuwa shughuli za uwekezaji nchini zinaendeshwa kwa kuzingatia misingi na malengo ya Sheria hii na madhumuni ya kisera ya kijamii na kiuchumi.

26. Wajibu wa mwekezaji

Mwekezaji anayetambulika na Sheria hii atakuwa na wajibu ufuatao:
(a)kutii sheria za nchi;
(b)kuwasilisha kwa wakati taarifa zinazohitajika na taasisi zinazohudumia wawekezaji ili kuziwezesha kutekeleza majukumu kwa ufanisi;
(c)kuendesha shughuli za uwekezaji kwa namna inayolinda walaji, mazingira, usawa wa kijinsia na kuendeleza ujuzi kwa wafanyakazi;
(d)kuwasilisha kwa Kituo taarifa za mwaka za utekelezaji na maendeleo ya mradi wa uwekezaji;
(e)kutumia malighafi na rasilimali nyingine zinazopatikana au kuzalishwa nchini; na
(f)kuruhusu maafisa wa Kituo kufanya ufuatiliaji wa vivutio vilivyotolewa kwa mujibu wa Sheria hii.

27. Dhamana dhidi ya kurekebishwa au kubadilishwa kwa manufaa

Kwa madhumuni ya kuweka mazingira ya uwekezaji yanayotabirika, taasisi ya kibiashara ambayo imepewa vivutio chini ya Sheria hii itakuwa na haki ya kunufaika na vivutio husika vilivyotolewa, na katika kipindi cha miaka mitano kuanzia tarehe ya kutolewa, vivutio hivyo havitarekebishwa au kubadilishwa kwa namna itakayomuathiri mwekezaji.

28. Dhamana ya uwekezaji, uhamishaji wa mitaji, faida na gawio

Kwa kuzingatia kifungu hiki, taasisi ya kibiashara inayosimamiwa na Sheria hii inahakikishiwa kuwa, kwa kupitia benki yoyote iliyoidhinishwa na kwa aina ya fedha inayoweza kubadilishwa kwa uhuru, itaweza kuhamisha bila masharti—
(a)faida halisi au gawio linalotokana na uwekezaji;
(b)malipo yanayohusiana na urejeshaji wa mkopo pale ambapo mkopo umepatikana kutoka nje ya nchi;
(c)mapato, baada ya makato ya kodi na malipo mengine, endapo taasisi ya kibiashara itauzwa au kufilisika au faida yoyote inayotokana na uwekezaji; na
(d)malipo ya stahiki na marupurupu mengine kwa wafanyakazi wa kigeni walioajiriwa nchini Tanzania katika taasisi ya kibiashara.

29. Kinga dhidi ya utaifishaji au utwaaji

(1)Kwa kuzingatia vifungu vidogo vya (2) na—
(a)taasisi ya kibiashara haitataifishwa au kutwaliwa na Serikali; na
(b)mtu anayemiliki mtaji wote au sehemu ya mtaji wa taasisi ya kibiashara hatalazimishwa na sheria kusalimisha maslahi yake ya mtaji kwa mtu mwingine.
(2)Serikali haitatwaa taasisi ya kibiashara au sehemu ya taasisi ya kibiashara inayosimamiwa na Sheria hii isipokuwa kama utwaaji huo ni kwa mujibu wa sheria inayoweka masharti ya-
(a)malipo ya fidia ya haki na kwa wakati; na
(b)haki ya kwenda mahakamani au kwenye vyombo vya usuluhishi kwa ajili ya uamuzi wa maslahi au haki ya mwekezaji na kiasi cha fidia anachostahili kupata.
(3)Fidia yoyote inayolipwa chini ya kifungu hiki italipwa kwa wakati na idhini ya kurejeshwa kwa fidia hiyo katika aina ya fedha inayoweza kubadilishwa itatolewa pale inapohitajika.

29A. Hadhi ya mwekezaji wa kigeni

(1)Kwa kuzingatia masharti ya Sheria hii, sheria nyingine za nchi, mikataba na makubaliano ya kimataifa ambayo Tanzania ni Nchi Mwanachama, mwekezaji wa kigeni atapata fursa sawa na ile anayostahili kupata mwekezaji Mtanzania kuhusiana na uanzishaji, utwaaji, uendelezaji, usimamizi, uendeshaji na uuzaji au uondoshaji mwingine wa uwekezaji ndani ya nchi.
(2)Kwa kuzingatia masharti ya Sheria hii, Sheria nyingine za nchi, mikataba na makubaliano ya kimataifa ambayo Tanzania ni Nchi Mwanachama, mwekezaji wa kigeni hatabaguliwa kwa misingi ya uraia wake, eneo la makazi au mahali alipoandikishwa au kusajiliwa au nchi ya asili ya uwekezaji.
(3)Masharti ya kifungu hiki hayatatafsiriwa—
(a)kuizuia Serikali kuchukua hatua za udhibiti au hatua nyingine ili kulinda maslahi ya umma, kama vile maadili ya umma, afya ya umma, usalama na ulinzi wa mazingira;
(b)kuizuia Serikali kuchukua jitihada zozote za kuwawezesha wawekezaji wa ndani;
(c)kuilazimisha Serikali kutoa kwa mwekezaji wa kigeni na uwekezaji wake manufaa ya matibabu, upendeleo au fursa yoyote iliyomo katika—
(i)eneo lolote la biashara huria, umoja wa forodha, makubaliano ya soko la pamoja, makubaliano yoyote ya kimataifa au mipango ambayo nchi anayotoka mwekezaji si mshirika; au
(ii)makubaliano yoyote ya kimataifa yaliyopo au ya siku zijazo au sheria ya ndani inayohusu ushuru.
[kifungu cha 29A kimeingizwa na kifungu cha 28 cha Act 4 of 2024]

30. Ukomo wa idadi ya wafanyakazi wa kigeni

Kila taasisi ya kibiashara iliyopewa cheti cha vivutio chini ya Sheria hii itaruhusiwa kuwa na wafanyakazi wa kigeni kwa kuzingatia ukomo wa idadi ulioainishwa katika sheria inayosimamia masuala ya ajira kwa wageni:Isipokuwa kwamba, kwa madhumuni ya masharti ya kifungu cha 18, Kituo kitaratibu na kuwezesha upatikanaji wa haki inayotolewa chini ya kifungu hiki.

31. Upatikanaji wa mikopo kwa wawekezaji wa kigeni kutoka vyanzo vya ndani.

(1)Kwa kuzingatia kifungu cha 2, mwekezaji wa kigeni anaweza, kuhusiana na biashara anayoendesha, kupata mikopo kutoka benki na taasisi za fedha za ndani hadi kufikia ukomo uliowekwa na Benki Kuu ya Tanzania kwa kushauriana na Kituo kwa kuzingatia kiasi cha mtaji wa kigeni uliowekezwa katika taasisi ya kibiashara.
(2)Mwekezaji wa kigeni anayepata mkopo kwa mujibu wa kifungu kidogo cha (1) atahakikisha kwamba mapato ya mkopo huo yanatumika kwa madhumuni ya kutekeleza shughuli zilizoainishwa katika maombi yake ya mkopo.
(3)Benki inayotoa mkopo inaweza, kwa madhumuni ya kifungu hiki, kuteua afisa au wakala wake ili kuthibitisha matumizi sahihi ya mkopo uliotolewa chini ya kifungu kidogo cha (1).

Sehemu ya tano – Masharti ya Jumla

32. Rufaa na mapitio

(1)Mtu ambaye hataridhika na uamuzi uliotolewa na Kituo chini ya Sheria hii anaweza kukata rufaa kwa Waziri.
(2)Mwekezaji ambaye hataridhika na uamuzi wa Kamati ya Taifa ya Uwekezaji kuhusu uidhinishaji wa vivutio anaweza kuwasilisha maombi kwa Kamati hiyo ili iweze kupitia tena uamuzi wake.
(3)Utaratibu wa kukata rufaa au kuwasilisha maombi ya mapitio utaainishwa kwenye kanuni.

32A. Utaratibu wa utatuzi wa malalamiko

(1)Endapo mwekezaji hakuridhishwa na mwenendo, kitendo au uamuzi wa taasisi ya Serikali kuhusu masuala ya uwekezaji, anaweza kuwasilisha maombi katika Kituo kwa ajili ya utatuzi wa malalamiko yake.
(2)Maombi kwa mujibu wa kifungu kidogo cha (1) hayataathiri haki nyingine za kisheria za mwekezaji katika kutafuta utatuzi wa kisheria wa malalamiko.
(3)Kituo kitachunguza na kufanya tathmini ya malalamiko na kuchukua hatua stahiki zinazokubalika na pande zote kutatua malalamiko husika.
(4)Utaratibu wa utatuzi wa malalamiko utazingatia misingi ya haki, uwazi na uzingatiaji wa sheria, na taasisi zote husika zitalazimika kushirikiana na Kituo katika jitihada zake za kutafuta suluhisho linalokubalika kwa pande zote.
(5)Kituo kitatakiwa kutatua malalamiko ndani ya siku thelathini kuanzia tarehe ya kupokea malalamiko hayo.
(6)Endapo mlalamikaji hakuridhishwa na uamuzi wa Kituo au kwa namna nyingine yoyote, hakuridhishwa na namna ambavyo Kituo kinashughulikia malalamiko hayo, anaweza kuwasilisa malalamiko hayo kwa Waziri kwa utatuzi.
(7)Taarifa na nyaraka zilizopokelewa na Kituo wakati wa utaratibu wa utatuzi wa malalamiko zitachukuliwa kuwa siri.
(8)Waziri anaweza, kwa kushauriana na Bodi, kutengeneza kanuni kwa ajili ya kuweka taratibu za utatuzi wa malalamiko ya wawekezaji.
[kifungu cha 32A kimeingizwa na kifungu cha 29 cha Act 4 of 2024]

33. Utatuzi wa migogoro

(1)Endapo mgogoro utatokea kati ya mwekezaji na Kituo au Serikali kuhusu taasisi ya kibiashara, juhudi zote zitafanywa ili kutatua mgogoro huo kwa njia ya majadiliano ili kufikia suluhu.
(2)Mgogoro kati ya mwekezaji na Kituo au Serikali kuhusu taasisi ya kibiashara ambao utashindwa kusuluhishwa kwa majadiliano unaweza kuwasilishwa katika vyombo vya usuluhishi kwa kuzingatia mojawapo ya njia zifuatazo kama zitakavyokubaliwa na pande zote-
(a)kwa mujibu wa sheria za usuluhishi za Tanzania;
(b)kwa mujibu wa kanuni za utaratibu wa usuluhishi wa Kituo cha Kimataifa cha Usuluhishi wa Migogoro ya Uwekezaji; au
(c)ndani ya makubaliano yoyote baina ya nchi mbili au zaidi kuhusu kinga ya uwekezaji yaliyofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya nchi anayotokea mwekezaji.

34. Makosa na adhabu

(1)Mtu ambaye wakati wa utekelezaji wa majukumu yake ya kikazi katika usimamizi wa Sheria hii anamiliki au anasimamia nyaraka au taarifa yoyote iliyopatikana chini ya Sheria hii na ambaye atawasilisha nyaraka au taarifa hiyo au sehemu ya nyaraka au taarifa hiyo kwa mtu mwingine yeyote ambaye hajaidhinishwa kwa sheria yoyote au na Bodi, anatenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyozidi shilingi milioni tano au kifungo kisichozidi mwaka mmoja au vyote.
(2)Mwajiriwa wa Kituo ambaye ana wajibu wa kutekeleza chini ya Sheria hii na ameshindwa kutekeleza wajibu huo au ametekeleza wajibu huo kwa uzembe atachukuliwa hatua za kinidhamu ambazo Bodi au mamlaka husika ya nidhamu inaweza kuamua.
(3)Mtu ambaye—
(a)kwa kujua au kwa uzembe anatoa taarifa za uongo au za kupotosha;
(b)anakataa au anapuuza kutoa taarifa ambayo Kituo kinaweza kuhitaji kwa madhumuni ya utekelezaji wa Sheria hii; au
(c)anakataa bila sababu halali kumruhusu afisa aliyeidhinishwa kuingia kwenye eneo lake la biashara au vinginevyo anazuia ukaguzi wowote unaofanywa na afisa aliyeidhinishwa katika kutekeleza majukumu yake ya ufuatiliaji, anatenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyopungua shilingi milioni tano na isiyozidi shilingi milioni kumi au kifungo kisichopungua miezi sita na kisichozidi miezi kumi na mbili au vyote.
(4)Endapo kosa limetendwa na taasisi mkurugenzi, mbia, afisa mkuu wa usimamizi au afisa anayehusika katika taasisi hiyo atachukuliwa pia kuwa ametenda kosa hilo.

35. Kanuni

Waziri, baada ya kushauriwa na Bodi, anaweza kutengeneza kanuni kwa ajili ya kutekeleza masharti ya Sheria hii.

36. Kufutwa kwa Sheria

Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya Mwaka 1997 inafutwa.[Na. 26 ya Mwaka 1997]

37. Masharti ya mpito

(1)Bila kujali kufutwa kwa Sheria chini ya kifungu cha 36, cheti cha vivutio kilichotolewa au makubaliano yaliyoingiwa chini ya Sheria iliyofutwa yataendelea kuwa halali kwa kuzingatia vigezo na masharti ya kutolewa au kuingiwa kwake kana kwamba cheti hicho cha vivutio kimetolewa au makubaliano hayo yameingiwa chini ya Sheria hii, na yatakuwa halali hadi mwisho wa muda ambao mmiliki au mnufaika wake alikuwa na haki ya kunufaika na manufaa, vivutio au kinga yoyote; na baada ya kumalizika kwa muda ulioainishwa masharti ya Sheria hii yataanza kutumika.
(2)Kwa kuzingatia kifungu kidogo cha (1), mtu mwenye cheti cha vivutio kwa mujibu wa vigezo na masharti ya Sheria iliyofutwa, hatadai manufaa, kinga au vivutio vyovyote chini ya Sheria hii hadi baada ya kumalizika kwa muda ulioainishwa katika kifungu kidogo cha (1).
(3)Suala lolote linaloendelea mbele ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania kilichoanzishwa chini ya Sheria iliyofutwa litahesabiwa kuwa linaendelea mbele ya Kituo.
(4)Makubaliano yoyote yanayoendelea kwa mujibu wa kifungu hiki yatatoa manufaa ambayo yalikuwa yakitolewa awali chini ya makubaliano hayo kabla ya kuanza kutumika kwa Sheria hii.
(5)Endapo taasisi ya kibiashara iliyokuwepo kabla ya kuanza kutumika kwa Sheria hii imezingatia ipasavyo masharti ya Sheria iliyofutwa, kuhusiana na matakwa yoyote ya kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji ulioainishwa katika Sheria iliyofutwa, taasisi hiyo ya kibiashara itachukuliwa kuwa halali bila kujali masharti yoyote ya Sheria hii yanayoeleza vinginevyo.

History of this document

22 March 2024 this version
31 December 2023
Chapter 38

Revised Laws 2023

Consolidation
Read this version
27 November 2022
Assented to

Subsidiary legislation

To the top