Sheria ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi, 2025

Act 6 of 2025

There are outstanding amendments that have not yet been applied. See the History tab for more information.
Sheria ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi, 2025
Ask AI
Ask questions and understand this document faster using AI.

Tanzania

Sheria ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi, 2025

Tenda 6 ya 2025

Sheria ya kuweka masharti ya uendelezaji wa uwekezaji na mazingira bora kwa wawekezaji Tanzania, kuweka mfumo wa kitaasisi kwa ajili ya uratibu, ulinzi, uvutiaji, uhamasishaji na uwezeshaji wa uwekezaji nchini, uendelezaji na usimamizi wa maeneo maalumu ya kiuchumi, kufuta Sheria ya Uwekezaji Tanzania, 2022, Sheria ya Maeneo Maalumu ya Uzalishaji kwa Mauzo ya Nje, 2002, Sheria ya Maeneo Maalumu ya Kiuchumi, 2006 na masuala yanayohusiana na hayo.

Sehemu ya kwanza – Masharti ya utangulizi

1. Jina

Sheria hii itajulikana kama Sheria ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi ya Mwaka 2025.

2. Matumizi

(1)Sheria hii itatumika kwa mwekezaji yeyote isipokuwa—
(a)mwekezaji aliyeidhinishwa kufanya shughuli za utafiti au uchimbaji wa madini chini ya Sheria ya Madini au anayeomba idhini ya kufanya shughuli nyingine zozote kama hizo;[Sura ya 123]
(b)mwekezaji aliyeidhinishwa kufanya shughuli za utafiti au uzalishaji mafuta au kujenga au kuendesha bomba la mafuta chini ya Sheria ya Petroli au anayeomba idhini ya kufanya shughuli nyingine zozote kama hizo; na[Sura ya 392]
(c)mwekezaji anayejishughulisha na utengenezaji, utafutaji wa masoko au usambazaji wa kemikali hatarishi, silaha au aina yoyote ya milipuko.
(2)Bila kujali kifungu kidogo cha (1), Mamlaka itawahudumia wawekezaji wote, bila kujali kuwa wako nje ya wigo wa Sheria hii, na kuwasaidia kupata vibali, idhini au suala lolote linalohitajika kisheria kwa mtu kuanzisha na kuendesha shughuli za uwekezaji.

3. Tafsiri

Katika Sheria hii, isipokuwa kama muktadha utahitaji vinginevyo:Bodi” maana yake ni Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka iliyoteuliwa chini ya kifungu cha 8;cheti” maana yake ni cheti cha uwekezaji kinachotolewa na Mamlaka kwa mwekezaji anayewekeza katika eneo lililo nje ya eneo maalumu la kiuchumi kwa kuzingatia masharti ya Sheria hii;eneo la forodha” maana yake ni eneo lililoteuliwa kama eneo la forodha kwa mujibu wa sheria inayosimamia masuala ya forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki;eneo maalumu la kiuchumi” maana yake ni eneo la ardhi lililoanzishwa kwa mujibu wa kifungu cha 26;leseni” maana yake ni idhini iliyotolewa na Mamlaka kwa ajili ya uendelezaji wa miundombinu, uendeshaji au uzalishaji katika eneo maalumu la kiuchumi;Mamlaka” maana yake ni Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania iliyoanzishwa chini ya kifungu cha 4;mamlaka ya forodha” maana yake ni Mamlaka ya Mapato Tanzania;mtaji” inajumuisha mchango wa fedha taslimu, mitambo, mashine, vifaa, majengo, vipuri, ardhi, hakimiliki na mali nyingine za biashara tofauti na hadhi ambazo hazitumiki katika shughuli za kawaida za biashara na zinazoweza kudumu kwa zaidi ya miezi kumi na mbili;mtaji wa kigeni” inajumuisha fedha zinazoweza kubadilishwa, mtambo, mashine, vifaa, vipuri, malighafi na mali nyinginezo za biashara tofauti na hadhi zinazoingia Tanzania bila malipo ya awali ya fedha za kigeni na zinazokusudiwa kuzalisha bidhaa na huduma zinazohusiana na biashara inayosimamiwa na Sheria hii;mwekezaji wa kigeni” maana yake ni—(a)mtu binafsi ambaye si raia wa Tanzania;(b)kampuni iliyosajiliwa chini ya sheria za nchi yoyote tofauti na Tanzania inayofanya uwekezaji wa moja kwa moja nchini;(c)kampuni iliyosajiliwa chini ya sheria za Tanzania ambapo asilimia hamsini au zaidi ya hisa zinamilikiwa na mtu ambaye si raia wa Tanzania; au(d)ikiwa ni ubia, ni ubia ambao sehemu kubwa ya maslahi inamilikiwa na mtu ambaye si raia wa Tanzania;mwekezaji wa ndani” maana yake ni mtu binafsi ambaye ni raia wa Tanzania, kampuni iliyosajiliwa chini ya sheria za Tanzania ambayo sehemu kubwa ya hisa inamilikiwa na raia wa Tanzania, au ubia ambao sehemu kubwa ya maslahi inamilikiwa na raia wa Tanzania;uwekezaji” maana yake ni mchango wa mtaji wa ndani au wa kigeni kutoka kwa mwekezaji unaohusisha uanzishaji au ununuzi wa mali mpya kwa ajili ya biashara, na inajumuisha upanuzi au ukarabati wa biashara iliyopo;vivutio” maana yake ni misamaha ya kodi, nafuu za kodi au manufaa mengine yoyote anayoweza kupata mwekezaji chini ya sheria yoyote inayotumika; naWaziri” maana yake ni Waziri mwenye dhamana ya uwekezaji.

Sehemu ya pili – Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania

4. Kuanzishwa kwa Mamlaka

(1)Kutakuwa na Mamlaka itakayojulikana kama Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania.
(2)Mamlaka itakuwa ni chombo huru chenye urithishano endelevu na lakiri na kwa jina lake itakuwa na uwezo wa—
(a)kumiliki mali zinazohamishika na zisizohamishika;
(b)kushtaki na kushtakiwa;
(c)kuingia mkataba au makubaliano mengine yoyote; na
(d)kufanya jambo lolote linaloweza kufanyika kwa mujibu wa sheria kwa ajili ya utekelezaji bora wa majukumu yake chini ya Sheria hii.
(3)Mamlaka itakuwa sehemu ya huduma mahala pamoja kwa wawekezaji na itakuwa ndicho chombo kikuu cha Serikali cha kuratibu, kuhimiza, kuhamasisha na kuwezesha uwekezaji Tanzania na kuishauri Serikali kuhusu sera ya uwekezaji na maeneo maalumu ya kiuchumi.

5. Malengo ya uanzishwaji wa Mamlaka

Mamlaka inaanzishwa kwa lengo la kuwa sehemu ya huduma mahala pamoja kwa wawekezaji na itakuwa ndicho chombo kikuu cha Serikali cha kuratibu, kuhimiza, kuhamasisha na kuwezesha uwekezaji Tanzania na kuishauri Serikali kuhusu sera ya uwekezaji.

6. Majukumu ya Mamlaka

Mamlaka itatekeleza majukumu yafuatayo:
(a)kuratibu uhamasishaji, uwezeshaji, usimamizi na uendelezaji wa uwekezaji nchini;
(b)kuratibu uimarishaji wa taswira na rajamu ya nchi katika uwekezaji;
(c)kufuatalia mwenendo wa uwekezaji na kuishauri Serikali kuhusu hatua za kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini kwa kuzingatia mabadiliko ya kiuchumi yanayotokea ndani na nje ya nchi;
(d)kukusanya, kupanga, kuchambua na kusambaza taarifa kuhusu fursa na vivutio vya uwekezaji na vyanzo vya mitaji ya uwekezaji;
(e)kupendekeza kwa Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji vivutio vya uwekezaji kwa wawekezaji wa kimkakati;
(f)kuhamasisha ushiriki wa sekta binafsi katika uwekezaji kwenye miradi ya ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi;
(g)kuwezesha wawekezaji kupata huduma muhimu za uwekezaji zinazohusu usajili na uendeshaji wa uwekezaji;
(h)kusajili wawekezaji wa ndani na wa kigeni;
(i)kutoa leseni kwa wawekezaji katika maeneo maalumu ya kiuchumi;
(j)kushughulikia malalamiko yanayohusu uwekezaji;
(k)kufanya ufuatiliaji na tathmini ya shughuli za uwekezaji zinazotekelezwa nchini;
(l)kusimamia, kuratibu na kujenga miundombinu ya msingi na wezeshi kwenye maeneo maalumu ya kiuchumi na kuratibu ushiriki wa sekta binafsi katika ujenzi wa miundombinu;
(m)kuainisha maeneo ya uwekezaji kwa kuzingatia aina ya uwekezaji kwa kushauriana na wadau muhimu katika sekta ya umma na sekta binafsi;
(n)kukusanya taarifa zinazohusu miradi ya uwekezaji kutoka taasisi mbalimbali kwa ajili ya kuhuisha rejesta ya uwekezaji na kuandaa taarifa ya uwekezaji;
(o)kutafuta, kuendeleza, kukodisha na kusimamia maeneo ya uwekezaji kwa kuzingatia sheria husika; na
(p)kutekeleza majukumu mengine yoyote kwa ajili ya kutimiza malengo ya Sheria hii.

7. Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji

(1)Kutakuwa na Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji itakayokuwa na wajumbe wafuatao:
(a)Waziri Mkuu ambaye atakuwa Mwenyekiti;
(b)Waziri mwenye dhamana ya uwekezaji, ambaye atakuwa Makamu Mwenyekiti;
(c)Waziri mwenye dhamana ya mambo ya nje;
(d)Waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha;
(e)Waziri mwenye dhamana ya mipango au uchumi;
(f)Waziri mwenye dhamana ya ardhi;
(g)Mwanasheria Mkuu wa Serikali;
(h)Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania;
(i)Kamishna Mkuu wa Mamlaka wa Mapato Tanzania;
(j)wajumbe watatu watakaoteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuiwakilisha sekta binafsi; na
(k)Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka, ambaye atakuwa pia Katibu wa Kamati.
(2)Bila kuathiri kifungu kidogo cha (1), Kamati inaweza kumualika waziri yeyote wa kisekta ambaye si mjumbe kushiriki kikao cha Kamati kwa madhumuni ya kutoa mchango kuhusu uwekezaji katika sekta anayoisimamia.
(3)Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji itakuwa na majukumu yafuatayo:
(a)kupendekeza kwa Baraza la Mawaziri uidhinishaji wa vivutio vya ziada kwa wawekezaji wa kimkakati;
(b)kuidhinisha mipango na mikakati ya kitaifa ya kuendeleza uwekezaji kwa mujibu wa vipaumbele vya Taifa;
(c)kuhakikisha kuwa kuna mazingira mazuri kwa uwekezaji katika sekta binafsi na miradi ya uwekezaji katika sekta binafsi inaendelezwa na kudumishwa;
(d)kusimamia miradi mikubwa yenye matokeo makubwa kitaifa kulingana na ukubwa, mtaji, manufaa ya kiteknolojia na ajira; na
(e)kuidhinisha uanzishwaji na usimamizi wa maeneo ya uwekezaji wa kimkakati.
(4)Kwa madhumuni ya kuwezesha utekelezaji wa majukumu ya Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji, kutakuwa na Kamati ya Wataalamu itakayoundwa na wajumbe kutoka katika taasisi za Serikali zinazohusika na uwekezaji.
(5)Waziri, baada ya kushauriwa na Bodi, atatengeneza kanuni kwa ajili ya kubainisha muundo na utaratibu wa uteuzi wa wajumbe wa Kamati ya Wataalamu na utekelezaji wa majukumu ya Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji na Kamati ya Wataalamu.

8. Bodi ya Mamlaka

(1)Kutakuwa na Bodi ya Mamlaka ambayo itakuwa na wajibu wa kusimamia uendeshaji wa shughuli za Mamlaka.
(2)Bodi itakuwa na wajumbe tisa kama ifuatavyo:
(a)Mwenyekiti ambaye atateuliwa na Rais; na
(b)wajumbe wengine nane watakaoteuliwa na Waziri kama ifuatavyo:
(i)mjumbe kutoka Wizara yenye dhamana ya uwekezaji;
(ii)mjumbe kutoka Wizara yenye dhamana ya fedha;
(iii)mjumbe kutoka Wizara yenye dhamana ya ardhi;
(iv)mjumbe kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali;
(v)mjumbe kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania; na
(vi)wajumbe wengine watatu kutoka sekta binafsi wenye taaluma, ujuzi na uzoefu katika masuala ya uwekezaji na biashara.
(3)Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka atakuwa Katibu wa Bodi.
(4)Utaratibu na masuala mengine kuhusu Bodi ya Mamlaka yatakuwa kama ilivyoainishwa katika Jedwali.

9. Majukumu na mamlaka ya Bodi

(1)Bodi ya Mamlaka itakuwa na majukumu na mamlaka yafuatayo:
(a)kuandaa sera za ndani na kutoa miongozo ya kimkakati ya utekelezaji wa miradi, mipango, programu na mikakati ya Mamlaka;
(b)kuidhinisha mipango, taarifa, hesabu na bajeti ya Mamlaka;
(c)kuhakikisha kuwa utekelezaji na uendeshaji wa shughuli za Mamlaka unazingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo;
(d)kuamua na kusimamia utekelezaji wa vipaumbele vya Mamlaka kwa kuzingatia mipango, mikakati na programu mbalimbali za kitaifa, kikanda na kimataifa;
(e)kufuatilia utendaji na kuhakikisha kuna matumizi sahihi na yenye ufanisi ya rasilimali za Mamlaka;
(f)kusimamia utekelezaji wa vipaumbele vya Wizara katika Mamlaka;
(g)kupitisha kanuni za fedha, kanuni za utumishi, miundo, motisha za watumishi kabla ya kuwasilishwa kwenye mamlaka za idhini;
(h)kuthibitisha vigezo vya uteuzi na masharti ya ajira kwa watumishi wa Mamlaka;
(i)kutoa malengo ya kiutendaji na kutathmini utendaji wa uongozi na kuchukua hatua stahiki;
(j)kuwa mamlaka ya nidhamu kwa wajumbe wa menejimenti ya Mamlaka kwa kuzingatia sheria na kanuni;
(k)kuidhinisha kanuni za maadili za watumishi wa Mamlaka; na
(l)kutekeleza majukumu mengine yoyote kadiri itakavyoonekana inafaa kwa ajili ya kukuza na kuwezesha utekelezaji wa malengo ya Mamlaka.
(2)Bila kuathiri kifungu kidogo cha (1), Bodi inaweza kukasimu utekelezaji wa majukumu yake kwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka.

10. Mkurugenzi Mkuu

(1)Kutakuwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ambaye atateuliwa na Rais.
(2)Mkurugenzi Mkuu atakuwa afisa masuuli na atakuwa na wajibu wa kusimamia shughuli za kila siku za Mamlaka.
(3)Mkurugenzi Mkuu atashika madaraka kwa kipindi cha miaka mitano na anaweza kuteuliwa kwa kipindi kingine kimoja.

11. Watumishi wa Mamlaka

(1)Kwa kuzingatia masharti ya sheria zinazosimamia utumishi wa umma, Bodi itaajiri watumishi kwa idadi na ngazi mbalimbali kama itakavyohitajika kwa ajili ya utekelezaji bora wa majukumu ya Mamlaka.
(2)Bila kuathiri mamlaka ya Bodi, Mkurugenzi Mkuu atasimamia nidhamu ya watumishi wa Mamlaka kwa kuzingatia sheria na taratibu za utumishi wa umma.

Sehemu ya tatu – Uwezeshaji wa uwekezaji

12. Kituo cha Huduma Mahala Pamoja

(1)Kwa madhumuni ya kuiwezesha Mamlaka kuwa Kituo cha Huduma Mahala Pamoja, taasisi zote za Serikali zitashirikiana kikamilifu na Mamlaka katika utekelezaji wa majukumu chini ya Sheria hii.
(2)Waziri anaweza, baada ya kushauriwa na Bodi, kumuomba Waziri anayesimamia sekta yoyote kuweka katika ofisi za Mamlaka maafisa wowote watakaobainishwa katika maombi husika kwa madhumuni ya kuhakikisha ufanisi katika utendaji wa Kituo cha Huduma Mahala Pamoja.
(3)Afisa wa umma anayehudumia wawekezaji katika Kituo cha Huduma Mahala Pamoja—
(a)atatoa huduma kwa wakati na kwa kuzingatia sheria na taratibu zinazosimamia majukumu yake; na
(b)endapo maombi yanashughulikiwa na mtu mwingine ambaye hayupo katika Kituo, atakuwa na wajibu wa kufanya ufuatiliaji ili kuhakikisha kuwa taasisi anayoiwakilisha inatoa huduma husika kwa wakati.
(4)Pamoja na utaratibu wa kuwa na Kituo cha Huduma Mahala Pamoja, Mamlaka inaweza kuanzisha ofisi za kanda kwa madhumuni ya kupanua wigo wa kuhudumia wawekezaji nchini.

13. Huduma zinazotolewa nje ya Kituo cha Huduma Mahala Pamoja

(1)Endapo huduma anayohitaji mwekezaji haipatikani katika Kituo cha Huduma Mahala Pamoja, Mamlaka itawasiliana kwa maandishi na taasisi husika ili kuhakikisha kuwa mwekezaji anapata huduma husika.
(2)Taasisi itakayopokea maombi chini ya kifungu kidogo cha (1) itatoa huduma inayohitajika au mrejesho kimaandishi wa ushughulikiaji wa maombi husika ndani ya siku saba za kazi baada ya kupokea maombi hayo.
(3)Endapo Mamlaka haitapata mrejesho wa ushughulikiaji wa maombi ndani ya muda ulioainishwa chini ya kifungu kidogo cha (2) au maombi yatakataliwa, Mamlaka itawasiliana na Waziri mwenye dhamana ya huduma inayoombwa.

14. Mfumo unganishi wa kielektroniki

(1)Kutakuwa na mfumo unganishi wa kielektroniki kwa ajili ya uwezeshaji na uhamasishaji wa uwekezaji ambao utasimamiwa na kuratibiwa na Mamlaka.
(2)Mfumo unganishi utakaoanzishwa kwa mujibu wa kifungu hiki utaunganisha mamlaka zote muhimu zinazohusika na utoaji wa leseni, vibali, idhini na ridhaa anazohitaji mwekezaji.
(3)Isipokuwa kama imeelekezwa vinginevyo katika sheria inayosimamia mamlaka husika, mamlaka zote zinazotoa huduma kwa wawekezaji zitahakikisha kuwa huduma zake zinaunganishwa na kuweza kutolewa kupitia mfumo unganishi wa kielektroniki.

15. Usajili wa wawekezaji

(1)Kila mwekezaji anayekusudia kufanya uwekezaji wowote Tanzania atapaswa kusajiliwa na Mamlaka kabla ya kuanza shughuli za uwekezaji.
(2)Utaratibu wa usajili chini ya kifungu hiki utaainishwa katika kanuni.
(3)Baada ya kusajiliwa na Mamlaka, mwekezaji atapaswa kuzingatia masharti na taratibu zinazosimamia shughuli ya uwekezaji anayokusudia kufanya.

16. Maombi ya cheti au leseni

(1)Mwekezaji anaweza kufanya maombi kwa Mamlaka kwa ajili ya kupata—
(a)cheti cha uwekezaji kwa shughuli za uwekezaji katika eneo tofauti na eneo maalumu la kiuchumi; au
(b)leseni ya uwekezaji kwa shughuli za uwekezaji katika eneo maalumu la kiuchumi.
(2)Cheti au leseni inaweza kutolewa kwa uwekezaji mpya, ukarabati au upanuzi.
(3)Utaratibu wa maombi, sifa na vigezo vya kupata cheti au leseni utaainishwa katika kanuni.

17. Maombi ya cheti au leseni

(1)Mwekezaji hatahamisha au kurekebisha cheti au leseni bila idhini ya Mamlaka.
(2)Mamlaka inaweza kufuta cheti au leseni iliyotolewa chini ya Sheria hii endapo itaridhika kwamba—
(a)cheti au leseni ilipatikana kwa njia ya udanganyifu au kwa kutoa taarifa za uongo;
(b)cheti au leseni imerekebishwa au kuhamishwa kwa mtu au uwekezaji mwingine bila idhini ya Mamlaka;
(c)mwekezaji ameshindwa kutimiza wajibu ulioainishwa chini ya Sheria hii;
(d)mwekezaji hajaanza kutekeleza mradi ndani ya miezi kumi na mbili kuanzia kutolewa kwa cheti au leseni bila sababu ya msingi; au
(e)mwekezaji hajawasilisha taarifa za utekelezaji na maendeleo ya mradi wa uwekezaji kwa miezi ishirini na nne mfululizo.

18. Kubadili au kuacha uwekezaji

(1)Endapo mwekezaji ataacha kufanya uwekezaji ulioainishwa kwenye cheti au leseni, ataitaarifu Mamlaka kwa maandishi na atastahili kupata haki zote na ataendelea kuwa na wajibu chini ya Sheria hii kutokana na uwekezaji wake hadi kufikia tarehe aliyoacha kufanya uwekezaji.
(2)Mwekezaji mwenye cheti au leseni ataitaarifu Mamlaka kwa maandishi pale ambapo—
(a)mtu mwingine tofauti amerithi uwekezaji;
(b)jina au taarifa za biashara zimebadilika; au
(c)uwekezaji umeongezeka au kuna mabadiliko makubwa katika uwekezaji.
(3)Mtu yeyote ambaye ameathirika na mabadiliko au ana maslahi katika mabadiliko yaliyofanyika katika uwekezaji, anaweza kuitaarifu Mamlaka ikiwa mwekezaji husika atashindwa kuitaarifu Mamlaka ndani ya miezi sita.

19. Vivutio vya uwekezaji

(1)Mwekezaji mwenye cheti anaweza kupata vivutio vya uwekezaji vya kikodi na visivyo vya kikodi vinavyotolewa chini ya Sheria ya Kodi ya Mapato, Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani au sheria nyingine inayotumika kwa wakati huo.
(2)Mwekezaji mwenye leseni katika eneo maalumu la kiuchumi anaweza kupata vivutio vifuatavyo kama vilivyoainishwa katika sheria husika:
(a)msamaha wa ushuru wa forodha, kodi ya ongezeko la thamani na kodi nyingine yoyote inayotozwa kwenye mali ghafi na bidhaa za mtaji katika uzalishaji;
(b)msamaha wa kodi ya mapato ya kampuni kwa kipindi cha miaka kumi ya mwanzo;
(c)msamaha wa kodi ya zuio kwenye pango, gawio na riba kwa miaka kumi ya mwanzo;
(d)msamaha wa kodi ya zuio kwenye riba katika mikopo kutoka nje ya nchi;
(e)msamaha wa kodi, ada na tozo zinazotozwa na mamlaka za serikali za mitaa kwa bidhaa zinazozalishwa katika maeneo maalumu ya kiuchumi kwa kipindi cha miaka kumi ya mwanzo;
(f)msamaha wa ushuru wa forodha, kodi ya ongezeko la thamani na kodi nyingine inayopaswa kulipwa wakati wa uingizaji wa gari moja kwa ajili ya huduma za utawala, magari ya kubebea wagonjwa, magari ya zimamoto na mabasi yasiyozidi mawili kwa ajili ya usafirishaji wa wafanyakazi kuelekea na kutoka katika maeneo maalumu ya kiuchumi;
(g)viza ya biashara wakati wa kuingia nchini kwa wafanyakazi kwa muda usiozidi miezi miwili;
(h)bidhaa zinazoingizwa nchini kwa ajili ya maeneo maalumu ya kiuchumi kupewa hadhi sawa na bidhaa zinazosafirishwa kwenda nchi nyingine kupitia Tanzania;
(i)msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani kwenye huduma za maji, umeme, gesi na simu;
(j)msamaha wa tozo za bandari;
(k)msamaha wa ushuru wa stempu kwenye nyaraka zozote zinazohusiana na uhamishaji, ukodishaji au uwekaji dhamana wa mali inayohamishika au isiyohamishika iliyo katika eneo maalumu la kiuchumi; na
(l)msamaha wa kodi ya ongezeko la thamani kwenye vifaa vya ujenzi na huduma za ujenzi.
(3)Vigezo vya kupata vivutio kwa kuzingatia aina ya leseni katika eneo maalumu la kiuchumi vitaainishwa katika kanuni.
(4)Kwa madhumuni ya kuondoa shaka, vivutio vilivyorejewa katika kifungu hiki vitatolewa kwa mujibu wa masharti na taratibu zilizoainishwa katika sheria zinazosimamia vivutio hivyo.
(5)Mamlaka, kwa kushirikiana na taasisi nyingine za Serikali, itabuni vivutio visivyo vya kikodi kwa ajili ya kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.
[Sura ya 332, 147 na 148]

20. Orodha ya vivutio vya uwekezaji

(1)Kwa madhumuni ya kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wawekezaji, Mamlaka itaandaa orodha ya vivutio vinavyotolewa kwa wawekezaji kwa mujibu wa sheria mbalimbali.
(2)Mamlaka itatangaza orodha ya vivutio iliyoandaliwa chini ya kifungu kidogo cha (1) katika Gazeti la Serikali na kupitia njia nyingine yoyote itakayowezesha taarifa kuhusu vivutio husika kufikiwa na wawekezaji kwa urahisi.

21. Mwekezaji wa kimkakati

(1)Mwekezaji anaweza kupewa hadhi ya kuwa mwekezaji wa kimkakati endapo—
(a)kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji
(i)si chini ya shilingi za Tanzania sawa na dola za Marekani milioni ishirini (US$ 20,000,000) kwa mwekezaji wa ndani; au
(ii)si chini ya shilingi za Tanzania sawa na dola za Marekani milioni hamsini (US$ 50,000,000) kwa mwekezaji wa kigeni;
(b)atatimiza vigezo vingine vitakavyoainishwa katika kanuni.
(2)Pamoja na vivutio vinavyoweza kutolewa kwa mwekezaji kwa mujibu wa sheria husika, mwekezaji wa kimkakati anaweza kupata vivutio vya ziada vitakavyopendekezwa na Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji.
(3)Baada ya Kamati ya Taifa ya Maendeleo ya Uwekezaji kupendekeza vivutio vya ziada chini ya kifungu kidogo cha (2), Waziri atawasilisha mapendekezo hayo Baraza la Mawaziri kwa ajili ya kuridhiwa.

22. Fursa kwa mwekezaji wa ndani

Waziri, kwa kushauriana na Waziri mwenye dhamana ya fedha, anaweza kubainisha maeneo mahsusi ambayo wawekezaji wa ndani wanaweza kupewa vivutio kwa kuzingatia Sheria husika.

23. Benki ya ardhi

(1)Kutakuwa na benki ya ardhi itakayokuwa chini ya usimamizi wa Mamlaka.
(2)Benki ya ardhi itakuwa ni kanzi data inayohifadhi taarifa kuhusu ardhi inayopatikana kwa ajili ya uwekezaji.
(3)Benki ya ardhi itajumuisha ardhi kutoka—
(a)maeneo yaliyotengwa na mamlaka husika kwa ajili ya uwekezaji;
(b)maeneo yatakayotwaliwa na Mamlaka kwa ajili ya shughuli za uwekezaji; na
(c)maeneo ya watu binafsi.
(4)Kwa madhumuni ya kuwezesha utekelezaji wa kifungu hiki, Mamlaka itafanya taratibu za kupata ardhi inayofaa kwa uwekezaji katika maeneo mbalimbali nchini.
(5)Katika kubaini ardhi inayofaa kwa ajili ya kujumuishwa katika benki ya ardhi, Mamlaka itazingatia eneo ardhi ilipo, ukubwa, gharama ya upatikanaji na shughuli za uwekezaji zinazoweza kufanyika kwa kuzingatia sifa ya eneo husika.
(6)Kabla ya ardhi inayomilikiwa na mtu binafsi kuingizwa katika benki ya ardhi, Mamlaka itajiridhisha kuhusu umiliki wa ardhi hiyo na endapo inafaa kwa ajili ya uwekezaji.
(7)Mtu ambaye ardhi yake imeingizwa katika benki ya ardhi atakuwa na wajibu wa kuitaarifu Mamlaka kuhusu mabadiliko yoyote yatakayotokea katika umiliki au yanayoweza kuathiri umiliki wa ardhi hiyo.
(8)Masharti ya kifungu hiki hayatatafsiriwa kumzuia mwekezaji kufanya shughuli za uwekezaji katika ardhi ambayo haipo katika benki ya ardhi:Isipokuwa kwamba, mwekezaji wa kigeni anayekusudia kufanya shughuli za uwekezaji katika ardhi ambayo haipo kwenye benki ya ardhi, atawasiliana na Mamlaka kuhusu kusudio hilo.
(9)Mamlaka itaratibu upatikanaji wa ardhi iliyorejewa katika kifungu kidogo cha (8) kwa ajili ya matumizi ya mwekezaji wa kigeni kwa kuzingatia masharti ya sheria husika.[Sura ya 113]
(10)Kwa kuzingatia masharti ya Sheria ya Ardhi, Mamlaka inaweza ikakodisha ardhi kwa mwekezaji kwa muda maalumu au ikammilikisha kwa utaratibu wa hati miliki isiyo ya asili.

24. Usimamizi wa ardhi ya uwekezaji

(1)Mamlaka itakuwa na wajibu wa kusimamia ardhi inayotumika kwa ajili ya shughuli za uwekezaji.
(2)Mamlaka inaweza kufuta hati miliki isiyo ya asili endapo itabaini kuwa mwekezaji ametelekeza mradi kwa kipindi cha miezi kumi na mbili au zaidi.
(3)Waziri, kwa kushirikiana na Waziri mwenye dhamana ya ardhi, atatengeneza kanuni kwa ajili ya kuweka utaratibu wa usimamizi wa ardhi itakayotumika kwa ajili ya uwekezaji.

Sehemu ya nne – Maeneo maalumu ya kiuchumi

25. Uanzishaji wa maeneo maalumu ya kiuchumi

(1)Maeneo maalumu ya kiuchumi yanaweza kuanzishwa katika sehemu mbalimbali kwa ajili ya kuvutia uwekezaji katika shughuli za kipaumbele za kiuchumi.
(2)Malengo ya uanzishwaji wa maeneo maalumu ya kiuchumi ni kuongeza tija katika uwekezaji, ushindani, ukuaji wa uchumi, uhamasishaji wa mauzo ya nje na uzalishaji wa ajira kwa Watanzania.
(3)Maeneo maalumu ya kiuchumi yanaweza kujumuisha maeneo yafuatayo:
(a)kongani za viwanda;
(b)maeneo maalumu ya uzalishaji kwa mauzo ya nje;
(c)maeneo ya biashara huru;
(d)maeneo ya bandari huru;
(e)kongani za utalii;
(f)maeneo ya kilimo;
(g)kongani za sayansi na teknolojia; au
(h)maeneo mengine yoyote kama Mamlaka inavyoweza kubainisha.
(4)Eneo maalumu la kiuchumi litakaloanzishwa chini ya kifungu hiki linaweza kuwa eneo—
(a)lililoendelezwa au ambalo halikuendelezwa;
(b)litakalotumika kwa ajili ya uzalishaji kwa mauzo ya nje pekee au matumizi mchanganyiko; na
(c)kwa ajili ya kiwanda kimoja au viwanda zaidi ya kimoja.

26. Utaratibu wa uanzishaji wa maeneo maalumu ya kiuchumi

(1)Mamlaka itatambua ardhi inayofaa kwa madhumuni ya kuanzisha maeneo maalumu ya kiuchumi na kuwasilisha mapendekezo kwa Waziri.
(2)Kwa madhumuni ya utekelezaji wa kifungu kidogo cha (1), Mamlaka inaweza kutambua ardhi inayofaa—
(a)kutoka katika ardhi iliyotengwa na mamlaka husika kwa ajili ya uwekezaji; au
(b)baada ya kupokea maombi kutoka kwa mtu binafsi anayemiliki ardhi.
(3)Waziri, baada ya kushauriana na Waziri mwenye dhamana ya ardhi na mamlaka nyingine zinazohusika, atatangaza eneo la ardhi husika kuwa eneo maalumu la kiuchumi, kwa notisi itakayochapishwa katika Gazeti la Serikali.
(4)Notisi itakayotolewa chini ya kifungu kidogo cha (3) itabainisha masuala yafuatayo:
(a)mipaka ya eneo maalumu la kiuchumi;
(b)aina ya eneo kwa kuzingatia kifungu cha 25(3);
(c)aina ya shughuli zitakazohamasishwa katika eneo husika; na
(d)taarifa nyingine yoyote kadiri itakavyoonekana muhimu.

27. Masuala ya forodha katika eneo maalumu la kiuchumi

(1)Kwa madhumuni ya forodha, baada ya eneo lolote kutangazwa kuwa eneo maalumu la kiuchumi, eneo hilo litakuwa chini ya udhibiti na usimamizi wa mamlaka ya forodha kwa kuzingatia sheria inayosimamia masuala ya forodha nchini.
(2)Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania anaweza kuweka utaratibu mahsusi wa usimamizi wa kodi katika maeneo maalumu ya kiuchumi, ikiwemo utaratibu wa uwasilishaji na usikilizaji wa mapingamizi ya kikodi kutoka kwa wawekezaji.

28. Uingizaji na utoaji wa huduma na bidhaa katika maeneo maalumu ya kiuchumi

(1)Isipokuwa kama imeelezwa vinginevyo katika Sheria hii au sheria nyingine yoyote—
(a)bidhaa au huduma inayoagizwa kutoka eneo la forodha na kuingizwa katika eneo maalumu la kiuchumi itatambulika kuwa imeagizwa kutoka Tanzania; na
(b)bidhaa au huduma inayoagizwa kutoka eneo maalumu la kiuchumi na kuingizwa katika eneo la forodha kwa matumizi ya ndani ya eneo la forodha itatambulika kuwa imeingizwa Tanzania.
(2)Bidhaa na huduma zilizokusudiwa kwa ajili ya eneo maalumu la kiuchumi zitafanyiwa ukaguzi wa forodha katika eneo maalumu la kiuchumi ambapo bidhaa na huduma husika imekusudiwa.
(3)Kwa kuzingatia kifungu kidogo cha (1), bidhaa zinazozalishwa katika eneo maalumu la kiuchumi kwa ajili ya mauzo ya nje hazitatolewa kutoka eneo hilo isipokuwa kwa madhumuni ya—
(a)kusafirishwa kwenda nje ya eneo la forodha kama bidhaa za nje; na
(b)kuingizwa katika eneo la forodha kwa kuzingatia—
(i)upatikanaji wa vibali muhimu kutoka kwa mamlaka ya forodha;
(ii)kulipwa kwa kodi zote za kuingiza bidhaa, ushuru na malipo mengine na kuzingatia taratibu zote za forodha; na
(iii)asilimia ya mauzo ya bidhaa hizo kutozidi asilimia ishirini ya uzalishaji wa mwaka wa mwekezaji.
(4)Bodi inaweza, kulingana na aina ya kiwanda au bidhaa au hali ya soko kwa wakati husika, kumruhusu mwekezaji kuuza katika eneo la forodha bidhaa zaidi ya kiwango kilichoainishwa katika kifungu kidogo cha (3).

29. Usimamizi wa eneo maalumu la kiuchumi

(1)Mwekezaji hataruhusiwa kufanya uwekezaji au biashara katika eneo maalumu la kiuchumi isipokuwa kwa leseni iliyotolewa na Mamlaka.
(2)Mamlaka inaweza kutoa kwa mwekezaji leseni zifuatazo katika maeneo maalumu ya kiuchumi:
(a)leseni ya uendelezaji wa eneo maalumu la kiuchumi;
(b)leseni ya uendeshaji wa eneo maalumu la kiuchumi; na
(c)leseni ya uzalishaji kwa ajili ya mauzo ya nje au kwa ajili ya soko la ndani.
(3)Vigezo na masharti ya kupata leseni, utaratibu wa maombi na utaratibu wa uendelezaji, uendeshaji au uzalishaji katika maeneo maalumu ya kiuchumi utaainishwa katika kanuni.
(4)Kwa madhumuni ya kifungu kidogo cha (3), vigezo na masharti ya kupata leseni yanaweza kujumuisha—
(a)kiwango cha uwekezaji;
(b)ukubwa wa eneo la ardhi kwa ajili ya uwekezaji;
(c)ajira zitakazozalishwa;
(d)uhawilishaji wa teknolojia;
(e)mnyororo wa thamani katika sekta;
(f)utaratibu wa kongani;
(g)viashiria muhimu vya utendaji;
(h)iwapo bidhaa zinazokusudiwa kuzalishwa hazizalishwi kwa utoshelevu katika soko la ndani; na
(i)vigezo au masharti mengine yoyote ambayo Mamlaka inaweza kuamua.
(5)Mamlaka inaweza kutoa maelekezo ya jumla au mahsusi kuhusu uendelezaji, uendeshaji au uzalishaji katika maeneo maalumu ya kiuchumi na kuchukua hatua zitakazofaa kuhakikisha utekelezaji wa maelekezo husika.

30. Watoa huduma katika eneo maalumu la kiuchumi

(1)Mtu anayekusudia kutoa huduma ndani ya eneo maalumu la kiuchumi ataomba kibali kwa Mamlaka.
(2)Katika kushughulikia maombi ya kibali chini ya kifungu hiki, miongoni mwa masuala mengine, Mamlaka itajiridhisha endapo mtu huyo ana leseni ya biashara kutoka kwa mamlaka inayohusika kutoa leseni ya biashara husika.
(3)Utaratibu wa kuomba kibali cha kutoa huduma ndani ya eneo maalumu la kiuchumi na kushughulikia maombi ya kibali utaainishwa katika kanuni.

Sehemu ya tano – Haki na wajibu wa Serikali na wawekezaji

31. Haki ya kusimamia uwekezaji

(1)Bila kuathiri masharti ya Sheria hii, Serikali itakuwa na haki ya kusimamia shughuli zote za uwekezaji kwa malengo ya kuhakikisha kuwa shughuli za uwekezaji nchini zinaendeshwa kwa kuzingatia misingi na malengo ya Sheria hii pamoja na malengo ya kisera ya kijamii, kimazingira na kiuchumi.
(2)Kwa madhumuni ya kifungu kidogo cha (1), afisa wa Mamlaka au afisa mwingine aliyeidhinishwa anaweza kuingia katika eneo linalotumiwa kwa shughuli za uwekezaji kwa ajili ya kufanya ufuatiliaji.

32. Wajibu wa mwekezaji

Mwekezaji atakuwa na wajibu ufuatao:
(a)kutii na kufuata masharti ya Sheria hii na sheria zote za nchi;
(b)kuwasilisha kwa wakati taarifa zinazohitajika na taasisi zinazohudumia wawekezaji ili kuziwezesha kutekeleza majukumu kwa ufanisi;
(c)kuendesha shughuli za uwekezaji kwa namna inayolinda walaji, mazingira, usawa wa kijinsia na kuendeleza ujuzi kwa wafanyakazi;
(d)kuwasilisha kwa Mamlaka taarifa za utekelezaji na maendeleo ya mradi wa uwekezaji ndani ya muda ulioainishwa;
(e)kutumia malighafi na rasilimali nyingine zinazopatikana au kuzalishwa nchini;
(f)kuruhusu maafisa wa Mamlaka au afisa mwingine aliyeidhinishwa kufanya ufuatiliaji wa maendeleo ya mradi na utekelezaji wa masharti ya Sheria hii; na
(g)kuzingatia masharti mengine yoyote yatakayowekwa na mamlaka husika.

33. Dhamana ya uhamishaji wa mitaji, faida na gawio

(1)Mwekezaji anaweza, kwa kupitia benki yoyote iliyoidhinishwa na kwa kutumia fedha za kigeni zinazoweza kubadilishika, kuhamisha nje ya Tanzania—
(a)faida halisi au gawio linalotokana na uwekezaji;
(b)malipo yanayohusiana na urejeshaji wa mkopo uliopatikana nje ya nchi;
(c)mapato yanayotokana na mauzo au ufilisi wa uwekezaji au faida yoyote inayotokana na uwekezaji, baada ya makato ya kodi na malipo mengine yaliyowekwa na sheria; na
(d)malipo kwa wafanyakazi wa kigeni walioajiriwa katika uwekezaji nchini Tanzania.
(2)Bila kujali kifungu kidogo cha (1), mwekezaji atanufaika na haki iliyoelezwa chini ya kifungu hiki baada ya kulipa madeni ya kodi, ada au tozo za Serikali na malipo mengine yaliyowekwa na sheria.

34. Kinga dhidi ya utaifishaji au utwaaji

(1)Kwa kuzingatia vifungu vidogo vya (2) na (3)—
(a)uwekezaji au mali za mwekezaji hazitataifishwa au kutwaliwa na Serikali; na
(b)mtu anayemiliki mtaji wote au sehemu ya mtaji wa uwekezaji hatalazimishwa na sheria kusalimisha maslahi yake ya mtaji kwa mtu mwingine.
(2)Serikali haitatwaa uwekezaji au mali za mwekezaji isipokuwa kama utwaaji huo ni kwa mujibu wa sheria inayoweka masharti ya—
(a)malipo ya fidia ya haki na kwa wakati; na
(b)haki ya kwenda mahakamani au kwenye chombo cha usuluhishi kwa ajili ya uamuzi wa maslahi au haki ya mwekezaji na kiasi cha fidia anachostahili kupata.
(3)Fidia yoyote inayolipwa chini ya kifungu hiki italipwa kwa wakati na idhini ya kurejeshwa kwa fidia hiyo katika fedha inayobadilishika itatolewa pale inapohitajika.

35. Fursa sawa kwa mwekezaji wa kigeni

(1)Kwa kuzingatia masharti ya Sheria hii, sheria nyingine za nchi, mikataba na makubaliano ya kimataifa ambayo Tanzania ni nchi mwanachama, mwekezaji wa kigeni
(a)atapata fursa sawa na mwekezaji wa ndani kuhusiana na uanzishaji, utwaaji, uendelezaji, usimamizi, uendeshaji na uuzaji au uondoshaji mwingine wa uwekezaji ndani ya nchi; na
(b)hatabaguliwa kwa misingi ya uraia, eneo la makazi, mahali alipoandikishwa au kusajiliwa au nchi ya asili ya uwekezaji.
(2)Masharti ya kifungu hiki hayatatafsiriwa—
(a)kuizuia Serikali kuchukua hatua za udhibiti au hatua nyingine ili kulinda maslahi ya umma, kama vile maadili ya umma, afya ya umma, usalama na ulinzi wa mazingira;
(b)kuizuia Serikali kuchukua hatua zozote za kuwawezesha wawekezaji wa ndani; na
(c)kuilazimisha Serikali kutoa kwa mwekezaji wa kigeni na uwekezaji wake upendeleo au fursa yoyote iliyo katika—
(i)eneo lolote la biashara huru, umoja wa forodha, makubaliano ya soko la pamoja, makubaliano yoyote ya kimataifa au mipango ambayo nchi anayotoka mwekezaji si mshirika; au
(ii)makubaliano yoyote ya kimataifa yaliyopo au ya siku zijazo au sheria ya ndani kuhusiana na ushuru.

36. Ukomo wa idadi ya wafanyakazi wa kigeni

Mwekezaji ataruhusiwa kuajiri wafanyakazi wa kigeni kwa kuzingatia ukomo wa idadi ulioainishwa katika sheria inayosimamia masuala ya ajira kwa wageni.

37. Upatikanaji wa mikopo kwa wawekezaji wa kigeni kutoka vyanzo vya ndani

(1)Mwekezaji wa kigeni anaweza kupata mikopo kutoka benki na taasisi za fedha za ndani kwa ajili ya uwekezaji anaofanya kwa kiwango kisichozidi ukomo uliowekwa na Benki Kuu ya Tanzania kwa kushauriana na Mamlaka kwa kuzingatia kiasi cha mtaji wa kigeni uliowekezwa.
(2)Mwekezaji wa kigeni anayepata mkopo kwa mujibu wa kifungu kidogo cha (1) atahakikisha kwamba mapato ya mkopo huo yanatumika kwa madhumuni ya kutekeleza shughuli zilizoainishwa katika maombi ya mkopo.
(3)Benki au taasisi ya fedha inayotoa mkopo inaweza, kwa madhumuni ya kifungu hiki, kuteua afisa au wakala wake ili kuthibitisha matumizi sahihi ya mkopo uliotolewa chini ya kifungu kidogo cha (1).

Sehemu ya sita – Ushughulikiaji wa malalamiko na utatuzi wa migogoro

38. Utaratibu wa kushughulikia malalamiko

(1)Endapo mwekezaji hajaridhika na mwenendo, kitendo au uamuzi wa taasisi ya Serikali kuhusu masuala ya uwekezaji, anaweza kuwasilisha malalamiko kwa Mamlaka.
(2)Mamlaka itachunguza na kufanya tathmini ya malalamiko na kuchukua hatua stahiki zinazokubalika na pande zote kutatua malalamiko husika.
(3)Utaratibu wa utatuzi wa malalamiko utazingatia misingi ya haki, uwazi na uzingatiaji wa sheria, na taasisi zote husika zitalazimika kushirikiana na Mamlaka katika jitihada za kutafuta suluhisho linalokubalika kwa pande zote.
(4)Mamlaka itapaswa kutatua malalamiko ndani ya siku thelathini kuanzia tarehe ya kupokea malalamiko.
(5)Taarifa na nyaraka zilizopokelewa na Mamlaka wakati wa utaratibu wa utatuzi wa malalamiko zitachukuliwa kuwa siri.
(6)Utaratibu wa kushughulikia malalamiko ya wawekezaji utabainishwa katika kanuni.

39. Rufaa

(1)Mtu ambaye hajaridhika na uamuzi uliotolewa na Mamlaka chini ya Sheria hii anaweza kukata rufaa kwa Waziri.
(2)Utaratibu wa kukata rufaa chini ya kifungu hiki utaainishwa kwenye kanuni.

40. Utatuzi wa migogoro

(1)Endapo mgogoro utatokea kati ya mwekezaji na Mamlaka au Serikali, juhudi zote zitafanywa ili kutatua mgogoro huo kwa njia ya majadiliano ili kufikia suluhu.
(2)Endapo mgogoro kati ya mwekezaji na Mamlaka au Serikali utashindwa kusuluhishwa kwa majadiliano, mgogoro huo unaweza kuwasilishwa katika chombo cha usuluhishi kilichokubaliwa na pande zote au kutatuliwa kwa njia nyingine yoyote iliyoainishwa katika makubaliano kati ya mwekezaji na Mamlaka au Serikali.
(3)Ikiwa hakuna makubaliano yaliyoingiwa au njia ya utatuzi wa mgogoro iliyoainishwa katika makubaliano kati ya mwekezaji na Mamlaka au Serikali, mgogoro husika unaweza kuwasilishwa katika mahakama yenye mamlaka ya kushughulikia suala hilo.

Sehemu ya saba – Masharti ya fedha

41. Vyanzo vya fedha za Mamlaka

Vyanzo vya fedha za Mamlaka vitajumuisha—
(a)fedha zitakazotengwa na Bunge;
(b)ada na tozo zinazotozwa katika huduma zinazotolewa na Mamlaka;
(c)fedha zinazotokana na misaada, zawadi na mikopo;
(d)fedha zitakazotokana na uwekezaji utakaofanywa na Mamlaka; na
(e)fedha nyingine zozote zitakazopatikana kwa ajili ya Mamlaka kutekeleza majukumu yake chini ya Sheria hii.

42. Bajeti ya Mamlaka

(1)Ndani ya miezi mitatu kabla ya mwisho wa kila mwaka wa fedha, Mkurugenzi Mkuu ataandaa na kuwasilisha kwa Bodi bajeti ya mwaka wa fedha unaofuata kwa ajili ya kuidhinishwa.
(2)Wakati wowote kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha, Mkurugenzi Mkuu anaweza kuandaa na kuwasilisha kwa Bodi makadirio ya nyongeza ya bajeti ya mwaka wa fedha husika kwa ajili ya kuidhinishwa.
(3)Matumizi hayatafanywa kwa fedha za Mamlaka isipokuwa kama yameidhinishwa na Bodi katika makadirio ya mwaka wa fedha husika au katika nyongeza ya bajeti ya mwaka husika.
(4)Bajeti ya mwaka au bajeti ya nyongeza iliyoidhinishwa na Bodi itawasilishwa kwa Waziri kwa ajili ya kuidhinishwa.
(5)Waziri anaweza kuitaka Mamlaka kufanya marekebisho ya bajeti ikiwa kwa maoni yake bajeti hiyo haiakisi makadirio sahihi na yenye uhalisia ya mapato na matumizi ya Mamlaka.
(6)Kwa idhini ya Bodi na baada ya kupata ridhaa ya Msajili wa Hazina, Mamlaka inaweza kuwekeza fedha zozote zisizohitajika kwa matumizi ya haraka kadri itakavyoona inafaa.

43. Hesabu na ukaguzi

(1)Mamlaka itatunza na kuhifadhi vitabu vya hesabu na kumbukumbu nyingine zinazohusu shughuli zake na kuandaa taarifa ya hesabu ya mwaka kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Umma.[Sura ya 348]
(2)Ndani ya kipindi cha miezi mitatu baada ya kuisha kwa kila mwaka wa fedha, Mamlaka itawasilisha kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, hesabu za Mamlaka zikiwa zimeambatishwa na—
(a)taarifa ya utendaji wa kifedha katika mwaka husika;
(b)taarifa ya hali ya kifedha ya Mamlaka katika siku ya mwisho ya mwaka husika; na
(c)taarifa au hesabu nyingine kama itakavyohitajika ili kubainisha kwa ukamilifu mali, madeni, faida, hasara na shughuli za Mamlaka.
(3)Hesabu za Mamlaka kama ambavyo zitakuwa zimethibitishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali au mtu mwingine yeyote aliyeteuliwa kwa niaba yake, pamoja na taarifa ya ukaguzi, zitawasilishwa kwa Waziri kila mwaka.
(4)Waziri atawasilisha Bungeni hesabu na taarifa ya ukaguzi iliyopokelewa chini ya kifungu kidogo cha (3) ndani ya miezi mitatu baada ya kupokea taarifa hiyo au katika kikao cha Bunge kinachofuata, chochote kitakachotangulia kati ya hivyo.

44. Taarifa ya mwaka

(1)Ndani ya miezi mitatu baada ya kuisha kwa mwaka wa fedha, Mamlaka itaandaa taarifa ya mwaka kuhusu utendaji wa Mamlaka na kuiwasilisha kwa Waziri ambaye ataiwasilisha Bungeni.
(2)Taarifa ya mwaka itajumuisha—
(a)maelezo ya kina kuhusu utendaji wa Mamlaka kwa mwaka husika;
(b)nakala ya hesabu za Mamlaka zilizokaguliwa pamoja na taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali; na
(c)maelezo mengine yoyote ambayo Mamlaka itaona ni muhimu au ambayo Waziri ataelekeza.

Sehemu ya nane – Masharti ya jumla

45. Makosa na adhabu

(1)Mtumishi wa Mamlaka au mtu mwingine aliyeidhinishwa ambaye wakati wa kutekeleza Sheria hii atapata nyaraka au taarifa yoyote chini ya Sheria hii na kuwasilisha nyaraka au taarifa hiyo kwa mtu mwingine ambaye hajaidhinishwa kwa sheria yoyote au na Bodi, anatenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyopungua shilingi milioni moja na isiyozidi shilingi milioni tano au kifungo kisichopungua miezi sita na kisichozidi mwaka mmoja.
(2)Mwajiriwa wa Mamlaka ambaye ana wajibu wa kutekeleza chini ya Sheria hii na ameshindwa kutekeleza wajibu huo au ametekeleza wajibu huo kwa uzembe atachukuliwa hatua za kinidhamu ambazo Bodi au mamlaka husika ya nidhamu inaweza kuamua.
(3)Mtu ambaye—
(a)kwa kujua au kwa uzembe anatoa taarifa za uongo au za kupotosha;
(b)anakataa au anapuuza kutoa taarifa ambayo Mamlaka inaweza kuhitaji kwa madhumuni ya utekelezaji wa Sheria hii;
(c)anakataa bila sababu ya msingi kumruhusu afisa aliyeidhinishwa kuingia kwenye eneo lake la biashara au vinginevyo anazuia ukaguzi wowote unaofanywa na afisa aliyeidhinishwa katika kutekeleza majukumu yake ya ufuatiliaji;
(d)anatumia vivutio vilivyotolewa kwa madhumuni tofauti na ilivyokusudiwa;
(e)ikiwa ni mwekezaji wa kigeni, anafanya shughuli za uwekezaji bila kusajiliwa chini ya Sheria hii;
(f)anafanya shughuli ya uwekezaji tofauti na iliyosajiliwa au kutambuliwa na Mamlaka; na
(g)kwa udanganyifu, anasafirisha bidhaa kwenda nchi nyingine akidai kuwa bidhaa hizo zimetengenezwa au kuzalishwa katika eneo maalumu la kiuchumi kwa lengo la kupata manufaa yoyote yanayotolewa kwa Jamhuri ya Muungano chini ya makubaliano au mkataba wa kimataifa au kikanda,
anatenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyopungua shilingi milioni tano na isiyozidi shilingi milioni hamsini au kifungo kisichopungua miezi sita na kisichozidi miaka mitano au vyote.
(4)Endapo kosa limetendwa na taasisi, mkurugenzi, mbia, afisa mkuu wa usimamizi au afisa anayehusika katika taasisi hiyo atachukuliwa pia kuwa ametenda kosa hilo.
(5)Pamoja na adhabu zilizoainishwa katika kifungu hiki, Mamlaka inaweza kuchukua hatua zifuatazo dhidi ya mwekezaji:
(a)kufuta au kusitisha cheti au leseni; au
(b)kupendekeza kwa mamlaka husika ufutaji wa baadhi au vivutio vyote.

46. Adhabu ya jumla

Mtu yeyote ambaye atakiuka masharti ya Sheria hii ambapo adhabu haikuainishwa, anatenda kosa na akitiwa hatiani atawajibika kulipa faini isiyopungua shilingi milioni mbili na isiyozidi shilingi milioni tano au kifungo kisichopungua miezi sita na kisichozidi miaka miwili au vyote.

47. Kinga dhidi ya uwajibikaji binafsi

Mjumbe wa Bodi, Mkurugenzi Mkuu au afisa wa Mamlaka hatafunguliwa shauri, madai au kuwajibishwa kwa nafasi yake binafsi kwa kitendo au jambo alilotenda au kutotenda kwa nia njema katika utekelezaji wa majukumu yake chini ya Sheria hii.

48. Rejesta ya uwekezaji

Mamlaka itatunza rejesta ya uwekezaji itakayokuwa na taarifa kuhusu wawekezaji wanaohudumiwa na Mamlaka, shughuli za uwekezaji zinazofanyika nchini na taarifa nyingine kadiri Bodi itakavyoamua.

49. Matumizi ya Sheria nyingine

(1)Kwa madhumuni ya Sheria ya Mipango Miji na kanuni zinazohusu majengo ndani ya maeneo maalumu ya kiuchumi, rejea ya mamlaka ya serikali za mitaa katika masharti yanayohusu idhini ya upangaji na kibali cha ujenzi itatafsiriwa kama rejea kwa Mamlaka.
(2)Leseni itakayotolewa kwa mwekezaji itatumika kama vile ni leseni iliyotolewa na mamlaka husika chini ya Sheria ya Usajili wa Biashara na Sheria ya Utoaji wa Leseni na Usajili wa Viwanda.[Sura ya 213 na Sura ya 46]
(3)Kwa madhumuni ya utoaji wa leseni chini ya Sheria hii, Mamlaka itashauriana na mamlaka zinazohusika na utekelezaji wa Sheria ya Usajili wa Biashara na Sheria ya Utoaji wa Leseni na Usajili wa Viwanda kwa lengo la kuwa na kumbukumbu zilizoratibiwa za watu au kampuni zinazofanya biashara Tanzania.

50. Kanuni

Waziri anaweza kutengeneza kanuni kwa ajili ya utekelezaji bora wa masharti ya Sheria hii.

51. Masharti ya mpito na kufutwa kwa Sheria

(1)Sheria ya Uwekezaji Tanzania ya mwaka 2022, Sheria ya Maeneo ya Uzalishaji kwa Mauzo ya Nje ya mwaka 2002 na Sheria ya Maeneo Maalumu ya Kiuchumi ya mwaka 2006 zinafutwa.[Sheria Na. 10 ya 2022 ; 11 ya 2002; 2 ya 2006]
(2)Bila kujali kufutwa kwa Sheria zilizoainishwa katika kifungu kidogo cha (1)—
(a)cheti cha vivutio au leseni iliyotolewa chini ya Sheria yoyote kati ya zilizofutwa itaendelea kuwa halali kwa kuzingatia vigezo na masharti ya kutolewa hadi mwisho wa muda ambao mnufaika wa vivutio au mmiliki wa leseni alikuwa na haki ya kunufaika na manufaa, vivutio au kinga yoyote; na
(b)makubaliano yaliyoingiwa chini ya Sheria yoyote kati ya zilizofutwa yataendelea kuwa halali kwa kuzingatia vigezo na masharti ya makubaliano hayo na yatakuwa halali hadi mwisho wa muda ambao mnufaika alikuwa na haki ya kunufaika na manufaa, vivutio au kinga yoyote, na baada ya kumalizika kwa muda ulioainishwa, masharti ya Sheria hii yataanza kutumika.
(3)Suala lolote linaloendelea mbele ya Kituo cha Uwekezaji Tanzania au Mamlaka ya Maeneo ya Uzalishaji kwa Mauzo ya Nje kwa mujibu wa sheria zilizofutwa litahesabiwa kuwa linaendelea mbele ya Mamlaka.
(4)Baada ya kuanza kutumika kwa Sheria hii, kanuni, miongozo au sheria ndogo nyingine zozote zinazohusu uwekezaji, uendelezaji au uendeshaji wa maeneo maalumu ya kiuchumi ambazo zilikuwa zinatumika kabla ya kuanza kutumika kwa Sheria hii zitaendelea kutumika kana kwamba zimetengenezwa chini ya Sheria hii, kwa kiwango ambacho hazikinzani na masharti ya Sheria hii, hadi pale zitakapobadilishwa au kufutwa.
(5)Endapo uwekezaji uliokuwa unatekelezwa kabla ya kuanza kutumika kwa Sheria hii umezingatia ipasavyo masharti yoyote ya kima cha chini cha mtaji wa uwekezaji yaliyoainishwa katika Sheria iliyofutwa, uwekezaji huo utachukuliwa kuwa halali bila kujali masharti yoyote ya Sheria hii yanayoeleza vinginevyo.

Sehemu ya tisa – Marekebisho ya Sheria mbalimbali

(a) – Marekebisho ya Sheria ya Ardhi, (Suraya 113)

52. Ufafanuzi

Sehemu Ndogo hii itasomwa pamoja na Sheria ya Ardhi ambayo hapa imerejewa kama “Sheria kuu”.[Sura ya 113]

53. Marekebisho ya jumla

Sheria kuu inafanyiwa marekebisho ya jumla—
(a)kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Act” popote yanapoonekana na badala yake kuweka maneno “Investment and Special Economic Zones Act”; na
(b)kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Centre” popote yanapoonekana na badala yake kuweka maneno “Tanzania Investment and Special Economic Zones Authority”.

54. Marekebisho ya kifungu cha 2

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 2 kwa kufuta na kuandika upya tafsiri ya msamiati “foreign company” kama ifuatavyo:“foreign company” shall have the meaning ascribed to the term “foreign investor” under the Investment and Special Economic Zones Act;”.

55. Marekebisho ya kifungu cha 6

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 6(1) kwa—
(a)kuongeza baada ya aya (b) aya mpya ifuatayo:
(c)land designated for investment;”; na
(b)kubadili mpangilio wa aya (c) na (d) kuwa aya (d) na (e), mtawalia.

56. Marekebisho ya kifungu cha 19

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 19(2)—
(a)kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Act” yaliyo katika aya (a) na badala yake kuweka maneno “Investment and Special Economic Zones Act”; na
(b)kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Act or issued under the Export Processing Zones Act” yaliyopo katika aya (b) na (c) na badala yake kuweka maneno “Investment and Special Economic Zones Act”.

(b) – Marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Ajira kwa Raia wa Kigeni, (Suraya 436)

57. Ufafanuzi

Sehemu Ndogo hii itasomwa pamoja na Sheria ya Usimamizi wa Ajira kwa Raia wa Kigeni ambayo hapa imerejewa kama “Sheria kuu”.[Sura ya 436]

58. Marekebisho ya kifungu cha 19

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 19 kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Centre and Export Processing Zones Authority” yanayoonekana katika kifungu kidogo cha (1) na (3) na badala yake kuweka maneno “Tanzania Investment and Special Economic Zones Authority”.

(c) – Sheria ya Kodi ya Mapato, (Suraya 332)

59. Ufafanuzi

Sehemu Ndogo hii itasomwa pamoja na Sheria ya Kodi ya Mapato ambayo hapa imerejewa kama “Sheria kuu”.[Sura ya 332]

60. Marekebisho ya kifungu cha 3

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 3 kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Act” katika tafsiri ya msamiati “strategic investor” na badala yake kuweka maneno “Investment and Special Economic Zones Act”.

61. Marekebisho ya kifungu cha 10

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 10(3)(b) kwa kufuta na kuandika upya aya ndogo ya (iii) kama ifuatavyo:
(iii)for a strategic investment approved by the Cabinet under the Investment and Special Economic Zones Act,”.

62. Marekebisho ya kifungu cha 143

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 143(4) kwa kufuta maneno “Tanzania Investment Centre under the Tanzania Investment Act” na badala yake kuweka maneno “Tanzania Investment and Economic Zones Authority under the Investment and Special Economic Zones Act”.

63. Marekebisho ya Jedwali la Pili

Sheria kuu inarekebishwa katika Jedwali la Pili katika kivuo cha aya (o) kwa kufuta maneno “category B investor in the Special Economic Zone as provided in the Special Economic Zones Act” na badala yake kuweka maneno “an investor in the special economic zone producing for sale into the customs territory”.

(d) – Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani, (Suraya 148)

64. Ufafanuzi

Sehemu Ndogo hii itasomwa pamoja na Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani ambayo hapa imerejewa kama “Sheria kuu”.[Sura ya 148]

65. Marekebisho ya kifungu cha 6

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 6 kwa kufuta na kuandika upya kifungu kidogo cha (1A) kama ifuatavyo:
(1A)Notwithstanding the provisions of subsection (1), the Minister shall, by order published in the Gazette, grant value added tax exemption on goods or services for implementation of strategic investment approved by the Cabinet under the Investment and Special Economic Zones Act:Provided that, exemption under this subsection shall not extend to office equipment, stationeries, furniture, sugar, beverages, spirits, tiles, non-utility motor vehicles, crockeries, air conditioners, fridges, petroleum products, cutleries, beddings, cement, steel re-enforcement bars, roofing sheets, PVC and HDPE pipes with HS Code 3917.23.00 and HS Code 3917.21.00 respectively, imported trailers classified under HS Code 8716.31.90 and 8716.40.90 and electronic equipment.”.

(e) – Sheria ya Ushuru wa Bidhaa, (Sura ya 147)

66. Ufafanuzi

Sehemu Ndogo hii itasomwa pamoja na Sheria ya Ushuru wa Bidhaa ambayo hapa imerejewa kama“Sheria kuu”.[Sura ya 147]

67. Marekebisho ya kifungu cha 128

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 128 kwa kufuta na kuandika upya kifungu kidogo cha (2B) kama ifuatavyo:
(2B)Notwithstanding the provisions of subsection (1), the Minister shall, by order published in the Gazette, remit excise duty on goods imported or purchased for implementation of strategic investment approved by the Cabinet under the Investment and Special Economic Zones Act:Provided that, exemption under this subsection shall not extend to office equipment, stationeries, furniture, sugar, beverages, spirits, tiles, non-utility motor vehicles, crockeries, air conditioners, fridges, petroleum products, cutleries, beddings, cement, steel re-enforcement bars, roofing sheets, PVC and HDPE pipes with HS Code 3917.23.00 and HS Code 3917.21.00 respectively, imported trailers classified under HS Code 8716.31.90 and 8716.40.90 and electronic equipment.”.

(f) – Sheria ya Tozo za Barabara na Mafuta, (Sura ya 220)

68. Ufafanuzi

Sehemu Ndogo hii itasomwa pamoja na Sheria ya Tozo za Barabara na Mafuta ambayo hapa imerejewa kama “Sheria kuu”.[Sura ya 220]

69. Marekebisho ya kifungu cha 8

Sheria kuu inarekebishwa katika kifungu cha 8 kwa kufuta na kuandika upya kifungu kidogo cha (2) kama ifuatavyo:
(2)Notwithstanding the provisions of subsection (1), the Minister shall, by order published in the Gazette, exempt strategic investments approved by the Cabinet under the Investment and Special Economic Zones Act from payment of fuel tolls.”

Jedwali (Limetengenezwa chini ya kifungu cha 8(4))

Taaratibu na masuala kuhusu Bodi ya Mamlaka

1.Muda wa kushika madaraka
(1)Mwenyekiti au mjumbe wa Bodi, isipokuwa kama uteuzi wake utatenguliwa au ataacha kuwa mjumbe kwa namna nyingine yoyote, atashika madaraka kwa muda wa miaka mitatu na anaweza kuteuliwa tena kwa kipindi kingine kimoja.
(2)Bila kujali aya ndogo ya (1), mjumbe wa Bodi atakoma kuwa mjumbe endapo—
(a)muda wake wa kutumikia Bodi utaisha;
(b)atajiuzulu, kwa kutoa notisi ya maandishi kwa mamlaka ya uteuzi;
(c)atashindwa kuhudhuria vikao vitatu vya Bodi bila ruhusa ya Mwenyekiti;
(d)atahukumiwa kifungo kinachozidi miezi sita;
(e)atatamkwa na mahakama kuwa amefilisika; na
(f)itathibitika kuwa hawezi kutekeleza majukumu yake kutokana na ugonjwa wa mwili au akili.
2.Uteuzi wa mjumbe wa mudaPale ambapo mjumbe yeyote wa Bodi, kwa sababu ya kutokuwepo nchini, ugonjwa au sababu nyingine ya msingi, atashindwa kutekeleza majukumu yake kama mjumbe kwa kipindi cha miezi sita, mamlaka ya uteuzi inaweza kuteua mjumbe wa muda katika nafasi yake na mjumbe huyo wa muda atashika madaraka hadi pale mjumbe wa awali atakaporejea katika majukumu yake au hadi muda wa mjumbe wa awali kushika madaraka utakapoisha, lolote litakalotangulia.
3.Mgongano wa maslahi
(1)Mjumbe wa Bodi atachukuliwa kuwa na mgongano wa maslahi kwa madhumuni ya Sheria hii ikiwa ana maslahi ya kifedha au maslahi mengine yanayokinzana au yanayoweza kukinzana na utendaji bora wa majukumu au mamlaka yake kama mjumbe wa Bodi.
(2)Pale ambapo mjumbe wa Bodi ana mgongano wa maslahi kuhusiana na—
(a)jambo lolote lililo mbele ya Mamlaka kwa ajili ya kujadiliwa au kuamuliwa; au
(b)jambo lolote ambalo Mamlaka ingelitarajia kuja mbele yake kwa ajili ya kujadiliwa au kuamuliwa,
mjumbe huyo ataweka wazi, mapema iwezekanavyo, maslahi aliyo nayo kwa wajumbe wengine au Katibu na kutoshiriki au kujitoa katika majadiliano au uamuzi wa jambo husika.
4.Vikao vya Bodi
(1)Bodi itakutana kwa kawaida angalau mara moja kila robo mwaka kwa ajili ya kuendesha shughuli zake.
(2)Mwenyekiti anaweza kuitisha kikao cha dharura wakati wowote pale ambapo kuna jambo la dharura linalohitaji kuamuliwa na Bodi au pale ambapo kuna maombi ya wajumbe wasiopungua wanne.
(3)Mwenyekiti ataongoza vikao vyote vya Bodi.
(4)Endapo katika kikao chochote cha Bodi Mwenyekiti hayupo, wajumbe waliohudhuria watamchagua mjumbe mmoja kati yao kuongoza kikao hicho.
(5)Bodi inaweza kumwalika mtu yeyote ambaye si mjumbe kuhudhuria na kushiriki katika majadiliano katika kikao chochote cha Bodi isipokuwa mtu huyo hatakuwa na haki ya kupiga kura.
5.AkidiAkidi katika kikao chochote cha Bodi itakuwa angalau wajumbe watano.
6.Uamuzi wa Bodi
(1)Kwa kuzingatia aya ndogo ya (2), masuala yanayopendekezwa kwenye kikao cha Bodi yataamuliwa kwa wingi wa kura za wajumbe waliohudhuria na kupiga kura, na endapo kura zitalingana, Mwenyekiti au mjumbe anayeongoza kikao atakuwa na kura ya uamuzi zaidi ya kura yake ya awali.
(2)Bodi inaweza kufanya uamuzi bila kuitisha kikao kwa kusambaza miongoni mwa wajumbe nyaraka zinazohusika na mawasilisho ya wajumbe kwa maandishi yatakuwa uamuzi wa Bodi, isipokuwa mjumbe yeyote anaweza kuomba uamuzi husika uahirishwe na suala hilo lijadiliwe katika kikao cha Bodi kitakachofuata.
7.Kamati
(1)Bodi inaweza kuunda na kuteua kutoka miongoni mwa wajumbe wake kamati kwa ajili ya kutekeleza majukumu ya Bodi chini ya Sheria hii.
(2)Kamati ya Bodi inaweza kumwalika mtu yeyote kuhudhuria na kujadili suala mahsusi kama kamati itakavyoamua, isipokuwa mtu huyo hatakuwa na haki ya kupiga kura.
(3)Kamati ya Bodi itatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia maelekezo ya Bodi.
8.Muhtasari wa vikaoMuhtasari wa kila kikao cha Bodi utaandikwa katika utaratibu sahihi na utaridhiwa au utasahihishwa na kuridhiwa na Bodi katika kikao cha Bodi kinachofuata na kusainiwa na mjumbe aliyeongoza kikao kinachohusika na muhtasari huo pamoja na Katibu.
9.Nafasi kuwa wazi kutobatilisha mwenendoKitendo chochote au mwenendo wa Bodi hautabatilishwa kutokana na nafasi ya mjumbe yeyote kuwa wazi au kasoro yoyote katika uteuzi wa mjumbe.
10.Ada na poshoWajumbe wa Bodi watalipwa ada na posho kama zitakavyoidhinishwa na mamlaka husika.
11.Bodi kuamua utaratibu wakeKwa kuzingatia masharti ya Jedwali hili, Bodi inaweza kuamua utaratibu wa kuendesha shughuli zake.

History of this document

01 July 2025 amendment not yet applied
Amended by Finance Act, 2025
30 June 2025 this version
04 March 2025
Assented to
To the top