Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka, 2025

Government Notice 430 of 2025

Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka, 2025
Ask AI
Ask questions and understand this document faster using AI.

Tanzania
Criminal Procedure Act

Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka, 2025

Tangazo la Serikali 430 ya 2025

[Zimetengenezwa chiniya kifungu cha 194(3)]

Sehemu ya kwanza – Masharti ya utangulizi

1. Jina

Kanuni hizi zitajulikana kama Kanuni za Ulinzi wa Mashahidi za Mwaka 2025.

2. Matumizi

Kanuni hizi zitatumika kwa mashahidi kama walivyotafsiriwa katika Kanuni hizi.

3. Tafsiri

Katika Kanuni hizi, isipokuwa kama muktadha utahitaji vinginevyo—amri ya ulinzi” maana yake ni amri ya mahakama inayoelekeza ulinzi wa shahidi;kihatarishi” maana yake ni uwezekano wa kutokea kwa tishio au hatari;kizimba maalum cha shahidi” maana yake ni sehemu ya kusimama au kukaa wakati wa kutoa ushahidi iliyoandaliwa mahsusi ili kumwezesha shahidi anayelindwa kutoa ushahidi bila kuonekana isipokuwa kwa jaji au hakimu anaeyeendesha shauri husika;mahakama” maana yake ni mahakama yenye mamlaka ya kusikiliza shauri ambalo amri ya ulinzi imeombwa;mahakama ya chini” maana yake ni mahakama ya wilaya au mahakama ya hakimu mkazi;mkutano kwa njia ya simu” maana yake ni utoaji wa ushahidi mahakamani kwa njia ya sauti kupitia simu au kifaa kingine cha mawasiliano;mkutano kwa njia ya video” maana yake ni utoaji wa ushahidi mahakamani kwa njia ya video na sauti;mtoto” maana yake ni mtu ambaye hajafikisha umri wa miaka kumi na nane;shahidi” maana yake ni mtu anayehitaji ulinzi kutokana na tishio au hatari iliyopo au inayoweza kutokea kutokana na kutoa taarifa katika chombo cha kusimamia sheria, kutoa au kukubali kutoa ushahidi kuhusiana na kosa au shauri la jinai au kwa sababu nyingine yoyote ambayo mahakama inaweza kuona kuwa inatosheleza, na anajumuisha mtu anayestahili ulinzi kwa sababu ya kuwa na uhusiano na mtu huyo;shahidi anayelindwa” maana yake ni shahidi aliye chini ya amri ya ulinzi;[Sura ya 20]Sheria” maana yake ni Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai;tishio” maana yake ni uwezekano wa matokeo mabaya kwa shahidi kutokana na kutoa ushahidi katika shauri na inajumuisha hatari yoyote ya kimwili au kisaikolojia, inayoweza kutokea kutokana na kushiriki kwake katika shauri hilo;uhariri” inamaanisha kuondoa taarifa za utambulisho kutoka kwenye hati au kitu;ulinzi wa shahidi” maana yake ni hatua au mbinu za kumlinda shahidi ambaye maisha, usalama, au mali yake inaweza kuwa katika hatari au tishio kutokana na kukubali kutoa ushahidi mahakamani katika shauri husika;vifaa saidizi vya mawasiliano” maana yake ni vifaa au mbinu yoyote inayoweza kumwezesha shahidi kuwasiliana kwa ufanisi wakati wa kutoa ushahidi mahakamani.

Sehemu ya pili – Ulinzi wa mashahidi

4. Maombi ya amri ya ulinzi

(1)Mkurugenzi wa Mashtaka, kabla ya kufungua mashtaka, au katika hatua yoyote ya mwenendo wa shauri chini ya Sheria, anaweza kuleta maombi ya upande mmoja ya amri ya ulinzi wa shahidi.
(2)Maombi chini ya kanuni hii yanaweza kuletwa kwa hati ya faragha ikiambatishwa na hati ya kiapo yakieleza hatua au aina ya ulinzi inayoombwa na sababu zake, lakini mahakama inaweza, kwa sababu za msingi, kuruhusu uletwaji wa maombi kwa njia ya mdomo.
(3)Baada ya kupokea maombi chini ya kanuni hii, mahakama itahakikisha kuwa taarifa zinazohusiana na hatua za ulinzi zinazoombwa hazifichuliwi hadi uamuzi wa maombi utakapotolewa.

5. Mamlaka ya mahakama kutoa amri ya ulinzi wa shahidi

(1)Mahakama inaweza kutoa amri ya ulinzi iwapo itaridhika kwamba mtu aliyebainishwa katika maombi ni shahidi kwa madhumuni ya Kanuni hizi na maisha yake, usalama wake, au mali yake inaweza kuwa katika hatari au tishio kutokana na yeye kuwa shahidi.
(2)Katika kutoa uamuzi chini ya kanuni hii, mahakama itazingatia mazingira ya shauri ikiwa ni pamoja na—
(a)uzito wa kosa ambalo linahusishwa na ushahidi au maelezo ya shahidi huyo;
(b)aina na umuhimu wa ushahidi au maelezo husika;
(c)aina ya hatari inayoweza kumkumba shahidi;
(d)uwepo wa njia mbadala zinazofaa kumlinda shahidi;
(e)kumbukumbu ya makosa ya jinai ya shahidi au mshitakiwa;
(f)uwezekano wa amri husika kuzuia ushahidi kudodoswa ipasavyo na mdaawa yeyote katika shauri au kutohatarisha maslahi ya haki; au
(g)hatari inayoweza kutokea kwa umma iwapo shahidi hatalindwa.
(3)Maombi ya amri ya ulinzi yatasikilizwa katika faragha.

6. Amri za ulinzi

(1)Mahakama inaweza kutoa amri ya ulinzi kwa kuelekeza hatua yoyote au mchanganyiko wa hatua zifuatazo kwa madhumuni ya:
(a)kuzuia kuwekwa wazi kwa umma au vyombo vya habari utambulisho au mahali alipo shahidi, au watu wanaohusiana naye au kuhusishwa naye kwa njia mbalimbali, ikiwemo;
(i)kuondoa taarifa zinazomtambulisha kutoka kwenye taarifa za mahakama zinazowekwa wazi kwa umma;
(ii)kuhariri taarifa zinazomtambulisha katika nyaraka au vitu;
(iii)kutofichua jina la shahidi au mhanga au kumpa jina bandia kwenye hati ya mashtaka au taarifa;
(iv)kutofichua maelezo au nyaraka zinazoweza kupelekea utambuzi wa shahidi;
(v)kutoa ushahidi kwa kutumia vifaa vya kupotosha au kubadilisha picha au sauti, au akiwa haonekani;
(vi)kumpa shahidi jina bandia ambalo halitasababisha utambulisho wake kwa namna yoyote ile;
(vii)kukataza mhusika yeyote katika shauri kuweka wazi taarifa zozote za shahidi kwa mtu asiyehusika;
(viii)kumpa shahidi chumba maalum na kilichojitenga cha kusubiria; au
(ix)kuendesha mwenendo wa shauri katika faragha;
(b)kuruhusu utoaji wa ushahidi bila uwepo wa shahidi mahakamani, ikiwa ni pamoja na—
(i)mkutano kwa njia ya video akionekana kwa jaji au hakimu anayesikiliza shauri; au
(ii)mkutano kwa njia ya simu;
(c)kuwezesha kutoa ushahidi ikiwa ni pamoja na—
(i)kutumia vifaa saidizi vya mawasiliano;
(ii)kutumia kizimba maalum cha shahidi;
(iii)kubadilisha eneo au tarehe ya kusikilizwa kwa shauri; au
(iv)kuharakisha usikilizwaji wa shahidi husika pale inapohitajika kulingana na mazingira ya shauri ili kutenda haki.
(2)Bila kujali masharti ya kanuni ndogo (1), mahakama inaweza kuelekeza hatua nyingine zozote za ulinzi inazoona zinafaa ambazo hazitaathiri haki ya kusikilizwa kwa usawa.

7. Ukomo wa amri ya ulinzi na athari zake

(1)Hatua za ulinzi wa shahidi zilizoelekezwa na mahakama zitadumu kwa muda wote wa usikilizwaji wa shauri au kwa kipindi ambacho mahakama itaamua isipokuwa kama amri husika itaashiria vinginevyo.
(2)Endapo amri ya ulinzi imetolewa, utoaji wa hati ya wito kwa shahidi na uendeshaji wa shauri vitazingatia masharti ya amri ya ulinzi.
(3)Endapo amri ya ulinzi imetolewa kabla ya kufunguliwa kwa hati ya mashtaka—
(a)endapo shauri linasikilizwa na mahakama ya chini, mashtaka yatawasilishwa kwa mujibu wa amri ya ulinzi na yataambatishwa na amri hiyo;
(b)endapo shauri linasikilizwa na Mahakama Kuu:
(i)mashtaka katika mahakama inayoendesha mwenendo wa ukabidhi yatawasilishwa kwa mujibu wa amri ya ulinzi na yataambatishwa na amri hiyo; na
(ii)hati ya mashtaka ya kufungua shauri Mahakama Kuu itaambatishwa na amri ya ulinzi pamoja na maelezo ya mashahidi waliokusudiwa na nyaraka husika.
(4)Mwenendo wa ukabidhi utaendeshwa kwa mujibu wa amri ya ulinzi.

8. Mabadiliko ya amri ya ulinzi

Amri ya ulinzi inaweza kufutwa au kubadilishwa na mahakama kwa utashi wake au kufuatia maombi ikiwa itaridhika kuwa kuna mabadiliko ya hali ya shahidi tangu kutolewa kwa amri hiyo ambayo yanalazimisha mabadiliko ya amri ya ulinzi.

9. Usikilizwaji wa faragha

(1)Mahakama inaweza kumzuia mtu yeyote, vyombo vya habari, au umma kushiriki sehemu au mwenendo mzima wa shauri, au kuagiza shauri lifanyike kwa faragha kwa sababu zifuatazo:
(a)kulinda haki za shahidi;
(b)kudumisha utulivu wa umma au maadili;
(c)kuhakikisha usalama, ulinzi, faragha, au kutofichua utambulisho wa shahidi;
(d)kudumisha heshima na staha ya mwenendo wa shauri;
(e)kulinda maslahi ya haki au ya umma; au
(f)sababu nyingine yoyote ambayo mahakama itaona inafaa.
(2)Katika mazingira ya kipekee na kufuatia maombi ya Mkurugenzi wa Mashtaka, mahakama inaweza kuelekeza kwamba mtu yeyote ambaye uwepo wake sio muhimu katika shauri au kundi la watu fulani, wasiwepo wakati wa uendeshaji wa shauri hilo na amri hiyo inaweza kuhusisha usomaji wa hukumu.
(3)Endapo anayetoa ushahidi ni mtoto, mahakama, kwa utashi wake, inaweza kuzuia uwepo wa mtu yeyote isipokua mzazi, mlezi, au afisa ustawi wa jamii au mtu mwingine yeyote ambae uwepo wake ni wa lazima au aliyeruhusiwa na mahakama.

10. Wajibu wa mahakama wakati wa kuhojiwa kwa shahidi na kupokelewa kwa vielelezo

Endapo usikilizaji wa shauri unahusisha shahidi aliye chini ya amri ya ulinzi, jaji au hakimu anayesikiliza shauri, atafanya yafuatayo:
(a)kudhibiti ipasavyo namna ya uulizwaji wa maswali kwa shahidi, ikiwa ni pamoja na kukataa swali ambalo linaloweza kupelekea kukiuka amri ya ulinzi au kusababisha bughudha, vitisho, hofu, au mkanganyiko kwa shahidi; na
(b)kuhakikisha kuwa mchakato wa kuidhinisha na kupokea vielelezo haukiuki amri ya ulinzi.

History of this document

11 July 2025 this version
10 July 2025
Assented to
To the top